Na. Grace
Semfuko, MAELEZO.24/06/2019
Wito
umetolewa kwa wakazi wa Makete waishio Jijini Dar es Salaam, kuanzisha Kampuni
ya Uwekezaji na Mfuko wa Maendeleo wa Wilaya hiyo utakaoangalia fursa za
kiuchumi zinazopatikana Makete, Mkoani Njombe, ili kukuza pato lao na Taifa kwa
ujumla.
Wito
huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC) Bw.
Geoffrey Mwambe, wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Wanachama wa Chama cha Maendeleo
Makete (MDA) uliofanyika Jijini Dar es Salaam.
Bwana
Mwambe akasema, fursa ya kuanzisha
kampuni na mfuko utawawezesha wakazi hao kununua hisa na umiliki pamoja na
kuwapa fursa za kutafuta masoko ya bidhaa na huduma zitakazotolewa ikiwa ni
sehemu ya kuitangaza Wilaya hiyo kwa wawekezaji wengine.
“Makete mna fursa nyingi za uwekezaji, kuna kilimo
cha ngano, pareto, viazi, matunda na mbogamboga, pia mnayo madini mbalimbali, mnao
utalii wa ndege na maua kule kwenye hifadhi ya Kituro, ndugu zangu, uwekezaji
katika sekta hizo inawezekana kabisa, pia mnayo ardhi ya kutosha, ni muhimu
muwekeze nyumbani” alisema Mwambe.
Mwambe
aliwataka wakazi hao kushirikiana na kuongeza nguvu katika kutangaza fursa na
vivutio vya utalii vilivyopo katika Wilaya hiyo ambayo imebarikiwa kuwa na hali
nzuri ya hewa ya kuweza kuzalisha mazao mbalimbali ya chakula na biashara.
“Ndugu
zangu uwekezaji unawezekana sana Makete, mna ardhi yenye rutuba,mna hali nzuri
ya hewa, umoja wenu ni bora zaidi kuliko utengano, nawaomba sana muungane na muanzishe
Mfuko na Kampuni ya Wanamakete vitakayokuwa na malengo ya kuiletea maendeleo Wilaya
ya yenu”alisema Mwambe.
Aidha
aliongeza Wilaya hiyo inao uwezo mkubwa wa kuzalisha ngano lakini bidhaa hiyo
kwa asilimia kubwa inaagizwa kutoka nje ya nchi na kuwataka ikutafakari hilo
ili kuzalisha ngano kwa wingi.
Kaimu
Mkuu wa Wilaya ya Makete, Bw. Burton Sinene
alisema kwa sasa Wilaya hiyo inahitaji wawekezaji katika kiwanda cha kutengeneza
njiti za meno (bamboo toothpick) kutokana na kuwepo kwa zao la mianzi, bidhaa ambayo kwa kiwango kikubwa inaagizwa nje
ya nchi kwa ajili ya matumizi ya mezani wakati wa kula.
Katika
majadiliano ya kikao hicho wakazi hao waliiomba Serikali izidi kuimarisha
miundombinu ya barabara ili kuweza kusafirisha mazao toka mashambani kwenda
kwenye masoko mbalimbali, suala ambalo pia litawavutia wawekezaji wengi zaidi.
No comments:
Post a Comment