Na:
Lillian Shirima – Habari MAELEZO
Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania,Dkt. John Magufuli
alizindua kitabu cha maisha binafsi ya Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin
Mkapa cha 'My Life My
Purpose' (Maisha Yangu, Kusudi Langu) , hafla hiyo
iliyofanyika katika Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Julius Nyerere jijini
Dar es Salaam na kuhudhuriwa viongozi wengi wakiwemo na marais wastaafu Ali
Hassan Mwinyi na Jakaya Kikwete.
Kitabu hicho
chenye kurasa 316, na sura 16 zilizogawanywa kwenye sehemu kuu tatu, kimesheheni wingi wa nasaha na ushauri lakini
pia kinatoa mafundisho mengi kwa viongozi wa baadaye jambo ambalo Rais John
Pombe Magufuli aliliona mapema pengine kabla ya kuandikwa kwenye kitabu hicho.
Katika sehemu ya mwisho ya kitabu inayoeleza kwa ufupi
maisha ya Mzee Mkapa baada ya kumaliza miaka kumi ya kulitumikia taifa kwa
ngazi ya urais, Mkapa anatoa ushauri kwa kutaja mambo sita ambayo kiongozi
anawajibu kwa kuyazingatia.
Mambo hayo ni kuonyesha nia na
bidii kwa majukumu unayopewa na wananchi, kuwa tayari kuwashirikisha wengine
katika mawazo, mafanikio, matatizo na upimaji wa utekelezaji, kutofanya kazi kwa kukurupuka
na kutotabirika.
Mengine ni kufuata na kutii sheria na taratibu,
kuwa tayari kusikiliza na mwisho kutafuta mlezi (mentor) kama ambavyo yeye mwenyewe Mzee Mkapa anavyoeleza mlezi
wake kuwa alikuwa Mwalimu Julius Nyerere.
Katika
mahojiano yaliyofanyika na mtaalam wa masuala ya siasa Bwana Severine Kapinga
kutoka Chuo Kikuu Cha Dar es salam, (UDSM), anasema, ushauri aliotoa Mzee Mkapa kuhusu wajibu wa kiongozi
na mambo anayotakiwa kuzingatia hapana shaka Rais John Magufuli alianza kuyaishi
na kuyazingatia kabla kitabu cha Mkapa
hakijaandikwa 2016.
Anaongeza
kuwa, nchi yoyote duniani toka ilipopata uhuru ikipita miaka 50 ni lazima nchi
hiyo ifikie wakati wa kuweza kujipambanua na kujielewa ipo wapi, inataka kufika
wapi na imekwama wapi; kazi ambayo sio ya sera pekee bali ni kazi itakayofanywa
na kiongozi mwenye nia ya kuwatumikia wananchi kwa dhati.
“Hii sio kazi ya kisera tu, ni kazi ambayo itaongozwa
na kiongozi ambaye amechaguliwa na watu na yeye sasa ndiye anayetakiwa kubeba
maono ya watu na dhamira ya walio wengi’. Anasema Bw. Kapinga.
Rais
Magufuli amethubutu katika hili kuonesha nia na bidii ya kazi katika majukumu
aliyopewa na wananchi na kwamba ameweza kuvaa taswira ya maono ya wananchi kwa namna
anavyoisimamia na kuiongoza nchi, uwajibikaji wake umekuwa chachu kwa wananchi
kufanya kazi kwa bidii.
Aidha, anasema
mageuzi makubwa yanayoonekana sasa
yanatokana na uwajibikaji wa Rais Magufuli katika kusimamia rasilimali za nchi,
nidhamu kwenye matumizi ya fedha za umma na maarifa katika kushughulikia matatizo
ya wananchi wanyonge.
Mara kadhaa tunashuhudia Rais Magufuli akifanya mikutano
na watendaji wa Serikali kuanzia Wakuu wa Mikoa, Wilaya, Makatibu Tawala wa Mikoa
na Wilaya na Makatibu Watendaji wa Tarafa. Mathalani, Septemba 2,mwaka huu, Rais Magufuli alikutana na Maofisa Watendaji
wa Kata kutoka nchi nzima Ikulu jijini Dar es Salaam..
Mbali na kuwashirikisha katika maamuzi kama ambavyo Mzee
Mkapa ameshauri katika kitabu chake, Rais Magufuli ameenda mbali zaidi na
kuwaasa kufanya kazi kwa bidii na kuhakikisha kata wanazozisimamia zinakuwa na
ulinzi na usalama.
Rais Magufuli aliwaambia, “hakuna shughuli za maendeleo zinazoweza
kufanyika bila kuwa na amani, ni lazima wananchi wafanye kazi bila hofu , bila
bugudha…”.
Ushauri wa Mzee Mkapa kwa viongozi wajao ni dhahiri ulianza
kutekelezwa kitambo. Kundi lingine lililokutana na Rais Magufuli Juni,mwaka huu
ni wafanyabiashara kutoka katika wilaya zote nchini kwa nia ya kutaka
kujadiliana kwa uwazi namna ya kutatua changamoto walizonazo na kubuni njia
bora za kuboresha mazingira ya biashara nchini.
Wengine ni Mabalozi wetu wanaotuwakilisha katika nchi
mbalimbali, wachimbaji madini na wadau wa sekta ya madini, na hata wachezaji wa
timu ya Taifa, (Taifa Star) Hakika Rais hafanyi kazi kwa kukurupuka au
kutotabirika isipokuwa kushirikisha kada tofauti katika mipango ya maendeleo, Ushauri
aliotoa Mzee Mkapa katika kitabu chake.
