Labels
Popular Posts
-
Mwili wa Marehemu unatarajiwa kuwasili Zanzibar majira ya mchana kwa Ndege na kuendelea na taratibu za Maziko yatafanyika katika Mtaa wa...
-
Makamanda wa JWTZ wakiwa wamebeba mwili wa Marehemu Waziri Kiongozi wa Kwanza wa Zanzibar na Brigedia Jenerali Mstaaf Ramadhani Haji Faki...
-
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduziu Mhe.Dk. Hussein Ali Mwinyi akimkabidhi Kombe la Ubingwa wa Michuano ya Mapinduzi Cup ...
-
Waziri wa Nchi Afisi ya Rais Tawala za Mikoa na Idara Maalum za SMZ Mheshimiwa Masoud Ali Mohammed amewasimamisha kazi Baadhi ya Maafisa wa ...
-
Mmiliki wa Hoteli akiongea na Waziri wa Utalii na mambo ya kale Laila Mohammed na pembeni yake ni Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini Sadifa Juma M...
-
CLICK ANY LETTER BELOW TO FILTER CENTRES BY ALPHABET ALL CENTRES A B C D E F G H I J K L ...
-
Leo tarehe 1701/2020. Kiongozi wa Chama (KC) Ndugu Zitto Zubeir Kabwe amekutana na kufanya Mazungumzo na Wajumbe wateule wa Baraza la Wawa...
-
MATOKEO YA MITIHANI YA KIDATO CHA PILI KWA MWAKA 2016 KIWILAYA MJINI MAGHARIBI "A" MAGHARIBI "B" KUSINI UNGUJA KATI...
-
The United Republic Of Tanzania National Examination Council of Tanzania Form Four Examination Results 2017/2018 The National E...

Home
HABARI
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al Hajj Dk. Ali Mohamed Shein Akitowa Salamu za Eid El Fitry leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Al Hajj Dk. Ali Mohamed Shein Akitowa Salamu za Eid El Fitry leo.
IDDI MUBARAK
BISMILLAHI RAHMANI RAHIM
Shukurani zote anastahiki
Mwenyezi Mungu Mtukufu Subhanahu Wa Taala, Muumba wa Mbingu na Ardhi
kwakuturuzuku neema ya uhai na afya, tukaweza kuikamilisha ibada ya saumu kwa
salama na amani na leo hii tunasherehekea sikukuu hii ya Idd El Fitri tukiwa na
furaha.
Ndugu Wananchi,
Kwa baraka za siku hii ya
Iddi, tunamuomba Mola wetu Mtukufu azikubali ibada zetu zote tulizozifanya
katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na miezi mengine. Kadhalika, tunamuomba
atujaaliye uwezo, ilituyatekeleze maamrisho yake na tujiepushe na makatazo
yake,tupate kufanikiwa hapa duniani na kesho mbele ya haki. Kwa hakika,
tunatamka kwa ulimi na kuitakidi kwa moyo kwamba, hapana Mola anayestahiki
kuabudiwa kwa haki isipokuwa Allah. Yeye ndiye anayemiliki uhai wetu na kwake
ndiyo marejeo yetu. Tunamuomba Allah, Azza Wa Jalla, atusamehe makosa yetu, na
turejee kwake akiwa ameturidhia.
Baada ya kumtukuza Mola wetu Mtukufu; Subhanahu Wa Taala na
kumtakia rehema na amani Mtume wetu Muhammad (SAW), natoa salamu zangu kwawananchi wote wa Zanzibar,
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja
na Waislamu duniani kote. Allah atujaalie sikukuu njema yenye furaha na amani
na aizidishie baraka nchi yetu.
Ndugu Wananchi,
Leo ni sikukuu ya Idd el
Fitri, ambapo Waislamu wa Zanzibar na wananchi wote tunaungana na wenzetu
katika mataifa mbali mbali katika kusherehekea sikukuu hii muhimu ya furaha,
ikiwa ni miongoni mwa sikukuu adhimu alizotuwekea Mwenyezi Mungu kwa kila
mwaka. Imepokelewa kutoka kwa Imam Ahmad, Hakim, Abu Daud na An-nisai kwamba
Bwana Mtume Muhammad (SAW) alipohamia Madina na kuwakuta wakaazi wake
wakisherehekea sikukuu kinyume na twaa ya Mwenyezi Mungu aliwaambia; maneno
yenye tafsiri ifuatayo:-
“Hakika
Mwenyezi Mungu amekubadilishieni sikukuu mbili, bora kuliko zenu mlizokuwa
mkizisherehekea. Sikukuu ya Idd el Fitri na Idd el Hajj.”
