Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Awazawadia Wanafunzi Bora wa Kidatu cha Sita na Nne Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein(katikati) akimzawadia Mwanafunzi Nasma Talib Saleh wa Skuli ya Sekondari ya SOS katika  hafla ya kuwapongeza  Wanafunzi  waliofaulu Mitihani ya Taifa ya kidato cha Nne na Sita pamoja  kuwaandalia chakula cha mchana katika hafla iliyofanyika leo  viwanja vya  Ikulu Mjini Zanzibar,(kulia) Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mhe.Riziki Pambe Juma


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein  ametangaza kuongeza nafasi 60 badala ya 30 alizozitoa mwaka jana za udhamini wa masomo kwa wanafunzi bora wa Kidato cha Sita wenye viwango vya juu kabisa vya ufaulu.

Hayo aliyasema leo katika hafla ya kuwapongeza wanafunzi bora wa Kidato cha Nne na cha Sita waliofanya vizuri katika mitihani ya Taifa, hafla ya kuwapa zawadi maalum pamoja na chakula cha mchana alichowaandalia wanafunzi hao huko katika viwanja vya Ikulu mjini Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kwamba idadi hiyo aliyoiongoza mwaka huu ni mara mbili ya nafasi za ufadhili wa masomo ambazo zlizitoa mwaka jana kwa wanafunzi bora wa Kidato cha Sita.

Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na utaratibu wa kuwapa udhamini wanafunzi bora wa Kidato cha Sita wenye viwango vya juu kabisa vya kufaulu kwa masomo ya sayansi na masomo ya sanaa.

Alifahamisha  kuwa mwaka huu ameongeza nafasi hadi kufikia 60 badala ya 30 za mwaka jana kwani aliahidi kuendeleza utaratibu huo ili kupata wataalamu wa fani mbali mbali watakaoendelea na masomo yao ndani na nje ya nchi.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa wanafunzi wote watakaopata fursa hio ya udhamini wa masomo na kuwasihi kuzitumia ipasavyo.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa wanafaunzi 187 waliofaulu kwa daraja la kwanza katika mtihani wa Kidato cha Nne mwaka jana pamoja na skuli bora kumi ambapo ufaulu wa mwaka jana ulikuwa ni wanafunzi 135.

Pongezi maalum alizitoa Rais Dk. Shein kwa kijana Hassan Ali Hamad wa Skuli ya Sekondari ya Lumumba kwa kupata pointi saba na kuwatangulia wenzake wanne kati ya vijana watano waliofanya vyema zaidi katika mitihani hiyo ya Kidato cha Nne mwaka 2018.

Kadhalika, aliwapongeza wanafunzi wote 188 wa Kidato cha Sita hasa vijana wanne waliofaulu kupata pointi nne kila mmoja na kuonesha uwezo mkubwa walionao zaidi ya wenzano.

Aliongeza kwua mwaka jana kwa Kidato cha Sita kwenye daraja la Kwanza walikuwa wanafunzi 126 ikiwa ni ongezeko la wanafunzi 62 sawa na ongezeko la asilimia 49.2 na kutoa pongezi maalum kwa Wahda Mbaraka Uzia kutoka Skuli ya Sekondari ya FEZA kwa kufanikiwa kuwa miongoni mwa wanafunzi bora wanawake kwa Tanzania kwa masomo ya Sayansi.

Alieleza kuwa kwa mara nyengine tena wanafunzi wa kike wameonesha uwezo wao mkubwa wa kufanya vyema katika mitihani ya Taifa na hasa kwa masomo ya Sayansi na kuwapongeza wanafunzi wa kike kwa kuonesha uwezo huo.

Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa hatua hiyo mbali na kuiletea sifa Zanzibar pia, ni mafanikio katika malengo ya Serikali ya kuimarisha elimu ya juu kwa watoto wa kike jambo ambalo hapo zamani halikuwa rahisi.

“Wazee walisema ‘Mcheza kwao, hutunzwa’ na ‘Chanda chema, huvikwa pete’. Kauli zote hizo za wazee wetu zinasibu kwenu. Kwa hivyo, tumeamua kuwaandalia hafla hii kwa ajili ya kukutunzeni, kwa sababu mmecheza vyema kwa ajili yenu na kwa ajili ya nchi yenu”,alisema Dk. Shein.

Aidha, alitoa pongezi kwa skuli za binafsi zilizopo Zanzibar ambazo zimeweza kuwakilisha vizuri kwa kutoa wanafunzi bora na kuzipongeza skuli zote zilizotoa wanafunzi wengi wa daraja la kwanza na hasa wale waliopata alama za juu kabisa.

