Habari za Punde

MKUU WA MKOA MJINI MAGHARIBI AZUNGUMZA NA WAANDISHI ZANZIBAR

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Idrissa Kitwana Mustafa akisisitiza Jambo wakati akijibu maswali ya Waandishi wa Habari kuhusiana na Tarifa  ya Operesheni  iliofanywa kukabiliana na Makundi ya Uhalifu katika Mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar.
Baadhi ya wajumbe wa Kamati ya Ulinzi na Usalama wa Mkoa  na Waandishi wa Habari waliohudhuria katika Mkutano wa Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Idrissa Kitwana Mustafa kuhusiana na taarifa ya Operesheni  iliofanywa kukabiliana na Makundi ya Uhalifu katika Mkoa wa Mjini Magharibi Zanzibar.

Na Khadija Khamis- Maelezo, Zanzibar 28/04/2024.

Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Idrissa Kitwana Mustafa 

amesema jumla ya watuhumiwa 251 wamekamatwa kufuatia 

operesheni maalum ya kukabiliana na vitendo vya uhalifu 

hapa Nchini.


Ameyasema hayo huko katika Ukumbi wa Ofisi ya Mkuu wa 

Mkoa Mjini Magharibi Vuga wakati akizungumza na 

waandishi wa habari wa  vyombo mbali mbali.


Amesema watuhumiwa waliokamatwa 22 wamekamatwa na 

mapanga na vifaa vya kuvunjia nyumba, 20 wamekamatwa 

kwa makosa ya unyan’ganyi, kujeruhi na kushambulia, 6 kwa 

makosa ya wizi wa pikipiki wakiwemo mafundi wa pikipiki 

wanaopokea mali za wizi na watuhumiwa 203 wamekamatwa 

kwa makosa ya uzembe na ukorofi.


Aidha, amefahamisha watuhumiwa wote waliokamatwa katika 

operesheni hiyo watafikishwa katika vyombo vya sheria na 

majalada yao yemeshafunguliwa kwa ajili ya kufikishwa katika 

Ofisi ya Mwendesha Mashtaka ili kuendelea na taratibu 

nyengine za kisheria.


Mkuu wa Mkoa huyo amesema operesheni hizi zitakua 

endelevu katika maeneo mbali mbali ya Mkoa wa Mjini 

Magharibi hadi kuhakikisha makundi hayo ya vijana 

wanaotumia silaha za jadi yamedhibitiwa kabisa kwa 

mashirikiano ya jeshi la polisi na vyombo vyengine vya ulinzi.

Pamoja na hayo, Amewaasa vijana ambao wanajiingiza katika 

matendo hayo kwamba Serikali haitoacha vitendo hivyo 

viendelee itapambana hadi kuhakikisha makundi haya 

yanatokomea.


“nitoe indhari kuwa Serikali ya Mkoa pamoja na Jeshi la Polisi 

halitakuwa tayari kumuachia kijana yoyote yule atakaebainika 

kujihusisha na vitendo vya kihalifu, ”amesema Mkuu wa 

Mkoa.


Amewataka wananchi waendelee kushirikiana na vyombo vya 

ulinzi hasa hasa jeshi la polisi kwa kuwapa taarifa sahihi za 

vikundi vya watu ambao wamekuwa wakijihusisha na vitendo 

vya uhalifu katika maeneo yao ili kuweza kudumisha amani na 

utulivu kwenye mkoa.


Nae Mkuu wa Wilaya Magharibi ‘B’ ambae pia  ni Kaimu wa 

Wilaya ya Magharibi  ‘A’  Hamida Mussa Khamis 

ameishukuru Kamati ya Usalama wa Mkoa kwa kuendelea 

kuzisimamia Wilaya zao na kutoa muongozo wa 

jinsi  ya  kukabiliana na uhalifu huo.


Akielezea wilaya yake amesema kuwa bado kumekuwa na 

changamoto kwa baadhi ya maeneo ambayo yamekuwa na 

vikundi vya uhalifu ikiwemo Kinuni Kwarara Hawai pamoja 

na Mchikichini.


Kwa upande wa Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi 

ACP Richard  Thadei Mchomvu amesema operesheni huo 

imefanyika kwa aina yake jambo ambalo limesaidia kuleta 

mafanikio ya kuwakamata wahalifu.


Hata hivyo amewapongeza masheha na wananchi kwa 

mashirikiano yao waliyoyatoa jambo ambalo limeweza 

kufanikisha zoezi hilo


Mali  zilizookolewa katika Operesheni hizo ni pikipiki 14, 

Televisheni 4 , simu 16, mifuko ya saruji 4, Tiles box  5, Viatu 

vya raba pair 6 , pasi za umeme 3, frame 44 za pikipiki aina ya 

klick na vespa pamoja na N’gombe 2.

Sambamba na hayo operesheni hiyo yameweza kukamata pombe za kienyeji lita 240 bangi gram 32, mitambo mitatu ya kutengenezea pombe za kienyeji pamoja na kukamatwa wanawake sita wanaojishughulisha na pombe hiyo sambamba na kuvunjwa vijiwe (maskani) 60 za vikundi vya vijana. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.