RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amewakumbusha viongozi wote waliotajwa kwenye
Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa mujibu wa vyeo na nafasi zao
kuhakikisha wanajaza fomu za Tamko la Rasilimali
na Madeni na kuzirejesha Ofisi za Tume ya Maadili si zaidi ya Disemba 31 mwaka
huu.
Amesema, kuchelewa
kurejeshwa fomu kwa wakati bila ya sababu za msingi kwa viongozi hao ni kosa la
kimaadili kwa mujibu wa Sheria, hivyo Serikali itawachukulia
hatua viongozi watakaochelewa
kurejesha fomu hizo.
Dk. Mwinyi ametoa indhari hiyo
kwenye kilele cha maadhimisho ya siku ya maadili
na haki za binadamu kwenye ukumbi wa Sheikh Idris Abdul Wakil, Kikwajuni, Mkoa wa Mjini
Magharibi.
Alisema, maadhimisho hayo yanatoa fursa ya kujadili kwa kina mustakabali wa nchi,
mafanikio ya utekelezaji wa maendeleo kwa ufanisi, kutafakari namna bora ya
kuimarisha na kusimamia utawala bora na misingi yake ikiwemo utawala wa sheria, haki, uwajibikaji, uwazi, uadilifu,
haki za binaadamu, ubadhirifu wa mali za umma na kupiga vita rushwa.
Alisema, jukumu la kuimarisha misingi ya Utawala Bora si la
Serikali na taasisi zake pekee bali ni la wote zikiwemo sekta binafsi, Asasi za Kiraia, Asasi za dini jumuia za kimataifa, vyombo vya habari na
wananchi kwa ujumla, wote wanawajibu wa kusimamia na kutekeleza
misingi ya utawala bora,
kuheshimu na kuimarisha maadili, haki za binadamu, uwajibikaji, uwazi na kupiga
vita rushwa kwa manufaa ya maendeleo ya taifa.
Alisema katika kuyatekeleza
hayo, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeanzisha taasisi mbalimbali
zinazosimamia masuala ya Utawala Bora nchini ikiwemo Ofisi ya Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na
Uhujumu wa Uchumi (ZAECA), Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Tume ya Haki za
Binaadamu na Utawala Bora pamoja na Idara ya Utawala Bora na kila taasisi kupewa majukumu yake ili kuimarisha
na kusimamia misingi ya Utawala Bora nchini.
Alisema maendeleo yaliyofanikiwa nchini yamechangiwa kwa uimara na umadhubuti wa taasisi hizo kwa ushirikiano na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka DPP na Mahkama.
Rais Dk. Mwinyi alisema Tume
ya Maadili ya Viongozi wa Umma ina
jukumu la kusimamia maadili ya viongozi wa umma
nchini, kupitia Sheria Na. 4 ya 2015 kwa lengo la kuimarisha misingi ya
utawala bora ikiwemo uwazi na uwajibikaji.
Akiizungumzia taasisi ya (ZAECA), Rais Dk. Mwinyi alisema, aliisifu
kwa kujenga ushirikiano wa karibu na
taasisi za haki jinai zikiwemo Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), Jeshi la
Polisi, Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na
Rushwa Tanzania (TAKUKURU), Mahakama pamoja
na vyombo vyengine vya ulinzi na usalama. Ushirikiano huo umeendelea kuleta ufanisi katika kudhibiti wa vitendo vya rushwa na uhujumu
uchumi nchini.
Alisema,
kwa kipindi cha utekelezaji kazi Januari hadi Oktoba 2023,
ZAECA ilifanikiwa kuokoa fedha kiasi cha Shilingi 2,385,386,720/=. Kati ya
fedha hizo, Shilingi 97,944,369/= zilirejeshwa kwa wananchi,
Shilingi 2,287,442,351/= zilirejeshwa Serikalini kutokana na makosa tofauti
ya rushwa, uhujumu wa
uchumi na ukiukaji wa maadili.
Akiiizungumzia Tume ya Maadili kwa mwaka 2022/23, Dk. Mwinyi alieleza kufanikiwa kushughulikia
malalamiko 19
na kuyafanyiakazi yakiwemo ukiukwaji wa Sheria ya Maadili dhidi ya Viongozi wa
Umma sawa
na asilimia 95 ya malalamiko yaliyopangwa ambayo yalihusu maeneo ya matumizi
mabaya ya madaraka (15),
unyanyasaji (1), uonevu (1), lugha za matusi (1) na kutelekeza familia (1).
Kuhusu Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora (THBUB) alieleza, taasisi hii ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayofanya kazi zake Tanzania Bara na hapa Zanzibar kupitia Sheria Na. 12 ya 2003 ambayo SMZ imeiridhia
Tume hiyo kutekeleza majukumu yake Zanzibar.
Alisema kwa kipindi
cha Januari hadi Novemba 2023, Tume hiyo imehughulikia jumla ya malalamiko 15, kati ya hayo 13 yalihusu uvunjwaji wa haki za binadamu na mawili ya ukiukwaji wa
misingi ya utawala bora.
Hivyo, aliwataka wananchi kuendelea kuitumia Tume hiyo kupeleka
malalamiko yao yanayohusiana na uvujifu wa haki za binadamu na ukiukwaji wa
misingi ya utawala bora ili yafanyiwe kazi na kupatiwa ufumbuzi mwafaka.
Pia, Rais Dk. Mwinyi alitoa
wito kwa Viongozi waliopewa dhamana serikalini wavitumie vyeo vyao kwa
mujibu wa sheria na taratibu zinazowaongoza, kwani Katiba
ya Zanzibar ya 1984 pamoja na Sheria ya
Maadili ya Viongozi wa Umma zinakataza matumizi mabaya ya Madaraka.
Alisema
Serikali itawachukulia hatua za
kinidhamu viongozi watakaobainika kuwa makosa, kwa mujibu wa sheria bila ya kumuonea
mtu.
Naye,
Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Asaa Ahmad Rashid, alisema
hatua ya viongozi kuzingatia misingi ya utawala bora inachochea ufanisi wa
utekelezaji wa mipango ya serikali kupatikana kwa huduma bora, maendeleo na
ustawi wa jamii kwa wananchi.
Aliwakumbusha viongozi wenzake kuhakikisha wanajaza na kuwasilisha fomu zao za mali kwenye Tume hiyo kutokana na viongozi wachache waliorejesha fomu hizo sawa na asilimia 36 ya waliorejesha.
Haki za Binaadamu zinatokana na tamko la kimataifa lililoidhinishwa na kupitishwa na Baraza kuu la Umoja wa Mataifa tarehe 10 Disemba mwaka 1948.
Madhumuni ya Tamko hilo ni kukuza na kuimarisha misingi ya Haki za Binaadamu Duniani. Barani Afrika masuala ya
haki za binadamu yamo katika tamko la Afrika la Haki za Binadamu na Watu, (African Charter on Human and
People’s Rights).
Tanzania imeingiza masuala
ya Haki za Binadamu kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka
1977 Sura ya Kwanza Sehemu ya Tatu na hapa Zanzibar masuala haya yameingizwa kwenye Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 Sura ya Tatu.
Maadhimisho ya siku ya maadili na haki za binadamu yenye kauli yake
“Tuimarishe
Utawala Bora na Haki za Binaadamu kwa Kuondoa Ubadhirifu na Kukuza Maadili kwa
Ustawi wa Jamii” yalilenga kutoa uelewa mpana kwa jamii.
IDARA YA MAWASILINO, IKULU ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment