Habari za Punde

Hotuba ya Bajeti ya Afisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi - 1


UTANGULIZI


1.       Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu, likae kama Kamati kwa madhumuni ya kupokea, kujadili, kuzingatia na hatimae kuidhinisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa mwaka wa fedha 2012/2013.

2.       Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema kwa kutujaalia uzima na afya njema na kuweza kukutana hapa katika kikao hiki muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu. Aidha, nachukua fursa hii adhimu kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kutuongoza, kutuelekeza na kusimamia ipasavyo utekelezaji wa majukumu ya Serikali kama ilivyoainishwa katika miongozo iliomo katika Mipango Mikuu ya Kitaifa, Kimataifa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2010 -2015.
 
3.       Mheshimiwa Spika, ni dhahiri juhudi zake anazozichukua katika kulitumikia Taifa na kuweza kutenga muda maalum wa kukutana na watendaji ili kupitia mipango ya utekelezaji wa bajeti ya kila Wizara bila ya kuchoka tena kwa uadilifu, umahiri na umakini mkubwa umeleta mabadiliko makubwa ya kiutendaji ndani ya Serikali. Hakika changamoto anazotupa zimetufanya tuwe na mtizamo mpya katika upangaji na utekelezaji wa kazi zetu. Hatua hii imeleta uwazi, ubunifu na uwajibikaji katika kusimamia maadili ya matumizi ya fedha za umma. Namuomba Mwenyezi Mungu ampe umri mrefu na afya njema ili aweze kuiongoza vema nchi yetu.

4.       Mheshimiwa Spika, nawapongeza Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad Makamo wa Kwanza wa Rais na Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi Makamo wa Pili wa Rais kwa kumsaidia kwa dhati kabisa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar katika utekelezaji wa kazi zake. Aidha, nawapongeza Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza la Mapinduzi kwa kazi nzuri wanazozifanya katika kuitumikia nchi yetu.

5.       Mheshimiwa Spika, naomba kukupongeza wewe binafsi, Naibu wako na Wenyeviti kwa kuliongoza vizuri Baraza letu. Umahiri wako katika kutuongoza umepelekea kukua na kuimarika kwa demokrasia na mijadala iliyo wazi, inayosisimua na inayovutia wananchi wetu. Hali hii imejenga imani kubwa ya wananchi kwa chombo chao cha kutunga Sheria pia kujenga imani na viongozi waliowachagua.  

6.       Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee natoa pongezi maalumu kwa Kamati za Kudumu za Baraza la Wawakilishi zinazofanya kazi na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Kamati hizo ni Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Hamza Hassan Juma, Mwakilishi wa kuchaguliwa na wananchi wa Jimbo la Kwamtipura ambae pia ni Mwenyekiti wa Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Baraza la Wawakilishi. Vile vile Kamati ya Kusimamia Hesabu za Serikali (PAC) inayoongozwa na Mheshimiwa Omar Ali Shehe, Mwakilishi wa Jimbo la Chake Chake. Ushauri na miongozo yao mizuri imesaidia sana katika kufanikisha utekelezaji wa majukumu yetu ya kila siku na tunawaahidi kuwa tutaendelea kutoa ushirikiano wetu kwao. Naomba pia kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza la wawakilishi ambao kwa namna moja au nyengine wamekuwa wakifanya kazi na Wizara zetu.

7.       Mheshimiwa Spika, Hotuba yangu hii inalenga kutoa maelezo ya kina ya utekelezaji wa malengo ya bajeti ya mwaka 2011/2012. Aidha, nitaeleza pia muelekeo wa vipaumbele vya bajeti na malengo yatakayotekelezwa na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika mwaka ujao wa fedha 2012/2013.

8.       Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa malengo ya bajeti kwa kipindi cha Julai- Machi 2011/2012 kwa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi umezingatia vipaumbele vilivyowekwa katika malengo ya bajeti ya mwaka wa fedha wa 2011/2012. Sambamba na malengo hayo, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar ilitekeleza miradi kumi ya maendeleo. Miradi hiyo ni kama ifuatayo:-

i.            Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali (State Lodges)
ii.                   Kuimarisha Mawasiliano Ikulu
iii.                  Mageuzi ya Serikali za Mitaa
iv.                 Uendelezaji Vitambulisho
v.          Ujenzi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kaskazini Unguja
vi.                 Ujenzi wa jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja
vii.                Shamba la Mfano la Mbogamboga-Bambi
viii.              Ujenzi wa Makao Makuu ya Valantia
ix.        Ujenzi wa Hospitali mpya ya Kikosi cha Kuzuia Magendo  (KMKM)
x.                   Ujenzi wa Chuo Kipya cha Mafunzo Hanyegwa Mchana

9.       Mheshimiwa Spika, Aidha, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ilitekeleza Mradi wa Mpango wa Kuimarisha Huduma za Miji Zanzibar (Zanzibar Urban Service Programme ZUSP). Usimamizi wa utawala na fedha wa mradi huu upo chini ya Ofisi ya Rais, Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo.

10.   Mheshimiwa Spika, matayarisho ya bajeti ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, kwa Mwaka wa fedha 2012/2013, yamezingatia mipango ya kisekta iliyowekwa katika Dira 2020 (Vision 2020), malengo ya maendeleo ya Milenia, Mkakati wa Kukuza Uchumi na Kupunguza Umasikini (MKUZA II) na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala cha CCM ya 2010 – 2015 pamoja na vipaumbele ambavyo vimewekwa ili kutatua changamoto mbali mbali. Kwa ujumla, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi inalenga kutekeleza vipaumbele katika mambo yafuatayo:-

