Habari za Punde

SMZ Haitawafumbia Macho Watumishi wa Umma Wasiotaka Kuwajibika Hasa Wanapopelekewa Kero

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akihutubia wakati wa Maadhimisho ya miaka miwili ya Mfumo wa SNR Sema na Rais Mwinyi yaliyofanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Golden Tulip Uwanja wa Ndege Kiembesamaki Wilaya ya Magharibi “B” Unguja leo 29-3-2023

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema, haitowafumbia macho watumishi wa umma wasiotaka kuwajibika hasa wanapopelekewa kero za wananchi kuzitatua kwenye taasisi zao na kutozifanyia kazi kwa wakati sahihi.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameyasema hayo hoteli ya Golden Tulip, Uwanja wa Ndege Zanzibar, kwenye maadhimisho ya miaka miwili ya mfumo wa Sema Na Rais Mwinyi, (SNR).

Alisema mfumo wa SNR umeleta tija kipindi kifupi tokea kuanzishwa kwak, umepokea malalamiko mengi ya wananchi na asilimia kubwa yamepatiwa ufumbuzi kwa watu wengi kupatiwa haki zao na kueleza kwamba Serikali itajitahidi kuondosha kero zaidi za wananchi.

Dk. Mwinyi alitoa onyo kwa baadhi ya watendaji wa taasisi za Serikali wasiotaka kutatua changamoto za wananchi zinazowasilishwa kwenye taasisi zao na kuwaeleza kwamba Serikali itawachukulia hatua.

Pia, Rais Dk. Mwinyi aliwaonya baadhi ya watendaji wa taasisi za Serikali wanaowapa vitisho maofisa wao wanaotoa taarifa za ubadhirifu kwenye mfumo wa SNR nakuwaahidi kuwapa ulinzi maofisa wanaotishiwa amani na kuwaeleza wafanye kazi bila woga.

“Asitokee kiongozi yeyeote wa Serikali, kuwatisha watoa taarifa kupitia mfumo wa SNR” alionya Dk. Mwinyi

Aidha, amewaonya baadhi ya maofisa wa mfumo huo kutohoji mamlaka wanapofikishiwa maagizo na kero za jamii, badala yake watekeleze wajibu wao kwa kuzitafutia ufumbuzi unaofaa pamoja na kuwataka watendaji wa serikali kuheshimu na kutii mamlaka za serikali haswa zinapokuja kesi ya utekelezaji wa maagizo ya Serikali.

“Kama kuna kitu ambacho hakina sababu, wala hatutaki kusikia ni kutokuwajibika kwa maofisa wa SNR kwamba hawatowajibika, Ofisa yoyote wa SNR asietaka kuwajibika, msitegemee Ikulu itachukua hatua, wakuu wa taasisi mko hapa tusije tukalizungumzia tena hapa” Alionya Rais Mwinyi.

Rais Dk. Mwinyi alisema mfumo huo utaendelea kufanyakazi kwa karibu na wanachi   na kueleza kwamba mfumo huo una utambuzi wa takwimu kubaini viongozi na taasisi zinazoharibu ama kufanya vizuri hivyo, alieleza wakati umefika kila mmoja aone umuhimu wa kuwajibika. 

Alizungumzia suala la taarifa za ubadhirifu wa mali za umma Dk. Mwinyi aliahidi kuchukuliwa kwa hatua dhidi ya kiongozi asiewajibika kwenye majukumu yake.

Rais Dk. Mwinyi pia alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini uhuru wa Mahakama, hivyo kupitia mfumo wa SNR Serikali itayafikisha malalamiko ya wananchi kupitia Jaji Mkuu ili yashughulikiwe mahakamani kwa kuondosha kasoro zinazojitokeza.

Aliitaka Wizara ya Fedha na Mipango kutenga bajeti ya kurejesha fidia kwa wananchi na kueleza sasa Serikali itahakikisha inalipa fidia kwa wananchi waliopitiwa na miradi ya maendelo kadri ya wakati ukatavyoruhusu.

Akizungumza kwenye hafla hiyo Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Ikulu, Jamal alisema kuanzishwa kwa mfumo wa SNR ni utekelezaji wa maagizo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, awamu ya nane kwa kuwataka viongozi na watendaji wa ndani ya Serjali wanawajibika kwa vitendo.

Naye, Mkuu wa kitengo cha Sema Na Rais, Haji Makame alisema tokea kuanzishwa kwa kitengo hicho miaka miwili iliyopita, kimefanikiwa kupokea changamoto na malalamiko mengi kutoka kwa wananchi wa Unguja na Pemba na kuyapatia ufumbuzi kwa baadhi yao.

Aliwaeleza mfumo umeziunganisha taasisi 65 za Seriakali na kueleza kwamba una mpango wa kuongeza nyengine zaidi, hivyo aliwaeleza waajiri na wakuu wa taasisi hizo kwamba wanawajibu wa kuwasimamia maofisa wa SNR wanaoshirikiana kufanyakazi kwa pamoja na kitengo hicho na kueleza kujumu la kitengo ni kuratibu majukumu yao.

Kitengo cha (SNR) kipo chini ya Ofisi ya Rais Ikulu, Zanzibar kilianzishwa Februari 27 mwaka 2021.

IDARA YA MAWASILIANO

IKULU, ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.