Habari za Punde

Mwenda awabana wamiliki wa vyombo vya Usafiri Baharini

Na Muandishi Wetu.

Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) Ndg. Yusuph Juma Mwenda amewataka wamiliki na wasimamizi wa vyombo vya usafiri Baharini Zanzibar kuhakikisha kuwa kabla ya Juni 2022 wawe wameunganisha mifumo yao ya kibiashara na Mfumo wa kutolea Risiti za Kielektroniki (VFMS) ZRB ili kuleta ufanisi katika ukusanyaji wa mapato nchini.

Agizo hilo amelitoa leo katika kikao cha pamoja na wamiliki na wasimamizi wa kampunzi za usafirishaji baharini katika kikao cha pamoja kilichofanyika katika ukumbi wa mkutano wa Ofisi za Bodi ya Mapato Mazizini Zanzibar.

Kamishna Mwenda amesema kuwa, wamiliki na wasimamizi hao wanatakiwa kuwasilisha ritani na malipo kulingana na idadi sahihi ya abiria na mizigo wanayosafirisha kama itakavyosomeka katika mfumo wa kutolea Risiti za Kielektroniki ili kuendana na uhalisia wa biashara wanayoifanya sambamba na kupunguza malalamiko ambayo wamekuwa wakihusishwa nayo.

Hivyo, Kamishna Mwenda amewasisitiza kuwa sheria inamtaka kila anayefanya shughuli za kiuchumi, na ambaye anapokea malipo ni lazima atoe risiti za kielektroniki. Na amewatanabahisha kuwa Vyombo vya usafiri Baharini kama ilivyo kwa biashara nyengine wanalazimika kuunganisha mifumo yao na mfumo wa VFMS ili Serikali ikusanye kodi stahiki kulingana na biashara inayofanywa.

Kwa upande wa wamiliki na wasimamizi wa vyombo hivyo vya usafiri Baharini wamesema kuwa, kupanda kwa gharama za mafuta na kutokubadilika kwa bei za usafirishaji, miundombinu ya hali ya Bandari  ni miongoni mwa changamoto zinazowapelekea kutokulipa kodi sahihi na kwa wakati.

Kikao hicho kilihusisha wamiliki na wasimamizi wa vyombo vya baharini kutoka kampuni ya Zanfast Ferries, Azam Marine, Ikram Sea Line na Flying Horse.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.