i)         Kuendeleza umoja wa kitaifa na mshikamano.
ii)       Kusimamia utekelezaji wa miundo ya utumishi na uhakiki wa kazi kwa watendaji.
iii)      Kuendelea kuimarisha makaazi na nyumba za Ikulu.
iv)     Kuendelea kuimarisha mawasiliano na utoaji wa habari.
v)       Kuendelea na jitihada za kufanya Mageuzi ya Serikali za Mitaa ikiwemo kufanya mapitio ya mipaka ya maeneo pamoja na kusimamia utungaji wa Sheria kama inavyoelekezwa na matamko ya Sera ya Serikali za Mitaa.
vi)     Kuimarisha uwezo na utoaji wa huduma ikiwemo usafi hasa mijini.
vii)    Kuendelea kuimarisha na kuongeza uwezo wa Idara Maalum za SMZ ikiwemo kuimarisha haki za binadamu kwa wanafunzi waliopo Chuo cha Mafunzo na kujenga Chuo kipya Hanyegwa Mchana.
viii)  Mafunzo kwa wafanyakazi juu ya haja ya kubadilika kiutendaji na kufahamu dhamana walizonazo hasa katika mazingira wanayofanyia kazi.
ix)     Kuimarisha tafiti kwa lengo la kupata taarifa zitakazowezesha kupanga mipango kulingana na matokeo ya tafiti hizo.
x)       Kuendelea kuimarisha mfungamano wa Kikanda ili Wazanzibari waweze kuzitumia fursa za kiuchumi zinazotokana na Jumuiya ya maendeleo ya Kusini mwa Afrika na Jumuiya ya Afrika ya Mashariki pamoja na Jumuiya nyengine za Kikanda.
xi)     Kuwashajihisha Wazanzibari wanaoishi nchi za nje kushiriki na kuchangia maendeleo ya kijamii na kiuchumi ya nchi yao.
xii)    Kutoa elimu kuhusu masuala mtambuka (cross cutting issues) yakiwemo huduma za watu wenye ulemavu, kujikinga na maambukizi mapya ya UKIMWI na VVU.
xiii)  Kwa kusaidiana na vyombo vyengine vya Kitaifa, kuimarisha ulinzi na usimamizi madhubuti wa mipaka yetu pamoja na kudhibiti magendo na uharamia.

11.   Mheshimiwa Spika, sambamba na malengo na vipaumbele vya jumla, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi itatekeleza jumla ya miradi minane ya maendeleo iliyopo hapa chini:-

i)         Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali (State Lodges)
ii)       Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano - Ikulu
iii)      Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa
iv)     Mradi wa Kuimarisha Kiwanda cha Ushoni Zanzibar Quality Tailoring cha Idara Maalum za SMZ
v)       Ujenzi wa Hospitali ya KMKM
vi)     Ujenzi wa Makao Makuu ya Kikosi cha Valantia
vii)    Mradi wa Shamba la Mfano la Mboga Mboga JKU
viii)  Ujenzi wa Chuo kipya cha Mafunzo Hanyegwa Mchana

12.   Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu Serikali ilikuwa katika mchakato wa kuandaa Sera ya Serikali za Mitaa ambayo ndiyo muongozo wa utekelezaji wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa, napenda kuliarifu Baraza lako Tukufu kwamba Sera hiyo sasa imekamilika. Utaratibu wa maandalizi ya Sera hii, umefuata hatua kadhaa zikiwemo, (a) Mapitio ya taarifa na Sera mbali mbali zikiwemo tafiti zilizofanywa juu ya mageuzi ya Serikali za Mitaa Zanzibar, (b) Mapitio ya MKUZA na DIRA ya Maendeleo ya 2020, (c) Mapitio ya Sheria mbali mbali zinazohusu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, (d) Kufanya mapitio ya muundo wa Serikali za Mitaa (e) Mahojiano na baadhi ya watendaji na             (f) Mikutano ya Wadau Unguja na Pemba kikiwemo kikao cha Makatibu Wakuu na  Kamati ya Uongozi ya Wizara na hatimae kupitishwa rasmi na Baraza la Mapinduzi.Sera hii inakwenda  sambamba na utekelezaji wa maazimio ya kupeleka madaraka kwa wananchi. Aidha, Sera ya Serikali za Mitaa inatoa Mamlaka na nguvu za Utawala katika Serikali za Mitaa na inalenga kutoa msukumo maalumu wa kuishirikisha jamii katika mipango ya kujiletea maendeleo kutoka katika ngazi ya chini kwa misingi ya ushirikishwaji.

13.   Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, sasa naliomba Baraza lako Tukufu liniruhusu kuwasilisha utekelezaji wa malengo ya bajeti ya mwaka wa fedha 2011/2012 pamoja na mwelekeo wa bajeti ya mwaka wa fedha 2012/2013 kwa Idara na Taasisi zote zilizo chini ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.

MUUNDO WA OFISI YA RAIS NA MWENYEKITI WA BARAZA LA MAPINDUZI


14.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi inajumuisha Ofisi, Idara, Vitengo na Taasisi zifuatazo:-
a)       Ofisi ya Faragha ya Rais
b)       Ofisi ya Baraza la Mapinduzi
c)       Idara ya Mipango, Sera na Utafiti
d)       Idara ya Uendeshaji na Utumishi
e)       Idara ya Mawasiliano Ikulu
f)        Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO)
g)       Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba
h)       Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho
i)         Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Uratibu wa Shughuli za Wazanzibari wanaoishi Nchi za Nje
j)         Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (inajumuisha Serikali za Mikoa, Wilaya na Serikali za Mitaa)
k)       Idara ya Uratibu wa Idara Maalum za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (inajumuisha Idara Maalum za SMZ).


OFISI YA FARAGHA YA RAIS


15.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha ya Rais inashughulikia kuratibu shughuli za kila siku za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, kusimamia ratiba za kazi, kuweka kumbukumbu za mazungumzo yanayofanyika na kutayarisha muhtasari wa ripoti. Kadhalika, Ofisi hii inasimamia upatikanaji wa huduma zote za Mheshimiwa Rais na kushughulikia utunzaji na matengenezo ya nyumba zote za Ikulu.
16.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2011/2012, Ofisi ya Faragha ya Rais iliidhinishiwa TZS 520 milioni kwa kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi Machi 2012, Ofisi hii iliingiziwa TZS 466.3 milioni sawa na asilimia 89.7 ya makadirio ya matumizi.
17.   Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Faragha ya Rais imetekeleza vyema mujukumu na malengo yake kwa kuratibu ziara za Mheshimiwa Rais ambapo alikutana na wananchi, viongozi wa Mikoa, Wilaya na baadhi ya Taasisi za Serikali. Kwenye ziara hizo, Mheshimiwa Rais alishuhudia hatua mbali mbali za maendeleo na alielezwa changamoto na hatua zinazochukuliwa katika kukabiliana nazo. Miongoni mwa Taasisi alizozitembelea ni Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), Shirika la Utangazaji Zanzibar, Mamlaka ya Maji (ZAWA) na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar. Katika Taasisi zote hizo alizozitembelea aliridhishwa na juhudi zinazochukuliwa na Taasisi hizo na wananchi katika kujiletea maendeleo na kutoa maelekezo ya namna ya kuimarisha huduma kwa wananchi.
18.   Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ziara za Mikoa, Ofisi ya Faragha ya Rais iliratibu ziara hizo kwa kushirikiana na uongozi wa Mikoa. Katika kila Mkoa, Mheshimiwa Rais alipokea taarifa za utekelezaji na kupata ufafanuzi wa baadhi ya mambo muhimu. Aidha, Mheshimiwa Rais alikagua miradi ya maendeleo ikiwemo ya Serikali na iliyoanzishwa na wananchi wenyewe. Katika ziara hizo aliwasisitiza viongozi wa Mikoa na Wilaya kuhakikisha kwamba wanatatua wenyewe migogoro ya ardhi iliyopo na kuepukana na kuanzisha migogoro mipya ya ardhi.
19.   Mheshimiwa Spika, mambo mengine yaliyojitokeza ni pamoja na vitendo vya uharibifu wa mazingira na udhalilishaji wa kijinsia ambapo Mikoa yote imeagizwa kuandaa mikakati ya kuvidhibiti vitendo hivyo haraka iwezekanavyo. Kwa ujumla ziara hizi zimeonesha mafanikio makubwa na kuwafurahisha wananchi, ambapo walipata fursa za kuainisha matatizo yao na kupatiwa ufumbuzi wa papo kwa papo. Kadhalika, ziara hizi zimesaidia kuongeza ukaribu kati ya wananchi na Serikali yao na pia kuhuisha matumaini yao katika kujiletea maendeleo na kuendeleza hali ya amani na utulivu.  
  
20.   Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha 2011/2012, Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi alifanya ziara katika Umoja wa Nchi za Falme za Kiarabu (Ras el Khaimah, Sharjah na Dubai). Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na ujumbe wake walikutana na Mtawala wa Ras el Khaimah Sheikh Saud Saqr Al Qasimi na Mtawala wa Sharjah Sheikh Dkt. Sultan bin Mohammed Al Qasimi. Serikali ya Ras el Khaimah na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimetia saini mkataba wa makubaliano (MOU) katika Nyanja kadhaa za kiuchumi na maendeleo ya jamii. Kadhalika, Hospitali Kuu ya Ras el Khaimah imetiliana saini (MOU) na Wizara Afya ya Zanzibar kwa lengo la kushirikiana katika matibabu ya maradhi ya kisukari, figo, moyo na saratani. Sharjah nayo imekubali kimsingi kuisaidia Zanzibar katika utafiti wa maji yaliotuwama chini ya ardhi. Kwa jumla ziara ya Mheshimiwa Rais katika Falme za Kiarabu imefungua milango mipya ya ushirikiano katika nyanja  zote muhimu na itasaidia kuongeza kasi ya maendeleo ya Zanzibar.
21.   Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha ushirikiano wa kimataifa  Mheshimiwa Rais wa Zanzibar amekutana na Viongozi na Mabalozi mbali mbali wakiwemo mwana wa Malkia wa Uingereza Mheshimiwa Prince Charles na mkewe Camilla Parker Bowles, Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Mheshimiwa Dkt Asha Rose Migiro, Waziri anaeshughulikia Maendeleo ya Kimataifa wa Finland Mheshimiwa Heldi Hantaka na Waziri wa Afya wa Norway Mheshimiwa Anne-Grete Strom-Erichsen.Viongozi wote hao  walimueleza Mheshimiwa Rais namna walivyofurahishwa na maendeleo ya Zanzibar pamoja na hali ya amani na utulivu. Viongozi wengine mashuhuri waliokutana na Mheshimiwa Rais wanaonekana katika Kiambatanisho Namba 1.
22.   Mheshimiwa Spika, mbali na mafanikio hayo, Ofisi ya Faragha ya Rais pia imetekeleza malengo yake mengine kama ifuatavyo:-
a)       Kufanya matengenezo ya sehemu ya kufulia na varanda katika Ikulu Kuu ya Mnazi mmoja pamoja na kufanya matengenezo ya kawaida Ikulu ya Chake Chake ikiwa ni pamoja na kuweka vipoza hewa. 
b)       Ofisi imewaongezea uwezo wa kiutendaji wafanyakazi wake watano (5) kwa kuwapatia mafunzo na kuwalipia ada na vifaa vya masomo katika nyanja za menejimenti na huduma za chakula na vinywaji katika Chuo cha Maendeleo ya Utalii Maruhubi. 
c)       Ofisi imeifanyia matengenezo makubwa maktaba ya Mheshimiwa Rais. Maktaba hiyo imo katika hatua za mwisho za ujenzi.
d)       Ofisi imenunua vifaa mbali mbali vya kazi za kila siku za ofisi ikiwa ni pamoja na vifaa vya kuandikia, majalada, magazeti, kompyuta sita (6) pamoja na uchapishaji wa kadi na vitabu vya hotuba mbali mbali za Mheshimiwa Rais.
e)       Ofisi imetoa huduma zote muhimu kwa wageni wa Mheshimiwa Rais pamoja na kufanikisha sherehe mbali mbali zinazofanyika Ikulu.
 
23.   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013, Ofisi ya Faragha ya Rais imepanga kutekeleza malengo yafuatayo:-
a)       Kuendelea kuimarisha shughuli za kila siku za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
b)       Kuimarisha mazingira ya wafanyakazi (Work environment) na kununua vitendea kazi.
c)       Kuendeleza matunzo ya nyumba za Ikulu na vifaa vinavyostahiki.
d)       Kuwajengea uwezo wa kiutendaji wafanyakazi wa Ofisi ya Faragha ya Rais.

24.   Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Faragha ya Rais iweze kutekekeza majukumu na malengo yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/13, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 1,908.3 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

OFISI YA BARAZA LA MAPINDUZI


25.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi inayoongozwa na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi imepewa uwezo wa Kikatiba na Kisheria wa kuratibu na kusimamia shughuli zote za Baraza la Mapinduzi na Kamati zake mbali mbali ikiwa ni pamoja na Kamati ya Kitaalamu ya Makatibu Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (Inter-Ministerial Technical Committee).

26.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 836 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi kufikia Machi 2012, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi iliingiziwa TZS 644 milioni sawa na asilimia 77.0 ya makadirio ya matumizi ya kawaida na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Imeandaa vikao 25 vya Baraza la Mapinduzi na vikao 21 vya Kamati ya Makatibu Wakuu na kujadili nyaraka mbali mbali zikiwemo Sera na Miswada ya Sheria (Viambatanisho 2 na 3) vinatoa ufafanuzi zaidi.
b)       Imeratibu na kusimamia vikao 8 vya Kamati Maalum ya Baraza la Mapinduzi, Kamati ya Fedha, Uchumi na Maendeleo ya Jamii pamoja na Kamati nyenginezo zilizopewa majukumu maalum ya kuyafanyia kazi. 
c)       Imeratibu mikutano 48 ya pamoja kati ya Mheshmiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Wizara za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
d)       Imenunua meza na viti vipya pamoja na kufunga mtambo wa sauti katika ukumbi wa Vikao vya Baraza la Mapinduzi.
e)       Imefanya matengenezo makubwa katika Ofisi zake ziliopo katika Jumba la wananchi, Forodhani ikiwa ni pamoja na kutengeneza chumba madhubuti (strong room) kwa ajili ya kuhifadhia kumbukumbu muhimu na kutengeneza Ofisi tatu za Mawaziri wasio na Wizara Maalum.
f)        Imehifadhi kumbukumbu za zamani za Baraza la Mapinduzi ili kuzinusuru kuharibika kwa kuzitengenezea vitabu pamoja na kuhifadhi nyaraka na kumbukumbu hizo kwa njia ya elektroniki.
g)       Imewapatia wafanyakazi wake watatu mafunzo ya muda mrefu katika fani za utawala, usimamizi wa fedha na uandishi wa sheria.
h)       Imeandaa mafunzo maalumu kwa wafanyakazi wake kuhusu mbinu na mikakati ya kupambana na maambukizi mapya ya UKIMWI.

27.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Baraza la Mapinduzi inakusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kuhakikisha kuwa Baraza la Mapinduzi na Kamati ya Makatibu Wakuu wanatekeleza ipasavyo majukumu yao ya kikatiba na kisheria.
b)       Kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi kwa Wajumbe wa Baraza la Mapinduzi na watumishi wa Ofisi ya Baraza la Mapinduzi.
c)       Kuwajengea uwezo watumishi ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
d)       Kutunza na kuhifadhi nyaraka na kumbukumbu muhimu za Ofisi
e)       Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia watendaji stahili zao
f)        Kutathmini utendaji na uwajibikaji wa Serikali.

28.         Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Baraza la Mapinduzi iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 1,362 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA MIPANGO, SERA NA UTAFITI


29.   Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti ina jukumu la kuandaa na kusimamia utayarishaji wa Sera, Sheria, Mipango na kufanya utafiti na tathmini kwa miradi ya maendeleo. Aidha, ina jukumu la kufuatilia, kukusanya na kuchambua takwimu zitakazosaidia kufanya tathmini na kupanga mipango ya maendeleo. Vile vile, Idara inaratibu utekelezaji wa DIRA 2020, MKUZA II, Mageuzi Makuu (Core Reforms), Ilani ya Uchaguzi ya CCM, Chama Tawala ya mwaka 2010 - 2015 na mipango mengine mikuu ya Kitaifa na Kimataifa. Jukumu jengine ni kuratibu kazi za kuandaa ripoti za utekelezaji wa Bajeti na Mipango ya Maendeleo.

30.         Mheshimiwa Spika, Idara ya Mipango Sera na Utafiti, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 240 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na hadi kufikia Machi 2012, Idara hii iliingiziwa TZS 158.5 milioni sawa na asilimia 66.0 ya makadirio ya matumizi ya kawaida na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Imetoa elimu ya uibuaji na uimarishaji wa miradi kwa maofisa 25 wa miradi.
b)       Imenunua samani pamoja na kukusanya vitabu kwa ajili ya kitengo cha nyaraka (Documentation Centre).
c)       Imeanzisha tovuti (Website) ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na kutayarisha Barua Pepe rasmi (Official E-mail Address) za maafisa wote na watendaji wengine.
d)       Imeanzisha kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA) na kukipatia samani na vitendea kazi vikiwemo kompyuta tatu, 3G computer modem, anti virus software na vifaa vya kuhifadhia kumbukumbu.
e)       Imewajengea uwezo watendaji wake kwa kufanya ziara za kujifunza katika Ofisi za Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) zilizopo Dodoma na Dar es Salaam. Aidha, wafanyakazi watatu wamepatiwa mafunzo ya muda mfupi, kati ya wiki mbili hadi nne katika fani za uchambuzi wa Sera, kufanya ufuatiliaji na tathmini kwa kuangalia matokeo pamoja na uwajibikaji katika bajeti, sambamba na kuendesha semina mbili kwa Maafisa Mipango 52 wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Unguja na Pemba ili waweze kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi na namna bora ya kuandika ripoti za utekelezaji.
f)        Imefanya mapitio ya Mpango Mkakati wa miaka mitano wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
g)       Imenunua vitendea kazi vikiwemo kompyuta nne, fotokopi kubwa moja, skana moja, na samani za Ofisi zikiwemo meza na viti.
h)       Imeandaa ripoti za utekelezaji wa malengo ya bajeti ya mwaka 2011/2012, utekelezaji wa miradi ya maendeleo na Ilani ya Uchaguzi ya Chama Tawala cha CCM ya mwaka 2010-2015.
i)          Imeratibu utekelezaji wa miradi 10 ya maendeleo inayotekelezwa na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kuitembelea na kufanya tathmini juu ya utekelezaji wake na kujua hatua iliyofikia.
j)         Kwa kushirikiana na Idara ya Utumishi na Uendeshaji, imetoa mafunzo juu ya kujikinga na maambukizi mapya ya UKIMWI na VVU kwa watendaji 34.

UTEKELEZAJI WA MIRADI YA MAENDELEO KWA MWAKA 2011/2012


31.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2011/2012, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi iliidhinishiwa kutekeleza miradi 9 ya maendeleo na fedha zilizotengwa kwa miradi hiyo ni TZS 1,930.0 milioni. Idara ya Mipango, Sera na Utafiti imeratibu utekelezaji wa miradi hiyo kwa ufanisi mkubwa. Naomba kuitaja miradi hiyo kama ifuatavyo:-

i)         Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali (State Lodges)
ii)       Kuimarisha Mawasiliano Ikulu
iii)      Mageuzi ya Serikali za Mitaa
iv)     Uendelezaji Vitambulisho
v)       Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kaskazini Unguja
vi)     Ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Mkuu wa Mkoa Kusini Unguja
vii)    Shamba la Mfano la Mboga Mboga Bambi
viii)  Ujenzi wa Makao Makuu ya Valantia
ix)     Ujenzi wa Hospitali mpya ya Kikosi cha KMKM        

Mradi wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali


32.      Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali uliidhinishiwa TZS 300 milioni na hadi kufikia mwezi Machi 2012, mradi huu umeingiziwa TZS 300 milioni sawa na asilimia 100.0 ya makadirio ya matumizi na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Kukamilisha matengenezo ya Ikulu ndogo ya Migombani kwa kuweka grill za chuma sehemu 16 eneo la pwani, kutengeneza  msingi unaopokea maji ya mvua mbele ya Geti kuu, kujenga ukuta mpya sehemu ya kufulia, kuweka paa, kutengeneza mageti matatu, kulipa gharama za matengenezo ya waya na vioo vya madirisha, kulipa gharama za  uwekaji wa viegesho vya gari (car parking shades), kulipa gharama za matengenezo ya Msikiti, kulipia gharama za matengenezo ya jiko la nje pamoja na kujenga ukuta (fence) sehemu ya pembeni ya eneo la nyumba ya Migombani.
b)       Kulifanyia ukarabati jengo la Ikulu Kuu (Mnazi Mmoja) kwa kutia rangi ukuta na kutengeneza sehemu ya vyoo.
c)       Kuanza ujenzi wa nyumba ya Ikulu ndogo ya Laibon Dar-es-salaam kwa kufanya marekebisho ya jikoni na kuweka makabati ya aluminium, kugharamia uwekaji wa mtambo wa Intercom na kulipa gharama za kutengeneza na kufunga viegesho vya gari (car parking shades).

Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano – Ikulu


33.      Mheshimiwa Spika, mradi wa Kuimarisha Mawasiliano - Ikulu uliidhinishiwa TZS 100 milioni na hadi kufikia mwezi Machi 2012, fedha zilizoingizwa ni TZS 100 milioni sawa na asilimia 100 ya makadirio ya matumizi. Fedha zote zimetumika kwa kununulia gari la mawasiliano aina ya Toyota VX na vifaa vyake vikiwemo mabomba, inverter, wireless microphones na amplifier.

Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa


34.      Mheshimiwa Spika, Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa uliidhinishiwa TZS 150 milioni na hadi kufikia mwezi Machi 2012, fedha zilizoingizwa ni TZS 86.3 milioni sawa na asilimia 57.5 na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Sera ya Serikali za Mitaa imekamilika. Viliandaliwa jumla ya vikao kumi vya wadau wa sera wakiwemo Makatibu wakuu, Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Madiwani, Wenyeviti wa Halmashauri na Mabaraza ya Miji, Maofisa wa wizara za SMZ na Taasisi zisizo za kiserikali (NGO’S) kwa kukusanya maoni ambayo yalisaidia sana katika kukamilisha sera hiyo.
b)       Imeandaa hadidu rejea za kutayarisha Mpango Mkakati.
c)       Imeandaa madodoso ya kufanya utafiti unaolenga ukusanyaji wa mapato na uwezo wa kiutendaji katika Serikali za Mitaa.

35.      Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa miradi mingine sita (6) niliyoitaja awali nitaitolea maelezo yake katika Idara husika.

36.      Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Mipango Sera na Utafiti imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kuimarisha uwezo wa Idara katika kupanga, kuandaa na kuchambua Sera, kufanya tafiti pamoja na kuratibu shughuli za mipango na bajeti za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
b)       Kufanya uchambuzi wa Sera ya Serikali za Mitaa ili iweze kutekelezeka na kufanya uchambuzi wa Mpango Mkakati wa Chuo cha Mafunzo na kuhakikisha utekelezaji wake.
c)       Kuandaa utafiti unaolenga kutanua wigo katika ukusanyaji wa Mapato kutoka Serikali za Mitaa kwa kushirikiana na Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.
d)       Kuratibu na kuandaa ripoti za utekelezaji wa malengo ya bajeti pamoja na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2010-2015.
e)       Kuandaa mfumo shirikishi wa ufuatiliaji na tathmini kwa Miradi ya Maendeleo inayotekelezwa na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi
f)        Kuimarisha uwezo wa watendaji kitaaluma.
g)       Kuimarisha na kutunza kitengo cha Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEKNOHAMA).
h)       Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia watendaji stahili zao, kununua vitendea kazi vya kisasa vya Ofisini na samani.

MIRADI YA MAENDELEO ITAKAYOTEKELEZWA KWA MWAKA 2012/2013


37.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2012/2013, Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi itatekeleza miradi ifuatayo:-

i)         Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali (State Lodges)
ii)       Mradi wa Kuimarisha Mawasiliano - Ikulu
iii)      Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa
iv)     Mradi wa Kuimarisha Kiwanda cha Ushoni cha “Zanzibar Quality Tailoring” cha Idara Maalum za SMZ

Mradi wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali (State Lodges)

 

38.         Mheshimiwa Spika, Mradi wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali utatekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kujenga nyumba mbili za wafanyakazi na walinzi ndani ya eneo la Ikulu ndogo ya Laibon Dar es Salaam.
b)       Kuezeka nyumba ya Ikulu ndogo ya Mkoani na kutengeneza kibanda cha walinzi.
c)       Kuanza ukarabati mkubwa wa nyumba tatu za Ikulu ya Chake Chake.
d)       Kukamilisha ujenzi wa nyumba ya Serikali ya mapumziko Micheweni.

Mradi wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Ikulu na Nyumba za Serikali unakadiria kutumia TZS 400 milioni.

Mradi wa Mawasiliano – Ikulu


39.         Mheshimiwa Spika, Mradi wa Mawasiliano – Ikulu utatekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kufanya matengenezo ya chumba kwa ajili ya utayarishaji wa vipindi
b)       Kununua vifaa vya kisasa kwa ajili ya kurikodia sauti na picha
c)       Kununua mashine za kufanyia uhariri wa vipindi

Mradi wa Mawasiliano - Ikulu unakadiria kutumia TZS 100 milioni.

 

Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa


40.         Mheshimiwa Spika, Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa utatekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kupitia na kuunda mipaka mipya ya Mamlaka ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
b)       Kusambaza na kusimamia utekelezaji wa Sera ya Serikali za Mitaa
c)       Kuunda vikundi kazi vitakavyotumika katika kupitia mfumo wa Kodi na Mapato wa Serikali za Mitaa na Muundo wa Serikali za Mitaa na Utawala.
d)       Kupitia na kufanya marekebisho ya Sheria Namba 1 ya mwaka 1998, ya Mamlaka ya Utawala wa Mikoa na Sheria Namba. 3 na 4 ya mwaka 1995 ya Serikali za Mitaa

 Mradi wa Mageuzi ya Serikali za Mitaa unakadiria kutumia TZS 150 milioni.