Kwa hivyo, tuna wajibu wa kumshukuru Mola wetu kwa kutuwezesha
kuifikia siku hii ya Idd el Fitri, tukiwa hai na wazima wa afya. Tumshukuru
Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia kusali sala ya Idd katika misikiti mbali mbali
kwa salama. Ni vyema tuendelee kuisherehekea siku hii kwa kufanya mambo yote ya
halali, pamoja na kuombeana dua za kheri, zikiwemo zile za kuwaombea wagonjwa
wetu waliomo katika nyumba zetu na hospitalini.
Tumeukamilisha Mwezi
Mtukufu wa Ramadhani, mwezi ambao una utukufu mkubwa kwa Waislamu. Huu ndio
mwezi ulioteremshwa kitabu kitukufu cha Qurani, ili uwe muongozo na uongofu
kwetu sote. Mwenyezi Mungu ametubainishia katika aya ya 185 ya Suratul Baqarah yenye tafsiri isemayo:
“Mwezi
wa Ramadhani ambao imeteremshwa ndani yake Qurani kuwa ni uongofu kwa watu, na
hoja zilizo wazi na uwongofu na upambanuzi,….”
Katika hadithi nyengine mashuhuri inayothibitisha ubora wa
Mwezi wa Ramadhani, Mtume Muhammad (S.A.W) amesema, katika tafsiri ifuatayo:
“Enyi
watu! Hakika umewaelekeeni nyinyi Mwezi wa Ramadhani kwa baraka, rehma na
msamaha, mwezi ambao ni bora mbele
ya Mwenyezi Mungu kuliko miezi yote, siku zake ni bora kuliko
siku zote, na saa yake ni bora na muhimu kuliko saa zote”.
Kwa mnasaba wa hadithi
hio, ni dhahiri kwamba ibada zote tulizozifanya katika Mwezi wa Ramadhani
zilikuwa na fadhila kubwa zaidi kuliko zile tunazozifanya katika miezi mengine.
Tumuombe Mwenyezi Mungu atujaalie tuwe miongoni mwa walionufaika na fadhila
kubwa za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani tulioukamilisha na aendelee kutudumisha
katika ibada.
Utukufu mwengine wa Mwezi wa Ramadhani ni kwamba, amali za
waja katika kufanya ibada huwa na fadhila kubwa zaidi kuliko miezi mengine,
ikiwa ni pamoja na kusamehewa makosa yote, iwapo tulifunga kwa imani na
kumtegemea Yeye, Mwenyezi Mungu. Imepokelewa kutoka kwa Imamu Al- Bukhariy na
Muslim, kwamba Mtume Muhammad (S.A.W) amesema, katika tafsiri ifuatayo:
“Atakayefunga
Ramadhani kwa imani na kutaraji malipo, ataghufiriwa madhambi yake
yaliyotangulia”
Tunamuomba Mwenyezi Mungu
Mtukufu azikubali saumu zetu, na ziwe sababu ya Yeye kutusamehe makosa yetu.
Ndugu Wananchi,
Kama mnavyofahamu kwamba
ni kawaida yetu baada ya kuikamilisha ibada ya saumu, tunaamkia na sala ya Iddi
ambayo waumini wengi hujumuika pamoja, kwa ajili ya sala hio, kwenye uwanja
uliokubaliwa rasmi na katika misikiti mingine mbali mbali ya Unguja na
Pemba. Kwa bahati mbaya, katika kipindi
hiki, nchi yetu imekumbwa na mtihani wa maradhi ya COVID-19. Maradhi haya
yameathiri mwenendo wa baadhi ya taratibu zetu za maisha na kutufanya
tuitekeleze ibada ya funga mwaka huu, katika hali maalum, tafauti na miaka
iliyopita.Tumelazimika tuziache baadhi ya taratibu na utamaduni tuliouzowea
kuufanya katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani wa mwaka huu, kama sote
tulivyoshuhudia na tunavyokumbuka. Kwa mfano, sala za jamaa na tarawehe
hazikusaliwa kama ilivyo kawaida;baadhi ya misikiti ilifungwa na hata vikao
vya itikaaf havikufanyika katika
utaratibu uliozoeleka. Vile vile, mashindano
ya Quran katika ngazi mbali mbali hayakuweza kufanyika, na tuliiacha ile
desturi yetu ya kualikana na kufutari kwa pamoja.
Katika sikukuu ya Idd El
Fitr ya mwaka huu,hatukuweza kukutana kwenye Baraza la Iddi, ambalo ni sehemu
muhimu katika historia na utamaduni
wa watu Zanzibar. Katika hali
hio, nimeona ni muhimu nitoe salamu zangu za Iddi kwa kuzungumza nanyi kwa njia
hii ya telivisheni na redio. Kwa hivyo, pokeeni salamu zangu za Idd el Fitri
Waislamu nawananchi wote wa Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa
jumla. Nakutakieni nyote na familia zenu sikukuu njema, yenye kheri na baraka
nyingi. Kwa baraka za siku hii, tumuombe Mola wetu Mlezi atuondoshee balaa na
majanga katika nchi yetu; na aizidishie nchi yetu amani na mshikamano, ili iwe
sababu ya kupiga hatua zaidi za maendeleo na ustawi wa jamii yetu.
