Habari za Punde

MIFUGO NA UVUVI YATUNUKIWA TUZO YA UTAWALA BORA

 

Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Bwana Tixon Nzunda (aliyeshika Tuzo) akiongea na baadhi ya watumishi kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma mara baada ya kukabidhiwa Tuzo ya mshindi wa pili ya Utawala Bora iliyotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022, Juni 21, 2022.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu (Mifugo), Dtk. Charles Mhina (kushoto) akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bwana Tixon Nzunda kuhusu vigezo vilivyotumiwa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwenye utoaji wa Tuzo za Utawala bora na zilizopelekea Wizara Mifugo na Uvuvi kushika nafasi ya pili kwa mwaka wa fedha 2021/2022. Makabidhiano hayo yamefanyika kwenye ofisi za Wizara zilizopo Mtumba Jijini Dodoma.
Katibu Mkuu Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Mifugo), Bw. Tixon Nzunda akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya watumishi wa Wizara mara baada ya kukabidhiwa Tuzo ya mshindi wa pili ya Utawala Bora iliyotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022

Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) imeshika nafasi ya pili kwenye tuzo za Utawala Bora zinazotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kufanya vizuri kwenye upande wa utendaji bora katika utoaji wa huduma kwa watumishi na wananchi kwa mwaka wa fedha 2021/2022.

Akipokea tuzo hiyo Jijini Dodoma Juni 21, 2022 Katibu Mkuu, Wizara ya Mifugo na Uvuvi anayeshughulikia Sekta ya Mifugo, Tixon Nzunda alisema kuwa tuzo hiyo imepatikana kutokana na ushirikiano mkubwa uliopo katika kufanya kazi kama timu, kwa weledi, uadilifu na uwajibikaji kwa umma.

“Nitumie fursa hii kuwashukuru watumishi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi kwa kuwezesha tuzo hii kupatikana, tumefanyiwa tathimini kwenye eneo la utawala bora ambapo tumeshika nafasi ya pili, tuchukue hii kama changamoto kwa kufanya vizuri zaidi kwenye tuzo zingine,” alisema

“Nishani hii ni kama chachu ya kufanya mabadiliko makubwa ili mwaka ujao tusiongoze tu kwenye masuala ya utawala bora, masuala ya ushughulikiaji wa malalamiko, taarifa za watumishi, lakini pia tuwe vinara katika kusimamia miradi ya maendeleo katika sekta zetu, kuanzia minada, mabwawa, visima, majosho, ufuatiliaji wa miradi na kuhakikisha kwamba thamani ya fedha ya miradi yetu inapatikana,” aliongeza

Awali, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Sekta ya Mifugo, Dkt. Charles Mhina alisema tuzo hiyo ya Utendaji Bora imetolewa Mei 27, 2022 kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi (Sekta ya Mifugo) kwa kufanya vizuri kwenye uingizwaji wa taarifa sahihi katika mfumo wa taarifa za utumishi na mishahara.

Vigezo vingine ni pamoja na uhuishaji wa taarifa kwenye mfumo kwa wakati, ushughulikiaji wa malalamiko ya watumishi na wananchi kwa wakati, kuzingatia na kutekeleza sheria, kanuni na taratibu za utumishi wa umma na sheria mbalimbali za nchi katika kazi zote za kila siku.

Tuzo hizo za Utawala Bora zinazotolewa na Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora kila mwaka na zinajumuisha wizara zote zilizopo Tanzania bara ambapo nafasi ya kwanza imechukuliwa na Ofisi ya Rais Ikulu, nafasi ya pili imechukuliwa na Wizara ya Mifugo na Uvuvi na nafasi ya tatu imechukuliwa na  Wizara ya Fedha na Mipango.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.