Mara kadhaa
Rais Magufuli amesikika akisema yeye si wa kundi lile, yeye ni wa wanyonge na
kwamba Watanzania wanyonge ndio watakajenga nchi hii.
Kwa kauli hii
Bwana Kapinga anasema, Rais Magufuli angekuwa upande wa watu wachache miradi mikubwa tunayoiona sasa
isingekuwepo lakini kwa kuwa ameamua kusimama upande wa Watanzania wanyonge
mwamko wa watu kujituma kufanya kazi umekuwa mkubwa.
Wakati wa uzinduzi wa Kitabu hicho,Rais Magufuli ambaye
alikuwa mgeni rasmi alimshukuru Mzee Mkapa kwani katika uongozi wake wa Awamu
ya Tatu mambo mengi yamefanyika ikiwa ni pamoja na kujenga barabara kwa fedha
za ndani.
Alieleza namna
alivyovutiwa na sura nyingi za Kitabu hicho ambazo zimeeleza jinsi ya
kujitegemea, jitihada ambazo zimekuwa
zikifanywa na kusisitizwa na Serikali ya Awamu ya Tano.
Akitoa mfano mdogo wa hatua ambazo Serikali ya Awamu ya
Tano imeleta mwamko wa watu, Bwana Kapinga amesema, kuanzishwa kwa mpango wa
utoaji wa vitambulisho kwa wajasiriamali wadogo wenye biashara chini ya
mzunguko wa shilingi milioni 3 kwa kiasi kikubwa umewaweka wajasiriamali katika
mazingira huru yakujitegemea.
Mara baada ya
zoezi la ugawaji wa vitambulisho kwa wafanyabiashara ndogondogo kukamilika,
wengi wao wameanza kutambua kuwa nchi ipo katika mageuzi ya kiuchumi na wanashiriki
kuchangia maendeleo ya nchi.
Anasema, ukifika Kariakoo, Tazara na maeneo ya
wafanyabiashara ndogondogo,
wamachinga,wanaweza kukueleza juu ya miradi mikubwa kama ujenzi wa reli
ya kisasa, madaraja na barabara za juu kwasababu wanatembea kwa amani wakifanya
biashara pasipo chuki na Serikali.
“Siku hizi tumesahau mambo ya kukimbizana na wamachinga
na mama ntilie mjini, kamatakamata ambayo haina mwelekeo haipo tena kwa sababu
Rais aliamua kutafuta majibu ya kero za wafanyabiashara ndogondogo kwa kuwapa
vitambulisho na ruhusa kufanya shughuli zao bila bughudha”, anasema Kapinga.
Tunamwona Rais akifanya ziara za ndani zaidi kuliko ziara
za nje ya nchi kwa msingi wa kuwa tayari kusikiliza matatizo ya wananchi na kutafuta
ufumbuzi wamatatizo hayo ikiwa ni pamoja na kuhakiki taarifa za maendeleo
anazopewa na wasaidizi wake.
Hakuna ziara anayofanya
bila kuwa na taarifa ya eneo husika hii ni kutokana na uzoefu
wa muda mrefu katika kulitumikia taifa ndio unaopelekea kuwepo kwa ziara za
kushtukiza.
Bwana Kapinga anasema, hatua hii ndio inayofanya wote
waliokuwa wavivu wa kwenda kwa wananchi kutambua kuwa kazi kubwa ipo kwa
wananchi na sio nje ya nchi na kwamba Awamu ya Tano imerudisha mamlaka kwa
wananchi kwasababu viongozi wakuu wa Serikali wanakwenda kwa wananchi mara kwa
mara.
“Huwezi kuwa na mamlaka na Serikali kama huioni, tunasema
hii ndio Serikali ya watu…. viongozi wanathamini watu, Rais amekaa nafasi ya
waliokosa, nafasi ya mwananchi mwenye hali ngumu, kwa sababu amepewa dhamana na
wao, anaumia kama anavyoumia yule mwananchi wa mwisho”, anasema Bwana Kapinga.
Ni katika kitabu hicho Mzee Mkapa ameshauri viongozi
kutafuta mlezi (mentor) na kwamba kwake yeye Mwalimu Nyerere alikuwa mezi wake.
Sio siri Mzee Mkapa ndiye aliyemuibua Rais Magufuli katika medani za siasa.
Ndiye aliyetambua uwezo wake wa kazi katika kusimamia maamuzi sahihi na
kuyatekeleza kwa ufasaha, na Mzee Mkapa ndiye aliyekuwa tayari kumtia nguvu pale
alipokutana na vikwazo katika utekelezaji wa majukumu ya kazi kwa maslahi ya
taifa.
Ushauri wa mambo sita yaliyotajwa
katika kitabu
cha Mzee Mkapa “Maisha Yangu
Kusudi Langu” tunaona kuwa,Rais John Pombe Magufuli
ameutekeleza mapema na ndiyo maana tunasema , alikisoma kitabu
kabla hakijaandikwa, alianza kuzingatia
mengi kwa vitendo na hata katika hotuba yake za uzinduzi wa kitabu
hiki amekiri kuwa Mzee Mkapa ndio shujaa wake, ametoa wito kwa Watanzania
kuwaenzi na kuwatunza wazee wote wakiwemo viongozi wastaafu ambao ama kwa
hakika tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwao.
No comments:
Post a Comment