Habari za Punde

Wasanii Zanzibar Watakiwa Kuongeza Kasi Katika Kuendeleza Sanaa Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akikabidhiwa Tuzo ya Sinema Zetu na Waziri wa Vijana Utamaduni Sanaa na Michezo Zanzibar Mhe. Balozi Ali Karume hafla hiyo imefanyika Ikulu Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amewataka wasanii kuitumia kikamilifu studio ya Muziki na Filamu iliopo Rahaleo, ili waweze kupata mafanikio ya kiuchumi pamoja na kuitangaza Zanzibar kimataifa.

Dk. Shein ametowa wito huo Ikulu Mjini hapa, katika hafla ya kupokea tuzo, Cheti na CD kutoka kwa wasanii wa filamu nchini, zilizotokana na ushindi walioupata katika mashindano yalioandaliwa na Kituo cha Azam TV.

Katika mashindano hayo yaliofanyika mwezi April, 2018 , filamu 200 kutoka nchi sita zilishindaniwa na wasanii wa Zanzibar waliibuka washindi kupitia filamu za ‘Bint Zanzibar’, ‘Sisi na wao’ pamoja na ‘Dema’.

Dk. Shein alisema  Studio ya Muziki na filamu iliipo Rahaleo, ni miongoni mwa studio bora na yenye vifaa vya kisasa, hivyo amewataka wasanii kuitumia kikamilifu, ili waweze kunufaika kutokana na Hati miliki ya kazi zao pale watakapoziuza.

Alisema safari ya wasanii hao bado ni ndefu, hivyo akawataka kuongeza bidii ili kupata mafanikio, sambamba na kuitangaza Zanzibar kimataifa, akibainisha baadhi ya Mataifa ikiwemo Marekani, India na Nigeria ambapo wasanii wake wamepata mafanikio makubwa kutokana na sanaa ya uigizaji.

Aidha, aliwataka kuongeza kasi katika kuendeleza sanaa, kwa kigezo kuwa jamii inahitaji kuliwazwa baada ya shughuli mbambali  za kazi.

Dk. Shein, aliwapongeza wasanii hao kwa kazi kubwa waliyofanya na kuiletea sifa Zanzibar.

“Mmefanya kazi kubwa , ni kazi ya thamani………mimi nimeonyesha njia……………..”, alisema.

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza wasanii waliojitokeza kuomba matengenezo ya Studio hiyo. 

Alisema Serikali imetumia fedha nyingi kwa ajili ya matengenezo ya studio hiyo na kuahidi kuendelea kuwaunga mkono wasanii pale mahitaji zaidi yatakapojitokeza katika studio hiyo.

Akigusia historia ya filamu Zanzibar, Dk. Shein alisema Zanzibar inajivunia kwa kuwa na magwiji wa sanaa mbali mbali, ikiwemo wa filamu pamoja na kupata bahati ya wasanii mahiri duniani kuja nchini kwa ajili ya kurekodi michezo yao.

Alisema baada ya Mapinduzi ya 1964, filamu ya mwanzo iliyojuilikana Zanzibar yasonga mbele” ilirikodiwa na baadae kusambazwa katika Mikoa yote mjini na mashamba.

Nae, Waziri wa  Vijana,Utamaduni, Sanaa na Michezo Balozi Ali Karume, alimshukuru Rais Dk. Shein kwa juhudi zake za kuendeleza sanaa nchini na kuunga  mkono  mahitaji ya wasanii, ambapo alifanikisha ujenzi wa Studio ya kisasa ya Muziki na Filamu.

Aidha, aliwapongeza wasanii kwa kazi nzuri ya uigizaji akibainisha heshima kubwa wanayopata wasanii mbali mbali duniani kutokana na kazi za sanaa, hivyo akawataka kuiga mfano wao.

Mapema, Katibu wa  Chama cha wasanii waigizaji, Salum Maulid ‘stika’ alisema wasanii wanahitaji kupatiwa mafunzo zaidi ya uigizaji ili kuongeza uwezo wao kiutendaji.

Alisema katika utendaji wao wakazi wamekuwa wakipata mashirikiano mazuri na viongoi wa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa an Michezo pamoja na COSOZA.

Aliiomba Serikali kuendelea kuwaunga mkono wasanii na kusema hatua hiyo itafanikisha azma ya kuutangaza Utalii kupitia sanaa.

Aidha, alisema Chama cha wasanii Zanzibar, kimejidhatiti kuwaelekeza wasanii juu ya umuhimu wa kufanya kazi zao kwa msingi wakulinda mila, silka na utamaduni wa Wazanzibari.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.