Na Jovina Bujulu, MAELEZO Dar es Salaam
Mkurugenzi wa Uchaguzi
Dkt. Wilson Mahera ametoa wito kwa watoa huduma za habari mitandaoni (online
media), kuwasisitiza na kuwahimiza wadau na wananchi kwa ujumla kuzingatia
Sheria za Uchaguzi, Kanuni na Maelekezo ya Tume katika kipindi hiki ambapo
Taifa liko katika kampeni za uchaguzi kuelekea katika uchaguzi wa Rais, Wabunge
na Madiwani Oktoba 28, 2020 ili uchaguzi uwe wa amani na utulivu.
Aidha, amewashukuru kwa
kuiwezesha Tume kutekeleza majukumu yake na kuiwezesha kuwa karibu na wadau wa
uchaguzi kwa njia ya taarifa na kutoa habari kwa wakati na kuiwezesha Tume
kutumia mitandao kwa kutoa ya elimu ya mpiga kura pamoja na kufafanua hoja
mbalimbali kutoka kwa wadau.
“Ipo mitandao ambayo
imetoa nafasi ya kuchapisha, kutangaza habari, na makala za kuelimisha umma
kuhusu Tume na majukumu yake, kupitia redio na runinga za mitandaoni, tume
imeshiriki vipindi mbalimbali kwa lengo la kutoa elimu kwa wapiga kura”,
amesema Dkt. Mahera.
Kipindi cha kampeni
kuelekea uchaguzi katika taifa lolote duniani ni hatua muhimu ambapo wananchi
wanatakiwa kuwa wamoja na kuonesha mshikamano ili kuepuka vurugu na fujo zisizo
na tija ambazo zinaweza kuchochewa na vyombo vya habari, iwe ni magazeti, runinga
au mitandao ya kijamii kwa kuchapisha au kutangaza habari zenye viashiria vya
uchochezi.
Hiki ni kipindi
kinachokuwa na joto kali la kisiasa linalotokana na baadhi ya watu kukosa
uvumilivu wa kisiasa, hali ambayo inaweza kuhatarisha amani na utulivu wa nchi.
Katika kipindi hiki vyombo vya habari vinapaswa kuwa makini kwa kuhakikisha
haviwi chanzo cha joto hilo kwa kuzingatia misingi na maadili ya kazi zao.
Dhamana ya vyombo vya
habari katika kipindi hiki ni kuhakikisha vinajiepusha kutumiwa na watu
wasioitakia mema nchi yetu kwa kujikita katika majukumu yao ya msingi ambayo ni
kuhabarisha na kuliemisha wananchi kupitia vyombo mbalimbali vya habari
yakiwemo magazeti, redio, runinga na mitandao ya kijamii.
Hivyo, ni jukumu la
vyombo hivi kuwa na umakini mkubwa sana ili kuhakikisha vinawatendea haki
wananchi wake kwa kuwapasha habari wanazotakiwa kuzisikia na kuzisoma ikiwa ni
pamoja na maendeleo yaliyofanywa na viongozi wao na wanayotarajia kuyafanya pamoja na na kuwapa nafasi wagombea uongozi
kunadi sera na Ilani za vyama vyao.
Dkt. Mahera amesema
Tume inawatambua watoa huduma za mitandao kwa kuwa wanatumika kama daraja
linalounganisha Tume na wadau kwa njia ya mawasiliano na pia kama mojawapo wa
wadau muhimu wa uchaguzi wenye dhamana ya kuhabarisha wananchi.
Dkt. Mahera amesema
hayo wakati wa kikao kati NEC na watoa huduma ya habari wakiwemo ‘Blogers’
pamoja na runinga (TV) na redio za mtandaoni kutoka maeneo mbalimbali nchini kilichofanyika
hivi karibuni jijini Dar-es-Salaam.
“Tume inaamini kuwa
mkipata uelewa mzuri wa michakato ya uchaguzi, basi itakuwa rahisi kwenu
kuwaelimisha na kuwahabarisha wananchi kupitia vyombo vyenu vya habari ili
kushiriki kikamilifu katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2020”, amesema Dkt. Mahera.
