Habari za Punde

Alhajj Dk.Hussein Ameiasa jamii kuendelea kutekeleza maarisho ya Mwenyezi Mungu na kufuata mafundisho ya Mtume SAW

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na kuwasalimia Wananchi baada ya kumalizika kwa Ibada ya Sala ya Ijumaa iliyofanyika katika Msikiti Mkuu wa Ijumaa Malindi Wilaya ya Mjini Unguja Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Al hajj Dk. Hussein Ali Mwinyi, ameiasa jamii kuendelea kutekeleza maarisho ya Mwenyezi Mungu na kufuata mafundisho ya Mtume SAW kwa kufanya yaliyo mema na kuacha mabaya yanayomchukiza Allah (S.W).

Al hajj Dk. Mwinyi alitoa nasaha hizo kwenye Msikiti Mkuu wa Ijumaa Malindi, Wilaya ya Mjini alikojumuila na waumini wa dini ya Kiislamu kwenye ibada ya sala ya Ijumaa.

Aliiasa jamii kuchunga familia zao na kuendeleza malezi ya pamoja badala ya kutelekeza familia kwa visingizio vya talaka, aliwataka familia wazichunge ndoa zao ili wajenge ustawi wa jamii iliyobora.

“Ndani ya jamii zetu  tuna mtihani mkubwa wa idadi kubwa ya wajane na wanapata shida kubwa ya maisha” Alieleza Al hajj Dk. Mwinyi.

Alisema wanawake wanaoachika kwenye ndoa zao, sio tuu huachwa peke yao na waume zao, bali hutwishwa mzigo mzito wa ulezi wa watoto peke yao, jambo alilolieleza huwasababishia wanawake wengi ugumu wa maisha na kuwa chanzo cha watoto wengi mitaani kuishi kwenye mazingira magumu.

Al hajj Dk. Mwinyi, alieleza hivi sasa ndani ya visiwa vya Unguja na Pemba kumeibuka vyama vingi na vikundi vya wajane waliojikusanya pamoja kupaza sauti zao huku wakiambulia jukumu zito la ulezi wa watoto peke yao na kuwatunza na kuongeza kuwa watoto wengi wa aina hio hukulia kwenye matatizo mengi.

“Watu wanaacha ovyo bila utaratibu, wanaisababishia jamii kupata watoto wengi waliotelekezwa, watoto wengi wa aina hii maisha yao yanakua magumu sana” kwa hisia alieleza Al hajj Dk. Mwinyi.

Hata hivyo, Al hajj Dk. Mwinyi aliwaomba waumini wa dini kuendelea kuwaombea du’a za kheir viongozi wao kwekwe jukumu kubwa la kuiongoza, Zanzibar.

Naye, Katibu Mtendaji kutoka Ofisi ya Mufti Zanzibar, Sheikh Khalid Ali Mfaume, ameitaka jamii hususani wanaume, watatue matatizo yao kupitia mafundisho ya Mtume (SAW) kwa kusoma sana du’a na kuleta adhkari kwa wingi, badala ya kutoa maamuzi mabaya yenye athari mbaya kwa jamii.

Akizungumza sheria za talaka msikitini hapo, khatibu wa ibada ya sala ya Ijumaa, Sheikh Ali Abdulfatah Yussuf alieleza, talaka ni halali alioichukia mno Allah (S.W).

Pia, aliitaka jamii kujichunga sana wakati wa utoaji talaka kwa kuzifuata sheria na sunna za talaka zilizowekwa kwa misingi ya dini pamoja na kujiepusha kufanya maamuzi ya siyo sahihi wakati wa kutoa talaka kwa wake zao.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.