Habari za Punde

Wadau Utalii Washauri Serikali Kuonheza Bajeti ya Kamisheni


Na Abdi Shamnah

WADAU wa Utalii kutoka sekta binafsi, wameishauri Serikali kuongeza maradufu bajeti ya Kamisheni ya Utalii Zanzibar, ili iweze kujitangaza vyema katika soko la utalii na kufikia dhana ya Zanzibar kuwa kituo bora cha utalii Duniani.

Wakizungumza na Waziri wa Habari, Utamaduni, Utalii na Michezo, Said Ali Mbarouk, katika ukumbi wa Hoteli ya Bwawani jana,  wadau hao wamesema Bajeti ya Kamisheni hiyo kwa mwaka ni ndogo mno kiasi ambacho haitoi taswira kuwa Serikali inalipa uzito unaostahili suala la kukuza Utalii.


Hii ni mara ya kwanza kwa Waziri Mbarouk kukutana na wadau hao kutoka taasisi za ZATI na ZATO pamoja na Mameneja wa Hoteli mbali mbali za kitalii hapa Zanzibar na kupata fursa ya kubadilishana uzoefu, tangu alipoteuliwa kushika wadhifa wa kuwa Waziri wa  Wizara hiyo inayohusika na Utalii. 

Walisema Zanzibar ina nafasi kubwa ya kujitangaza katika soko la Utalii Duniani na kupata mafanikio makubwa kama ilivyo Mauritius na baadhi ya nchi zilizo katika ukanda wa Mashariki ya  Afrika, pindipo itatenga bajeti kubwa katika kujitangaza kupitia masoko mbali mbali.

Walisema Zanzibar imebarikiwa kuwa na vivutio vizuri zaidi ya Mauritius, lakini nchi hiyo imepata mafanikio makubwa baada ya kutenga bajeti kubwa ya kujitangaza na kuimarisha miundo mbinu yake ya kiutalii.

‘Mauritius hutenga bajeti ya US Dolla Milioni 26 kwa mwaka ,wakati bajeti ya Kamisheni ya Utalii Zanzibar ni T.Shilingi Milioni 225 tu, hii haionyeshi kuwa Serikali iko ‘serious’ katika dhamira ya kukuza utalii, alisema meneja wa Hoteli ya Blue bay.

Mapema, akielezea dhima waliyonayo wekezaji katika Sekta ya utalii Zanzibar, Mkurugenzi Mtendaji wa ZATI Julia  Bishop, alisema tayari kuna mafanikio yaliokwisha kupatikana katika maendeleo ya utalii,  ikiwemo uhifadhi wa maeneo ya vivutio vya utalii, kuongeza mitaji na kupunguza umasikini kwa jamii.

Alisema kuwepo kwa matamasha ikiwemo lile la Sauti za Busara lililofanyika mapema mwaka huu (February), limesaidia sana kuongeza idadi ya ujio wa watalii hapa nchini.

Hata hivyo alisema mbali na mafanikio hayo pia kuna changamoto kadhaa zinazokwaza maendeleo ya sekta hiyo, na kuyataja baadhi ya mambo hayo kuwa ni pamoja na utaratibu usioeleweka wa ukusanyaji wa mapato, usalama wa wageni, vifaa duni na kuwepo urasimu katika uwanja wa ndege, vizuizi vingi vya Polisi na bughudha za mapapasi kuingilia kazi za watembeza watalii.

Akitoa nasaha zake, Waziri Mbarouk aliwahakikishia wadau hao kuwa Serikali imeupokea na itaufanyia kazi ushauri wote uliotolewa ili kufikia lengo la kuimarisha utalii na kukuza uchumi wa nchi.

Alisema katika kufanikisha dhana hiyo anakusudia kuwa karibu sana na wadau hao na kuahidi kukutana nao kila baada ya miezi mitatu ili kuona kunakuwepo ushirikiano wa kutosha baina ya Serikali na wadau wa sekta binafsi.

Nae Mshauri maalum wa Rais katika mambo ya Utalii, Issa Mohammed, alimhakikishia Waziri Mbarouk kuwa  wadau hao kutoka sekta binafsi watashirikiana vyema na Serikali, ili kufikia dhana ya ‘utalii kwa wote’.

Wakati huo huo Waziri wa Habari, utamaduni ,utalii na michezo, Said Ali Mbarouk
akifuatana na Balozi mdogo wa Oman aliopo Zanzibar Mansour Al Busaid, jana walitembelea na kukagua maeneo mbali mbali ambapo Oman inalenga kuisaidia Zanzibar, ikiwa ni utekelezaji wa makubaliano yaliotiwa saini kati ya nchi hiyo na Zanzibar “momerundum of understandng’ Agost 17, 2010.

Miongoni mwa maeno hayo ni pamoja na makumbusho mawili yaliopo Mnazimmoja, Beit el Ajaib, Makaburi ya ukoo wa kifalme Forodhani pamoja na gofu la Maruhubi Palace.

Hatua hiyo inalenga kuyafanyia matengenezo majengo ii kuyarejesha katika hali yake ya asili na kuendeleza uhifadhi wa historia, kwa lengo la kuendeleza utalii.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.