Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango akijadiliana jambo na Mkurugenzi Mkuu wa UTT AMIS, Simon Migangala.
Na. Mwandishi Wetu
WATANZANIA wengi wanatafuta mafanikio maishani mwao lakini
bila kuwa na bidii, ustahimilivu, nidhamu na shauku kubwa, huwezi kupata
mafanikio ya kweli.
Kuna mbinu mbalimbali ambazo kila mwananchi anayetafuta
mafanikio anaweza kuzitumia ili kufikisha lengo alilonalo.
Jambo la kwanza ni kujua unataka nini, ukijua unachotaka
utakuwa na msimamo wa kutaka kufikia malengo yako.
Kama hujui unachotaka, jambo la msingi, chukua kalamu na
karatasi kisha jiulize unataka kufanikiwa kitu gani?
Ni muhimu wakati unajiuliza, usifikirie mawazo hasi au
mabaya ya kujiona kama utashindwa kufanikiwa bali kiajimi.
Ondoa wasiwasi wowote ambao utakuwa nao, orodhesha mambo
yote unayotaka kufanikiwa, anza kupanga mipango kwa kujiwekea malengo,
kutekeleza moja baada ya jingine.
Utajiri siyo fedha ambazo mtu anakusanya bali ni fedha
ambazo huwekwa na kufanya kazi.
Tamaduni zetu zimeifanya jamii kubwa kuhifadhi fedha ndani
kwenye vyungu, magodoro hata vibubu. Njia hizo zimekuwa zikibadilika taratibu
sawa na ukuaji wa elimu na teknolojia.
Uwekaji akiba na uwekezaji ni dhana mbili tofauti. Uwekaji
akiba ni tabia nzuri lakini bila kuziwekeza ni bure.
Ili uwe muwekaji akiba mzuri, unapaswa kuwa na nidhamu ya
hali ya juu kwani uwekezaji una uwiano mkubwa na muda. Muda unapozidi kuwa
mrefu na uwekezaji wako unazidi kukuwa mkubwa. Mara zote pesa ndani ya
uwekezaji UTT AMIS zinawekezwa katika mpango wa faida jumusihi ambapo muda huwa
ni jambo la msingi kabisa.
UTT AMIS ni taasisi ya Serikali ambayo imepewa dhamana ya
usimamizi wa mali kupitia Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja.
Nchini Tanzania unaweza kuwekeza fedha zako katika masoko ya
fedha, mitaji. Hatua hiyo inahusisha akaunti za muda maalum na zisizo za muda
maalum katika benki za biashara.
Pia hati fungani za Serikali za muda mfupi, mrefu, kampuni
na hisa zilizo orodheswa katika Soko la Hisa Dar es Salaam (DSE) ambazo zina
nafasi kubwa ya kurejesha gawio zuri.
Uwekezaji unaofanywa na taasisi hiyo kupitia mifuko ambayo
wanaisimamia ni fursa mbadala inayowezasha mtu, watu, vikundi, taasisi, kampuni
kuwekeza pesa zao kwa Meneja wa UTT.
Meneja wa mfuko huzichukua fedha hizo, kuziwekeza kwenye
masoko ya fedha na mitaji kulingana na waraka wa makubaliano. Waraka wa
makubaliano ni maandiko ya kisheria yanayo zungumzia haki za pande zote mbili
meneja na mwekezaji pia huanisha sehemu za kuwekeza na uwiano wa kuwekeza.
Faida inayopatikana hugawanywa kwa wawekezaji kulingana na
uwiano wa uwekezaji uliofanyika kwenye mfuko husika. Awali UTT ilipewa dhamana
ya usimamizi wa mifuko mitano.
Mifuko hiyo ni Mfuko wa Umoja, Wekeza Maisha, Watoto, Mfuko
wa Kujikimu na Mfuko wa Ukwasi. Hivi sasa taasisi hiyo imeongeza mfuko mwingine
wa Hati Fungani.
