Habari za Punde

Dkt.Mwakyembe: SADC Inatambua Mchango wa Wanahabari wa Ukanda Huu wa Afrika

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akifuatilia nyimbo za taifa kutoka Tanzania na Nchi wanachama wa SADC muda mfupi kabla ya kufugua Mkutano huo uliofanyika kwa njia ya video katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania, kulia ni Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt.Hassan Abbasi na Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Habari-MAELEZO, Bi. Zamaradi Kawawa.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.Hassan Abbasi akifafanua Jambo kwa Waziri wa Wizara hiyo Dkt.Harrison Mwakyembe kabla ya kufungua Mkutano wa Kamati ya Kutafuta Washindi wa Tuzo za Waandishi wa Habari za SADC uliofanyika kwa njia ya video katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt. Harrison Mwakyembe akifungua Mkutano wa Kamati ya Kutafuta Washindi wa Tuzo za Waandishi wa Habari za SADC uliofanyika kwa njia ya video katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Tanzania.
(Picha na Idara ya Habari-MAELEZO)

Na Mwandishi Wetu-MAELEZO.                                                                                              
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dkt.Harrison Mwakyembe amesema Jumuiya ya maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC) imeendelea kutambua mchango mkubwa wa wanahabari kwa nchi wanachama wa ukanda huo.

Akizungumza katika Ufunguzi wa Mkutano wa Kamati ya Kutafuta Washindi wa tuzo za Wanahabari wa Habari za SADC uliofanyika katika kituo cha mikutano cha kimataifa cha Julius Nyerere Jijini Dar es Salaam, Waziri Mwakyembe alieleza kuwa uongozi wa SADC chini ya Mwenyekiti wake Rais wa Tanzania Dkt. John Magufuli unaendelea kuwathamini waandishi wa habari katika ukanda huo wa Afrika.

“SADC chini ya uenyekiti wa Mhe, Dkt. Magufuli inaendeleza utamaduni wake wa kutambua mchango mkubwa wa wanahabari katika nchi wanachama sio tu katika kuandika habari njema za SADC  kama vile za utekelezaji miradi ya maendeleo na sera bali pia katika kuelimisha na kuhabarisha wanachi wakati wa majanga mbalimbali yakiwemo ya milipuko ya magonjwa, vimbuga,  vurugu katika jamii, ukame pamoja na uvamizi wa nzige”, Alisema Dkt. Mwakyembe.

Alisema kuwa waandishi wa habari wametumia vyema njia mbalimbali za kutoa habari zikiwemo mitandao ya kijamii, Redio, Televisheni na Magazeti katika kutekeleza majukumu yao ya kusambaza taarifa sahihi na za kweli kwa umma kuhusu mwenendo wa ugonjwa wa Covid-19 uliozikumba nchi za ukanda wa SADC, kwani kazi hiyo ya kuelimisha wananchi ukanda wa SADC imekuwa nzuri na inapaswa kuthaminiwa kwa nchi zote za SADC.

Waziri Mwakyembe aliwashukuru waandishi wa habari kwa kutekeleza majukumu makubwa ya kuwahabarisha wananchi katika Mkutano Mkuu wa  39 wa Wakuu wa Nchi za SADC  uliofanyika mwezi Agosti mwaka jana na kuhudhuliwa na wakuu wa nchi wanachama takribani 16.

“Napenda kutumia fursa hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa waandishi wa habari wote walioshiriki kutoa taarifa za Mkutano sa 39 wa Wakuu wa Nchi na Serikali za SADC, uliofanyika Jijini Dar es Salaam, Tanzania Mwezi Agosti mwaka jana”, Alisema Dkt.Mwakyembe.

Aidha, Dkt.Mwakyembe ameipa kamati hiyo muda wa siku mbili ili kuweza kuwapata washindi wa tuzo hizo ambapo kamati hiyo imepokea kazi za   magazeti 9, Televisheni 5, Redio 8 na  picha 6, na ameitaka kamati hiyo kuchakata majina hayo kwa umakini na weledi mkubwa ili kuwezesha upatikanaji wa washindi wenye kazi bora.

Kwa Upande wake Katibu Mkuu wa  Wizara hiyo, Dkt. Hassan Abbasi alisema kuwa mpaka sasa kazi zilizopokelewa na kamati hiyo zinakidhi kuingia katika ushindani ambao kila mmoja ataweza kupata nafasi ya kushindana na ubora wa kazi yake baina ya washiriki kutoka ukanda huo wa Afrika.

“Mpaka sasa kazi zilizopokelewa na ambazo zitafanyiwa mchakato ni kazi 28 amabapo kazi za magezeti ni 9, Televisheni kazi 5, Redio kazi 8 na picha 6 na kazi hizi zimepokelewa kutoka nchi mbalimbali wananchama wa SADC, kwa hiyo kamati ipo kutekeleza jukumu la kutupatia washindi wenye kazi bora kwa kuwa kazi zote zimekidhi ushindani”, Alisema Dkt.Abbasi.

Jumuiya hiyo ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), inatimiza miaka 40 tangu kuanzishwa kwake na kuziweka nchi 16 za ukanda huo wa Afrika kuwa na ushirikiano katika masuala mbalimbali yakiwemo ya kiuchumi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.