Ndugu Wananchi,
Mafunzo makubwa
tuliyojifunza katika kipindi chote cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni uchamungu.
Maulamaa wengi wamekubaliana kuwa uchamungu ni kutekeleza maamrisho ya Mwenyezi
Mungu na kujitenga na madhambi na kila
alichokikharamisha Yeye. Hapana shaka, katika kipindi chote cha utekelezaji wa
ibada ya saumu, jamii yetu ilijipamba vazi la uchamungu kutokana na namna
tulivyodhamiria kushikana na mwendo mwema. Kwa hakika uchamungu
si kufunga na kusali tu,
bali uchamungu umekusanya mambo mengi mema,yakiwemo subira, kuhurumiana,
kupendana, uaminifu na uadilifu. Mambo yote haya yanatuwezesha kuishi vizuri
katika jamii kwa kutendeana mema, kuzitii sheria, pamoja na kufuata maadili na
maelekezo mbali mbaliyanayotolewa na Serikali, yanayolenga kutuepusha na
matatizo yanayoweza kuepukika.
Katika kipindi cha Mwezi
Mtukufu wa Ramadhani, tulijifunza subira kwa kukaa kutwa bila ya kula, kunywa
na kujinyima mambo mengine ya halali. Vile vile, tulijifunza kusubiri kwa
kujizuia na vitendo viovu na badala yake tukajitahidi kufanya mambo mema, kama
vile kujitafutia riziki za halali, kuacha kusema uongo, kusengenya, kuvaa
mavazi ya heshima yenye kufuata mafundisho ya dini na mambo mengineyo
tuliyoyaelekeza katika kumtii Mwenyezi Mungu. Kwa ujumla, subira ilihuisha
imani na utii wetu mbele ya Mola wetu. Funga zetu zilikuwa baina yetu na Mola wetu tukiwa na imani kwamba
anatuona na anayajua yote tunayoyafanya, na Yeye ndiye atakayetulipa.
Mwenyezi Mungu Mtukufu
anatuahidi malipo ya subira katika tafsiri ya sehemu ya aya ya 10 ya Surat
Azzumar kwa kumuagiza Mtume wetu Muhammad (S.A.W) atwambie, katika tafsiri
isemayo:
“Sema:………Na
ardhi ya Mwenyezi Mungu ni kunjufu. Hakika wenye subira watapewa ujira wao bila
ya hesabu”
Kwa hivyo,tumuombe Mola
wetu atulipe malipo bora kama alivyotuahidi katika aya niliyoitaja.Kadhalika,
kwa mnasaba wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani,
hadithi ya Mtume Muhammad (S.A.W) inasema, katika tafsiri ifuatayo:
“Huu
mwezi wa Ramadhani ni mwezi wa kusubiri na hakika subira malipo yake ni pepo”
Kwa mantiki hii, hatuna
budi tuendelee na mwendo huu wa kuwa na subira kwa manufaa yetu hapa duniani na
kesho akhera. Tumuombe Mwenyezi Mungu, atuwezeshe kuwa na subira, ili tupate
malipo hayo ya Pepo.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika, tulijifunza
kupendana na kuhurumiana, ambapo baadhi ya wenye uwezo waliwasaidia wananchi
wenzao wasio na uwezo katika kuwapa sadaka na zaka za aina na viwango tafauti.
Vile vile, nilipata taarifa kwamba baadhi ya wafanyabiashara waliuza bidhaa zao
kwa bei nafuu, ili kuwawezesha wananchi wenzao wanunue mahitaji yao ya
Ramadhani. Hili ni jambo jema sana na ni miongoni mwa faida za Mwezi Mtukufu wa
Ramadhani. Mwenyezi Mungu katika sehemu ya mwisho ya aya ya 2 ya Suratul Maidah
anatwambia katika tafsiri ifuatayo:
“ …..Na
saidianeni katika wema na taqwa, wala msisaidiane katika dhambi na uadui. Na
mcheni
Mwenyezi
Mungu , hakika Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuadhibu”.
