Habari za Punde

Zanzibar Itandelea Kujifunza Kutoka Katika Nchi Hiyo. Vietnam Imepata Mafanikio Makubwa Katika Nyanja Zote Kiuchumi




RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza kuwa Zanzibar ina mengi ya kujifunza kutoka Vietnam kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana nchini humo chini ya Chama cha Kikomunisti cha (CPV).

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo Ikulu Mjini Zanzibar wakati alipokuwa na mazungumzo na  Mjumbe na Katibu wa Kamati Kuu ya Uongozi wa Chama cha Kikomunisti cha Vietnam (CPV) Bwana Pham Minh Chinh akiwa amefuatana na ujumbe wa viongozi kutoka Chama hicho.

Katika maelezo yake Rais Dk. Shein alisema kwamba nchi hiyo imepata mafanikio makubwa katika nyanja zote zikiwemo za kiuchumi, kijamii na kisiasa na kueleza kuwa Zanzibar itaendelea kujifunza kutoka nchi hiyo.

Rais Dk. Shein aliipongeza Vietnam kwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo ambao umeweza kuleta mafanikio makubwa sambamba na mahusiano kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha Kikomunisti cha Vietnam (CPV).

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa ziara ya kiongozi huyo hapa nchini inaimarisha na kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Vietnam na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar pamoja na vyama vikuu vinavyotawala katika nchi mbili hizo.

Alieleza kuwa uhusiano huo ulianza tokea mwaka 1965 kati ya Vietnam na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania umeweza kuleta manufaa katika kuimarisha sekta za maendeleo zikiwemo kilimo, uwekezaji, elimu, biashara pamoja na sekta nyenginezo.

Rais Dk. Shein alimuhakikishia kiongozi huyo kuwa Chama Cha Mapinduzi CCM, kitaendeleza urafiki na udugu uliopo kati yake na Chama cha Kikomunisti cha Vietnam (CPV) ikiwa ni pamoja na kuendelea kutembeleana kati ya viongozi wa vyama hivyo na wale viongozi wa Serikali.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein hakuchelea kumueleza kiongozi huyo hatua nzuri na mafanikio yaliopatikana katika ziara yake aliyoifanya nchini humo mnamo mwaka 2012 kufuatia mwaliko wa Rais wa nchi hiyo Troung Tan Sang.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa katika ziara hiyo alipata fursa ya kukutana na kuzungumza na Rais  wa nchi hiyo pamoja na viongozi wengine wakuu na kujadili masuala mbali mbali yaliyojikita kukuza uhusiano na ushirikiano wa pande mbili hizo ikiwa ni pamoja na ushirikiano katika sekta ya kilimo, uvuvi, utafiti, biashara na sekta nyenginezo.

Aidha, Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa nchi hiyo kutokana na kuendelea kukua kwa uchumi wake pamoja na kuendelea kuwepo kwa amani, utulivu na usalama ambao umeweza kuipaisha nchi hiyo katika nyanja za Kimataifa hatua ambayo inafaa kuigwa na mataifa mengine.

Alimueleza kuwa Tanzania ni nchi ya amani na inafarajika kuona nchi nyengine zinakuwa na amani kwani panapokuwa na amani maendeleo hupatikana kama ilivyo Vietnam, ambapo aliahidi kuendelea kushirikiana katika sekta za maendeleo ikiwemo biashara, kilimo na uwekezaji.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo Kuipongeza Serikali ya Vietnam na chama chake cha (CPV) kwa kuwahamasisha wawekezaji wa Kampuni ya Halotel kutoka nchini humo kuja kuekeza Tanzania katika sekta ya mawasilianio.

Rais Dk. Shein alimueleza kiongozi huyo kuwa wafanyabiashara wa Zanzibar bado wanaendelea kufanya biashara nchini humo hasa biashara ya mchele hasa ikizingatiwa kwamba nchi hiyo ni ya pili duniani katika uzalishaji wa bidhaa hiyo.

Nae  Mjumbe na Katibu wa Kamati Kuu ya Uongozi wa Chama cha Kikomunisti cha Vietnam (CPV) Bwana Pham Minh Chinh alimpongeza Rais Dk. Shein kwa mafanikio makubwa yaliopatikana hapa Zanzibar chini ya uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Kiongozi huyo wa chama cha (CPV) alimueleza Rais Dk. Shein kuwa nchi yake inaona fahari mkubwa kuwepo kwa mashirikiano na uhusiano mwema kati yake na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar.

Alieleza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ni rafiki mkubwa wa Vietnam kwani imeweza kuiunga mkono nchi hiyo katika mambo mbali mbali ya Kitaifa na Kimataifa ikiwa ni pamoja na suala zima la usalama kupitia Umoja wa Mataifa (UN) sambamba na kuunga mkono mapambano katika uvamizi wa nchi yao.

Aidha, kiongozi huyo wa chama cha (CPV), alimueleza Rais Dk. Shein kuwa ziara yake hiyo yeye na viongozi wengine wa chama hicho hapa nchini ina lengo la kukuza uhusiano, ushirikiano na udugu uliopo kati ya (CPV) na (CCM), pamoja na mahusiano kati ya Serikali za nchi hizo.

Pamoja na hayo, kiongozi huyo alimueleza Rais Dk. Shein jinsi nchi hiyo ilivyopata mafaniko na kupiga hatua katika kuimarisha uchumi wake sambamba na uendelezaji wa amani na utulivu huku kiongozi huyo akisisitiza haja ya kuendeleza utamaduni wa kutembeleana kati ya viongozi wa vyama hivyo na Serikali kwa lengo la kukuza uhusiano na ushirikiano uliopo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.