Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akifungua Kongamano la kuadhimisha na kusherehekea siku ya Wanawake Duniani na Miaka 25 Baada ya mkutano wa beijing katika Ukumbi wa Mikutano wa Hyatt Regency Jijini Dar es salaam leo March 04,2020. . ambapo kauli mbiu Uwajibikaji wa Uongozi katika kujenga Kizazi cha Usawa wa Jinsia.
Mheshimiwa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar
Es Salaam;
Mheshimiwa Sofia Mjema, Mkuu wa Wilaya ya
Ilala;
Bi Hodan
Addou, Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalo husika na Usawa wa Jinsia na Uwezeshaji wa
Mwanamke (UN Women) Tanzania;
Mheshimiwa Paul Sherlock, Balozi wa Ireland
nchini Tanzania;
Mheshimiwa Frederic Clavier, Balozi wa
Ufaransa nchini Tanzania;
Mheshimiwa Elizabeth Jacobsen, Balozi wa Sweeden
nchini Tanzania;
Mheshimiwa
pamela O’Donnel, Balozi wa Canada nchini Tanzania;
Wadau wa
Maendeleo;
Wawakilishi
kutoka Asasi za Kiraia;
Waandishi wa
Habari;
Mabibi na
Mabwana;
Habari
za Asubuhi!
Awali
ya yote, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha
kujumuika leo hii kuadhimisha Siku ya Wanawake Duniani. Kwa niaba ya Serikali
inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania, ninayo furaha kubwa kuungana nanyi kwenye kuadhimisha
siku hii. Pili, naomba kutoa shukrani zangu za dhati kwa Mfuko wa Wanawake Tanzania kwa heshima
mliyonipa kuwa Mgeni Rasmi katika kusherehekea siku ya Wanawake Duniani. Maadhimisho
ya mwaka huu ni ya kihistoria duniani kote na hapa kwetu Tanzania. Mwaka huu jumuiya
ya Kimaifa inakumbuka na kuadhimisha miaka 75
ya kuundwa kwa Umoja wa Mataifa uliotoa tamko kwamba binadamu wote ni sawa.
Aidha,
ni mwaka wa 25 tangu mataifa ya umoja huu kutamka mpango kazi wa Beijing
uliozitaka nchi wanachama na mashirika yote kuchukua hatua stahiki za kuwezesha
upatikanaji wa haki za wanawake na wasichana. Kwa sisi hapa Tanzania ni miaka
20 tangu tuanze kutekeleza Dira yetu ya Taifa yenye kuelekeza kutokomeza aina
zote za ubaguzi ikiwemo ubaguzi wa jinsia. Sambamba na hayo pia huu ni mwaka wa
Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani utakasababisha kuundwa kwa Serikali
na Bunge mihimili ambayo tutaipa dhamana ya kuongoza Dola kwa miaka mitano
ijayo kwa turufu ya kura za wananchi wote pamoja na sisi wanawake.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Bila
shaka, tuna kila sababu za kujumuika hapa kutafakari kama safari yetu ya
kutetea haki za wanawake na wasichana na kupambana na mifumo inayotubagua
imefanikiwa. Katika kuitafakari safari hiyo ni vyema tukabainisha mambo gani
tumefanya katika nafasi tulizo nazo ili kuleta mabadiliko tunayotamani kuyaona,
kumekuweko na fursa zipi, ni changamoto zipi zimejitokeza na tumekabiliana nazo
kivipi, na hatimaye, tunataka kuelekea wapi.
Nafahamu
kuwa kaulimbiu inayoongoza maadhimisho haya kwa mwaka huu inasema” Kizazi cha usawa kwa maendeleo ya sasa na baadaye”.
Kaulimbiu hii imekuja wakati muafaka kabisa ambapo Serikali inaelekeza nguvu
kubwa katika kujenga uchumi wa viwanda ili kuleta maendeleo. Serikali inatambua
kwamba, tusipochukua hatua za makusudi za kuwekeza kwenye kujenga jamii
inayoongozwa na usawa wa jinsia, jitihada zetu za kujenga uchumi wa viwanda na
kulikomboa taifa hili kutoka umaskini na kufikia uchumi wa kati haziwezi
kufanikiwa.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Sote
ni mashuhuda wa jitihada kubwa zilizochukuliwa na serikali katika kutekeleza
azma ya kuondoa ubaguzi wa kijinsia na kujenga jamii inayoongozwa na usawa wa jinsia.
