Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.,Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Uongozi wa Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza dhamira ya Serikali katika kulipa kipaumbele suala la kufanya utafiti, kuwa inalenga kuzitafutia majibu na ufumbuzi changamoto mbali mbali zinazojitokeza katika Wizara za Serikali.

Dk. Shein amesema hayo Ikulu mjini Zanzibar, wakati akipokea taarifa ya Utekelezaji wa Mpango kazi kwa Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais kwa mwaka 2018/2019.

Alisema ni muhimu kwa Idara na taasisi zote za serikali kufanya utafiti, badala ya jukumu hilo kuiachia Idara ya Mipango, Sera na Utafiti pekee.

Alisema katika kufanikisha jambo hilo, Idara zinaweza kuwatumia wataalamu wake na pale wanapokosekana, ni vyema ikatowa mafunzo kwa wafanyakazi wenye elimu ya kutosha, ili hatimae waweze kutumika kwa kazi hiyo, na kubainisha kuwa baadhi ya tafiti hazihitaji fedha nyingi.

Aliwataka viongozi wa Idara za Serikali kujenga mapenzi ya kufanya tafiti, sambamba na kujenga uwezo wa kitaaluma ili waweze kutekeleza shughuli hizo kwa ufanisi.

Aidha, aliitaka Wizara kupitia Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya kitaifa kuwasilisha waraka Serikalini, ili kupata muafaka baada ya kubainika kuwepo kwa  baadhi ya Wizara zilizonunua vifaa mbali mbali vya sherehe, ikiwemo mashamiana  kwa lengo la kuvikodisha , jambo ambalo kimsingi linapaswa kufanywa na Idara hiyo.

Akigusia mchakato wa serikali kuihamishia mjini Dodoma Idara ya Uratibu wa shughuli za Serikali iliopo Dar es Salaam, Dk. Shein alisema eneo la ardhi la ekari 30 ililopatiwa serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania ni kubwa, hivyo akasisitiza azma ya Serikali ya kuihamishia Ofisi hiyo Dodoma, mara baada ya hatua ya ujenzi kukamilika.

Alisema eneo hilo linapaswa kutumika vizuri kwa  kuwepo mipango mizuri ya ujenzi , kuambatana na maelekezo ya Mainjinia, pamoja na kutoa indhari ya kuhakikisha ardhi hiyo inabaki salama.

Aidha, Dk. Shein alieleza kuwa Serikali kupitia vyombo vyake vya Ulinzi na Usalama imejipanga vyema na vimekuwa vikifanya juhudi kubwa  kukabiliana na uingizaji wa dawa za kulevya,hivyo akabainisha umuhimu wa kuzifanyia kazi taarifa za uhalifu katika maeneo yote, ikiwemo baharini.

Katika hatua nyengine, Dk Shein aliwakumbusha watendaji wa Ofisi hiyo, kuwa  Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais kama ilivyo Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, zinahitaji wafanyakazi wanaoheshimika na  kufanya kazi zao kwa misingi nidhamu, weledi na uwajibikaji.

Alisisistiza haja ya watendaji hao kuondokana na hali ya kufanyakazi kwa mazoweya, ili kuweza kupata ufanisi katika malengo wanayojiwekea.

Aidha, alisema utaratibu wa Bango kitita ni wa kilimwengu, akibainisha uzuri wake, kwa misingi kuwa unawawezesha wafanyakazi kujitathmin kutokana na utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema miongoni mwa mambo yanayoleta ufanisi katika kazi ni pamoaj na  kuwepo kwa maeneo na ofisi nzuri za kufanyia kazi, jambo ambalo Serikali imekuwa ikiendelea na juhudi za kuimarisha.

Dk. Shein aliwapongeza watendaji wa Ofisi hiyo kwa juhudi kubwa wanayofanya katika utekelezaji wa majukumu yao pamoja  kazi nzuri waliyofanya katika uwasilishaji wa mpango kazi kwa mwaka 2018/2019.

Nae, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, aliwataka watendaji wa Ofisi hiyo kujifunza na kutekeleza kwa ufanisi yale yote walioelekezwa, kuambatana na shabaha na malengo waliyojipangia.

