Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Hemed Suleiman akiwathibitishia Wanamichezo waliopata ajali kwamba Serikali Kuu itahakikisha wanaendelea kupatiwa huduma za Afya kadri ya mahitaji yao yatakavyojiri.
Picha na – OMPR – ZNZ.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mheshimiwa Hemed Suleiman Abdulla Abdulla amemuagiza Kamishna wa Polisi Zanzibar kupitia Kamanda wa Polisi Mkoa Mjini Magharibi kufanya uchunguzi wa kina na wa haraka utakaobainisha chanzo cha ajali iliyosababisha ajali ya Wanamichezo waliokuwa mazoezini katika eneo la Migombani.
Ajali hiyo iliyotokea mapema asubuhi ilisababishwa na Dereva Nassor Jabir Magondi mwenye umri wa Miaka 32 hivi sasa akiwa chini ya ulinzi wa Polisi ambapo hadi sasa Wanamichezo 14 wanaendelea kupatiwa kuhuduma za Matibabu katika Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja.
Mheshimiwa Hemed Suleiman aliwaonya na kuwakumbusha Madereva wote Nchini wakati wanapoendesha vyombo vya Moto lazima waelewe na kuzingatia kwamba Bara bara zilizojengwa kwa madhumuni ya huduma za usafiri ni za Watu wote hata wale wanaotembea kwa miguu.
Alisema Serikali Kuu isingependa kuona bado kunajichomoza matukio ya ajabu yanayotishia uhai na maisha ya Wananchi wake yakihusishwa na uzembe unaofanywa na baadhi ya Madereva kwa kutokuzingatia Sheria, miongozo na kanuni zilizowekwa za matumizi sahihi ya Bara bara.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliwapongeza Madaktari na Watendaji wa Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja kwa jitihada walizochukuwa za kuwahudumia Wanamichezo hao na kuridhika na hatua hiyo iliyompa faraja kubwa.
Mheshimiwa Hemed pia aliwashukuru Wanamichezo na Viongozi wa Chama cha Mazoezi ya Viungo Zanzibar {ZABESA} kwa hatua waliyochukuwa mara moja ya kuwashughulikia majeruhi hao muda mfupi tu baada ya kupata taarifa ya ajali hiyo.
Aliwathibitishia majeruhi hao kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Afya itaendelea kuwapatia huduma za Kimatibabu kutokana na athari walizipata kadri hali halisi ya matukio yao yalivyojiri.
Alisema pale itakapohitajika miongoni mwa wagonjwa hao kupata rufaa ya hudumazaidi za matibabu kwa Hospitali zilizo Nje ya Zanzibar Serikali Kuu itabeba dhamana na gharama ya kumsafirisha mgonwa ye yote miongoni mwao.
Mapema Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja Dr. Marijani Msafiri alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba jumla ya Wanamichezo 14 wamepokelewa Hospitalini hapo mapema asubuhi na kuanza kupata huduma za Matibabu.
Dr. Marijani alisema kati ya Wagonjwa hao 14 ambao wote afya zao sio mbaya Watano wamelazwa kwa uchunguzi zaidi ya hali zao, Wawili wamefanyia Exray, Wawili wamepelekwa chumba cha upasuaji na Watano wamepatiwa huduma na kuruhusiwa kurejea nyumbani.
Mmoja kati ya wapatwa na ajali hiyo alisema Gari hiyo iliyokuwa ikiendeshwa kwa mwendo wa kasi iliivamia gari iliyokuwa pembezoni mwa Bara bara hapo Migombani Jeshini na hatimae kuserereka na kuwavamia wakiwa wanatembea kwenye mazoezi yao ya kawaida.
Alisema inasikitisha kuona kwamba dereva huyo licha ya kuonyeshwa ishara ya kupunguza mwendo kwa kibendera chekundu kilichoshikwa na kupeperushwa juu na mmoja wa wanamichezo hao lakini akashindwa kufanya hivyo na matokea yake kutokea janga hilo.
Wanamichezo hao waliounda shirikisho la Vikundi Vitano vya mazoezi Liitwalo MUWAFAKI vya Kitambi Nomba cha Zanzibar, Figther na Wakali vya Dar e salaam na Muungano Kutoka Dodoma vilikuwa katika maazoezi ya kawaida mara baada ya kumalizika kwa Bonaza la Wanamichezo Zanzibar.
Bonaza hilo la Zanzibar linalofanyika Tarehe Moja Januari ya Kila Mwaka ni miongoni mwa mwanzo wa Maadhimisho ya Sherehe za Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Mwaka 1964 yanayofikia Kilele chake Tarehe 12 Januari.
No comments:
Post a Comment