Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.
Harrison Mwakyembe akifuatilia nyimbo za taifa kutoka Tanzania na Nchi
wanachama wa SADC muda mfupi kabla ya kufugua Mkutano huo uliofanyika kwa njia
ya video katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es
Salaam, Tanzania, kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt.Hassan Abbasi na
Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari-MAELEZO, Bi. Zamaradi Kawawa.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na
Michezo, Dkt.Hassan Abbasi akifafanua Jambo kwa Waziri wa Wizara hiyo Dkt.Harrison
Mwakyembe kabla ya kufungua Mkutano wa Kamati ya Kutafuta Washindi wa Tuzo za
Waandishi wa Habari za SADC uliofanyika kwa njia ya video katika Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.
Harrison Mwakyembe akifungua Mkutano wa Kamati ya Kutafuta Washindi wa Tuzo za
Waandishi wa Habari za SADC uliofanyika kwa njia ya video katika Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania.
(Picha na Idara ya Habari-MAELEZO)
Na Mwandishi Wetu-MAELEZO.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison
Mwakyembe amesema Jumuiya ya maendeleo ya
Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) imeendelea kutambua mchango mkubwa wa
wanahabari kwa nchi wanachama wa ukanda huo.
Akizungumza katika Ufunguzi wa Mkutano wa Kamati ya
Kutafuta Washindi wa tuzo za Wanahabari wa Habari za SADC uliofanyika katika
kituo cha mikutano cha kimataifa cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam,
Waziri Mwakyembe alieleza kuwa uongozi wa SADC chini ya Mwenyekiti wake Rais wa
Tanzania Dkt. John Magufuli unaendelea kuwathamini waandishi wa habari katika
ukanda huo wa Afrika.
“SADC chini ya uenyekiti wa Mhe, Dkt. Magufuli
inaendeleza utamaduni wake wa kutambua mchango mkubwa wa wanahabari katika nchi
wanachama sio tu katika kuandika habari njema za SADC kama vile za utekelezaji miradi ya maendeleo
na sera bali pia katika kuelimisha na kuhabarisha wanachi wakati wa majanga
mbalimbali yakiwemo ya milipuko ya magonjwa, vimbuga, vurugu katika jamii, ukame pamoja na uvamizi
wa nzige”, Alisema Dkt. Mwakyembe.
Alisema kuwa waandishi wa habari wametumia vyema njia
mbalimbali za kutoa habari zikiwemo mitandao ya kijamii, Redio, Televisheni na
Magazeti katika kutekeleza majukumu yao ya kusambaza taarifa sahihi na za kweli
kwa umma kuhusu mwenendo wa ugonjwa wa Covid-19 uliozikumba nchi za ukanda wa
SADC, kwani kazi hiyo ya kuelimisha wananchi ukanda wa SADC imekuwa nzuri na
inapaswa kuthaminiwa kwa nchi zote za SADC.
Waziri Mwakyembe aliwashukuru waandishi wa habari kwa
kutekeleza majukumu makubwa ya kuwahabarisha wananchi katika Mkutano Mkuu
wa 39 wa Wakuu wa Nchi za SADC uliofanyika mwezi Agosti mwaka jana na kuhudhuliwa
na wakuu wa nchi wanachama takribani 16.
“Napenda kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu za
dhati kwa waandishi wa habari wote walioshiriki kutoa taarifa za Mkutano sa 39
wa Wakuu wa Nchi na Serikali za SADC, uliofanyika Jijini Dar es Salaam,
Tanzania Mwezi Agosti mwaka jana”, Alisema Dkt.Mwakyembe.
Aidha, Dkt.Mwakyembe ameipa kamati hiyo muda wa siku mbili
ili kuweza kuwapata washindi wa tuzo hizo ambapo kamati hiyo imepokea kazi
za magazeti 9, Televisheni 5, Redio 8
na picha 6, na ameitaka kamati hiyo
kuchakata majina hayo kwa umakini na weledi mkubwa ili kuwezesha upatikanaji wa
washindi wenye kazi bora.
Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Hassan Abbasi alisema kuwa
mpaka sasa kazi zilizopokelewa na kamati hiyo zinakidhi kuingia katika
ushindani ambao kila mmoja ataweza kupata nafasi ya kushindana na ubora wa kazi
yake baina ya washiriki kutoka ukanda huo wa Afrika.
“Mpaka sasa kazi zilizopokelewa na ambazo zitafanyiwa
mchakato ni kazi 28 amabapo kazi za magezeti ni 9, Televisheni kazi 5, Redio
kazi 8 na picha 6 na kazi hizi zimepokelewa kutoka nchi mbalimbali wananchama
wa SADC, kwa hiyo kamati ipo kutekeleza jukumu la kutupatia washindi wenye kazi
bora kwa kuwa kazi zote zimekidhi ushindani”, Alisema Dkt.Abbasi.
Jumuiya hiyo ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika
(SADC), inatimiza miaka 40 tangu kuanzishwa kwake na kuziweka nchi 16 za ukanda
huo wa Afrika kuwa na ushirikiano katika masuala mbalimbali yakiwemo ya
kiuchumi.
No comments:
Post a Comment