Katika kuhakikisha hilo, Serikali yetu imeridhiria mikataba yote ya kimataifa
na kikanda inayotupa wajibu wa kuchukua
hatua za makusudi kuondoa ubaguzi wa jinsia na kuwezesha wanawake na wasichana
kupata haki zao bila ubaguzi wa aina yoyote. Tukiwa wanachama wa Umoja wa
Mataifa, Serikali yetu ilishiriki kikamilifi katika Mkutano wa Beijingmwaka
1995 (ambao mimi nilibahatika kushiriki nikiwa bado kijana) ulioongozwa na Mama
Getrude Mongella. Katika mkutano huo nchi yetu iliridhia Tamko na Mpango Kazi
wa Beijing. Mpango Kazi huu ulibainisha maeneo 12 ya kupewa kipaumbele ili
kufanikisha juhudi za kuondoa ubaguzi wa kijinsia na kuwezesha wanawake na
wasichana kupata haki sawa na wanaume.
Serikali
ya Awamu ya Tatu chini ya Mheshimiwa Benjamin Mkapa,ilipokea Mpango Kazi wa
Beijing kutoka kwa ujumbewetu uliokwenda Beijing, kwenye mkutano uliyojulikana
kwa jina la “Rudisha Beijing Nyumbani”
ikabainisha maeneo kadhaa ya kipaumbele kama vile Wanawake na Umaskini,
Ushiriki wa Wanawake katika Meza ya Maamuzi, Elimu na Afya. Aidha Serikali za
awamu zote zilibeba na zinaendelea kubeba wajibu wa kutokomeza ubaguzi wa aina
yoyote ikiwemo ubaguzi wa kijinsia. Wajibu huu umehusisha pia kuboresha au
kutunga sheria zinazoongoza utekelezwaji wa misingi ya usawa, sera, mipango na
mikakati ya kuwezesha taifa kuondoa ubaguzi wa aina yoyote ikiwa ni pamoja na
ubaguzi dhidi ya wanawake na wasichana.
Wageni Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Katiba
zetu zote mbili yaani ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (1977) na Katiba ya
Zanzibar (1984) ambazo ndio sheria mama zinazoongoza sheria zote zinatamka
bayana kuhusu usawa wa binadamu na kukataza ubaguzi wa aina yoyote. Katiba hizi
pia zinabainisha kuhusu ushiriki wa raia wote Wake kwa Waume kwenye uongozi wa
Taifa letu. Mbali ya ushiriki katika uongozi, Katiba hizi zinatamka kuhusu
uwepo wa viti maalum vya uwakilishi wa wanawake katika Bunge la Jamhuri ya
Muungano na Baraza la Wawakilishi.
Kazi
kubwa iliyofanywa na serikali zetu ni kutafsiri misingi ya vifungu vya katiba
na kutunga Sera za kuongoza utekelezaji wa vifungu hivyo.Sera hizo ni kama vile
sera ya Maendeleo ya Wanawake na Jinsia ambayo sasa hivi iko kwenye mchakato wa
maboresho, sera za elimu, afya, maji na nishati ambazo zote hizo zinalenga
kutekeleza azma ya kujenga misingi ya usawa na kuondoa ubaguzi wa kijinsia.
Aidha, Dira ya Maendeleo ya Taifa 2025, inalenga kuwa na taifa lisilokuwa na
aina yoyote ya ubaguzi ifikapo mwaka 2025, ambayo ni miaka miaka mitano ijayo
kuanzia sasa. (je itawezekana? ili
iwezekane tufanyeje?)
Ili
kufanya utekelezaji wa Sera zilizotungwa kuwa na uhalali wa Kisiasa na Kijamii,
Sheria mbalimbali zinazobainisha usawa wa jinsia na zinazokataza aina zote za
ubaguzi dhidi ya wanawake zimetungwa. Kwa mfano, kwa upande wa Tanzania Bara, Sheria
za Ardhi za mwaka 1999, Sheria kuhusu Makosa ya Kujamiiana(SOSPA) ya mwaka 1998
na Sheria ya Vyama vya Siasa ya mwaka 2019. Aidha, Sheria ya Kupambana na
Kuzuia Rushwa ya mwaka 2007 inabainisha kuwa rushwa ya ngono ni kosa la jinai linalotokana
na matumizi mabaya ya mamlaka,na imebainishwa kuwa ni kitendo cha uhujumu
uchumi, kwa kuwa inahujumu rasilimali watu ambao ndiyo wajenzi wa uchumi wa
nchi.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Serikali
yetu imeweka mikakati na mipango madhubuti ya kuimarisha uchumi na kuondoa
ubaguzi wa kijinsia katika nyanja zote muhimu za uchumi. Mipango na mikakati
hiyo imelengakuondoa umasikini na kukuza uchumi kwa upana na ulinganifu (broad-based
and inclusive) ili kuwanufaisha wanawake na wanaume, watoto wa kike na wa
kiume. Kwa mfano mpango wa kuwezesha wanawake kiuchumi umelenga kifedha na pia
kuwajengea uwezo katika shughuli zao za kiuchumi. Kwa sasa halmashauri zote
nchini zinatakiwa kwa mujibu wa sheria kutenga asilimia 10 ya mapato yake ya
ndani kwa lengo la kuwakopesha bila riba wanawake (asilimia 4), vijana (asilimia
4) na watu wenye ulemavu (asilimia 2). Ingawa kiasi hicho ni kidogo
kulinganisha na mahitaji, lakini tunashuhudia matokeo yenye manufaa kwa wale
wanaozipata na kuzifanyia kazi kama walivyokusudia. Maelekezo yangu kwa halmashauri imekuwa ni
kupunguza utitiri wa vikundi na kuwapa fedha kidogo na badala yake watoe fedha
za kutosha kwa vikundi vichache ili kuweza kupata matokeo chanya na fedha hizo
ziweze kurudishwa kwa wakati.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Serikali
ya Awamu ya Tano imeamua kwa makusudi kugharamikia elimu katika ngazi ya awali,
msingi na sekondari. Jitihada hizi zimeongeza idadi ya watoto wanaosajiliwa
kujiunga na shule ambapo watoto wa kike wameendelea kuwa wengi kwenye ngazi ya
kusajiliwa katika shule za msingi na hatasekondari kwa kidato cha kwanza mpaka
cha nne. Sera hii ya elimu bure imemfungulia mtoto wa kike milango ya elimu,ikiwa
ni njia sahihi ya kumpa nyenzo za kukabiliana na mifumo kandamzi yenye
kumbagua. Changamoto kubwa kwa watoto hawa walioandikishwa ni kuwawezesha
kumaliza elimu yao na kufikia ngazi za juu. Kwa upande wa watoto wa kike, mimba
za utotoni ni changamoto nyengine kwa baadhi yaokutowezakutimiza ndoto zao, na
lengo la dira ya taifa la kuwa na taifa la wasomi.
Ili
kuhakiksha mimba za utotoni zinakoma hatuna budi jamii yote kuwajibika kuanzia kwenye
kaya zetu kwa kuondokana na mila na desturi za kumbagua au kutomthamini mtoto
wa kike. Katika shule zetu, tuendeleze kumpa nyenzo na shauku mtoto wa kike adhamirie
kutimiza ndoto zake. Kwenye ngazi hii, ipo changamoto kwa baadhi ya waalimu wa
kiumena wazazi ama walezi kutumia mamlaka yao vibaya na kuwalaghai watoto hatimaye
kupata mimba. Serikali inakemea vikali vitendo hivi na itaendelea kuchukua hatua
kali za kisheria dhidi ya wale wanaofanya vitendo hivyo.
Kwa
upande wenu ninyi kama watetezi wa haki za wanawake na watoto, tunatambua kazi
kubwa mnayoifanya,na kwa kuwa nanyi mnaishi ndani ya jamii, hamna budi kuwa
wepesi wa kuwabainisha wale wanaoendeleza vitendo vya ukiukwaji wa haki na
maadili kwa Wanawake na Watoto ili sheria ichukue mkondo wake. Tunahitaji
mshikamano wa kitaifa kukomesha vitendo vya kudhalilisha Wanawake na watoto
wetu.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Katika
kutekeleza agizo la kutoa afya bora kwa kila Mtanzania, kumekuwepo na jitihada
nyingi za kupanua huduma za afya ili kumfikia mwananchi wa kawaida hususan hudumaza uzazi salama na
afya ya mama na mtoto. Jitihada hizi zimeonesha mafanikio kwa kupunguza vifo vya
watoto kwa kiasi kikubwa. Changamoto imebaki kwenye vifo vya mama wajawazito ambavyo
ni takribani vifo 400 kati ya wamama100,000. Aidha, Serikali inaendelea na
jitihada za kuhakikisha vifo vya mama wajawazito vinapungua kwa kuendelea kujenga
zahanati, vituo vya afya na hospitali za Wilaya na zote zikiwa na wodi maalum
kwa ajili ya mama wajawazito na watoto.Hata hivyo, jukumu la usalama wa mama
wajawazito haliwezi likaachiwa serikali peke yake. Serikali inaweka miundombinu
na wataalam lakini jamii ina jukumu la kuhakikisha akinamama wajawazito wanatunzwa
na kujifungulia kwenye vituo vya afya.