Aliwataka watendaji hao kuendelea na mshikamano wao na kufanya kazi kwa pamoja, akibainisha kuwa ndio siri ya mafanikio waliyoyapata, mbali na baadhi nyakati kukabiliana na matatizo mbali mbali.

Mapema, akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji wa Mpango kazi  Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, Waziri wa Wizara hiyo Mohamed Aboud, alisema  Ofisi hiyo imepata mafanikio makubwa katika kipijndi hicho, ikiwemo kuratibu ujenzi wa nyumba ya makaazi ya Makamu wa Pili wa Rais unaoendelea kufanyika katika eneo la Pagali, kisiwani Pemba,

Alisema ujenzi huo unafanyika chini ya kikosi cha KMKM ambapo hadi kufikia sasa tayari umefikia asilimia 75 ya kazi.

Alisema Ofisi imefanikiwa kuratibu na kuendesha Uchaguzi mdogo wa Jimbo la Jang’ombe, sambamba na kuendelea kutoa elimu kwa wapiga kura kwa makundi mbali mbali ya kijamii, ikiwemo walimu na wanafunzi wa sekondari na vyuo vya elimu ya juu vilivyopo Zanzibar.

Aidha, alisema Tume ya Uchaguzi imefanikiwa kubadilisha mfumo wa Uandikishaji na kutengenza mfumo mpya kwa kutumia wataalamu wa ndani.

Alieleza kuwa ndani ya kipindi hicho, Wizara ilibeba dhima ya kuwaelimisha wafanyakazi, wanafunzi wa skuli za msingi na sekondari pamoja na  wananchi katika shehiya mbali mbali Unguja na Pemba juu ya athari ya matumizi ya dawa za kulevya.

Sambamba hilo, alisema Ofisi ilifanikiwa kuteketeza dawa za kulevya zilizokuwa maeneo ya uhifadhi wa kisheria, jambo ambalo kwa mara ya mwisho lilifanyika mnamo mwaka 2009.

Waziri Aboud, alieleza kuwa Ofisi ya Baraza la Wawakilishi  imeendelea na shughuli zake za kuratibu mikutano ya Baraza pamoja na kazi za Kamati za kudumu kwa ufanisi mkubwa.

“Jumla ya mikutano minne ilifanyika, ambapo kutokana na  mikutano hiyo jumla ya miswada mitano ya sheria ilijadiliwa na kupitishwa na Baraza”, alisema.

Alisema kazi za kamati za kudumu zilifanyika kupitia Wizara zote za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na mashirika yake.


Aidha, alisema Ofisi ilifanikiwa kuendeleza ujenzi wa Kituo cha Tiba na marekebisho ya tabia katika hatua ya tatu pamoja na kutoa  mafunzo katika masuala ya UKIMWI, afya ya uzazi na uzingatiaji wa masuala ya UKIMWI kwa watendaji wa vyuo vya Mafunzo na Asasi za kiraia.

Katika hatua nyengine, Waziri Aboud alisema Ofisi ilichukuwa hatua ya kulihami eneo la fukwe huko Msuka ili lisiendelee kumong’onyoka kutokana na maji ya bahari, kwa kuandaa utaratibu wa kujenga ukuta maalum utakaogharamiwa na Serikali ikiwa ni hatua ya muda.

Aidha, Ofisi iliwapatia mafunzo ya kazi na utaratibu wa maisha wafanyakazi wa Ofisi, ikiwemo mafunzo ya sheria na kanuni za Utumishi wa Umma, masuala ya Ukimwi na Homa ya Ini, rushwa na uhujumu uchumi, udhibiti na utunzaji wa kumbu kumbu  na siri za serikali, pamoja na mkataba wa Huduma za umma.

Waziri Aboud, alibainisha kuwa pamoja na mafanikio hayo pia kulijitokeza changamoto mbali mbali, ikiwemo upungufu wa gari katika baadhi ya Idara, ufinyu wa nafasi katika mamlaka ya Usimamizi wa Mazingira, Idara ya Mazingira pamoja na Tume ya Uchaguzi za Wilaya.

Nae, Katibu Mkuu Wizara ya Nchi, Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, Shaaban Seif Mohamed, alimpongeza Rais Dk. Shein kwa kuanzisha utaratibu wa kuwasilisha  Mpango kazi na kusema una faida kubwa katika utekelezaji wa malengo ya maendeleo ya Wizara za serikali.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.