Kwa hivyo, mbali
yakuongeza jitihada zetu katika kufanya ibada mbali mbali, zikiwemo kusali sala za faradhi na sunna,
kusoma Qurani, na kujizuia kufanya maovu mbali mbali,kwa kutarajia fadhila na
radhi za Mola wetu. Bila ya shaka Mwenyezi Mungu atatujaalia kupata faida
nyengine muhimu na kutuepusha na adhabu Zake kali,iwapo tutaendelea na mwenendo huu wa kupendana na
kusaidiana katika mambo mema. Tujiepushe na husda, kuchukiana na uhasama kwa
visingizio mbali mbali.Mara nyingi mambo haya husababishwa na kibri, dharau na
kejeli miongoni mwa wanaadamu. Ni khulka mbovu ambazo zinaletwa na ushawishi wa
shetani. Katika aya ya 21 ya Surat Nur, Allah Subhanahuu Wa Taala anatuonya
tusifuate ushawishi wa shetani katika tafsiri isemayo:
“Enyi
mlioamini! Msifuate nyayo za Shetani; na atakayefuata nyayo za Shetani
(atapotea) kwani yeye huamrisha mambo ya aibu na maovu;…..”
Kwa mnasaba wa aya hii,
Mola wetu Mlezi anatuzindua kuwa iwapo tutamfuata shetani tutapotea. Kwa hivyo,
tuone kwamba tabia za kuchukiana, kudharauliana na kukejeliana hazitatuletea
faida yoyote, ila zinakuwa kichocheo kikubwa cha kuharibu amani na utulivu
tulio nao. Ili tuweze kudumisha amani na ustawi wa jamii yetu, ni lazima tuyaache mambo hayo maovu. Katika hadithi ya Bwana Mtume
Muhammad(S.A.W), iliyopokelewa na Imamu Bukhariy, Kiongozi wetu huyo anatuusia
kwa kusema maneno yenye tafsiri ifuatayo:-
“Msihusudiane,
msichukiane, wala kuoneana. Na kuweni na umoja na mshikamano, mambo yatanyooka”.
Kwa hivyo, tujitahidi
katika kufungamana na wasia huo wa Mtume wetu (S.A.W), ili tunyookewe na mambo
yetu katika maisha yetu ya kila siku.
Tunamuomba Mola wetu
azidi kututia imani,mapenzi na huruma,ili tuendelee kuzishukuru neema zake, na
atudumishe katika kuyafuata maamrisho yakena tuzitii sheria za nchi yetu.
Ndugu Wananchi,
Mafunzo mengine
tuliyoyapata katika ibada ya saumu, ni uaminifu na uadilifu. Wengi wetu tulijitahidi
natulijidhatiti katika kufanya haki na kuepuka kufanya vitendo viovu kwa ajili
ya kupata radhi za Allah. Vile vile, tukumbuke kwamba tunaposhirikiana na
Serikali katika kuimarisha uchumi, kudhibiti mapato na kuzilinda rasilmali zetu
mbali mbali, ni njia moja ya uaminifu na kufanya uadilifu. Sote tuendeleze
tabia hii ya uaminifu na uadilifu katika kutekeleza majukumu yetu kwenye
familia zetu, jamii au katika dhamana tulizokabidhiwa na Serikali yetu. Tuepuke
kufanya vitendo viovu kama vile vya uonevu na hujuma ambavyo vinaweza
kutupeleka katika mustakabali mbaya.
Ni wajibu wetu
tuyaendeleze mafunzo haya tuliyoyapata katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani popote
na wakati wote katika maisha yetu ya kila siku.Katika hadithi iliyopokelewa na
masahaba wawili, nao ni, Jundub Ibn Junaida, kwa umaarufu akiitwa Abu Dharr na
Mu’adh Ibn Jabal au Abu Abdul Rahman, Bwana Mtume Muhammad (SAW), ametuhimiza
tuwe wachamungu kwa kumcha Mwenyezi Mungu wakati wote na popote tulipo. Haya
yamo katika tafsiri ya hadithi isemayo:
“Mche
Mwenyezi Mungu popote ulipo, na fuatanisha kitendo kibaya kwa kitendo kizuri,
na ishi na watu kwa uzuri”
Kwa hivyo, ni vyema
tukatanabahi kuwa mafunzo tuliyoyapata katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani,
ambayo yote yamefungamana na ucha mungu, ni wajibu wetu tuyaendeleze na
tuyadumishe wakati wote katika maisha yetu na yasiwe katika Mwezi Mtukufu wa
Ramadhani peke yake. Tuziendeleze khulka zote njema huku tukizingatia kuwa sote
ni waja wa Mwenyezi Mungu, Azza wa Jalla, Yeye ndiye tunayemtegemea na Kwake
ndio marejeo yetu.
Ndugu Wananchi,
Tumetekeleza ibada ya Saumu
mwaka huu, ikiwa tumo katika msimu wa mvua za masika. Mvua za masika za mwaka
zimenyesha zaidi ya viwango vya kawaida
katika ukanda huu wa Afrika Mashariki.
Inasemekana kuwa mvua
hizi zimefuatana na mvua za vuli
zilizonyesha kwa wingi na kwa kipindi kirefu, hali ambayo imesababisha mafuriko
hapa Zanzibar yaliyopelekea wananchi wa
maeneo mbali mbali hasa ya nje ya Mji waathirike kwa namna mbali mbali.