Mfuko wa Umoja, ulioanzishwa Mei 16, 2005 ukilenga kutimiza
mahitaji tofauti ya wawekezaji. Awali bei ya kipande ilikuwa sh. 70, kwa sasa
sh. 582.
Sifa zilizopo katika mfuko huo ni vipande kuuzwa kwa thamani
halisi (hakuna gharama za kujiunga). kiwango cha chini cha kujiunga ni vipande
10 tu, malipo ya mauzo hutozwa asilimia moja ya thamani halisi, pia ni rahisi
kujiunga na kutoka, manunuzi na mauzo hufanyika kila siku ya
kazi.
Mfuko wa Watoto una lengo la kuwasaidia watoto katika
maendeleo yao nchini. Awali bei ya kipande ilikuwa sh. 100, mfuko ulianzishwa
Oktoba 1, 2008.
Na kwa sasa thamani
ya kipande katika mfuko wa watoto ni shilingi 348 Sifa za mfuko huo ni
uwekezaji kwa ajili ya mtoto mwenye umri chini ya miaka 18. Kiwango cha chini
cha uwekezaji sh. 10,000, unaruhusiwa kuwekeza kidogo kidogo kwa sh. 5,000.
Sifa nyingine ni vipande kuuzwa kwa thamani halisi (hakuna
gharama za kujiunga), mfuko hutoa mipango ya aina mbili, kwanza malipo ya ada,
pili mpango wa kukuza mtaji.
Malipo ya ada na mauzo ya vipande yanaruhusiwa pale mtoto
anapofikisha miaka 12. Mfuko huo ni miongoni mwa mifuko inayotatua changamoto za kielimu hasa katika
ulipaji ada kwa wanafunzi, kutoa mtaji baada ya ukomo wa shule kufikia.
Pia mfuko una mipango miwili mikubwa, mpango wa ada za shule
na mtaji kwa mwanao. Ili mzazi aweze kuchangia kupitia mfuko huo, anapaswa
kuweka sh. 10,000 kima cha chini na hakuna ukomo kwenye kiwango cha juu.
Mwekezaji anaweza kuwekeza mara kwa mara kadri anaweza.
Mfuko wa Jikimu una lengo la kukidhi mahitaji ya wawekezaji
wanaohitaji uhakika wa mapato ya mara kwa mara, ulianzishwa Novemba 3, 2008 ukiwa na sifa za mipango ya
uwekezaji, kiwango cha uwekezaji, mpango wa gawio robo mwaka.
Kiwango cha chini kuwekeza
ili kupata gawio mara nne kwa mwaka yaani kila robo mwaka ni
shilingi milioni 2. Mpango wa gawio wa
mwaka (kiwango cha chini cha uwekezaji sh. milioni moja), tatu mpango wa mwaka
wa kukua (sh. 5,000).Vipande vinauzwa kwa thamani halisi (hakuna gharama za
kujiunga).
Mfuko wa Ukwasi unaotoa nafasi ya uwekezaji mbadala kwa
wawekezaji wakubwa au taasisi ambao wangependa kuwekeza fedha zao za ziada kwa
kipindi kifupi ama cha kati huku wakikuza mtaji wao.
Ulianzishwa Aprili 30, 2013, bei ya kipande ikiwa sh.
100.00, hivi sasa imepanda hadi zaidi ya sh. 219 hii ikiwa ina maana ya kuwa
mfuko umekua mara 2.19 ndani ya miaka mitano au umekuwa kwa asilimia 119 huu ni
ukuwaji mzuri sana kibiashara. Sifa za
mfuko huo ni rahisi mwekezaji kupata fedha zake za mauzo ya vipande ndani ya
siku tatu za kazi baada ya maombi ya kuuza vipande kupokelewa Makao Makuu ya
UTT AMIS.
Mfuko huo hauna ada ya kujitoa wala kujiunga, una unafuu wa
gharama za uwekezaji, unafaa kwa wawekezaji mmoja mmoja au taasisi, kiwago cha
chini cha kuwekeza sh. 5,000,000.00.
