Habari za Punde

Teknolojia ya Habari na Mawasiliano Ina Nafasi Kubwa ya Kuleta Mabadiliko ya Maendeleo Katika Mabunge ya Nchi za Jumuiya ya Madola.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa hafla ya ufunguzi wa Mkutano 50 wa Chama Cha Mabunge cha Jumuiya ya Madola (CPA) uliofanyika leo katika ukumbi wa Hoteli ya Madinat Al Bahr Mbweni Wilaya ya Magharibi B Unguja.  

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kwamba teknolojia ya habari na mawasiliano ina nafasi kubwa ya kuleta mabadiliko ya maendeleo katika Mabunge ya nchi za Jumuiya ya Madola.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika ufunguzi wa Mkutano wa 50 wa Chama Cha Mabunge cha Jumuiya ya Madola (CPA) Kanda ya Afrika unaofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya  Madinatul Bahr, iliyopo Mbweni nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Rais Dk. Shein alisema kwamba iwapo teknolojia ya habari na mawasiliano itatumika ipasavyo hasa katika kuimarisha kanzi data mbali mbali hatua hiyo itarahisisha suala zima la kufanya maamuzi kwa wakati na kuweza kufikia malengo yaliokusudiwa.

Aliongeza kuwa uendeshaji wa Bunge kwa kutumia njia za kisasa kunawaweka karibu zaidi Wabunge na wananchi, jambo  ambalo linatoa fursa pana zaidi kwa wananchi ya ya kutoa maoni yao na hoja mbali mbali za maendeleo zinazogusa maisha yao ya kila siku.

Alieleza kuwa Bunge Mtandao ni nyenzo nzima ya kupunguza harama za mambo mbali mbali kama vile usafiri sambamba na kuokoa muda.

Hata hivyo, Rais Dk. Shein alisema kwamba juhudi zinazochukuliwa na nchi wananchama wa Jumuiya hiyo za kuimarisha Bunge Mtandao lazima ziende sambamba na juhudi za uhamasishaji wa teknolojia ya habari katika skuli zilizo katika Majimbo yao na nchi nzima kwa jumla.

Akieleza Kaulimbiu ya Mkutano huo mwaka huu, inayosema “Bunge Mtandao  ni nyenzo muhimu katika kuimarisha ustawi wa demokrasia “ Rais Dk. Shein alisifu kauli mbiu hiyo inayokwenda sambamba na mabadiliko ya teknolojia na masuala mbali mbali ya utandawazi.

“Nafahamu kwamba matumizi ya teknolojia ya mawasiliano ikiwemo mitandano ni muhimu sana katika utekelezaji wa majumuku ya Wabunge duniani likiwemo suala la utungaji wa sheria, kuwasilisha hoja za wananchi pamoja na kusimamia utekelezaji wa shughuli za Serikali”alisema Dk. Shein.

Rais Dk. Shin alitumia fursa hiyo kupongeza juhudi zinazochukuliwa na Wabunge pamoja na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi za kushirikiana na uongozi wa skuli mbali mbali zilizozomo katika Majimbo yao katika suala zima la kuhamasisha utoaji wa elimu ya habari na mawasiliano.

Akielezea kwa upande wa Zanzibar, alisema kuwa hivi sasa tayari skuli mbali mbali zimefaidika na matumizi ya kompyuta za aina zote ambazo hutolewa na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kwa ajili ya skuli zilizopo katika Majimbo yao.

Alieleza imani yake kwamba juhudi kama hizo tayari zinafanywa wa Wabunge wa nchi nyengine wa Jumuiya ya Madola hivyo, alisisitiza haja ya kupewa kipaumbele ili zipate kuendelezwa na Wabunge wote wa nchi za Jumuiya hiyo.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kueleza  juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar za kuimarisha Demokrasia na Utawala Bora pamoja na utoaji wa huduma kwa wananchi kwa kaunzisha Serikali Mtandao.

Alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetekeleza mradi mkubwa wa Serikali Mtandao ambao aliuzindua rasmi Januari mwaka 2013.

Aliongeza kuwa kuwepo kwa Serikali Mtandao kumesaidia sana katika kuimarisha Demokrasia na Utawala Bora kwa kuimarisha uwazi, ufanisi na uwajibikaji kama ilivyoelekezwa katika Sheria na Utumishi wa Umma Namba 2 ya mwaka 2011.

Alisema kuwa juhudi zinazoendelezwa na Serikali za kuimarisha teknolojia ya habari na mawasiliano  hapa nchini zimekuwa na mchango mkubwa katika kuimarisha utekelezaji mipango ya maendeleo ya nchi hasa MKUZA III na  Dira ya Maendeleo ya Zanzibar 2020.

Aidha, Rais Dk. Shein alifahamisha kwamba Serikali imekuwa ikitekeleza awamu ya II ya Serikali Mtandao ambapo jumla ya waya zenye urefu wa kilomita 419 zimelazwa katika maeneo mbalimbali ya Unguja na Pemba ambapo jumla ya Taasisi 112 zimeshaunganishwa na Mtandao huo likiwemo Baraza La Wawakilishi.