Natoa pole kwa wananchi
wote waliokumbwa na mafuriko na hasa wale
wote ambao nyumba na mali zao
zimeathiriwa kutokana na mvua zilizonyesha. Namuomba Mwenyezi Mungu awape
subira, nguvu na uwezo waathirika wote wa mafuriko hayo, ili waweze kurejesha
mali walizopoteza na waendelee kuishi katika hali ya kawaida na furaha.
Hivi sasa, Serikali inaendelea kufanya tathmini katika
maeneo yote ya Unguja na Pemba
yaliyoathirika, ili iweze kurejesha miundombinu iliyoharibika na ichukue
hatua nyengine za haraka, ili ione namna inavyoweza kuwahudumia walioathirika. Nawaagiza viongozi wa
Manispaa, Mabaraza ya Miji na Halmashauri waongezekasi katika kuimarisha
usafi wa Miji, ili tujikinge na maradhi
ya miripuko, ikiwa ni pamoja na
kuhakikisha kwamba tunayadhibiti maradhi ya kipindupindu.
Kwa upande mwengine, sote
tunafahamu kwamba mvua ni neema, kwa hivyo, nawahimiza wakulima waitumie neema
hio, kwa kuzidisha nguvu katika kilimo
cha mazao mbali mbali pamoja na miti ya kudumu, ilituimarishe mazingira pamoja
na kuongeza upatikanaji wa chakula
nchini.
Ndugu Wananchi,
Katika Mwezi Mtukufu wa
Ramadhani tulijifunza kufanyakazi kwa bidii, kwa lengo la kukidhi mahitaji ya
familia zetu kwa jasho letu wenyewe. Ni
wajibu wetu tuuendeleze moyo huu wa kujituma kwa njia za halali wakati
wote wa maisha yetu, kwa kadri afya zetu zinavyoturuhusu. Mara nyingi nimekuwa
nikisisitiza kwamba, ili kazi tunazozifanya ziwe na tija, ni lazima tuzifanye kwa bidii, maarifa na kwa
kuzingatia misingi ya uaminifu, na tujiepushe na tamaa na ghilba. Nawahimiza viongozi wawewabunifu ,
wenye kujiamini katika kazi kwa kutumia vizuri ujuzi, elimu na maarifa
waliyonayo. Uislamu unatufundisha kwamba uaminifu, elimu, na ujuzi ni vigezo
muhimu ambavyo mwajiri anapaswa avizingatie
wakati anapotaka kumwajiri mfanyakazi.
Tunajifunza hayo katika
maisha ya Nabii Mussa (A. S), kwamba
aliwahi kupendekezwa na mtoto wa Nabii Shuaib aajiriwe na baba yao, kwa sababu
ya nguvu (uwezo) na uaminifu aliokuwa nao. Haya yanathibitika katika Suratul
Qasas, kwenye aya ya 26, pale Mola Wetu Mtukufu anapotufahamisha katika tafsiri
isemayo:
Alisema
mmoja wa Wale wawili :
“Ewe
baba yangu! Mkodi huyu. (awe anachunga
wanyama wako badala yetu). Bila ya Shaka mbora uwezaye kumwajiri ni ambaye
mwenye nguvu, mwaminifu (Na huyu ana sifa zote hizo.)”
“Nifanye
mtazamaji wa hazina za nchi (yote) hakika mimi ni mlinzi na mjuzi hodari.”
Tuzingatie elimu na
hekima iliyomo katika aya hizo,ili
tuzidi kuhamasika kufanya kazi
kwa kutumia vizuri elimu, ujuzi, uzoefu na maarifa yetu zaidi. Nazidi
kuwahimiza na kuwakumbusha wafanyakazi wenzangu tulioko kwenye ajira ya Serikali
na katika sekta binafsi, tuithamini na tuishukuru neema ya kupata ajira kwa kutekeleza dhamana na majukumu
tuliyokabidhiwa kwa uadilifu na kwa
kuzingatia sheria na kanuni mbali mbali
zinatuongoza. Tuziheshimu mali za umma na za waajiri wetu natuhakikishe kwamba
familia zetu zinanufaika na tunavyovichuma vya halali hivi sasa na baadaye
tutakapokuwa tumeshatangulia mbele ya haki. Ni lazima tupambane na vishawishivyote vinavyoweza kututumbukiza
katika vitendo vya rushwa na ubadhirifu wa mali za umma.
Serikali kwa upande
wake itahakikisha kwamba inaendelea
kuwapatia wafanyakazi fursa za kujiendeleza kwa elimu na ujuzi zaidi, ili
kuwajengea uwezo wa kutekeleza majukumu yao kwa weledi na ufanisi. Sambamba na
utekelezaji wa azma hio, Serikali itaendelea kupambana na vitendo vya rushwa,
kwa kuwachukulia hatua za kisheria wale
wote watakaothibitika kushiriki au kuchochea vitendo vya rushwa na
ubadhirifu wa mali ya umma.
