Habari za Punde

Hatufanyi Biashara kwa Kuanzisha Vifurushi-Bi. Anne Makinda

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bi. Anne Makinda akiongea wakati wa uzinduzi wa kampeni ya uhamasishaji wa wananchi kujiunga na vifurushi vya Bima ya Afya, leo Mkoani Dodoma
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bi. Anne Makinda akiwapatia kadi za Bima ya Afya baadhi ya wakazi wa Dodoma waliojiunga na vifurushi vya bima ya afya leo Mkoani Dodoma



Na Mwandishi Wetu                                                                                                                     
 Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya Bi. Anne Makinda amesema kuwa mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya umejielekeza katika kumhudumia mtanzania wa kila aina kulingana na uwezo wake na sio kufanya biashara kama inavyoelezwa na baadhi ya watu.

Akiongea wakati wa uzinduzi wa kampeni ya uhamasishaji wa wananchi kujiunga na Vifurushi vya Bima ya Afya Bi. Makinda amesema kuwa NHIF kuanzisha vifurushi kwamba ni kufanya biashara si kweli bali ni kuhakikisha watanzania ambao nchi yao ipo huru na wana amani wapate pia amani ya huduma ya afya.

“Mfuko huu ulianzishwa na Serikali, sio mfuko wa kufanya biashara, tunachukua hela za wanachama, ili wakatibiwe , unalipa 192,000 kwa mwaka halafu unaenda hospitali mara nne mara tano kwa mwaka kwa gharama zaidi ya pesa uliyowekeza, lengo letu ni kumhudumia mtanzania”-Bi Anne Makinda.

“Ukitaka kwenda hospitali leo, kumuona daktari ni shughuli, hapo bado matibabu, sasa bima ya afya ni hela unayoweka ukiwa na uwezo, ukienda hospitalini utatibiwa kwa mamilioni hata usiowahi kuyatoa wewe, utatibiwa tu na hela yako ndogo uliyokata nayo wewe kwa mwaka mzima”-Alisema Bi. Anne Makinda

Aidha Bi. Anne  Makinda amewataka watanzania kujiunga na Bima ya Afya hasa baada Mfuko huo kuja na vifurushi vya bima ya afya vinavyotoa wigo kwa watu wengi kujiunga kulingana na uwezo wake ili kusaidia Katika huduma za matibabu ambazo zimezidi kuwa kubwa kwa sasa.

Akiongea kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Chemba Bw. Simon Odunga ameupongeza mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kuja na mpango wa vifurushi kwani umejumuisha makundi tofauti katika jamii na kuwawezesha kila mmoja kujipimia kwa uwezo wake na hivyo kuwa na uhakika wa huduma za afya.

Naye Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Taifa ya Bima ya Afya Bw. Bernard Konga amesema katika wiki tatu tangu waanzishe mpango huu wa Vifurushi vya Bima ya Afya Idadi kubwa ya watanzania wamejitokeza kujiunga.

“Ndani ya wiki tat utu tangu tuzindue vifurushi hivi idadi ya watanzania wanaojiunga na mfuko imekuwa kubwa ambapo mpaka sasa tumeshaunga watanzania zaidi ya elfu ishirini na idadi hii imeendelea kuongezeka siku hadi siku”-Alisema Bw. Konga

Muwakilishi kutoka Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Bw. Edward Mbanga amewataka watumishi wa NHIF kuendelea kutoa elimu kwa wananchi kujiunga na vifurushi hivyo na kuachana na kelele zapembeni.

Wawakilishi wa Vyama via BodaBoda na Machinga wamepongeza mango huo na kuahidi kuhamasisha wanachama wao kujiunga na mango huo kwani ni mkombozi kwa afya ya watanzania wote. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.