Habari za Punde

LIPUMBA ATAHADHARISHA “UCHAGUZI USIWE CHANZO CHA UVUNJIFU WA AMANI NCHINI”

Mgombea udiwani wa kata ya Kihanga kwa tiketi ya CUF Bi,Anastella Kibake akimwombea kura kwa kupiga magoti, Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CUF na mwenyekiti wa chama hicho Prof.Ibrahimu Lipumba katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kihanga.
Wananchi na wakazi wa mji wa Kayanga wilayani Karagwe waliojitokeza kumsikiliza Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CUF na mwenyekiti wa chama hicho Prof.Ibrahimu Lipumba katika mkutano wa kampeini.

Na Allawi Kaboyo Karagwe.

Wakati Tanzania ikiwa katika kipindi muhimu cha uchaguzi mkuu wa madiwani,wabunge na Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania ambapo vyama vya siasa vimejitokeza kugombea nafasi hizo, Mgombea urais kwa tiketi ya CUF Prof. Ibrahimu Lipumba, amesema uchaguzi huu usiwe chanzo cha uvunjifu wa amani ya Tanzania.

Lipumba ametoa kauli hiyo leo septemba 24, mwaka huu kwenye mkutano wake wa hadhara wa kuomba kura katika uwanja wa changalawe uliopo mjini Kayanga wilaya ya Karagwe mkoani Kagera ambapo amesema Tanzania imekuwa kisiwa cha amani kwa kipindi kirefu hivyo watanzania wanao wajibu wa kuhakikisha amani hiyo inadumu hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi.

Amesema kuwa vyama vya siasa vinatakiwa kuwa mfano wa kuigwa katika kuhubiri amani huku akiomba tume ya uchaguzi nchini kuhakikisha inasimamia uchaguzi huu unakuwa wa huru na haki suala litakalopelekea nchi kudumu katika amani kwa kuwa haki itatendeka.

“Amani hii tuliyonayo tunapaswa kuilinda na kuhakikisha inadumu, niiombe tume yetu ya uchaguzi ihakikishe uchaguzi huu unakuwa wa huru na haki na ikifanya hivyo hakika amani yetu itastawi katika misingi ya tuliyoasisiwa, CUF tunaamini katika amani na sera yetu imejikita katika haki sawa kwa wote” Amesisitiza Prof. Lipumba.

Ameongeza kuwa anatambua pia wananchi wa wilaya ya Karagwe wanazo changamoto nyingi ikiwemo kero sugu ya maji pamoja na migogoro ya ardhi inayowapelekea wengi wao kupoteza haki na hivyo kuwaomba wanankaragwe kumchagua ili kuweza kuwasaidia kutatua kero hizo kwa muda mfupi.

Hata hivyo mgombea udiwani kata ya Kihanga wilayani humo kupitia chama hicho Bi,Anastella Kibake, amemuomba mwenyekiti wake na mgombea urais endapo atapewa ridhaa na watanzania kuiongoza nchi hii kuwasaidia wakina mama wajane na watoto yatima kwakuwa wamekuwa wakidhurumiwa haki zao.

Anastella ameongeza kuwa wananchi wa kata hiyo wanakabiliwa na changamoto ya huduma za afya hasa wakina mama wajawazito kwa kutozwa fedha nyingi wanapokwenda kujifungua hali inayowapelekea wanawake hao kuhatarisha maisha yao pamoja na watoto wao kwakuwa wamekuwa wakijifungulia majumbani kwa kuogopa gharama.

Nje ya kero hizo amesema kuwa wanawake wamekuwa wakitaabika kwa kutembea mwendo mrefu kufata huduma ya maji ambapo wamekuwa wakishindwa kufanya shughuli nyingine za kuwaongezea kipato na wengine kuhatarisha ndoa zao.

Akijibu hoja hizo Prof.Lipumba kwanza amewaomba wananchi wa Kihanga kumchagua diwani huyo kwakuwa anayo maono na hasa matatizo yanayowakumba wakina mama na yeye atahakikisha anamsaidia.

Lipumba amesema katika kipindi chake cha uongozi endapo atachaguliwa huduma za afya zitakuwa karibu na wananchi na kuwa rafiki lakini pia kuweka ufumbuzi wa kudumu katika kuhakikisha wananchi wananufaika na mema ya nchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.