Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Mhe. Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa akisaini hati ya makubaliano ya Ujenzji na Ukarabati wa Hospitali ya Wete Pemba na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo wa Abu Dhabi. Sheikh Mohammed Saif Ali Suwaid, hafla hiyo imefanyika katika Ofisi za Mfuko huo Abu Dhabi leo.
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Umoja wa
Falme za Kiarabu (UAE) kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi zimetiliana saini
Mkataba wa Makubaliano (MOU) juu ya ujenzi na matengenezo ya Hospitali ya Wete
Pemba.
Makubaliano hayo yataipelekea Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kupata Dola za Kimarekani Milioni 10 sawa na Shilingi za
Kitanzani Bilioni 23 kupitia Mfuko huo ambazo zitasaidia katika ujenzi na
matengenezo ya Hospitali hiyo ikiwewa ni pamoja na upanuzi wake.
Hafla hiyo ya utiliaji saini imefanyika katika
ofisi ya Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi mjini Abudhabi ambapo kwa upande wa
Zanzibar Waziri wa Fedha na Mipango Balozi Mohamed Ramia Abdiwawa alisaini kwa
niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi
Mohammed Saif Al Suwaid alisaini kwa niaba ya Serikali ya (UAE).
Mara baada ya utiliaji saini wa Mkataba huo
Waziri Abdiwawa alieleza kuwa, fedha hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa katika
kuimarisha sekta ya afya Zanzibar.
Alieleza kuwa kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar na wananchi wake wote wanatoa pongezi na shukurani za dhati kwa Umoja
wa Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) kwa juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono
Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya.
Balozi Ramia aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar inathamini sana juhudi hizo ambazo zimekuwa chachu katika
kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo baina ya pande mbili
hizo.
Aidha, Balozi Ramia alitumia fursa hiyo kutoa
shukurani za pekee kwa Sheikh Khalifa Bin Zayed Al Nahyan Rais wa Nchi za Umoja
huo kwa msaada wake huo na kueleza kuwa hatua hiyo inatoa taswira nzuri ya
mashirikiano yaliopo kati ya viongozi wa umoja huo na viongozi wa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wao.
Nae Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Maendeleo wa
Abudhabi, Mohammed Saif Al Suwaid alieleza kuwa Mfuko huo unajivunia kupata
fursa hiyo na kusisitiza kuwa Serikali ya Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu
utaendelea kuinga mkono Zanzibar.
Alieleza kuwa mradi wa ujenzi na matengenezo ya Hospitali
ya Wete ni mradi mkubwa kwani unawagusa moja kwa moja wananchi hivyo,
aliipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais Dk.
Shein kwa kuweka kipaumbele hicho hasa ikizingatiwa kuwa mradi huo ni muhimu
katika maisha ya wananchi.
Sambamba na hayo, Al Suwaid alieleza kuwa Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi utachukua juhudi na ari za makusudi
katika kahakikisha mradi huo unafanikiwa na unatekelezwa kwa muda uliopangwa.
Fedha hizo zilizotolewa na Serikali ya Umoja wa
Nchi za Falme za Kiarabu (UAE) kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Abudhabi zinatokana
na agizo maalum la Rais wa Umoja wa nchi hizo Sheikh Khalifa Bin Zayed Al
Nahyan katika kuhakikisha Serikali anayoiongoza inaiunga mkono Zanzibar katika
kuimarisha sekta ya afya.
Katika hafla hiyo baadhi
ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walishuhudia tukio hilo akiwemo Waziri Ofisi ya Rais na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Issa Ussi Haji Gavu, Waziri wa Ardhi, Maji,
Nishati na Mazingira Salama Aboud Talib, Mwanasheria Mkuu wa Serikali Said
Hassan Said pamoja na Balozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Nchi za
Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) Mbarouk Omar Mbarouk.
Hatua hiyo ni matunda ya ziara ya Rais Dk. Shein
aliyoifanya katika nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) mnamo mwezi Januari
mwaka 2018 kufuatia mwaliko wa Sheikh Mohammed bin Zayed Al Nahyan,
Mrithi wa Mtawala wa Abu Dhabi na Naibu Amiri Jeshi Mkuu wa Vikosi vya Ulinzi
wa Nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE).
Katika kuhakikisha
mazungumzo ya viongozi hao na makubaliano yao yanafanyiwa kazi mnamo mwezi wa
Agosti mwaka 2018, Ujumbe wa timu ya Wataalamu kutoka Serikali ya Nchi za Umoja
wa Falme za Kiarabu (UAE) ulikuja Zanzibar na kufanya ziara ya kutembelea
maeneo mbali mbali ya Zanzibar ukiongozwa na Mshauri wa Waziri wa Nchi
Ushirikiano wa Kimataifa wa Serikali ya Nchi za Falme za Kiarabu Bi Najla Al
Kaabi.
Ujumbe huo ulifanya
ziara ya siku moja katika Kisiwa cha Pemba na kutembelea barabara ya Chake
Chake hadi Mkoani, Hospitali ya Abdalla Mzee, Bandari ya Mkoani, Hospitali ya
Wete, Bandari ya Wete, pamoja na kutembelea kikundi cha Wajasiriamali cha
Upendo cha mjini Wete.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment