Habari za Punde

Hotuba ya Mheshimiwa Naibu Waziri Biashara, Viwanda na Masoko Mama Thuwaybah Kissasi - Uzinduzi wa Ijtimai ya Kimataifa


HOTUBA YA MHESHIMIWA NAIBU WAZIRI WA BIASHARA, VIWANDA NA MASOKO MH. THUWAYBAH KISSASI KATIKA UZINDUZI WA IJITIMAI YA KIMATAIFA FUONI - UNGUJA TAREHE 29-APRIL-2012.



Bismillahi Rahmani Rahim

Amir Mkuu wa Fiiysabililah Tabligh Markaz Zanzibar,
Ndugu Viongozi mbali mbali,
Maamiri,  Masheikh , Maduati, Tull-bul ilmu na
Wageni waalikwa wote,
Ndugu Waumini mabibi na mabwana mliofika katika ulingano huu kutoka kwa Mola wetu

Assalamu Aleykum Warahmatullahi Wabarakatuh”

Ndugu zangu katika Uislam
Kwanza kabisa nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu alieturuzuku neema kubwa ya uislamu; na akatuwezesha kukutana katika uzinduzi wa ijitimai yetu hii pahala hapa pa kheri tukiwa wazima na wenye Amani. 
Pia Rehma na Amani zimshukie Kiongozi wetu na Kigezo chetu, Mtume Muhammad (S.A.W), jamaa zake, Masahaba zake, wafuasi wake, pia wazee na Masheikh wetu wote walio hai na waliokwisha kutangulia mbele ya haki.



Ndugu zangu katika Uislam
Kwa kuitikia amri ya Mtume (S.A.W) isemayo “Hamshukuru Mwenyezi Mungu asiewashukuru watu” basi pia nitoe shukrani zangu za dhati kwa Jumuiya ya Fii-sabilillah Tabligh Markaz na wale wote waliochangia kwa hali na mali katika kuifanikisha maandalizi ya uzinduzi wa Ijitimai hii. Wananchi wa Fuoni wanatambua na kuthamini  juhudi kubwa kabisa walizozichukuwa maamiri katika kuandaa mkusanyiko huu kwa kuitekeleza aya isemayo “nia ya kheri na kuamrisha mema na kukataza maovu…” Ala Imran aya ya 104. Aidha niseme asanteni sana kwa kunialika ili kujumuika nanyi leo hii  katika kheri hii. Namuomba Mwenyezi Mungu atutakabalie na aiweke juhudi hii katika mizani ya mema yetu- Amin.

Lengo kubwa la Ijitimai  ni kukumbushana mambo ya kheri, kuamrishana mema na kukatazana maovu. Na hii ndio sababu iliyopelekea umma wetu huu wa Mtume Muhammad (SAW) kuwa ni bora zaidi kuliko wote waliokuja kabla yetu kama alivyosema Mwenyezi kwamba ‘’Hakika ninyi ni Umma bora, mumeletwa ninyi kwa ajili watu, naamrishana mema na mnakatazana maovu na mnamuamini Mwenyezi Mungu”. Al-Imraan aya 110. Pia mkusanyiko huu wenye waumini kutoka pande mbali mbali ni fursa nzuri ya kuelewana, kujenga umoja na mshikamano, na kushauriana katika kutafuta mbinu za kujiletea maendeleo ya dini na dunia yetu.




Ndugu zangu katika imani,

Taasisi zetu za dini zimekuwa zikitoa mchango mkubwa katika nchi yetu hii, Sote ni mashahidi namna viongozi wa dini walivyoshikamana katika kuunganisha jamii hasa pale jamii yetu ilipofarakana kwa sababu za kisiasa. Aidha tunashuhudia kazi kubwa inayofanywa na mashekhe, maduati, maulamaa na taasisi za dini katika kuelimisha umma, kujenga tabia na maadili mema, kuhimiza uadilifu na uwajibikaji.
Ndugu Waislamu na ndugu Wananchi, kazi ya kulingania ni shughuli yetu sote, hivyo ni jukumu la kila mmoja wetu kujituma kwa mujibu wa uwezo wake aliojaaliwa na Allah (SW).  Hata hivyo hatuna budi kutambua kuwa kazi hii ina miiko na maadili yake (Lingania katika njia ya Mola wako kwa hekma na mawaidha mazuri na jadiliana nao kwa namna njema zaidi). An-Nahli aya ya 125. Hekma ina maana kubwa lakini kwa wepesi kabisa tunaweza kusema kuwa ni kukiweka kila kitu katika pahala pake panapostahiki. Hivyo katika ulinganio wetu tuangalie mahitaji yetu na shida zinazotukabili ili tuweze kuisaidia jamii yetu katika changamoto inazokabiliana nazo na kuleta maendeleo. Iwapo maadili na miiko hii haitofuatwa, mlinganiaji anaweza kubomoa badala ya kujenga na akaleta madhara makubwa badala ya kuinufaisha jamii.  Na kama tunavyofahamu, sasa Nchi yetu inakabiliwa na masuala mawili muhimu, moja ni:-
Ø mchakato wa kurekebisha Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania basi niwaombe masheikhe wetu, walimu wote, na Maaulamma , tuwaaidhi watu katika hali ya Amani na Utulivu, ili kujenga mustakbali mwema katika nchi yetu. Kwani Mwenyezi Mungu anatuhimiza kushikamana kwa kusema “Shikamaneni katika kamba ya Mwenyezi Mungu na wala msifarikiane” Aya ya 103 Al-Imran.
Ø suala la pili ni zoezi zima la kuhesabu watu (Sensa ya Watu na Maakazi), zoezi ambalo linatarajiwa kufanyika kuanzia usiku wa kuamkia Jumapili ya tarehe 26-agosti 2012.
Ni dhahir kuwa mpangilio wa masuala ya kuwapelekea maendeleo wananchi wake, katika Nchi yoyote ile duniani si rahisi kufanyika kwa ufanisi kama Nchi hiyo haitokuwa na uhakika wa idadi ya wananchi wake. Sote tunakumbuka kuwa kwa mara ya mwisho watu walipohesabiwa ni karibu miaka kumi iliyopita, na sote ni mashahidi ya jinsi tulivyoongezeka na jinsi huduma zinavyoonekana hazitoshelezi. Kwa mfano, hivi sasa tunaambiwa kutokana na makisio tu, inakadiriwa kuwa Zanzibar tuko watu karibu 1,200,000 lakini kwa kuangalia na kwa hesabu za harakaharaka, wako wanaosema kuwa tuko zaidi ya hesabu hiyo. Lakini ukweli ni pale tunapoona kuwa huduma kama za hospitali, maskulini, na masuala mengine kama kuwafikishia umeme na maji wananchi tunavyoona, pamoja na jitihada zote za Serikali yetu,lakini bado huduma hizo hazitoshi.
Hivyo ni wajibu wetu kuwaelimisha jamiii umuhimu wa kutoa mashirikiano kadri itakavytakiwa katika kuhakikisha mpango huu muhimu kwa Nchi yetu unafanikiwa kwa manufaa yetu, Nchi yetu na Taifa kwa jumla.

Ndugu Waislam ,
Sisi waumuni tumezunguukwa na nur kila pembe ya maisha yetu ‘Allah  Nur, Wa Muhammad Nur, Wal Quran.

Ndugu waislam na ndugu wananchi,

Masheikh na Tull-Ibul-ilmi, hivi sasa tunaishi katika ulimwengu uliopiga hatua kubwa katika nyanja za habari na mawasialiano.  Kwa vile na sisi ni sehemu ya dunia, tujifunze na tuyatumie maendeleo hayo na faida zake kwa kujiletea manufaa ya kidunia na akhera, hata hivyo tusije tukasahau kuwa dini yetu imetuwekea dira ya kufuata tunaposikia habari yoyote.  Tusiwe na pupa, jazba, wala tusiwe wepesi wa kushawishika; bali tunaposikia chochote tupime na kuthibitisha. 

Ndugu Waislamu, nakuombeni tuitumieni fursa yetu ya kukutana pamoja kwenye Ijitimai hii kwa kutafakari matatizo yanayozikabili jamii zetu na kutafuta mbinu muwafaka za kiimani zitakazotusaidia kuondosha au kupunguza matatizo hayo. Tutumieni muda wetu kushauriana juu ya hayo na kutafuta njia muwafaka ya kupambana nayo kwa mbinu bora tulizofundishwa na dini yetu. Tunasihiane wala tusitukanane, tujadiliane wala tusishindane kwa uadui, tuombeane kheri na uongofu wala tusilaaniane na kuhukumiana ukafiri au unafiki. Mwenyezi Mungu pekee ndie amjuae mchamungu na ndio ajuae yaliyofichwa vifuani mwetu. Wajibu wa muislamu ni kulingania tu na hidaya inatoka kwake Mwenyezi Mungu. Tufuate mwenendo wa Mtume wetu ambae pamoja na udhia mkubwa alioupata kutoka kwa Makureish hakukata tamaa kuwalingania kwa kila njia na kuwaombea kwa kusema “Mola wangu wasamehe kaumu yangu bila shaka wao hawatambuwi”.  Na sote tunaelewa historia yake ilivyoanza mpaka akapata ushindi mkubwa na watu wakawa wanaingia katika dini makundi kwa makundi.

Ndugu Waislamu, katika Ijitimai hii tutapata fursa ya kuwasikiliza masheikh, wanavyuoni na walinganiaji mbali mbali na kutoka sehemu tofauti.  Tukumbuke kuwa lengo sio kusikia tu, bali kinachotakiwa ni kufuata.  Hivyo kila mmoja wetu aweke azma kuwa atayatumia mafunzo atakayoyapata hapa katika maisha yake yote.  Atazidi kuyatekeleza yale mazuri aliyonayo, atayawacha mabaya yaliyokatazwa, atadumisha mashirikiano na wenzake, atajipamba kwa subira na atatenga baadhi ya muda wake kwa kujifunza zaidi.  Ni matumaini yangu basi tukitoka hapa tutakuwa tumetengeneza vyema imani zetu.

Lakini kabla ya kumalizia naomba pia nichukue fursa hii kutoa wito kwa waislaam wote kuichangia kwa hali na mali, si lazima kikubwa, hata kidogo ulichonacho, kwani mbele ya Mwenyezi Mungu hakuna kidogo, ili Ijitimai yetu hii iweze kufanikiwa na Inshaallah malipo yake tutayakuta kwa Allah (SW).

Mwisho namuomba Mwenyezi Mungu aujaalie mkusanyiko huu uwe wa kheri, fanaka na faida nyingi, vile vile tumuombe Mwenyezi Mungu atujaalie Matayarisho ya Katiba Mpya yawe ya Amani na tulivu katika Nchi yetu. Pia ninawakaribisha wageni wote waliotoka sehemu mbali mbali za Tanzania na nje ya Tanzania wajione kuwa wapo nyumbani  kwa kuwa Jimbo hili la Fuoni limepata bahati kubwa ya kuwa na wageni wa namna hii basi tuwakirimu wageni wetu kwa njia nzuri  na ninaamini kwamba kuwepo kwao sisi tutafarajika zaidi na ninaishukuru tena Jumuiya ya Fiisabilillah Tabligh Markaz na wote waliofanikisha mkusanyiko huu.  

“SASA NAOMBA NITAMKE KUWA IJITIMAI YA KIMATAIFA YA MWAKA 2012, MARKAZI FUONI KUANZIA TAREHE 6-8 JULAI
IMEZINDULIWA RASMI”

Wabillah Tawfiq

Ahsanteni sana

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.