Kadhalika Rais Dk. Shein alizipongeza skuli ambazo zimetoa wanafunzi japo si kwa idadi kubwa lakini na wao wameweza kupata wanafunzi waliofaulu kwa daraja la kwanza na hata la pili.  “Nafahamu matokeo haya hayaji kwa sadfa lakini yametokana na jitihada na mikakati mahsusi ya kufanya vizuri”,alisisiatiza Dk. Shein.

Kwa mnasaba huo Rais Dk. Shein aliwapongeza walimu, Kamati za Skuli na Wazazi kwa kuandaa mikakati bora ambayo imewezesha vijana kupata matokeo mazuri katika mitihani yao ya Taifa.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali pamoja na walimu wa skuli zote zilizowaandaa wanafunzi wao kwa ajili ya mitihani yao.

Pia, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa walimu kuendelea kuutekeleza kwa moyo thabit, uzalendo na huruma, wajibu wao huo na kutambua kuwa Serikali na wananchi wote kwa jumla wanathamini jitihada zao hizo.

Kadhalika aliwataka walimu  wasiozingatia  vyema majukumu yao na kuyakiuka maadili ya ualimu wajirekebishe kwani kazi hiyo ni ya  watu wenye heshima kubwa katika jamii.

Alieleza kuwa nidhahiri kwamba matokeo hayo yametokana na jitihada za pamoja na ushirikiano ambao siku zote huwa na matokeo mazuri na kutoa wito wa kuendeleza mikakati na kushirikiana ili mafanikio hayo yawe endelevu na isije ikaonekana ni matokeo ya bahati mbaya ama ‘nguvu za soda’.
Kwa kuzingatia umuhimu wa elimu kwa Taifa lolote, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar tangu Awamu ya Kwanza ya Uongozi imekuwa ikichukua jitihada mbali mbali katika kuimarisha sekta hiyo muhimu kwa maendeleo.

Alisema kuwa jitihada hizo zinahusisha uimarishaji wa elimu ya ngazi mbali mbali ikiwemo elimu ya Sekondari kama Mwasisi wa Mapinduzi Marehemu Mzee Abeid Amani Karume alivyosisitiza na kuhakikisha watoto wanapata fursa ya elimu hiyo ya  Sekondari kwa wingi zaidi jambo ambalo halikuwepo wakati wa ukoloni.

Alieleza kuwa azma hiyo imeendelezwa katika Awamu zote za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar hadi hivi sasa, katika Awamu hii ya Saba ya Uongozi wake.

Alisema kuwa Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya mwaka 2010-2015 ilipoanza Awamu ya Saba ya Uongozi ilielekeza Serikali baada ya kuundwa, kuimarisha elimu ngazi zote ikiwemo elimu ya Sekondari kwa kufanya mambo kadhaa yakiwemo kuongeza idadi ya skuli za Sekondari  Unguja na Pemba jambo ambalo limefanywa kwa mafanikio makubwa.

Rais Dk. Shein mbali ya kuwaandalia chakula hicho cha mchana wanafunzi hao pia, aliwapa zawadi maalum wanafunzi waliofanya vizuri zaidi kutoka Skuli zote za Zanzibar zikiwemo za Serikali na Binafsi.

Nae Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alieleza mafanikio yaliopatikana katika sekta ya elimu na kutumia fursa hiyo kutoa pongezi za pekee kwa rais Dk. Shein kwa juhudi zake za makusudi za kuimarisha sekta ya elimu hapa nchini.

Waziri Pembe alieleza kuwa Rais Dk. Shein anaendeleza nyayo za waasisi wa Taifa hili Marehemu Mzee Abeid Karume pamoja na Baba wa Taifa Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere za kuimarisha sekta ya elimu na kukuza sekta zote za maendeleo kwa watu wote.

Mapema Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dk. Idrisa Muslim Hijja alieleza kuwa mafanikio yote yaliopatikana katika sekta ya elimu ni juhudi za Rais Dk. Shein katika kuhakikisha anaweka mazingira bora katika sekta hiyo huku akitumia fursa hiyo kuwataja wanafunzi wote waliofanya vizuri.

Akitoa neno la shukurani Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  Issa Haji Ussi Gavu alitoa shukurani kwa Rais Dk. Shein kwa kuendelza utamaduni wake huo na kueleza kuwa fursa ya kupata elimu hivi sasa ni ya watu wote wa mjini na vijijini.

Huo ni utamaduni alioweka Rais Dk. Shein wa kila mwaka wa kuwaalika Ikulu wanafunzi wanaopata matokeo ya daraja la Kwanza katika mitihani ya Taifa ya Kidato cha Nnne na cha Sita kwa malengo maalum ambapo pia, Viongozi mbali mbali walihudhuria katika hafla hiyo akiwemo makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd na viongozi wengineo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.