Kuongeza uwekezaji wako sh. 1,000,000.00, pia unaruhusu
uhamishaji vipande kutoka kwa mwekezaji mmoja kwenda mwingine, kuruhuusu
uhamishaji vipande kwenda kwenye mifuko mingine, kuviuza kwa thamani halisi.
Mfuko wa Wekeza Maisha unamwezesha mwekezaji kupata faida
pacha (mapato mazuri pamoja na mafao ya bima).
Mfuko huo ulianzishwa Mei 16,2007, wawekezaji kati ya miaka
18 na 55 ndio wanaoruhusiwa kujiunga. Unatoa mipango ya aina mbili, kuchangia
uwekezaji awamu ya kwanza, mkupuo mmoja.
Vipande vinauzwa kwa thamani halisi, hakuna gharama za
kujiunga. Kujiunga ni sh. 8,340.00 tu kwa mwezi. Mafao ya bima yanayopatikana
ni bima ya maisha, ulemavu wa kudumu na bima ya ajali.
Mfuko unamwezesha mwekezaji kuwekeza kwa mpangilio,
kuchangia kwa mwezi, mara mbili kwa mwaka, mara moja kwa mwaka ambapo faida za
uwekezaji katika Mifukoya Uwekezaji wa Pamoja ni kukuza mtaji kwa kutoa faida
nzuri ukilinganisha na mifuko mingine kwenye masoko ya fedha.
Faida nyingine ni kutawanya hatari za uwekezaji, mwekezaji
hupunguza athari za uwekezaji kwa kuwekeza katika uwekezaji anuai, wawekezaji
kufaidika na unafuu wa gharama za uwekezaji.
Pia wawekezaji wanaweza kufuatilia maendeleo ya masoko ya
fedha kwa kufuatilia maendeleo ya mifuko.
Mfuko mpya Hati Fungani unaojulikana kama ‘Bond Fund’ ni
kati ya mifuko ya uwekezaji wa pamoja inayoendeshwa na UTT AMIS ulioanzishwa
kwa malengo maalum.
Malengo hayo ni kubuni, kuendeleza, kuanzisha na kusimamia
Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja, kuwekeza, kununua, kumiliki na kuuza dhamana,
kutimiza malengo, wajibu, haki na sheria.
Mengine ni kutoa huduma za usimamizi wa fedha kwa kampuni na
wawekezaji binafsi, kutoa ushauri wa uwekezaji kwa taasisi na watu binafsi,
kutunza taarifa za wawekezaji wa mifuko na kuhamasisha wananchi kujiwekea
akiba.
Kuanzishwa kwa Mfuko wa Hati Fungani kumetokana na mahitaji
ya wawekezaji na uchambuzi wa bidhaa za kifedha zilizoko kwenye soko la mitaji
kwa sasa.
Mfuko utawawezesha wawekezaji wadogo na wa kati kuzifikia
fursa za uwekezaji ambazo kwa hali ya kawaida ni wawekezaji wachache na wakubwa
ndio wanaozifikia.
Pia utawekeza kwenye hati fungani zilizoorodheshwa kwenye
soko la hisa kwa asilimia 90 na asilimia 10 itakuwa kwenye uwekezaji wenye
ukwasi mkubwa.
Lengo ni kuwawezesha wawekezaji wanaohitaji kuchukua fedha
kutokana na uwekezaji wao katika mfuko wafanye hivyo.
Mfuko umeundwa ili kumwezesha kila mwekezaji kuchagua kama
anapenda kukuza mtaji au kupokea gawio kwa mwezi, kila miezi sita kutokana na
mahitaji yake ya kifedha.
Sheria ya Masoko ya Mitaji inataka Mifuko ya Uwekezaji wa Pamoja kuwa na
Meneja, Mdhamini, Wakaguzi wa Mahesabu, Wanasheria na Msajili.
Mfuko huo
utasimamiwa na UTT AMIS kama Meneja na Benki ya CRDB kama Mdhamini. Utakaguliwa
na KPMG ambayo ni taasisi ya kimataifa ya ukaguzi wa mahesabu ya fedha.
