MSARIFU na Mwenyekiti wa Bodi ya Taasisi ya Zanzibar Maisha Bora Foundation (ZMBF), Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mariam Mwinyi ametoa rai kwa watafiti kulifanyia utafiti zao la mwani ili kulitambulisha zaidi duniani na kutoa mwamko kwa jamii kuendelea kuzalishwa.
Mama Mariam Mwinyi alitoa rai
hiyo alipozungumza kwenye Mkutano wa kimataifa unaojadili mfumo wa chakula
kwenye mada ya Nafasi ya Mwanamke kwenye sekta ya kilimo na chakula, ukumbi wa
Selious Jengo la Mikutano ya Kimataifa la Julius Nyerere, Dar es Salaam.
Alisema, Zanzibar ni nchi ya
kwanza Afrika inayoongoza kwa uzalishaji mwani na inakamata asilimia tatu ya
pato la taifa baada ya Utalii unaochangia asilimia 30 ya pato la taifa na
kilimo cha Karafuu.
Alisema, asilimia 70 ya dunia
ni bahari na 30 ni ardhi hiyo alisema Zanzibar ina eneo kubwa la kulimia mwani
bado halijatuka, hivyo ameitaka jamii kujikita zaidi kwenye kilimo hicho kwani
kinafursa nyingi za uchumi na maendeleo.
Mama Mariam Mwinyi alieleza
taasisi ya “Zanzibar Maisha Bora Foundation” inaunga mkono jitihada za Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia sera yake ya Uchumi wa Buluu unaoshajihisha
wananchi zaidi kuzitumia fursa ya bahari kwa kuleta maendeleo ya kiuchumi na
kujiongezea kipato.
Alisema ZMBF imewawezesha
kiuchumi wanawake na kinamama wakulima wa mwani baada ya kuwaweka pamoja
vikundi 16 vya kinamama 20 kwa Unguja na Pemba kwa lengo kuwapa mikopo nafuu
ili kuendeleza zao hilo.
“Kilimo cha mwani Zanzibar
asilimia 90 ya wakulima wake ni wanawake, ZMBF imewawezesha ili kiwaletee tija
baada ya kujikita kwenye kilimo hicho kwa zaidi ya miaka 15 nyuma bila ya
mafanikio kwa kuwapa vifaa (Chanja za kuanikia Mwani), mafunzo na mbinu za
kisasa za ukulima huo ” alifafanua Mama Mariam Mwinyi.
Akitaja faida ya zao la Mwani
mama Mariam Mwinyi alieleza mwani unaongoza kuwa na virutubisho vingi kuliko
mazao mengine, hutumiwa kwa mapambo na kutengenezewa urembo huko duniani pia
husaidia lishe kwa watoto na mama wajawazito kwani jamii ikitumia zao hilo kama
chakula linasaidia kwa madini ya chuma ambayo ni muhimu kwa afya ya binaadamu.
Alisema, Zanzibar ina
changamoto ya utapiamlo kwa watoto wadogo hivyo aliiomba jamii kuweka utamaduni
wakutumia bidhaa zilizosarifiwa kwa zao la mwani ili kujiepusha na tatizo hilo
na kueleza kati ya watoto watano wanaozaliwa mtoto mmoja hukumbwa na tatizo la utapiamlo na kuwataka kina mama
wajawazito kutumia kwa wingi bidhaa zinazotokana na zao la Mwani.
Alisema, mbali ya changamoto
nyingi wanazokumbana nazo wakulima wa zao hilo, ikiwemo kulima mwani usiokuwa
na ubora, kutokuwa na mashine za kusarifia mwani wenye kiwango kwajili ya kuuza
kwa bei ya juu zaidi na mabadiliko ya tabia nchi ambayo huwasababishia wakulima
hao kwenda kina kirefu cha maji hivyo, ZMBF iliwasaidia kinamama hao, vifaa vya
kisasa ikiwemo mashine ya kusarifia mwani,
boti na mashine na mafunzo ya kuogeleza ambapo kwasasa wanauza mwani kwa
bei ya elfu kumi badala ya elfu moja ambao imewasaidia kina mama wengi kwa
kutumia teknolojia ya kisasa.
Naye, Waziri wa Maendeleo
anayeshughulikia masuala ya kimataifa nchini Norwe, bibi Anne Beathe
Trinnereim, alieleza kwenye mkutano huo namna wanavyowasaidia wajasirimali
wadogo wadogo nchini humo kuwainua kiuchumi na kuwawezesha wanawake kutimiza
ndoto zao za maendeleo.
Alieleza jinsi Serikali ya
Norway ilivyoweka mikakati ya kukabiliana na njaa na utapiamlo kwa
kuwashajihisha wananwake wa vijijini kuongeza jitihada kwenye kupeleka
mapinduzi ya kilimo na kuimarisha usalama wa chakula kwa kuzitumia vyema fursa
za kilimo nchini humo.
Taasisi ya Zanzibar Maisha
Bora Foundation (ZMBF) iliasisiwa rasmi Febuari mwaka jana, mwezi Machi mwaka
huu, ilizindua Mpango Mkakati wa miaka mitatu.
Aidha, taasisi hiyo inafanya
kazi kwa karibu na tasisi za Serikali zikiwemo Mahakama ya Zanzibar, Wizara ya
Afya, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Wizara ya Uchumi wa Buluu, Wizara ya
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee Wazee na watoto, Wizara ya Habari na Wizara
ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda.
IDARA YA MAWASILIANO IKULU, ZANZIBAR.
No comments:
Post a Comment