Daktari wa Maradhi ya Saratani Hospitali ya Mnazi Mmoja Abrahman Halfani Saidi, akielezea kuhusu Saratani katika Maadhimisho ya Siku ya Saratani Duniani, hafla iliyofanyika Hospitali ya Mnazi Mmoja Mjini Zanzibar.
Muwakilishi wa Balozi wa Uturuki Nchini Tanzania Baris Ozyurt ,akifafanuwa zaidi kuhusu Maradhi ya Saratani katika Maadhimisho ya Siku ya Saratani Duniani, hafla iliyofanyika Hospitali ya Mnazi Mmoja Mjini Zanzibar.
Muhanga wa Maradhi ya Saratani Najim Saidi Najim, akitoa shukurani kwa Madakatari wanaowahudumia , katika Maadhimisho ya Siku ya Saratani Duniani, hafla iliyofanyika Hospitali ya Mnazi Mmoja Mjini Zanzibar.
(PICHA NA MARYAM KIDIKO – HABARI MAELEZO).
Na Pili Ali, Habari Maelezo Zanzibar,
Wananchi wametakiwa kuwa na utamaduni wa kufika vituo vya huduma za afya mapema mara tu wanapoona dalili za ugonjwa wa Saratani katika miili yao ili kupatiwa matibabu haraka iwezekanavyo.
Hayo yameelezwa na Waziri wa Afya Ustawa wa Jamii Wanawake Jinsia na Watoto, Nassour Ahmed Mazrui huko ukumbi wa Hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar katika Siku ya Maadhimisho ya siku ya Saratani Duniani.
Amesema mgonjwa wa saratani anapogundulika na maradhi hayo mapema atafanyiwa matibabu kwa haraka iwezekanavyo na kunauwezekano mkubwa wa kutibika na kupona kabisa.
Hivyo amesema kila mtu anawajibu wa kujilinda na vitu ambavyo vinaweza kusababisha ugonjwa huo ili kupunguza idadi ambayo inaongezeka siku hadi siku.
Nae Mkurugenzi mtendaji wa Hospitali kuu Mnazi Mmoja Dr. Msafiri Marijani, ameiasa jamii kuachana na matumizi ya sigara, tumbaku na madawa ya kulevya ambayo ni miongoni mwa vyanzo vinavyosababisha maradhi ya saratani kwa binaadamu kwani imeonekana wazi kuwa asilimia 40 ya mardhi ya Saratani yanatokana na matumizi ya tumbaku.
Hivyo amesema kwa sasa ipo haja ya kuwahamasisha wananchi hasa vijana juu ya suala zima la kupata chanjo ya kinga ya Saratani ya shingo ya kizazi ili kupunguza wahanga wa ugonjwa huo.
Aidha Dr. Marijani ameitaka jamii kuwa na tabia ya kuchunguza afya zao angalau kwa mwezi mara moja ili kuepuka madhara yatokanayo na ugonjwa huo.
Nae Daktari wa kitengo hicho Abdulrahman Halfan Said amewaomba watu wenye uwezo wa kifedha kuiunga mkono serikali kwa kutoa misaada ili kupunguza wingi wa wahanga wa maradhi hayo.
Hata hivyo, Baadhi ya wahanga wa maradhi ya Saratani wameiomba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupatiwa watu wa ushauri nasaha, kuongezewa madaktari, viti vya kukalia wagonjwa sambamba na kupatiwa dawa na vipimo ili waweze kupata huduma kwa wakati .
Maadhimisho ya Siku ya Saratani duniani hufanyika kila ifikapo tarehe 4 ya mwezi wa 2 ya kila mwaka ambapo Kauli Mbiu ya Maadhimisho hayo ni “Imarisha Huduma za Saratani Ziwafikie Wote”.
No comments:
Post a Comment