Wanasheria watakuwa
Kampuni ya Abenry and Company ambao wana uzoefu mkubwa katika mifuko ya
uwekezaji wa pamoja na Msajili atakuwa UTT AMIS.
Akiuzungumzia
mfuko huo, Mkuu wa Masoko na Uhusiano wa UTT AMIS, Daudi Mbaga, alisema umelenga kuondoa changamoto ambazo wawekezaji
wanakutana nazo.
Anasema soko la fedha lina bidhaa nyingi zilizobuniwa ili
kukidhi mahitaji tofauti ya watumiaji.
Baadhi ya bidhaa hizo zinaeleweka kirahisi hata namna ya
kuzifikia na kuwekeza lakijni wakati mwingine hazitoi faida shindani kwa wawekezaji.
Anasema baadhi ya wawekezaji hasa wadogo ni vigumu kuwekeza
kwenye baadhi ya bidhaa katika soko la fedha. Mfuko wa Hati Fungani umeratibiwa
ili kuondoa changamoto hizo.
Mwekezaji anapata faida sawa na wawekezaji wakubwa,
akihitaji fedha anauza baadhi ya umiliki wake kwenye mfuko kwa utaratibu rahisi
bila kupoteza faida aliyoipata.
Pia mfuko huo unawafaa wawekezaji wakubwa kwa sababu ya
faida shindani, gharama ndogo za kuwekeza, ukwasi wa kutosha, usalama wa mtaji,
hatari ndogo za uwekezaji.
Mfuko unatoa fursa kwa wawekezaji kuwekeza, kushiriki katika
masoko ya mitaji, kufaidika na uwekezaji huo.
Kwa mantiki hiyo, mfuko umeandaliwa ili kutoa fursa kwa
wawekezaji wa kipato cha chini, kati na kipato cha juu ambapo watu binafsi,
kampuni, taasisi na vikundi rasmi wanaweza kushiriki katika uwekezaji kwenye
mfuko huo.
Lengo kuu la mfuko ni kuwawezesha wawekezaji katika ushiriki
mpana kupitia uwekezaji wa vipande na kuhamasisha utamaduni wa kuweka akiba
kupitia hati fungani, masoko ya fedha.
Mfuko huo hutoa fursa ya uwekezaji rahisi wa muda mrefu kwa
wawekezaji ambao wangependa kuwekeza ili kukuza mtaji wao, kupata gawio kila
mwezi au kila baada ya miezi sita kama mwekezaji anavyohitaji.
Mbaga anasema, mfuko una mipango miwili ya uwekezaji ili
kukidhi matakwa tofauti ya wawekezaji. Kuna mpango wa kukuza mtaji, gawio kila
mwezi na gawio kila miezi sita, mpango wa kukuza mtaji.
Gawio la mara
kwa mara halitatolewa kwa wawekezaji badala yake faida iliyopatikana itarudishwa
kwenye uwekezaji wa awali kwa kununua vipande vitakavyonunuliwa kwa bei ya
wakati huo.
Mpango huo utawafaa wawekezaji wanaohitaji kuweka akiba kwa
malengo maalum mfano kujenga nyumba au wafanyakazi wenye kipato kama wangependa
kuwa na fedha ya akiba.
Wawekezaji katika mpango huo wanaweza kuuza kiasi chochote
cha uwekezaji wakiwa wamekidhi vigezo vinavyohusu uuzwaji wa vipande.
Wawekezaji
wanaohitaji kuchukua faida kila mwezi kama wastaafu wanaopata fedha zao za mkupuo,
kuwekeza kwenye mfuko, wanashauriwa kuchagua kupokea gawio kila mwezi ili
wapate kipato cha kuishi bila kupoteza fedha walizopata.
Mbaga anasema wawekezaji wengine wanaopata fedha nyingi mara
moja mfano wachimba madini, wanaweza kuchagua gawio kila mwezi ili wafanye
shughuli zao bila kuathiri mtaji wao.