Alifahamisha kwamba kwa ujumla Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejidhatiti katika kuhamasisha matumizi ya teknolojia ya Habari ambapo Baraza la Wawakilishi ni miongoni mwa Ofisi zilizo mstari wa mbele katika kuhamasisha suala hilo.

Vile vile, Rais Dk. Shein alibainisha kwamba Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepata mafanikio makubwa sana katika utoaji wa huduma na ukusanyaji mapato kwa kuanzisha mifumo mbali mbali yenye kurahisisha utoaji wa huduma na ulipaji wa kodi.

Kutokana na faida zinazopatikana kutokana na matumizi ya teknolojia ya habari na mawasiliano Rais Dk. Shein aliwasisitiza Wabunge wa Jumuiya ya Madola kutilia mkazo kwa vijana juu ya matumizi ya teknolojia ya habari kwa kutumia njia sahihi.

Alisema hivi sasa teknolojia ya habari ni sehemu muhimu ya maisha ya mwanaadamu kwa kuwa imegusa na kuathiri kila nyanja ya maisha ya mwanaadamu kama vile elimu, afya, biashara pamoja na suala zima la usalama.

Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi wa Jumuiya hiyo kwa ubunifu walio nao katika suala zima la kuhamasisha uwekezaji sambamba na kuzichangamkia fursa mbali mbali za kiuchumi zilizo katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Madola.

Rais Dk. Shein aliwashukuru wajumbe wa mkutano huo kwa uwamuzi wao wa kuja kufanya mkutano huo mkuu wa 50 hapa Zanzibar na kuwapongeza Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yusnino Ndugai na Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid kwa matayarisho mazuri na  kufanikisha mkutano huo.

Dk. Shein alipongeza mfumo wa Jumuiya ya Madola na Taasisi zake kwa kufanya shughuli zake kwa mzunguko jambo ambalo linaimarisha umoja na mshikamano katika nchi za Jumuiya hiyo pamoja na wananchi wake.

Alieleza kuwa hatua hiyo inatoa fursa kwa wananchi wa nchi za Jumuiya ya Madola kuifanahamu vyema Jumuiya hiyo sambamba na Taasisi zake.

Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwakumbusha wajumbe wa mkutano huo kuwa tayari Tanzania imeshawahi kufanyika mkutano wa Majaji mnamo Septemba 2017 ambapo wajumbe wake walipata fursa maalum ya kuitembelea Zanzibar na kuweza kuangalia fursa kadhaa zilizopo.

Alieleza kuwa Zanzibar imekuwa mshiriki mkubwa wa mikutano ya Jumuiya ya Madola ambapo katika mkutano kama huo wa 49 ambao ulifanyika mjini Gaborone nchini Botswana ilituma ujumbe mkubwa kutoka Baraza la Wawakilishi la Zanzibar ambao ulioshiriki kikamilifu katika mkutano huo.


Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwaalika washiriki wa mkutano huo kama ni wanachama wa Jumuiya hiyo na wawakilishi wa nchi zao waje kuekeza Zanzibar  katika sekta zote za kiuchumi na kijamii kwani Zanzibar ni nchi yenye amani na utulivu mkubwa na imekuwa kivutio muhimu kwa wawekezaji wanaotoka nchi mbali mbali duniani.

Sambamba na hayo, Rais Dk.  Shein alieleza kuwa ikiwa huo ni mkutano wa 50 ni matarajio yake kwamba huu ni wakati muwafaka wa kutathmini mafanio yaliopatikana pamoja na changamoto zilizopo.

Alisema kwamba anaamini maazimio yatakayopitishwa yatakuwa na umuhimu mkubwa katika kuimarisha demokrasia na Utawala Bora  pamoja na kuyafikia malengo ya Jumuiya hiyo.  

Nae Nae Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo ambae pia ni Spika wa Bunge la Kenya Justin Muturi alisifu juhudi zilizochukuliwa na spika wa Bunge kwa kushirkiana na Spika wa Baraza la Wawakilishi kwa kufanikisha mkutano huo hapa Zanzibar na kutumiafursa hiyo kueleza dhamira ya Jumuiyahiyo ya kujenga hoteli ya kisasa ya nyota tano huko Dodoma, na kupongeza mashirikiano mazuri wanayoyapata kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Nae Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Ndugai pamoja na Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid waliwakaribisha wajumbe hao wa mkutano huo na kuwaeleza fursa mbali mbali zilizopo Zanzibar zikiwemo za uwekezaji na hata za utalii kwani Zanzibar imejaaliwa kuwa na vivutio vingi.

Nao  baadhi ya Maspika wa Mabunge   ya nchi za Jumuiya hiyo walitoa salamu zao na kusifu juhudi za mashirikiano zinazochukuliwa na Jumuiya hiyo huku mwakilishi maalum kutoka Bunge la Pakistan alitoa salamu za Spika wa nchi hiyo Asad Qaiser na kueleza umuhimu wa Bunge Mtandao na nafasi ya mwanamke katika maendeleo.

Mkutano huo ni wa wiki moja ambao ulianza Agosti 30 kwa kamati mbalimbali unatarajiwa kumaliza Septemba 5 mwaka huu.

Rajab Mkasaba, Ikulu
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.