Na Fauzia Mussa - Maelezo Zanzibar 03/04/2012
Jamii imetakiwa kuendelea kujitokeza kwa wingi katika mafunzo ya ndoa ili kupata amani na utulivu wa moyo katika maisha ya ndoa na vizazi vilivyobora vyenye kufuata misingi na maadili mema.
Hayo ameyasema Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabi wakati wa kufunga mafunzo ya ndoa mkupuo wa tisa huko Ukumbi wa Masjid Jaamiiu Zinjibar Mazizini Zanzibar.
Amesema kuna umuhimu mkubwa wa kila mtu kupata mafunzo ya ndoa kwani yanapelekea kujengeka kwa familia zilizo imara na malezi bora kwa watoto na kumfanya mja kuwa karibu na Mola wake.
alisema ndoa huwalinda watu na machafu ikiwemo zinaa ambayo husababisha maradhi mbalimbali ya kuambukiza hivyo ni vyema wanandoa kuzitunza ndoa zao ili kuepukana na machafu hayo.
“Ukiwa na ndoa yenye utulivu, mawada na mahaba utaepukana na uzinifu, ukiacha zinaa umejilinda na kaswende, gono hata HIV tujitahidini kuzitunza ndoa zetu”, alisema Mufti Mkuu.
Sheikhe Kabi amewasisitiza washiriki wa mafunzo hayo kuyafanyia kazi na kuwa walimu kwa wale ambao ni vgigumu kupata nafasi hiyo kutokana na sababu mbalimbali ili kuleta mabadiko chanya katika ndoa na jamii kwa ujumla.
Akitoa maelezo ya mafunzo hayo Mkuu wa kitengo cha Fatwa na Utatuzi wa Migogoro Ali Muombwa Hasan amesema jumla ya wanafunzi 1293 wamehitimu mafunzo hayo kutoka mwaka 2018 hadi 2021 kwa Zanzibar nzima.
Nao washiriki wa mafunzo hayo katika risala yao wamesema elimu waliyoipata wataitumia vyema kwa lengo la kupunguza au kuisha kabisa kwa talaka kwa wale waliomo na wanaotaka kuingia kwenye ndoa, kutatua migogoro katika familia pamoja na kuwa na nidhamu, subira na ujasiri katika kujenga ndoa zenye mahaba na mawada ili ziendee kudumu.
Wameishauri Ofisi ya Mufti kuingizwa somo la ndoa na talaka katika mitaala ya masomo kwa wanafuzi wa kidato cha tatu hadi vyuo vikuu kwani huko kuna walengwa wengi wanaotarajia kuingia katika ndoa pamoja na kupatiwa vitabu vyenye mada zinazofundishwa ili kujifunza zaidi wakiwa nyumbani.
Jumla ya wanafunzi 186 wamehitimu mafunzo ya Ndoa yaliyotolewa na Ofisi ya Mufti Zanzibar na kukabidhiwa vyeti wakiwemo wanaume 75 na wanawake 111ambapo mafunzo hayo hutolewa kwa muda wa wiki 10, kauli mbiu ni “TUZIDUMISHE,TUZITUNZE NA TUZITUNZE NDOA ZETU TALAKA SASA BASI”
No comments:
Post a Comment