Wageni
Waalikwa, Mabibi na Mabwana,
Shughuli
ya kumtua Mama ndoo kichwani inaendelea vyema, kwa sasa, maeneo mengi
yaliyokuwa na shida ya upatikanaji wa Maji yameanza kupata Maji au miradi
inaendelea. Kumekuwa na Miradi mikubwa ya Maji maeneo ya Kanda ya Ziwa kwa
kutumia Ziwa Victoria na mradi huo unatarajiwa kuhudumia mpaka maeneo ya Tabora
na Singida. Mradi wa Same Mwanga na Tanga kwa upande mwa Kaskazini mwa
Tanzania, Mradi mkubwa wa maji unaohudumia Dar es Salaam, Kisarawe, Chalinze na
Babamoyo (Ruvu Juu na Ruvu Chini), Mradi wa Arusha, Manyara, na maeneo ya
Kigoma. Pamoja na miradi hiyo mikubwa, kumekuwa na jitihada za kuchimba visima
katika maeneo yasiyo na vyanzo vikubwa vya Maji ili kupunguza uhaba wa
rasilimali hio.
Umeme
Vijijini ni mradi utakaowanufaisha sana wanawake na kazi hii inaendelea vyema.
Kwenye
suala la ushiriki wa wanawake katika meza ya maamuzi, Serikali zetu zimechukua
hatua kadhaa ili kuondoa vizingiti vinavyowazuia wanawake wasishiriki
kikamilifu katika meza ya maamuzi. Kwa mfano katika mihimili yetu mitatu ya
Dola, kumekuwa na mabadiliko makubwa ya uwiano wa kijinsia. Katika Bunge,
wanawake ni asilimia 36.7, Baraza la
Wawakilishi Zanzibar, wanawake ni asilimia 38.
Katika Mahakama ya Rufani ambayo ni
Mahakama ya juu kabisa nchini wanawake ni asilimia 38. Aidha, katika Baraza la Mawaziri la Serikali hii ya Awamu ya
Tano wanawake ni asilimia 18 wakati
Naibu Mawaziri ni asilimia 33. La kutia moyo zaidi ni kwamba kwa mara ya
kwanza katika historia kwa nchi yetu Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania ni mwanamke. Changamoto ninayoiona kwenye suala hili ni ya uchache wa
wanawake wenye uwezo kugombania nafasi mbalimbali iwe kwenye uongozi wa
kisiasa, biashara, asasi za kiraia na sekta binafsi. Ni jukumu lenu kama
watetezi wa haki za wanawake kushawishi wanawake wenye uwezo kujitokeza kwa
wingi kugombea nafasi mbalimbali katika nyaja tofauti.
Ninapokaribia
kuhitimisha hotuba yangu mniruhusu kwa mara nyingine nikupongezeni Mfuko wa
Wanawake Tanzania kwa kazi kubwa na nzuri mliyoifanya kufanikisha uzinduzi huu.
Mimi binafsi na kwa niaba ya Serikali inayoongozwa na jemedari wetu Mheshimiwa
Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania naomba niwahakikishie
kuwa tutawaunga mkono na tuko tayari kushirikiana nanyi katika shughuli zenu
zenye mnasaba wa kumtetea na kumkomboa Mwanamke na Mtoto. Wito wangu kwenu ni
kuendelea kushikamana na kutambua kwamba wanawake ni jeshi kubwa katika uchumi,
siasa na katika kuleta ustawi wa jamii zetu. Na kwamba tunao uwezo mkubwa wa
kuleta mabadiliko tunayoyataka katika kuhakikisha kuwa haki zetu tunazitetea, zinapatikana,
na hatimaye tunazilinda.
Mwisho
kabisa, napenda tena kuwashukuru waandaji wa shughuli hii kwa kunialika kuja
kufanya ufunguzi rasmi wa Kongamano hili. Bila maneno mengi zaidi, sasa natamkakuwa
KONGAMANO LA KUADHIMISHA NA KUSHEREHEKEA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI NA MIAKA
25 BAADA YA MKUTANO WA BEIJINGlimefunguliwa
rasmi. Nawatakia majadiliano mema na yenye tija.
MUNGU IBARIKI
TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
ASANTENI KWA
KUNISIKILIZA
No comments:
Post a Comment