Habari za Punde

Taarifa kwa Vyombo vya Habari

Kwa kipindi cha mwezi Oktoba 2023 hali ya usalama Mkoa wa Songwe imeendelea kuwa shwari hii ni kutokana na ushirikiano uliopo baina ya Jeshi la Polisi, vyombo vingine vya ulinzi na usalama pamoja na wananchi.  Hata hivyo katika jitihada za kuzuia na kutanzua uhalifu, mkoa wa Songwe umeendelea kupata mafanikio mbalimbali kutokana na oparesheni, misako, doria pamoja na dhana ya ushirikishwaji wa jamii.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linawashikilia watuhumiwa 14 wa makosa mbalimbali ambapo mnamo Oktoba 3, 2023 majira ya 02:00hrs huko kijiji cha Mbala kata ya Mwambani wilayani Songwe walikamatwa watuhumiwa wanne (04) wanaume wakidaiwa kuhusika na kosa la wizi wa Kaboni idhaniwayo kuwa na Dhahabu yenye uzito wa kilo 400 ambayo alitegemea kupata kilo 02 ya Dhahabu yenye thamani ya zaidi ya shilingi  Milioni 200  mali hiyo ambayo ni ya Reck Mwaipopo mwenye umri wa miaka 22 mkazi wa Mbala.
 

Chanzo cha tukio hilo ni kujipatia mali isivyo halali ni kwamba kundi la watu zaidi ya 12 waliokuwa na silaha za jadi aina ya Panga na Rungu waliwavamia wafanyakazi wa Plant hiyo na kisha kuwashambulia na kuwafunga kamba za Manila miguuni na mikononi kisha kuvunja kufuli za mageti katika eneo la Plant na kuiba Kaboni. Kaboni hiyo imehifadhiwa katika Ofisi ya mkoa ya Madini kwa ajili ya kuwasilishwa mahakamani kama kielelezo pindi tu upelelezi utakapokamilika. 

 

Aidha mnamo Oktoba 11, 2023 majira ya 17:00hrs huko mtaa wa Ipanga kata ya Ichenjezya wilaya ya Mbozi walikamatwa wanaume 02 mmoja akiwa mtumishi wa Hospitali ya Rufaa mkoa wa Songwe mwenye umri wa miaka 22 ambao wanashikiliwa kwa kosa la wizi wa ULTRA SOUND, MICROSCOPE MASHINE, CENTRIFUGE MASHINE, PRINTER MASHINE ikiwa pamoja na madawa ya binadamu na vifaa tiba mbalimbali vyenye thamani ya zaidi ya Milioni 40 ambavyo alivihifadhi katika nyumba yake na Maabara iitwayo Kamatingo iliyopo kitongoji cha Isangu. Tukio hilo lilitokea Oktoba 07, 2023 majira ya 01:50hrs huko Hospital ya Rufaa ya mkoa wa Songwe iliyopo wilaya ya Mbozi ambapo mtuhumiwa huyo mtumishi alivunja ofisi ya idara ya Mionzi katika Hospital hiyo na kuiba vitu hivyo. Chanzo cha tukio hilo ni kujipatia mali isivyo halali na mbinu iyotumika ni kuingia ofisini na kuiba vifaa hivyo.  

 

Pia Mnano Septemba 13, 2023 majira ya 15:45hrs katika shule ya msingi Kisangani  iliyopo kata ya Muungano wilayani Momba walikamatwa walimu wawili (02) mmoja akiwa ni Mwalimu Mkuu wa shule hiyo mwenye umri wa miaka 36, akiwa na mwenzake mwenye umri wa miaka 27 wote wakazi wa Kisangani ambao wanashikiliwa kwa kosa la kujaribu kufanya udanganyifu wa Mitihani kwa kutoa majibu ya somo la Sayansi katika Mtihani wa kumaliza darasa la Saba mwaka 2023.

 

Kwenye tukio hilo pia alikamatwa Mwanafunzi mmoja (01) wa darasa la tano mwenye umri wa miaka 14 kutoka shule ya msingi Mkombozi ambazo shule hizo zipo jirani akiwa katika vyoo vya shule ya Kisangani na baada ya kupekuliwa alikutwa na karatasi nyeupe ikiwa na majibu kuanzia swali la 01 hadi 40 na mwanafunzi huyo alipohojiwa alieleza kuwa ametumwa na mwalimu wa shule hiyo ambaye ni mwalimu wa kujitolea ili aweke chooni humo chini ya ndoo.  Hadi sasa Jeshi la Polisi bado linaendelea na mahojiano na watuhumiwa na watafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.

 

Katika tukio lingine mnamo Oktoba 14, 2023 majira ya saa 22:00hrs huko mtaa na kata ya Mpemba wilayani Momba askari Polisi wakiwa doria maeneo mbalimbali ya mji wa Tunduma walifanikiwa kumkamata Mwanaume mmoja (01) mwenye umri wa miaka 26 mkazi wa Mbeya akiwa na Vitenge Jora 50 ambavyo ameviingiza nchini bila ya kufuata utaratibu wa Forodha. Mtuhumiwa huyo atafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika.

 

Oktoba 14, 2023 majira 22:30hrs maeneo ya kijiji cha Machindo katika nyumba ya Vitus Sikalengo iliyopo kata ya Myunga wilaya ya Momba walikamatwa wanaume saba (07) mmoja kati yao akiwa ni raia wa Zambia kwa kosa la kufanya shughuli za Uganga bila kibali huku wakiwa na vifaa vya kufanyia uganga.

 

Hata hivyo, Oktoba 10, 2023 majira ya 08:00hrs katika ofisi ya kijiji cha Itumbula kata ya Ivuna wilaya ya Momba. Afisa Mtendaji wa kijiji aitwaye Focas Kadule mwenye umri wa miaka 53 aligundua kupatikana kwa bunduki 02 aina ya Gobole zilizotengenezwa kienyeji zikiwa zimetelekezwa katika mlango wa ofisi yake. Chanzo cha tukio hilo ni usalimishaji wa silaha haramu baada ya kupewa elimu ya madhara ya umiliki wa silaha isivyo halali kupitia mikutano mbalimbali ya uelimishaji na hasa  elimu ya Polisi Jamii.

 

Aidha, Jeshi la Polisi Mkoa wa Songwe linakemea vikali uwepo wa matukio ya imani gombanishi za kishirikina pamoja na vitendo vya kihalifu pia linawataka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa Jeshi la Polisi ili kudhibiti na kutokomeza vitendo hivyo.

 

Imetolewa na;

Theopista Mallya - ACP

Kamanda wa Polisi

Mkoa wa Songwe

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.