Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimsikiliza Hope Mahokola (kushoto) ambaye ni Afisa Masoko wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ambaye alitoa maelezo kuhusu majiko yanayotumia umeme kidogo, wakati alipotembelea banda la maonesho la STAMICO katika Tamasha la Azimio la Kizimkazi lililofanyika Kilimahewa Majumbakumi, Ruangwa, Desemba 31, 2024. Kulia kake ni Mkuu wa Mkoa wa Lindi , Zainab Telack, wa pili kulia ni Mwakilishi wa Mkurugenzi wa TBC, Nestory Madirisha na kulia ni Mkurugenzi wa Idara ya Radio TBC, Anna Kwambaza. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu)
WAZIRI MKUU, Kassim Majaliwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameiheshimisha Tanzania katika hamasa ya matumizi ya nishati safi ya kupikia kutokana na umuhimu wake kwenye afya ya binadamu na utunzaji wa mazingira.
Amesema kuwa kutokana na jitihada hizo, mashirika ya kimataifa yameonesha nia ya kumuunga mkono ikiwemo kufanya mkutano mkubwa wa nishati safi Afrika hapa nchini. “Watanzania tumuunge mkono Rais Dkt. Samia katika kampeni hii na kuhakikisha tunaongoza kwenye matumizi ya nishati safi barani Afrika”
Amesema hayo leo (Jumanne, Desemba 31, 2024) wakati wa Tamasha la Azimio la Kizimkazi ambalo lilienda sambamba na ugawaji wa majiko 1000 ya gesi kupitia kampeni ya matumizi ya nishati safi ya kupikia. Tukio hilo limefanyika katika eneo la Kilimahewa Majumbakumi, Ruangwa mkoani Lindi.
“Tunapaswa kumuunga mkono kwasababu agenda imeanzishwa na Rais wetu, dunia lazima iitambue Tanzania kama ambavyo imetambua na kuleta mkutano mkubwa wa nishati safi hapa nchini, sisi tusiwe nyuma, tuwe mstari wa mbele”
Aidha, Mheshimiwa Majaliwa ametoa wito kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuibeba ajenda ya nishati safi ya kupikia na kuhamasisha umuhimu wa matumizi ya nishati hiyo ikiwemo umeme, gesi na mkaa rafiki.
Akizungumza katika tukio hilo, Mkuu wa Mkoa wa Lindi Zainab Telack amesema kuwa azimio la kizimkazi linakwenda kuwa mkombozi kwa mwanamke kupata nishati safi ya kupikia.
Mmoja ya wanufaika wa mpango huo wa ugawaji wa mitungi ya Gesi Hawa Mpinga mkazi wa Kata ya Nachingwea amesema awali walipata changamoto za kiafya kutokana na matumizi na nishati chafu “Moshi wa kuni umetuharibu sana macho”
Katika tukio hilo Mheshimiwa Majaliwa amewaga mitungi ya gesi 1000, ambayo 800 imetolewa na Shirika la Utangaji Tanzania kupitia Bongo Fm na mitungi 200 imetolewa na Taifa gesi.
Baadhi ya washiriki wa Tamasha la Azimio la Kizimkazi lililofanyika Kilimahewa Majumbakumi, Ruangwa wakimshangilia mgeni rasmi Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa alipozungumza
Waziri Mkuu, Kassim Kajaliwa akimkabidhi jiko la gesi Salma Naonje wakati alipogawa majiko 1000 katika Tamasha la Azimio la Kizimkazi lililofanyika Kilimahewa Majumbakumi, Ruangwa
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa akimkabidhi jiko la gesi Fanzie Mtumba wakati alipogawa majiko 1000 katika Tamasha la Azimio la Kizimkazi lililofanyika Kilimahewa Majumbakumi, Ruangwa
No comments:
Post a Comment