Pia wawekezaji watakao jiunga na mpango huo wanaweza kuuza
vipande kidogo au vyote ili mradi wawe wamekidhi vigezo vya mfuko vinavyohusu
uuzwaji vipande.
Mpango wa gawio kila miezi sita, Mbaga alisema hutegemea na mahitaji ya fedha
ya mwekezaji na anavyochagua kwenye fomu ya maombi ya kuwekeza kwenye
mfuko.
Kwa wawekezaji ambao wanahitaji kuchukua faida kila miezi
sita mfano wafanyakazi wanaohitaji kuweka kiasi cha fedha ili faida
inayopatikana itumike kulipa ada kusomesha watoto, wanaweza kuchagua kupokea
gawio kila miezi sita.
Pia kuna wawekezaji wanaopata fedha nyingi mara moja kama
wakulima wa mazao mbalimbali ya msimu, wanaweza kuchagua kupata gawio kila
miezi sita.
Lengo ni kupata fedha wakati wa kutayarisha, kulima mashamba
na wakati wa kuvuna ili waweze kuendesha shughuli zao kwa kufuata msimu bila
kupoteza mtaji walio nao. Pia hawa wanahitaji pesa wakati wote huku kilimo
kikiwa ni cha msimu mpka msimu. Wakati wanasubiri msimu mpya wana chukuwa pesa
za kwa mwezi ili kukidhi mahitaji ya kila siku.
Wawekezaji watakao kujitoa kutoka mpango huo wanaweza kuuza vipande kidogo au
vipande vyote ili mradi wawe wamekidhi vigezo vya mfuko.
Akizungumzia sera ya uwekezaji, Mbaga
anasema muundo wa mgawanyo katika mfuko wa Hati Fungani unatoa mapato ya
muda mrefu ikijumuisha hati fungani zinazotolewa na Serikali.
Uwekezaji kwenye hati fungani ili mfuko uwe na mapato ya
kudumu utakuwa si chini ya asilimia 90 ya thamani ya mfuko, asilimia 10
itawekezwa kwenye rasilimali zenye ukwasi ili wawekezaji wanaohitaji kuchukua
fedha wafanye hivyo.
Meneja atawekeza kwenye rasilimali zenye ukwasi ili
kuhakikisha uwezo wa kulipa wawekezaji pale fedha zao zitakapohitajika unakuwa
imara.
Mbaga anasema wawekezaji wote wa ndani, nje ya
Tanzania kama Sheria ya Soko la Mitaji na Dhamana inavyoruhusu wanaweza
kuwekeza kwenye mfuko huo.
Kuhusu ununuzi wa
vipande, alisema vinanunuliwa siku yoyote ya kazi isipokuwa kipindi cha
kufunga vitabu ambacho hakitazidi siku saba za kazi.
Kuanzia Septemba 16 hadi Oktoba 16, mwaka huu itakuwa
kipindi cha mauzo ya awali hivyo Watanzania wachangamkea fursa hiyo kwani
kiwango cha chini kitakuwa sh. 50,000 na thamani halisi ya kipande itakuwa sh.
100.
Maombi ya kununua vipande yanaweza kuwakilishwa katika tawi
lolote la Benki ya CRDB, ofisi za madalali waliosajiliwa wa Soko la Hisa la Dar
es Salaam; Ofisi za Shirika la Posta; Wakala yoyote atakayeteuliwa na UTT AMIS.
Wawekezaji walio nje ya Tanzania anayetaka kuwekeza katika
mfuko huo awasiliane na ofisi za madalali waliosajiliwa wa Soko la Hisa la Dar
es Salaam au kuwasiliana moja kwa moja na Ofisi za UTT AMIS ili kupata taarifa
na muongozo zaidi.
Anaongeza kuwa, thamani ya mwanzo ya kipande itakuwa
sh. 100. Thamani ya kuuza na kununua
kipande itakuwa sawa na thamani halisi ya kipande bila gharama yoyote.
