Habari za Punde

Vijana Watakiwa Kuwa Wabunifu na kuchangamkia fursa za Ajira zinazopatikana katika maeneo wanayoishi badala ya kusubiri Ajira

 Waziri wa Habari, Vijana ,Utamaduni na Michezo Mhe Tabia Maulid Mwita amewataka Vijana kuwa wabunifu  na  kuchangamkia fursa za Ajira  zinazopatikana katika maeneo  wanayoishi badala ya kusubiri Ajira zinazotolewa na  Serikali. 


Akizungumza Kwa Niaba ya Waziri wa  Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Katibu Mtendaji wa Baraza la Vijana Zanzibar Ali Haji Hassan  katika Kongamano la Vijana wa Mkoa wa Kusini lililofanyika  katika  Ukumbi wa Skuli ya Sekondari Kizimkazi Mkunguni .

Amesema Vijana ndio msingi wa Maendeleo hivyo ni vyema kuwa wabunifu katika kuzifuata fursa za Ajira zilizopo katika maeneo mbali mbali ili kuweza kujinyanyua kiuchumi na kuachana na utegemezi na kujiingiza katika makundi yasiofaa. 


Aidha ameyasema  kwa sasa Zanzibar kumekuwa fursa nyingi za ajira kutokana na uwepo wa  miradi mbali mbali ya kimaendeleo ikiwemo sekta Rasmi na zilizokuwa sio Rasmi .

Akitolea mfano wa ajira hizo kwa Vijana ni kujiajiri katika sekta ya  Utalii, Uvuvi na kuhifadhi Mazingira hivyo kuwataka Vijana kujiajiri katika Sekta hizo ili kukuza Uchumi wao na pato la Taifa. 

" Vijana tutambue Serikali zetu hizi haziwezi kutoa Ajira kwa Vijana  isipokuwa inatuandalia mazingira bora ya kujiajiri ikiwa ni pamoja kutupatia fursa za kutujengea uwezo wa kutuajiri na kutupatia mikopo  nafuu" alisema ndugu Hassan 

 Akizungumzia suala  Amani Katibu Ali amewasisitiza Vijana  kulinda Amani na kujiepusha katika kuchangia uvunjifu wa Amani  kabla wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu na kusema ili maendeleo ya Nchi na ustawi wa Wananchi uimarike  kunatakiwa kuwepo kwa Amani.

Aidha amewataka Vijana hao kuwa Mabalozi wa kuyasemea na kuyatangaza maendeleo yaliotekelezwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dokta Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dokta Hussen Ali Mwinyi. 

Akielezea Dira ya Maendeleo ya Zanzibar ya mwaka 2050 na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2025 -2030 amesema imekusudia kuimarisha Uchumi na Ustawi wa Jamii hivyo kuwataka Vijana kuhakikisha wanatekekeza kwa vitendo kwa kuzichangamkia fursa ili kufikia lengo lilolokusudiwa.


Kwa upande wa Katibu Mkuu Taifa CHAMATA Association Peter Christopher Ngwele amesema Kongamano hilo litawasaidia Vijana  wa Mkoa huo kutambua fursa za kiuchumi zinazopatikana ndani ya Mkoa wa Kusini na Umuhimu wa matumizi ya nishati mbadala ili kuhifadhi Mazingira na kuzuia athari za mabadiliko ya Tabianchi. 

Aidha katika Kongamano hilo Vijana wa Mkoa kupitia Taasisi ya CHAMATA watapatiwa elimu itakayowasaidia kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 kwa njia ya Amani na kuchagua Viongozi watakaoliongoza Taifa la Tanzania na kuendelea kuleta maendeleo kwa Wananchi. 

Kongamano hilo la siku moja limeaandaliwa kwa mashirikiano ya  Taasisi ya CHAMATA Association, Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Kusini Unguja na Baraza la Vijana Wilaya ya Kusini Unguja.

Imetolewa na Kitengo Cha Habari 
WHVUM.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.