Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Ali Mwinyi Amejumuika na Wananchi Katika Ibada ya Sala ya Ijumaa Msikiti wa Forodhani Unguja Leo

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika leo 17-2-2023 , katika Msikiti wa Ijumaa Forodhani Wilaya ya Mjini Unguja.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Ali Mwinyi akishiriki kuitikia dua ikisomwa na Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh. Saleh Omar Kabi, baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika leo 17-2-2023, katika Mskiti wa Ijumaa Forodhani Wilaya ya Mjini Unguja. 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na Viongozi wa Dini baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti wa Ijumaa Forodhani Wilaya ya Mjini Unguja leo 17-2-2023. 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Serikali inajitahidi kufanya kila linalowezekana kuwapunguzia wananchi changamoto ya ugumu wa maisha uliochangiwa na athari za kupanda kwa gharama za bidhaa nchini.

Al hajj Dk. Mwinyi aliyasema hayo wakati akizungumza na wananchi na waumini wa kiislamu waliohudhuria ibada ya sala ya Ijuma huko Msikiti wa Forodhani, Wilaya ya Mjini, Mkoa wa Mjini Magharibi - Unguja.

Alisema kupanda kwa ghamara za bidhaa kumechangiwa na athari mbalimbali nje ya Zanzibar na kueleza kwamba wananchi wa visiwa vya Unguja na Pemba mbali ya kutegemea bidhaa za chakula kutoka nje ya nchi lakini kwa baadhi ya vyakula hutoka Tanzania bara ambako nako bidhaa zimepanda bei kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo ukame ulioathiri baadhi ya Mikoa inayozalisha sana chakula kushindwa kupata mavuno mazuri yenye kutosheleza mahitaji ya watu wote.

Alisema hali hiyo, imechangia Zanzibar bidhaa kupanda bei maradufu na kueleza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inajitahidi kukabiliana na hali hiyo ili kuleta nafuu kwa wananchi hasa kipindi hiki wananchi na waumini wa dini ya kiislam wakielekea kwenye Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Al hajj Rais Mwinyi alisema, Serikali pia imechukua hatua kadhaa za kukabiliana na hali hiyo ikiwemo kutoa ruzuku kwa baadhi ya bidhaa hususan mafuta ambayo yameathiri zaidi sekta ya usafirishaji nchini inayobeba dhima nzima ya uchumi na kugusa maisha ya wananchi.

Akizungumzia bidhaa za chakula, Al haj Rais Mwinyi alisema kuelekea mwenzi mtukufu wa Ramadhani, Serikali imehakikisha kwamba bei za vyakula inapungua nchini.  

Aidha, aliwasihi waumini wa dini ya kiislam na Watanzania kwa ujumla kuendeleza ibada kwa kufanya mema yanayompendeza Mwenyezi Mungu na kuachana na yanayomchukiza hasa kwenye miezi hii Mitukufu ya Rajabu, Shaabani na Ramadhani kwa kuongeza ibada na kuendelea kumuomba kuifungulia neema nchini ili bidhaa zishuke bei.

“Tunamuomba Mwenyezi Mungu atufungulie neema ya mvua nzuri ili mazao yastawi vizuri bidhaa zipatikane kwa wingi na zishuke bei” alieleza Al hajj Mwinyi.

Hata hiyo, aliwasihi waumini wanaosali msikitini hapo kuendelea kuutunza na kuukarabati kwa sehemu zinazohitaji matengenezo ili msikiti udumu.

“Waliotangulia waliitunza misikiti hii, ndio maana  na sisi tumeikuta, hivyo tunawajibu wa kwa hali na mali kukarabati na kuitunza misiki yote” alinasihi Al hajj Dk. Mwinyi.

Alhaj Dk. Mwinyi alitoa ahadi ya kuchangia shilingi milioni tano ikiwa ni sehemu ya mchango wake msikitini hapo.

Akizungumza kwenye ibada ya sala hiyo, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Khalid Ali Mfaume aliwataka waumini hao kutakiana mema na kuacha kuhusudiana kutokana na neema alizowaruzuku Mungu.

Alisema Mwenyezi Mungu amewaumba binaadamu na kuwatofautisha kupitia neema zake, hivyo aliwasihi kuendelea kutendeana mazuri  badala ya kuhusudiana.

IDARA YAMAWASILIANO – IKULU, ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.