Mradi wa Kuimarisha Kiwanda cha Ushoni cha “Zanzibar Quality Tailoring” cha Idara Maalum za SMZ


41.         Mheshimiwa Spika, Mradi mpya wa Kukiimarisha Kiwanda cha Ushoni “Zanzibar Quality Tailoring” cha Idara Maalum za SMZ unakusudia kukipa uwezo kiwanda hicho kwa kununua vifaa vya kisasa vikiwemo vyarahani na mashine za kufumia. Mradi huu utakapokamilika unategemewa kushona aina zote za Sare za Idara Maalum za SMZ na kuondokana na utaratibu wa kuagizia vifaa hivyo kutoka nje.

Mradi wa Kuimarisha Kiwanda cha Ushoni cha Idara Maalum za SMZ unakadiria kutumia TZS 256 milioni.

42.         Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Mipango, Sera na Utafiti iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 466.9 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida na TZS  906 milioni kwa matumizi ya kazi za maendeleo.

IDARA YA UENDESHAJI NA UTUMISHI


43.         Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi ina jukumu la kusimamia shughuli za Utawala na Utumishi zikiwemo kusimamia Sheria na Kanuni za Utumishi kwa wafanyakazi, kuweka mazingira mazuri ya utendaji kazi, kusimamia Sheria ya Ununuzi na uondoaji wa mali chakavu za Serikali, kuwaendeleza wafanyakazi kielimu pamoja na kusimamia maslahi yao.

44.         Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 1,858.5 milioni kwa kazi za kawaida. Fedha hizi zilitumika pia kwa kulipia mishahara ya Ofisi ya Faragha ya Rais, Idara ya Mawasiliano – Ikulu, Idara ya Uendeshaji na Utumishi, Idara ya Mipango, Sera na Utafiti na Idara ya Uratibu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hadi kufikia mwezi Machi 2012, Idara hii iliingiziwa TZS 1,810.4 milioni sawa na asilimia 97.4 ya makadirio ya matumizi ya kawaida na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Idara imenunua zana na samani za Ofisi zikiwemo Kompyuta sita, Vespa moja,  meza 13, viti 19, makabati mawili, mafriji manne, Mafeni manne, Vipoza hewa (Air Candition) vitano, fotokopi mashine moja pamoja na kufanya matengenezo ya Ofisi na matengenezo ya magari.
b)       Idara imesimamia maslahi ya wafanyakazi wakiwa kazini na baada ya kustaafu kwa kuwalipa maslahi yao.
c)       Idara imeendesha vikao sita vya Bodi ya Zabuni na vikao vitatu vya Kamati ya Ukaguzi wa ndani
d)       Idara imewajengea uwezo wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu wafanyakazi sita na mafunzo ya muda mfupi wafanyakazi watatu. Aidha Idara imetoa taaluma ya kujikinga na maambukizi mapya ya UKIMWI kwa wafanyakazi 38 wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi sambamba na kutoa taaluma inayohusu maadili ya kazi na utunzaji wa siri za ofisi kwa watendaji 45 wa kada ya masjala. Idara pia imeratibu mafunzo kwa watendaji wa Idara zote zilizo chini ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi  
e)       Idara imetoa motisha kwa wafanyakazi kwa kuwapatia malipo baada ya saa za kazi kwa wafanyakazi 28, sare kwa wafanyakazi 26 pamoja na kutoa zawadi kwa wafanyakazi bora watatu.
f)        Idara imeweka mfumo bora wa usimamizi na utoaji wa taarifa katika uwajibikaji kazini kwa kuendesha semina ya uandaaji wa taarifa za kiutumishi na Sheria ya Utumishi  wa Umma kwa Maofisa Utumishi 35 wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa Unguja na Pemba.
g)       Idara imefanya uhakiki wa mahitaji ya mafunzo ya wafanyakazi pamoja na kuandaa mpango wa mafunzo hayo. Kazi hiyo ipo katika hatua za mwisho kukamilika.
h)       Idara imepitia majukumu ya kazi ya wafanyakazi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na kuyagawa majukumu hayo kwa wafanyakazi.

45.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Uendeshaji na Utumishi imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia wafanyakazi stahili zao, kununua vitendea kazi vya kisasa na samani.
b)       Kusimamia sheria ya manunuzi pamoja na kuratibu vikao vya kamati ya ukaguzi wa ndani.
c)       Kuwaendeleza wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu wafanyakazi 3 katika ngazi za Shahada ya Uzamili, Shahada na Stashahada katika fani za Uongozi, Utawala na Uhasibu. Muda mfupi wafanyakazi 2 katika fani za Udereva, na Katibu Mukhtasi. Aidha, Mfanyakazi mmoja kujifunza lugha ya alama.
d)       Kuanda Mafunzo ya Maadili na Kazi za Ofisi ya Rais (Ikulu).
e)       Kusimamia upatikanaji wa Hati Miliki za Majengo yote ya Ikulu na Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi.
f)        Kutoa taaluma katika masuala mtambuka ikiwemo kujikinga na maambukizo mapya ya UKIMWI na huduma za watu wenye ulemavu.
g)       Kuandaa mpango wa matumizi ya Rasilimali watu pamoja na kupitia muundo wa Utumishi na kupandisha daraja watumishi (scheme of services).
h)       Kufanya uhakiki wa kazi na kutoa nyongeza ya mishahara ya wafanyakazi
i)         Kukamilisha kufanya uhakiki wa mahitaji ya mafunzo na kuandaa mpango wa mafunzo.

46.         Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Uendeshaji na Utumishi iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 1,247.3 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

IDARA YA MAWASILIANO – IKULU


47.         Mheshimiwa Spika, Idara ya Mawasiliano Ikulu ina jukumu la kutoa, kuratibu na kupokea taarifa za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuhusu utekelezaji wa Sera na Mipango ya Serikali inayolenga kuwaletea maendeleo wananchi. Aidha, Idara hii ina jukumu la kuthibitisha na kuhakikisha kuwa taarifa zote za Mheshimiwa Rais zinazotolewa kwa wananchi na wadau wengine ni sahihi na zinatolewa kwa wakati muafaka.

