Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein. Atowa Salamu za Kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein alipokuwa akitoa Salamu za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa   Wananchi  wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla. Pia aliwatakia waislamu wote mfungo mwema  wa Mwezi huu wa Ramadhani kwa kufanya ibada mbali mbali ikiwemo sadaka na zaka na mengineyo  pia kuondokana na mikusanyiko isiyofaa kuyaepuka maradhi   yaliyoingia Duniani kote na kufuatana maelekezo yanayotolewa na Viongozi wao pamoja  na kujihifadhi na kuyashinda mambo mbali mbali  yanayobatilisha funga kwa ujumla. 

WAFANYABIASHARA wote wametakiwa kuendesha biashara zao kwa uadilifu na huruma na kamwe wasitumie sababu ya kuwepo kwa janga la maradhi ya COVID 19 kwa kuwawekea mazingira magumu wananchi katika kuwauzia bidhaa kwa bei kubwa hasa katika kipindi cha mwezi Mtukufu wa Ramadhanii.



Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika risala ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani aliyoitoa kupitia vyombo vya habari, ikiwa ni utaratibu wake aliuoweka kila ukikaribia mwezi huo Mtukufu kila mwaka.
Katika risala yake hiyo Alhaj Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza wafanyabiashara kwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kwamba bidhaa zote muhimu hasa za chakula zinapatikana kama kawaida tangu yalipoingia maradhi hayo na kueleza matumaini yake kwamba hali hiyo itaendelea katika mwezi wa Ramadhani na miezi mengine inayokuja.
Alhaj Dk. Shein aliwahimiza waumini wa dini ya Kiislamu kumkumbuka sana Mwenyezi Mungu na kumgtukuza pamoja na kusoma dua mbali mbali katika funga na sala zao  za faradhi na sunna katika mwezi wa Ramadhani na miezi mingene ili kuzidi kupata rehema na ulinzi wake.
Aliwaeleza wananchi kuwa mwaka huu wa 2020 mwezi Mtukufu wa Ramadhani unakaribishwa huku kukiwa na mtihani wa maradhi yanayosababishwa na virusi vya Korona vinavyojulikana kwa jina la COVID 19.
Alhaj Dk. Shein alisisitiza kuwa miongoni mwa mambo muhimu katika mapambano dhidi ya COVID 19 ni kujiepusha na mkusanyiko wa watu ingawa suala hilo limekuwa changamoto kubwa lakini ni lazima litekelezwe kwa sababu mikusanyiko ndio njia mojawapo inayosababisha maambukizo.
Aliwanasihi wananchi kuepuka mikusanyiko na kuukubali ushauri na nasaha wanazopewa kwa ajili ya kuudhibiti ugonjwa huo katika familia na jamii kwa jumla.
Hivyo, Rais Dk. Shein amewagiza Wakuu wa Mikoa na Wilaya pamoja na Masheha wahakikishe kwamba katika maeneo yao ya utawala wanavidhibiti vitendo vyote vinavyoweza kuathiri juhudi na mipango ya Serikali katika kupambana na maradhi hayo ikiwemo mikusanyiko ya watu.
Kwa kutilia mkazo suala hilo Rais Dk. Shein amewataka viongozi hao wasichelee kumchukulia hatua za kisheria mtu yeyote atakayejaribu kwenda kinyume na miongozo iliyotolewa na Serikali katika kupambana na maradhi hayo.
Aidha, Alhaj Dk.Shein aliwanasihi wananchi wote wasisikilize taarifa zisizo rasmi wanazozitoa watu wasiohusika ambao hawana mamlaka ya Kiserikali ya kutangaza taarifa za Serikali.
Aliongeza kuwa Serikali inafuatilia kwa karibu sana na kwa umakini mwenendo wa maradhi hayo nchini na tukio lolote linalohusu ugonjwa huo hapa nchini na matukio mengine yatatolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa wakati.
Alieleza kuwa hadi tarehe 22 Aprili, 2020 jumla ya wagonjwa 83 wameripotiwa kati yao watatu wamefariki na wane wamepona na wameruhusiwa kurudi nyumbani huku akisisitiza kuwa kazi ya kutoa taarifa itaendelezwa na Wizara ya Afya kwa kuzingatia utaratibu uliowekwa.
Aidha, Rais Dk. Shein alisisitiza mambo matatu muhimu ambayo yanapaswa kuzingatiwa ikiwa ni pamoja na kuyafuata na kuyatekeleza maelekezo ya madaktari na wataalamu wa afya kutokana na yote yanayoelekezwa kuhusu ugonjwa unaosababishwa na COVID-19.
Pia, alisisitiza haja ya kuyasikiliza na kuyatii kwa ukamilifu maelekezo yanayotolewa na viongozi mbali mbali wa Serikali, viongozi wa dini na wengineo kwenye jamii.
Pamoja na hayo, Alhaj Dk. Shein aliwataka wananchi kuendeleza utamaduni uliojengeka miaka mingi kwa wananchi kuchangia huduma za jamii ili lengo la kupambana na maradhi hayo liweze kufanikiwa.
Hivyo ilivyokuwa janga hilo ni tatizo la watu wote anaamini kwamba wananchi watakuwa tayari kuchangia juhudi za Serikali katika Mfuko Maalum wa kukabiliana na COVID 19, ulioanzishwa tarehe 4 Aprili, 2020.
Aliongeza kuwa Mfuko huo utasimamiwa na Wizara ya Fedha na Mipango na Akauti mbili tayari zimeshafunguliwa kwenye Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), ambapo namba yake ya Akauti alizitaja kuwa ni 0748946001 na ile ya benki ya CRDB ambayo ni 0150485100.
Kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa waliothibitika kuambukizwa na maradhi hayo Serikali imelazimika iongeze nguvu na uwezo katika kuyafuatiliya, kuyashughulikia na kuyadhibiti maradhi hayo.
Hivyo, Alhaj Dk. Shein alisema kuwa Serikali itaendelea kutimiza wajibu wake na kuongoza mapambano dhidi ya maradhi hayo ambayo yanahitaji mchango wa kila mmoja. “Tukishirikiana sote kwa umoja wetu na kila mmoja akitimiza wajibu wake bila ya shaka tutafanikiwa kuyashinda maradhi haya”, alisema Alhaj Dk. Shein.
Rais Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wote kutowanyanyapaa wale ambao waliugua maradhi ya COVID 19.
“Wakishathibitishwa na madaktari na wataalamu wetu wa afya kwamba wamepona na kuruhusiwa warudi kwenye makaazi yao ya kawaida ni wajibu wetu tushirikiane nao na tuwape moyo na maneno ya faraja ili waweze kuyakabili maisha yao ya ykila siku na shughuli zao bila ya kuwanyanyapaa”,alisema Alhaj Dk. Shein.
“Nasema haya kwa sababu hawa ni wananchi wenzetu na  ni ndugu zetu lazima tuwathamini. Inshaallah, tuwaombee kwa Mwenyezi Mungu awape nafuu na maisha bora”,aliongeza Dk. Shein.
Aidha, Alhaj Dk. Shein aliwatakia wananchi wote kheri na Baraka za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na kumuomba Mwenyezi Mungu awape nguvu na uwezo wa kuendeleza ibada za saumu na ibada nyengine zote katika Mwezi wa Ramadhani na miezi ijayo.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi kuendelea kufanya kazi kwa kasi zaidi na kwa bidii ili kupunguza athari za janga la COVID 19 ikiwa ni pamoja na kuzitumia mvua za masika zilizokwishaanza  katika kuimarisha kilimo cha mazao mbali mbali ili kuweza kukidhi mahitaji ya chakula.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.