Kutokana na kukua kwa
teknolojia, vyombo vya habari vya mitandao vimekuwa vikitoa habari kwa uharaka
zaidi kuliko vyombo vya habari vilivyozoeleka kwa jamii hasa magazeti ambayo
habari zake huwa zinasomwa siku inayofuata. Hivyo, mabadiliko hayo wakati
mwingine yanawafanya vyombo vya habari vya mitandao kukosa umakini na wakati
mwingine kuandika habari zenye kupotosha jamii.
Kipindi hiki cha
kuelekea uchaguzi, watoa huduma ya habari za mtandao wanatakiwa kuwa makini
zaidi kwa kuwahamasisha wananchi hasa wapiga kura kushiriki katika kampeni ili
waweze kuwapima sera za wagombea na hatimaye kujitokeza kwa wingi kupiga kura.
Ili kuhakikisha
wanaandika, kuchapisha au kutangaza habari zenye ulinganifu, watoa huduma ya
habari mtandaoni wanatakiwa kutoa kipaumbele kwa masuala yanayoelekea kujenga
umoja wa kitaifa badala ya kutoa habari zinazochochea vurugu huku wakizingatia
kuwa Tanzania sio kisiwa na kwamba wasipotumia vizuri taaluma yao wanaweza
kuingiza nchi kwenye machafuko kama ilivyotokea katika baadhi ya nchi.
Vyombo vya habari,
vinatakiwa kuwa na uvumilivu wanapotafuta habari kuhusu uchaguzi kwa kutafuta
ufafanuzi kutoka katika chombo kinachohusika ambacho ni Tume ya Taifa ua
Uchaguzi (NEC), ambacho kimeahidi kuwapa ushirikiano wa kutosha pale
watakapohitaji ili kuhakikisha Watanzania wanapata taarifa sahihi na kwa
wakati.
Kwa upande wake,
Kamishna wa NEC, Asina Omari aliwakumbusha watoa habari hao kuwa vyombo vyao ni
muhimu kwa wapiga kura na kuwasisitiza wao wenyewe pia wazingatie majukumu yao
ya msingi.
Fauka ya hayo,
amewataka watoe elimu ya uchaguzi kufuatana na muktadha wa vyombo vyao, kutoa
habari kutoka kwenye vyanzo sahihi na wawe na taarifa sahihi kabla
hawajachapisha au kutangaza jambo lolote kuhusu mchakato mzima kabla ya uchaguzi,
wakati wa uchaguzi hata baada ya uchaguzi ili sote tubaki tukiwa Watanzania.
Naye Mkurugenzi
Msaidizi Habari na Elimu ya Mpiga Kura kutoka NEC, Dkt. Cosmas Mwaisobwa amewahimiza
watoa huduma hao watambue wajibu wao wa kuchapisha na kutangaza habari za mchakato
wa uchaguzi, mahali pa kupigia kura, haki na wajibu wa mpiga kura ni masuala
muhimu ya kuwaelimisha wananchi kuhusu Sheria, Kanuni na Taratibu za Uchaguzi
ili waweze kutumia haki yao ya msingi ya kupiga kura na hatimaye kupata viongozi
bora nchini.
Aidha, amevitaka vyombo
hivyo kuwa na uelewa juu ya mamlaka na majukumu ya NEC ikiwa ni pamoja na
uanzishwaji wa Tume Kikatiba, uteuzi wa viongozi wa Tume na utofauti wa
uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaosimamiwa na TAMISEMI na Uchaguzi Mkuu wa
Rais, Wabunge na Madiwani pamoja na kuwa
na ufahamu kuhusu Sheria za Uchaguzi na
matakwa yake.
Dkt. Mahera amesema
kwamba Daftari la Kudumu la Wapiga Kura lina jumla ya wapiga kura 29,188,347 na
vituo vya kupiga kura 80,155 ambapo kila kituo kitakuwa na wapiga kura
wasiozidi 500.
MWISHO
No comments:
Post a Comment