48.         Mheshimiwa Spika, majukumu mengine ni kutambua fursa ambazo zinaweza kutumika ili kuimarisha mawasiliano baina ya Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Taasisi za Serikali na wananchi pamoja na kuhakikisha kuwa wananchi wanaarifiwa kila hatua za yale yote yaliyoahidiwa kwao na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi. Lengo ni kuweka taswira nzuri baina ya Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, wananchi na washirika wengine wa maendeleo. Aidha, Idara ya Mawasiliano ina jukumu la kuandaa utaratibu utakaomuwezesha Mheshimiwa Rais kukutana na kuzungumza na wahariri na waandishi wa habari juu ya mambo yanayohusu Zanzibar na maendeleo yake na kwa mnasaba huo huzungumza na wananchi kila baada ya miezi mitatu.

49.         Mheshimiwa Spika, Idara ya Mawasiliano Ikulu, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 80.7 milioni kwa kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi Machi 2012, Idara hii iliingiziwa TZS 53.7 milioni sawa na asilimia 66.5 ya makadirio ya matumizi ya kawaida na kutekeleza yafuatayo:-
a)       Imeandaa vipindi 25 vya televisheni kuhusu utekelezaji wa ahadi za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kama zilivyoelezwa kwenye Ilani ya Chama Tawala cha CCM pamoja na ahadi alizotoa wakati wa ziara za Mikoani.
b)       Imetoa mafunzo kwa maafisa mawasiliano wa Wizara na Taasisi za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Mafunzo hayo yaliyotolewa ni juu ya wajibu wa maafisa mawasiliano katika kutoa taarifa za Serikali kwa wananchi.
c)       Imewapatia mafunzo wafanyakazi watatu ambapo mfanyakazi mmoja anasomea fani ya ukatibu muhtasi, mmoja kujifunza programu maalum ya uhifadhi wa taarifa kwenye Kompyuta na mfanyakazi mwengine anasomea taaluma ya kazi kwa Vijana katika Chuo cha Mwalimu Nyerere Tawi la Zanzibar.
d)       Imechapisha matoleo matatu ya majarida ya Ikulu na toleo moja la kipeperushi lenye ujumbe wa mambo kumi ya msingi yanayopaswa kuzingatiwa na watendaji pamoja na wananchi.
e)       Imetembelea na kukutana na wakuu na waandishi wa vyombo mbali mbali vya ndani na nje ya Zanzibar kwa lengo la kuimarisha mawasiliano.
f)        Imenunua vitendea kazi vikiwemo vifaa vya kuandikia, seti ya kompyuta na vifaa vya kutengenezea gari.

50.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Idara ya Mawasiliano Ikulu imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kulinda na kuendeleza taswira ya Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa kutoa habari sahihi na kwa wakati.
b)       Kuratibu mikutano ya Mheshimiwa Rais na Vyombo vya Habari.
c)       Kuwajengea uwezo wafanyakazi watatu kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi.
d)       Kuwaendeleza wafanyakazi kwa kuwapatia mafunzo ya muda mrefu wafanyakazi wawili katika ngazi za Shahada na Cheti katika fani za Teknolojia ya Habari na Programu ya Kazi kwa Vijana. Muda mfupi mfanyakazi mmoja katika program maalum ya kuchambua habari za Magazeti.
e)       Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia watendaji stahili zao, kununua vitendea kazi vya kisasa na samani.

51.         Mheshimiwa Spika, ili Idara ya Mawasiliano Ikulu iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 174.9 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

 

KITENGO CHA USALAMA WA SERIKALI (GSO) ZANZIBAR


52.         Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) Zanzibar kimeanzishwa kwa Sheria Namba 3/1983 na kinatekeleza majukumu yake sambamba na Sheria ya Utumishi wa Umma “Public Service Act No. 2/2011”. Sheria hizi zimeainisha majukumu ya Kitengo cha Usalama wa Serikali kuwa ni udhibiti wa shughuli za Usalama wa Serikali na Utumishi wa Umma.

53.         Mheshimiwa Spika, Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) Zanzibar, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 kiliidhinishiwa TZS 49.8 milioni kwa kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi Machi 2012, kitengo hiki kiliingiziwa TZS 27.5 milioni sawa na asilimia 55.2 ya makadirio ya matumizi ya kazi za kawaida na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Kimefanya upekuzi kwa watumishi 554 kutoka katika Taasisi mbali mbali za Serikali na kutoa ushauri unaofaa baada ya upekuzi huo.
b)       Kimekagua jumla ya Taasisi 12 za Serikali katika kuangalia utunzaji wa siri za Serikali (idadi ya Taasisi zilizokaguliwa zinaonekana katika Kiambatanisho Namba 5).
c)       Kimeweza kufanya ukaguzi wa Taasisi 12 zenye vituo muhimu katika kuangalia usalama wa vituo hivyo na kupendekeza njia bora za kudumisha usalama.
d)       Kitengo kilitoa mafunzo ya Usalama na kuwaelimisha watumishi wa Taasisi nane ambazo zipo katika Kiambatanisho Namba 6.

54.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) kimekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kufanya upekuzi wa awali na upekuzi endelevu kwa watumishi 500 wa Serikali.
b)       Kuendeleza ushirikiano na Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora katika kusimamia kanuni za utumishi na kuhakikisha zinatekelezwa hususan zile zinazogusa usalama wa mali na nyaraka za serikali.
c)       Kuendelea kushirikiana na Maafisa Usalama wa Taasisi za Serikali katika kusimamia na kuhakikisha utekelezaji wa sheria zinazohusu utunzaji wa siri za Serikali.
d)       Kuweka mazingira bora ya kazi na kuimarisha utoaji wa huduma kwa wananchi.

55.         Mheshimiwa Spika, ili Kitengo cha Usalama wa Serikali (GSO) kiweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 54.9 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

 

OFISI YA AFISA MDHAMINI – PEMBA


56.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba ina jukumu la kuratibu na kusimamia shughuli za utawala na huduma za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi zinazofanyika Pemba. Aidha, Ofisi hii inaratibu ziara za Viongozi Wakuu wa Kitaifa na Kimataifa wanaotembelea Pemba. Majukumu mengine ni pamoja na kuratibu usimamizi wa nyumba za Ikulu. Vile vile, Ofisi ya Afisa Mdhamini inaratibu shughuli za Idara Maalum za SMZ pamoja na Mamlaka za Serikali za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa upande wa Pemba.

