Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Shein Afungua Kongamano na Mkutano Mkuu wa 10 wa Jumuiya ya Wapathollojia Tanzania .

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuwekeza kwa nguvu zake zote katika kuiendeleza fani ya patholojia kwa ajili ya maendeleo ya afya hapa nchini hasa ikitambua kwamba afya ndio mtaji wa maisha ya mwanaadamu.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo huko katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil, mjini Zanzibar wakati alipofungua mkutano wa 10 wa Jumuiya ya Wapatholojia wa Tanzania (APT), ambalo mwaka huu linafanyika hapa Zanzibar.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kwamba tayari Serikali imewapeleka masomoni madaktari saba kujifunza maeneo mbali mbali ya fani hiyo ambapo wanne wapo nchini Misri, mmoja yupo nchini India, mmoja nchini Cuba na wengine wawili wapo Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili nchini Tanzania.

Aliongeza kuwa juhudi za makusudi zitachukuliwa na Serikali anayoiongoza katika kuhakikisha angalau Wapatholojia 15 wanarudi ama wanaendelea na masomo pale atakapomaliza muda wake wa uongozi.

Rais Dk. Shein ambaye pia, ni mlezi wa Wanapatholojia Tanzania alisema kuwa huduma za uchunguzi wa maradhi mbali mbali zimeimarika katika hospitali ya Mnazi Mmoja ambapo wananchi hivi sasa wanaweza kupatiwa huduma zote muhimu za uchunguzi wa maradhi katika maabara ya Patholojia bila malipo.

Katika jitihada za kupiga vita maradhi ya kuambukiza na yale yasio ya kuambukiza, Serikali ya Mapinduzi Zanzibar imekuwa ikiongeza bajeti ya kila mwaka kwa ajili ya ununuzi wa dawa na nyenzo za utibabu.

Alisema kuwa kima cha fedha kilichotengewa sekta ya afya kimepanda kutoka TZS bilioni 7 mwaka 2017/2018 hadi kufikia bilioni 12.7 mwaka 2018/2019 na kwa mwaka huu wa 2019/2020 kiwango hicho kimefikia TZS 15.7 ambacho ni sawa na ongezeko la asilimia 124.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilizindua mradi wa uchunguzi wa saratani ya mlango wa kizazi katika mwezi wa Disemba 2018 ambapo mradi huo ni wa miaka mine ambapo unaendeshwa kwa mashirikiano baina ya Jamhuri ya Watu wa China na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kuwa huduma za kisasa za kutumia mionzi katika kuchunguza maradhi mwilini zinapatikana wakati wote kwenye hospitali ya Mnazi Mmoja ambapo tangu zilizofungwa mashine za CT Scan mwaka 2009 pamoja na mashine ya MRI na  mashine 3 za X-ray zinazotumia mfumo wa dijitali zilizofungwa mwaka 2019.

Alieleza kuwa huduma hizo zinazopatikana katika hospitali ya Mnazi Mmoja na hospitali ya Abdalla Mzee Mkoani Pemba zinatolewa bure.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza haja ya kufanya kazi kwa pamoja kati ya Wizara ya Afya ya Zanzibar na Hospitali ya Muhimbili hasa katika maradhi ya uchunguzi na kueleza umhimu wa kushughulikia masuala ya uchunguzi wa maradhi ili kuwatibu wananchi hapa hapa nchini.

Kwa upande wa ugonjwa wa Ebola Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali zote mbili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ziafanya jitihada kubwa kuzuia ugonjwa huo usiingie nchini.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa madaktari bingwa wastaafu wakiwemo wa patholoji wasiharakishwe kustaafu na badala yake waandaliwe mazingira mazuri ili waendelee kutoa huduma kwa jamii.

Aidha, alieleza umuhimu wa kuwaandaa vijana kusoma masomo ya patholojia ili waje kuziba pengo la wataalamu ambao watastaafu kabisa kutoa huduma hizo.

Sambamba na hayo, alieleza kuwa kwa upande wa Zanzibar, jitihada za kukuza maendeleo ya janmii katika sekta ya afya zinakwenda sambamba na matakwa ya Kanuni za afya za Kimataifa pamoja na Ajenda ya Usalama wa Afya Ulimwenguni.

Rais Dk. Shein aliwapongeza Wapatholojia hao kwa uwamuzi wao wa kuja kufanya mkutano wao hapa Zanzibar na kuahidi kushirikiana nao huku akitumia fursa hiyo kuwakaribisha kuitembelea Zanzibar wakati wowote.

Nae Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed alimpongeza Dk. Shein ambaye ni mmoja miongoni mwa waanzilishi wa Jumuiya hiyo katika mwaka 1991 na muwasisi wa Wapatholojia  na kumuelezea kuwa ana ubinaadamu wa hali ya juu.

Alisema kuwa tokea Dk. Shein aingie madarakani hali ya Amani na utulivu imeendelea kuwepo hapa nchini hali ambayo imeweza kwuavutia watu mbali mbali wakiwemo Wanapatholojia hao ambao wameamua kuja kufanya mkutano wao hapa Zanzibar.

Alimpongeza Dk. Shein kwa kusimamia Sera ya mwaka 1964 chini ya chama cha Afro Shirazi Party (ASP), ya kuhakikisha huduma za afya zinatolewa bure huku akitumia fursa hiyo kueleza jinsi uchumi wa Zanzibar unavyoimarika.

Mapema, Mwenyekiti wa Wapatholojia Tanzania Dk. Charles Massambura akitoa usalamu zake alitoa pongezi wka Rais Dk. Shein kwa kuimarisha sekta ya afya hapa nchini ikiwa ni pamoja na kuhakikisha maabara ya Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja inapandishwa hadhi katika masuala mazima ya uchunguzi.

Rais wa Chama cha Madaktari Tanzania Dk. Elisha Osati alitoa pongezi kwa Serikali zote mbili kwa kuendeleza sekta ya afya na kusisitiza haja ya kuwaendeleza madaktari na kuwaenzi huku akiwataka madaktari kukumbushana katika kutelekeza majukumu yao ya kazi.

Profesa Eligius Lyamuya akiwasilisha mada kuu katika hafla hiyo alieleza umuhimu wa wapathojia katika kutambua maradhi kadhaa kwa binaadamu, wanyama na mimea pamoja na uchunguzi wa visababishi vya magonjwa mbali mbali.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822  

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.