Ndugu Wananchi,
Wakati tuna furaha ya
kusherehekea Sikukuu hii ya Eid el Fitri, ni muhimu tukakumbushana na kuzingatia kwamba bado nchi
yetu imekabiliwa na janga la maradhi ya COVID 19, yanayosababishwa na Virusi
vya Korona. Maradhi haya bado yapo,
licha ya mafanikio ya kuridhisha tunayoendelea kuyapata kutokana najitihada
mbali mbali zinazochukuliwa na Serikali kwa kushirikiana na Taasisi mbali mbali.Tunafarijika
kuona namna wananchi walivyokuwa imara katika kupambana na COVID-19 kwa
kuzingatia maelekezo yanayotolewa wakati wote, mambo ambayo yamechangia kwa
kiasi kikubwa kupunguza kiwango cha
maambukizo katika sehemu zote za Unguja na Pemba. Hadi
tarehe 20 Mei, 2020, jumla ya wagonjwa 34 walioambukizwa maradhi hayo
wanaendelea kupata matibabu katika
vituo vitano tulivyovianzisha, kutoka
miongoni mwa idadi yawagonjwa 134 iliyowahi kufikiwa tarehe 1 Mei, 2020.Wagonjwa wote hao wanaendelea
vizuri na hapana mwenye hali mbaya.
Licha ya sababu mbali
mbali za kitaalamu, ambazo zinaaminika kuhusiana na kuibuka ghafla kwa maradhi
haya ya COVID-19; hata hivyo, Mwenyezi Mungu katika Quran ametuelezea kwamba
misukosuko itatukuta katika maisha. Katika Aya ya 155 ya Surat Al Baqarah, Mola
Mtukufu anatueleza juu ya mitihani ya aina hio katika tafsiri isemayo:
“Na
tutakutieni katika msukosuko wa ( baadhi ya mambo haya), hofu
na njaa na upungufu wa mali na wa watu na matunda. Na wapashe habari njema wanaosubiri.”
Kwa hivyo, pamoja na
vifaa na ujuzi wa wataalamu wetu, inatupasa tuongeze nguvu katika kutumia umoja
wetu na mshikamano tulionao, maelewano, bidii,subira na tuendelee kushirikiana katika
kupambana na ugonjwa huu na katika ibada zetu tuendelee kumuomba Mola wetu
Mtukufu kama tunavyomuomba wakati wote, ili atupe ushindi katika vita
hivi na atukinge na kila janga na balaa.
Tunapaswa tuzingatie kwamba
jitihada zetu hizo zinahitaji zaidi usikivu wetu katika kufuata maelekezo na
kuiheshimu miongozo inayoendelea kutolewa na Viongozi wa Serikali,Madaktari na Wataalamu
wetu wa afya. Hatuna budi, ni lazima tuyatekeleze
mambo tunayoelekezwa naWakuu wa Mikoa,
Wilaya, Mabaraza ya Miji na Manispaa, Halmashauri na viongozi katika ngazi
mbali mbali. Tuendelee kujenga ujasiri
na kuondoa hofu katika mapambano yetu dhidi ya ugonjwa wa COVID 19. Tuendelee
kufanya shughuli zetu, ili tuweze kuchangia katika kuimarisha uchumi wetu ambao
umepata changamoto tanguyalipoingia
maradhi haya.
Ndugu Wananchi,
Kwa mara nyengine, natoa
pongezi zangu za dhati kwa Mwenyekiti wa Kamisheni ya Kupambana na Maafa ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, ambaye ni
Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar
pamoja na wajumbe wote, na Mwenyekiti wa
Kamati ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ya Kupambana na Maradhi haya
ya COVID 19, Mheshimiwa Kassim Majaaliwa Majaaliwa, ambaye ni Waziri Mkuu wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; pamoja na wajumbe wote, kwa kufanya kazi nzuri
kwa kushirikiana na uzalendo wa hali ya
juu.Mambo yote waliyoyafanyia kaziyametoa
matokeo mazuri, katika kuwahudumia wananchi wa pande zote mbili za
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Vile vile, shukurani
zangu nazitoa kwa viongozi wengine mbali mbali wa Serikali, vyombo vya ulinzi
na usalama; viongozi wa dini, wafanyabiashara,
madereva wa vyombo vya usafiri wa nchi kavu na baharini na wananchi wote kwa jumla kwa kuziunga mkono
juhudi za Serikali katika kupambana na maradhi haya. Kila Taasisi ilitekeleza
wajibu wake kwa kulingana na majukumu na uwezo wa Taasisi hio.Kadhalika, shukurani
zangu za dhati nazitoa kwa madaktari na wataalamu wa afya, ambao tangu
yalipoanza maradhi haya, wamekuwa wakifanya juhudi kubwa za kutoa elimu kwa
wananchi, pamoja na kuwapa huduma mbali mbali wale wote walioathirika au walioonesha
dalili za maradhi hayo.
Kadhalika, navipongeza vyombo
vya habari mbali mbali kwa kufanya kazi kubwa ya kuendelea kuwaelimisha
wananchi kuhusu maradhi haya. Nawahimiza
waandishi wa habari waendelee na ari na uzalendo wa kuyalinda maslahi ya nchi yetu, kwa kufanya
kazi kwa kuzingatia maadili yao.
Natoa pole kwa wananchi
wote waliopata msiba kwa kuondokewa na ndugu na jamaa zao kutokana na maradhi
ya COVID-19, Mwenyezi Mungu awape subira na wale wote waliokwishatangulia mbele
ya haki kutokana na maradhi haya, Mwenyezi Mungu awalaze mahala pema peponi.Amin.
Ndugu Wananchi,
Kutokana natamko rasmi la
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar lililotolewa tarehe 19 Machi, 2020, kuhusu
hali ya ugonjwa wa COVID 19 hapa Zanzibar, na mambo kumi muhimu yaliyopaswa yatekelezwe,
katika kuwahudumia waathirika wa maradhi hayo na kuyadhibiti Maambukizo yake. Vile vile,kwakuzingatia hali ya maradhi na
mwenendo wake ulivyo, Serikali ya Mapinduziya Zanzibar inakusudia kuregeza
masharti yaliyowekwa hapo awali katika mambo hayo kumi, hatua kwa hatua. Hata hivyo, uamuzi wa kuregeza masharti hayo kwa
upande wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar utatolewa wakati wowote kuanzia
sasa.
Ndugu Wananchi,
Kuanzia tarehe 6 Mei,
2020, Baraza la Wawakilishi la Zanzibar lilianza vikao vya kutekeleza majukumu
yake ya Kikatiba ya kupitisha Bajeti ya Serikali ya mwaka 2020/2021. Hadi leo, tunaposherehekea Sikukuu ya Idd El
Fitri tayarijumla ya Wizara nane (8) zimeshawasilisha makadirio ya mapato na
matumizi ya Wizara zao. Bajeti kuu ya Serikali itawasilishwa tarehe 15 Juni,
2020. Nakuhimizeni wananchi muendelee kufuatilia vikao hivyo, ilimuweze
kuifahamu kwa undani mipango mbali mbali ya maendeleo ya nchi yetu iliyopangwa
na Serikali kwa mwaka wa fedha wa 2020/2021.
Natoa pongezi kwa
Mheshimiwa Zubeir Ali Maulid, Spika wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, na
Waheshimiwa Wawakilishi wote, kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kuwawakilisha wananchi na kuisimamia
Serikali. Nimekuwa nikifuatilia mijadala ya vikao vya Baraza na nimeridhishwa
sana na michango ya Waheshimiwa Wajumbe inayoonesha wazi dhamira yao ya
kuongeza kasi na kuimarisha jitihada za maendeleo ya nchi yetu.
Kadhalika, natoa shukurani kwa viongozi wa Serikali
katika Baraza la Wawakilishi, wakiongozwa na Mheshimiwa Makamo wa Pili wa Rais,
kwa namna wanavyoiwakilisha Serikali na kujibu hoja za Waheshimiwa Wawakilishi.
Nalitakia Baraza letu kila la kheri na mafanikio katika kumalizia kazi yao hio
ya kikatiba kwa wizara wanazoendelea nazo.
Vile vile, naipongeza
Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), kwa jitihada zao za kuwasambazia maji wananchi
katika kipindi chote cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa wale
waliokuwa hawapati huduma hizo. Nawahimiza viongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) wahakikishe
kwamba miradi mikubwa ya maji safi na salama
tuliyoitekeleza kwa ufanisi hivi karibuni, inatoa tija iliyokusudiwa kwa
wananchi. Wananchi tuna wajibu wa kushirikiana na ZAWA katika kuilinda
miundombinu ya miradi ya maji, ili tuhakikishe kuwa miradi hio inakidhi lengo
la Serikali lililokusudiwa kwa maslahi ya wananchi wote.
Ndugu Wananchi,
Tunamshukuru Mwenyezi
Mungu kwa kutuwezesha kufunga mwezi wa Ramadhani bila ya kuwepo tatizo la
bidhaa muhimu za chakula, licha ya kuwepo kwa changamoto ya maradhi ya COVID 19.
Natoa pongezi kwa Wafanyabiashara, wakulima, wavuvi na wafugaji kwa
kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha kwamba nchi yetu inakuwa
na chakula cha kutosha wakati wote.
