Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraz la Mapinduzi Dk.Ali Mohmed Shein (kulia) akifuatana na mgeni wake Balozi Mdogo wa China anaefanyia kazi zake hapa Zanzibar Bw. Xie Xiaowu baada ya mazungumzo yao leo alipofika Ikulu Mjini Zanzibar
SERIKALI ya Jamhuri ya Watu wa China
imemuhakikishia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali
Mohamed Shein kuwa Watanzania wote walioko nchini China wako salama huku nchi
hiyo ikiendelea kutafuta tiba ya kudumu ya virusi vya corona.
Balozi Mdogo wa Jamhuri ya Watu wa China
anaefanyia kazi zake hapa Zanzibar Xie Xiaowu aliyasema hayo wakati alipofanya
mazungumzo na Rais Dk. Shein, Ikulu Jijini Zanzibar ikiwa ni pamoja na kumpa
taarifa ya ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona ulioanzia nchini China.
Katika maelezo yake Balozi Xie Xiaowu alimueleza Rais Dk. Shein kuwa Serikali ya Jamhuri
ya Watu wa China inaendelea na juhudi zake katika kuhakikisha maradhi yanayosababishwa
na virusi vya corona yanapatiwa tiba ya kudumu.
Balozi Xie Xiaowu alieleza kuwa Serikali ya China
chini ya kiongozi wake Rais Xi Jinping inaendelea na juhudi zake na tayari
imeanza kupata mafanikio katika kupunguza kasi ya kuenea kwa virusi vya homa ya
corona nchini humo na kuiomba Jumuiya ya Kimataifa pamoja na Shirika la Afya
Duniani (WHO) kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na China.
Hivyo, Balozi Xie Xiaowu alimueleza Rais Dk. Shein
kuwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China inaendelea kupambana na maradhi hayo
nchini humo na kumuhakikishia kuwa Watazania wote wanaoishi nchini humo
wakiwemo wanafunzi wako salama.
Aliongeza kuwa kwa vile Jamhuri ya Watu wa China
inathamini uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania nchi hiyo inaendelea kuwatunza na kuwapa huduma zote
muhimu Watanzania waliopo nchini humo kama inavyofanya kwa wananchi wake.
Balozi huyo alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa
nchi yake inaendelea kuwapa uangalizi mkubwa Watanzania wote waliopo nchini China
sambamba na kuhakikisha wanaishi kwa salama na amani hasa katika kipindi hichi
cha mripuko wa ugonjwa huo.
Aidha, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein kuwa
Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China itaendelea kutoa ushirikiano wake kwa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Afya ikiwa ni pamoja na kutoa
elimu na kinga juu ya kusambaa kwa virusi vya corana.
Alisisitiza kuwa kwa vile Zanzibar ni visiwa ambavyo
vimekuwa ni vivutio vya utalii hali ambayo inapelekea wageni kutoka mataifa
mbali mbali kuja kuitembelea, hivyo, ipo haja ya kuwekwa mikakati maalum na
kuchukua tahadhari kubwa katika kupambana maambukizi ya na virusi vya corona kutoka
kwa wageni wote wanaoingia nchini.
Balozi huyo alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli pamoja na Chama
Cha Mapinduzi (CCM) kwa kutuma salamu za pole na rambirambi kwa Rais Xi Jinping
kufuatia China kukumbwa na ugonjwa huo uliopelekea vifo pamoja na wananchi
kadhaa kuugua.
Wakati huo
huo,
Balozi Xie Xiuowu alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China kupitia Benki ya Exim imeshakuwa tayari kutoa fedha kwa ajili ya uendelezaji
wa ujenzi wa jengo la Abiria (Terminal III) la uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid
Amani Karume Zanzibar.
Balozi huyo alimueleza Rais Dk Shein kuwa
changamoto zilizokuwepo ambazo zilipelekea kuchelewesha kupatikana kwa fedha
hizo kutoka Benki hiyo ya Exim tayari zimepatiwa ufumbuzi na wakati wowote
fedha hizo zitatolewa kwa ajili ya kukamilisha taratibu za ujenzi kama
ilivyopangwa hapo mwanzo.
Aidha, Balozi huyo alimuahidi Rais Dk. Shein kuwa atahakikisha
anachukua juhudi za makusudi za kuitaka Kampuni inayojenga uwanja huo kutoka
nchini China inamaliza ujenzi wa jengo hilo kwa wakati uliopangwa na kwa kiwango
kizuri kilichokusudiwa ili kukidhi haja ya kuhudumia ndege za ndani na za
Kimataifa.
Nae Rais Dk. Shein kwa upande wake alitumia fursa
hiyo kwa kutoa pole kwa janga hilo lililoikumba nchi hiyo na kueleza kuwa
wananchi wa Zanzibar na Jamhuri yote ya Muungano wa Tanzania wako pamoja na
ndugu zao wa China katika kuwaombea.
Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar itaendelea
kushirikiana na ndugu zao wa China katika wakati wote wa shida na raha.
Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo
kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Watu wa China Xi Jinping kwa juhudi kubwa
alizozichukua yeye na Serikali yake wakiwemo madaktari pamoja na wataalamu wa nchi
hiyo katika kukabiliana na ugonjwa huo.
Katika maelezo hayo, Rais Dk. Shein
alimuhakikishia Balozi huyo wa China kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
itaendelea kutoa indhari kwa wananchi na kufanya juhudi katika kuhakikisha inajikinga na
maambukizo ya virusi vya corona.
Aidha, Rais Dk. Shein aliipongeza taarifa aliyopewa
na Balozi huyo ya upatikanaji wa fedha kutoka Benki ya Exim ya China kwa ajili
ya uendelezaji wa ujenzi wa uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume
wa (Terminal III).
Rais Dk. Shein alisema kuwa ujenzi huo hivi sasa
unaendelea na umefikia asilimia 56 baada ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kuendeleza ujenzi huo kwa fedha zake za ndani ambapo hadi sasa Serikali imeshamlipa
Mkandarasi Kampuni ya BCEG jumla ya Dola za Kimarekani milioni 22 kati ya
milioni 58 zilizokubaliwa hapo awali kwa madhumuni ya kumaliza ujenzi huo.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza
matumaini yake makubwa kuwa ujenzi wa mradi huo wa uwanja wa ndege wa Kimataifa
wa Abeid Amani Karume utakamilika kwa wakati mzuri ambapo utazidi kuimarisha
uchumi wa Zanzibar huku akipongeza azma za Serikali ya China ya kuiunga mkono
Zanzibar katika kuendeleza mradi huo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment