Habari za Punde

Benki ya NMB yadhamini mashindano ya kitaifa ya sayansi, teknolojia na ubunifu

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Prof.Joyce Ndalichako (kushoto) akipokea mfano wa hundi ya thamani ya sh milioni 15 kutoka kwa Mhazini Mkuu wa Benki ya NMB, Azizi Chacha jana kwa ajili ya udhamini wa mashindano ya Kitaifa ya Sayansi na Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) yaliyoanza jana uwanja wa Jamhuri Jijini Dodoma. Wengine katika picha kutoka kushoto ni Naibu Waziri Elimu, Omari Kipanga na watatu ni Katibu Mkuu wa wizara hiyo Dk Leonard Akwilapo.

Na.Mwandishi Wetu Dodoma.

BENKI ya NMB imekabidhi kitita cha shilingi milioni 15 kwa ajili ya udhamini ya Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi,Teknolojia na Ubunifu (Makisatu) yaliyofunguliwa rasmi  jana Jijini Dodoma.

Akizungumza jana Mhazini Mkuu wa Beniki ya NMB, Azizi Chacha alisema benki hiyo imetoa fedha hizo ikiwa ni udhamini wa mashindano hayo yanayoandaliwa na Serikali kupitia wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Chacha alibainisha kuwa lengo la NMB  kutoa fedha hizo ni kuisaidia Serikali katika kufanikisha mashindano hayo ya Kitaifa ambayo yamekuwa na malengo ya kuibua wabunifu wapya kila mwaka.

Alisema NMB  inashiriki katika mashindano hayo kwa kuwa ni wadhamini na wamekuwa wakiwasaidia baadhi ya wabunifu katika kufanikisha ndoto zao za kuendeleza ubunifu huo kwa kuwapa mikopo.

Alibainisha kuwa kuna baadhi ya wabunifu wamekuwa na miradi ambayo inaajiri watu wengine hivyo wakiwezeshwa watatoa ajira zaidi kwa vijana na makundi mengine.

Kadhalika alisema NMB imekuwa ikishirikiana  na Serikali katika mashindano hayo kila mwaka ili kuhakikisha wabunifu wapya wanaibuliwa kila mwaka kwa lengo la kulisaidia taifa.

Aidha alisema NMB inamilikiwa na serikali kwa asilimia 38 hivyo ni jukumu la benki kuiunga mkono serikali katika kuwezesha miradi na mipango mizuri iliyokusudiwa.

Aliongeza kuwa NMB imekuwa ikisaidia Jamii katika maeneo mbalimbali ikiwa ni juhudi za kuunga mkono Serikali katika kuwahudumia wananchi.

Hata hivyo alisema NMB imekuwa ikitoa misaada mbalimbali katika shule za msingi na sekondari kwa kutoa madawati, meza na viti kwa ajili ya wanafunzi kutumia wakati wa masomo .

Kwa upande wake Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia, Prof. Joyce Ndalichako  aliwashukuru Benki ya NMB na wadau wengine  kwa kuwaunga mkono katika mashindano hayo kwa kutoa kiasi hicho cha fedha.

Prof.Ndalichako  aliwaomba NMB kuendelea kudhamini mashindano hayo ambayo yamekuwa yakifanyika kila mwaka kwa washiriki kufanya maonesho kwa wiki moja.

Aliongeza kuwa Serikali itaendelea kutenga bajeti zaidi ili kuhakikisha mashindano hayo yanafanyika kwa lengo la kuibua wabunifu wapya kila kona ya nchi.

Alisema mashindano hayo yanashirikisha wabunifu kutoka vyuo vya ufundi, shule za msingi, vyuo vikuu na wabunifu binafsi kutoka maeneo mbalimbali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.