Kadhalika,natoa shukurani
zangu za dhati kwa wananchi waliotoa zaka na sadaka kwa ajili ya
kuwakirimu wananchi wengine na ndugu zao
wenye kustahiki kupata haki na riziki hizo. Bila ya shaka, waliofanya hivyo
wana ujira mkubwa kwa Mola wetu Mlezi, kama alivyotuambia katika Surat Al
Baqarah kwenye aya ya 262, katika tafsiri isemayo:
“Wale wanaotoa mali zao kwa njia ya Mwenyezi Mungu,
kisha hawafuatishii- waliyoyatoa-
masumbulizi wala udhia, wao wana ujira wao kwa Mola wao, wala haitokuwa khofu
juu yao wala hawatahuzunika”.
Tunamuomba Mwenyezi Mungu
atuzidishie imani na hamu ya kutoa kwa yale aliyoturuzuku, ili tupate
radhi zake na ujira mkubwa hapa Duniani na Akhera tuendako.
Nawahimiza wazazi na walezi tuendelee kusimamia malezi,
usalama na afya za watoto wetu katika Sikukuu hii, ambapo viwanja vya kufurahishia
watoto vimefungwa. Tusiwaachie watoto wakaranda ovyo mitaani na tujuwe mahali
maalumu walipo na nini wanachofanya, ili tuweze kuzilinda afya zao na usalama
wao.
Namalizia hotuba yangu
kwa kukutakieni nyote sikukuu njema yenye furaha na amani. Tumuombe Mola wetu Mtukufu atuzidishie amani,
umoja na mshikamano. Aizidishie neema
nchi yetu na atupe uwezo mkubwa zaidi wa
kupanga na kuitekeleza mipango yetu ya maendeleo. Atupe neema ya mvua zenye
kheri na atukinge na maradhi pamoja na majanga mbali mbali. Namuomba Mwenyezi
Mungu atuondoshee balaa hili la maradhi ya COVID-19, na tuweze kurudi katika
hali zetu za kawaida, katika kuendesha maisha yetu.
IDD MUBARAK
WAKULLU AAMUN WAANTUM BIKHAYR
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
Subscribe to:
Post Comments (Atom)
BLOGU RAFIKI
-
-
Ufungaji wa Tamasha la saba la Biashara, Serikali kushirikiana na wafanya biashara - *Issa mzee Maelezo 18/01/2021* Kaimu Waziri wa Biashara na Maendeleo ya Viwanda Mh Mudrik Ramadhan Soraga amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar...4 hours ago
-
MAHOJIANO YA TAUSI SUEDI NA AMRI NGOYE KUHUSU CSI KUPITIA KWANZA PRODUCTION NCHINI MAREKANI - Pata habari motomoto kupitia facebook kwa kulike huu ukurasa wetu https://www.facebook.com/pages/Pamojapureblogspotcom/312633955485619?ref=hl2 years ago
-
Matukio : Waziri, Dk. Kigwangalla afuturisha wabunge Dodoma, asisitiza Upendo, Umoja na Mshikamano wa kitaifa. - Waziri wa Maliasili na Utalii, Dkt. Hamisi Kigwangalla (kushoto) akimkaribisha Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Ndugai nyumbani kwa...2 years ago

Popular Posts
-
The United Republic Of Tanzania National Examination Council of Tanzania Form Four Examination Results 2017/2018 The National E...
-
Mwili wa Marehemu unatarajiwa kuwasili Zanzibar majira ya mchana kwa Ndege na kuendelea na taratibu za Maziko yatafanyika katika Mtaa wa...
-
Na Miza Kona/Rahma Khamis Maelezo-Zanzibar Jumla ya wanafunzi 16,744 wamechaguliwa kuendelea masomo ya kidatu cha tatu kati ya wanafun...
-
Makamanda wa JWTZ wakiwa wamebeba mwili wa Marehemu Waziri Kiongozi wa Kwanza wa Zanzibar na Brigedia Jenerali Mstaaf Ramadhani Haji Faki...
-
TAARIFA YA MATOKEO YA MITIHANI YA TAIFA YA KIDATO CHA PILI, DARASA LA SITA NA DARASA LA NNE YA MWAKA 2017, JUMATATU TAREHE 29 JANUARI 2018....
-
Meneja Mwendeshaji wa kampuni ya Shamy Tours and Travel Agent Zanzibar, Bw. Khamis Mwinjuma Simba akitoa maelezo ya shughuli mbalimbali z...
-
Na Tatu Makame, Laylat Khalfan WATU wawili akiwamo askari mmoja wamenusurika kifo baada ya kupigwa risasi na watu wanaosadikiwa kuwa ni...
-
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) Mhe. Jesha Salim Jecha akitangaza Matokeo ya Kura za Urais za Majimbo mawili ya Fuon...

No comments:
Post a Comment