Kiwango cha chini kitakuwa sh. 50,000, hakuna ukomo kwenye
kiwango cha juu ambapo hiyo ni fursa kwa kila Mtanzania.
Baada ya muda wa mauzo ya awali, mwekezaji anaweza kuwekeza
kuanzia sh. 5,000, mara nyingi kadri awezavyo.
Malipo ya mauzo ya
vipande yanaweza kufanywa kwa fedha taslimu au hundi ya benki itakayolipwa
kwenye akaunti ya ‘Mfuko wa Hati Fungani’ iliyopo Benki ya CRDB.
Wawekezaji wanaweza
kwenda kwenye tawi lolote la Benki ya CRDB na kufanya malipo. Pia malipo yanaweza
kufanyika kwa kupitia M-Pesa, Tigo Pesa, Airtel Money.
Kiwango
cha chini cha uwekezaji wakati wa mauzo ya mwanzo kwa Mpango wa Kukuza Mtaji ni
vipande 500. Kwa kuwa thamani ya mwanzo ya kipande ni sh. 100, thamani ya chini
ya vipande katika mauzo itakuwa sh. 50,000.
Unaposema Mfuko wa Kukuza Mtaji maana yake mwekezaji atakuwa
anawekeza mara kwa mara kwa malengo Fulani ili kutimiza azima fulani huko
mbele. Na kila anacho wekeza kitakuwa kinakuwa kutokana na mwenendo wa soko
Kuhusu mpango wa gawio kila mwezi, kiwango cha chini cha
uwekezaji wakati wa mauzo ya mwanzo kwa mpango wa gawio kila mwezi ni vipande
100,000. Kwa kuwa thamani ya mwanzo ya kipande ni sh. 100, thamani ya chini ya
vipande katika mauzo itakuwa sh. 10,000,000.
Mpango wa gawio kila miezi sita, kiwango cha chini cha uwekezaji wakati wa mauzo ya mwanzo kwa
mpango wa gawio kila miezi sita ni vipande 50,000. Kwa kuwa thamani ya mwanzo
ya kipande ni sh. 100, thamani ya chini ya vipande katika mauzo itakuwa sh.
5,000,000. Kuhusu ununuzi na mauzo ya baadaye yatakayoanza Oktoba Mosi, mwaka huu, idadi ya chini ya vipande inayoweza
kuuzwa ni vipande vyenye thamani ya sh. 5,000, vitaonekana katika mgawanyo wa
desimali nne.
Maombi ya mauzo, manunuzi ya vipande yatapokelewa na
kukubalika siku za kazi tu.
Mauzo ya vipande yatafanyiwa kazi baada ya kupokelewa kwa
fomu ya kuuza vipande ambayo itakuwa imeambatanishwa na taarifa ya akaunti,
nakala ya kitambulisho, kielelezo kingine kitakachohitajika na Meneja wa Mfuko.
Malipo ya mauzo ya vipande kwenda kwa mwekezaji yatafanyika
kwa njia ya benki au kupitia Shirika la Posta ndani ya siku 10 za kazi tangu
kupokelewa maombi yaliyo kamili.
Lazima mwekezaji ajaze fomu ya maombi ya kujiunga ili aweze
kununua vipande na kuwekeza, fomu hiyo ipelekwe kwa wakala yeyote aliyeteuliwa
na Meneja wa Mfuko.
MWISHO.
CAPTION:
PICHA 1
Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Mpango akijadiliana
jambo na Mkurugenzi Mkuu wa UTT AMIS, Simon Migangala.
PICHA 2
Rais Dkt.
John Magufuli Aakimkagua samaki na kumnunua kwa mfanyabiashara wa soko la
Samaki Feri, jijini Dar es Salaam alipofany ziara ya kutembelea wafanyabiashara
wadogo wanaotumia vitambulisho vya wajasiriamali ambao wanaweza kukuza mtaji
wao kupitia uwekezaji kwenye Mfuko wa Hati Fungani.
No comments:
Post a Comment