Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Ujumbe wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland cha Nchini Norway Ikulu Jijini Zanzibar leo.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Ujumbe wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland cha Nchini Norway, ukiongozwa na (CEO) Mr. Eivind Hansen (kulia kwa Rais) walipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo na Rais leo 22-11-2019

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameupongeza uongozi wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland ya nchini Norway kusaidia ujenzi wa Hospitali ya wagonjwa wa akili, Kidongo Chekundu ambayo itakuwa ya kisasa kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipokutana na kufanya mazungumzo na uongozi wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland ya nchini Norway ukiongozwa na Trond Mohn aliyefuatana na rafiki zake pamoja na familia yake wakiwa pamoja na uongozi wa Wizara ya Afya.

Rais Dk. Shein alisema kuwa hiyo ni habari njema na ya kujivunia inayotokana na uhusiano, ushirikiano na urafiki wa muda mrefu unaoendelezwa kati ya Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland ya nchini Norway na Hospitali Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja.

Aliongeza kuwa Hospitali ya wagonjwa wa akili iliyopo Kidongo Chekundu ni hospitali kongwe katika hospitali kadhaa hapa nchini ambayo ina historia kubwa inayotokana na utoaji huduma zake kwa wakati huo ilipojengwa na wakoloni wa Kiengereza mnamo miaka ya 50 ambapo ilipewa jina na jamii kwa kuitwa “Jela ya Wendawazimu”.

Hivyo, hatua za kuijenga upya Hospitali hiyo na kuwa ya kisasa na ya pekee katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati itakuwa ni faraja kubwa kwa Wazanzibar kwa kuiimarisha sambamba na kutoa huduma za kisasa za wagonjwa wa akili na kuwa msaada mkubwa kwa wagonjwa wa ndani na nje ya nchi.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kutoa ushirikiano wake mkubwa kwa uongozi wa Hospitali hiyo chini ya kiongozi wake mkuu Trond Mohn ambayo imekusudia kujenga Hospitali ya wagonjwa wa akili ya Kidongo Chekundu na kuwa ya pekee katika ukanda huu wa Afrika Mashariki na Kati.

Rais Dk. Shein aliongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini sana mashirikiano inayotoa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Hakeland katika kusaidia kuimarisha sekta ya afya hapa nchini ikiwa ni pamoja na kusaidia ujenzi wa majengo kwa ajili ya huduma za afya na tiba, vifaa, wataalamu pamoja na mafunzo kwa madaktari wa Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein aliupongeza uongozi huo kwa kufanya kazi na Wizara ya Afya kupitia Hospitali Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja kwa muda wa miaka kumi hivi sasa hatua ambayo imeweza kukuza na kuimarisha sekta ya afya nchini sambamba na kuendeleza huduma za kijamii na kukuza uchumi wa Zanzibar.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendelea na Sera yake ya kutoa huduma za afya bure, Sera ambayo iliasisiwa na Jemedari wa Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 Marehemu Sheikh Abeid Amani Karume na hadi hivi leo inaendelezwa.

Aliongeza kuwa juhudi za makusudi zimekuwa zikichukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha sekta ya afya inaimarika ambapo pia, nchi marafiki pamoja na mashirika ya Kimataifa yamekuwa yakiendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuhakikikisha sekta ya afya inaimarika na wananchi wanapata huduma za afya.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein aliukaribisha Zanzibar uongozi wa Hospitali hiyo ulioongozwa na Kiongozi Mkuu na Mfadhili wa Hospitali wake Trond Mohn na kuueleza jinsi sekta ya utalii ilivyoimarika hapa nchini na vipi inachangia uchumi wa Zanzibar.

Nae Afisa Mtendaji Mkuu wa Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland Eivind Hansen alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Hospitali hiyo inajivunia uhusiano na ushirikiano mzuri uliopo kati yake na Hospitali Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja ambapo tayari imeshatimia miaka 10 tokea kuanzisha mashirikiano hayo.

Afisa Mkuu huyo alieleza kuwa Hospitali ya Haukeland imeweza kushirikiana na Hospitali ya Mnazi Mmoja kwa kuanzisha na kuendeleza miradi mbali mbali ikiwemo ya ujenzi wa majengo kwa ajili ya kutoa huduma za afya, mafunzo wka madaktari, vifaa na wataalamu.

Alieleza kuwa mbali ya mashirikiano hayo pia, kumekuwa na mashirikiano mazuri ya kubadilishana wataalamu na utaalamu kati ya madaktari wa Hospitali ya Haukeland na Hospitali Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja jambo ambalo kuna haja ya kuendelezwa.

Pamoja na hayo alieleza kuwa, Hospitali hiyo ya Haukeland imekuwa ikitoa ufadhili wa mafunzo kwa madaktari wa Hospitali ya Mnazi Mmoja kwa kila mwaka utamaduni ambao uongozi huo umeahidi kuuendeleza.

Uongozi huo wa Hospitali ya Haukeland ulieleza kuwa tayari mradi wa ujenzi wa Hospitali ya wagonjwa wa akili ya Kidongo Chekundu umeshafikia asilimia 50 ambapo majengo mapya zaidi yatajengwa, pamoja na ukarabati wa majengo ya zamani katika eneo hilo huku akieleza kuwa mradi huo pia, utahusisha mafunzo kwa wafanyakazi.

Aidha, uongozi huo ulisisitiza kwamba azma na lengo lao ni kuifanya Hospitali hiyo ya Kidongo Chekundu kuwa ya pekee itakayotoa huduma za kisasa kwa wagonjwa wa akili katika nchi za Bara la Afrika.

Waliongeza kuwa katika ziara yao ya hapa Zanzibar pia, wamepanga kukutana na kukaa pamoja na uongozi wa Wizara ya Afya pamoja na Hospitali Kuu ya Rufaa ya  Mnazi Mmoja kwa ajili ya kujadiliana masuala mbali mbali ya uendelezaji na uimarishaji wa miradi ya sekta ya afya hapa nchini.

Katika maelezo yao uongozi huo pia, ulieleza azma yake ya kuunga mkono juhudi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta ya afya kwa kuendeleza na kuanzisha miradi mipya ya sekta ya afya sambamba na kuimarisha mashirikiano na Hospitali Kuu ya Rufaa ya Mnazi Mmoja.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.