57.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 365.5 milioni kwa kazi za kawaida na hadi kufikia mwezi Machi 2012, Ofisi hii iliingiziwa TZS 322.5 milioni sawa na asilimia 88.2 ya makadirio ya matumizi ya kawaida na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Imeratibu ziara sita za Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na ziara moja ya Mheshimiwa Makamo wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kisiwani Pemba.
b)       Imewapatia nafasi za mafunzo wafanyakazi sita, wanne katika ngazi ya stashahada, wawili katika ngazi ya cheti na mfanyakazi mmoja amepatiwa mafunzo ya muda mfupi Tanzania Bara.
c)        Imetoa mafunzo kwa wafanyakazi 50 juu ya umuhimu wakupima VVU ili kujua afya zao, kubadili tabia na kuacha unyanyapaa kwa wafanyakazi wanaoishi na VVU na UKIMWI.
d)       Wafanyakazi 16 wamepatiwa mafunzo ya siku mbili (2) juu ya umuhimu wa Daftari la kudumu la mali za Serikali (Fixed Asset Register).
e)       Imefanya ukarabati wa jengo la Ofisi ya Afisa ya Mdhamini na imenunua vitendea kazi vikiwemo vespa moja, kompyuta mbili na samani.

58.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-
a)       Kuratibu, kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa shughuli zote za Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwa upande wa Pemba ikiwemo ziara za Viongozi Wakuu.
b)       Kuwajengea uwezo wa kitaaluma wafanyakazi saba kwa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi na mrefu katika kiwango na fani tofauti.
c)       Kufanya matengenezo madogo ya jengo la Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba.
d)       Kuratibu mafunzo ya kujenga uwezo wa Taasisi za Mabaraza ya Miji na Halmashauri katika kuzidi kuinua kiwango cha ukusanyaji mapato na uibuaji wa miradi ya jamii.
e)       Kuendelea kuwajengea uelewa wafanyakazi juu hatua za mapambano ya UKIMWI, utunzaji mazingira na uimarishaji wa utawala bora sehemu za kazi.
f)         Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia wafanyakazi stahili zao, kununua vitendea kazi vya kisasa na samani.

59.         Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Afisa Mdhamini Pemba iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 462.4 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida zikijumuisha TZS 115.7 kwa ajili ya ruzuku za Halmashauri za Pemba.

OFISI YA USAJILI NA KADI ZA UTAMBULISHO


60.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho imeanzishwa rasmi mwaka 2005 chini ya Sheria Namba 7/2005 ikiwa na wajibu wa kuwasajili na kuwapatia vitambulisho Wazanzibari wakaazi wenye umri wa miaka 18 na kuendelea. Aidha, Ofisi ina wajibu wa kutunza taarifa zote za wananchi zilizokusanywa kwa ajili hiyo.

61.         Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho, kwa mwaka wa fedha 2011/2012 iliidhinishiwa TZS 1,248 milioni kwa kazi za kawaida na TZS 150 milioni kwa kazi za maendeleo na hadi kufikia mwezi Machi 2012, Ofisi hii iliingiziwa TZS 886.9 milioni sawa na asilimia 71.1 ya makadirio ya matumizi ya kazi za kawaida na TZS 150 milioni sawa na asilimia 100 kwa kazi za maendeleo na kutekeleza yafuatayo:-

a)       Imesajili Wazanzibari wakaazi 10,578 waliotimiza masharti ya usajili na kutengeneza upya vitambulisho 3,932 ambavyo vimemaliza muda wake wa matumizi na kuvigawa kwa wahusika.
b)       Imetengeneza vitambulisho 10,393 vya wafanyakazi wa Serikali na Taasisi zake ambazo zimewasilisha taarifa za wafanyakazi kwa kutengenezewa vitambulisho.
c)       Imeandaa Rasimu ya marekebisho ya Sheria ya Usajili Namba 7 ya 2005 ili kuruhusu utoaji wa vitambulisho vya wageni wanaoishi nchini, rasimu hiyo tayari imeshapita Baraza la Mapinduzi na inasubiri kuwasilishwa kwenye Baraza lako Tukufu. Taratibu zote za kiutendaji zimekamilika ikiwa ni pamoja na mfumo wa utengenezaji wa vitambulisho hivyo, pamoja na fomu za maombi ya usajili.
d)       Ofisi imerusha hewani jumla ya vipindi 18 kupitia Shirika la Utangazaji la ZBC, juu ya kuelimisha matumizi bora ya kitambulisho cha Mzanzibari mkaazi.
e)       Imeendelea kuwajengea uwezo wafanyakazi 9 kwa kuwasomesha katika viwango vya Cheti na Stashahada pamoja na Shahada ndani na nje ya nchi.
f)        Imenunua Kompyuta 7 mpya kwa kubadilisha za zamani zilizokwisha muda wake.

62.         Mheshimiwa Spika, shughuli nyengine zilizofanywa na Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho ni kufanyiwa ukaguzi wa kimataifa kwa mara ya sita juu ya muundo, mfumo na taratibu zake za kiutendaji na imethibitishwa kuwa inaendelea kufanya kazi zake kwa mujibu wa viwango vya kimataifa vilivyowekwa na International Standard Organisation na IQ Net. Aidha, imekarabati vyumba viwili katika jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Kati ili Ofisi yake ya Tunguu iweze kuhamia Dunga kuondosha usumbufu wa kufuata huduma Tunguu katika jengo la Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja.

63.         Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho imekusudia kutekeleza malengo yafuatayo:-

a)       Kuendelea kuwasajili Wazanzibari Wakaazi 10,500 wanaotimiza masharti ya usajili na kuwapatia Vitambulisho.
b)       Kuendelea kutengeneza vitambulisho vipya kwa ajili ya kubadilisha vitambulisho vilivyomaliza muda wake wa matumizi. Pia kuwabadilishia vitambulisho vipya vya Wazanzibari Wakaazi walioomba kufanya mabadiliko halali ya taarifa zao binafsi na waliopoteza.
c)       Kuendelea kubadilisha na kutengeneza vitambulisho vya wafanyakazi wa Wizara, Idara na Taasisi za Serikali kwa kuzingatia muundo mpya wa Mawizara ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. 
d)       Kuanza kutoa vitambulisho maalum kwa wageni wanaoishi nchini kwa ruhusa maalum (Residence Permit) na kutunza taarifa zilizokusanywa kwa ajili hiyo katika database ya Serikali mara baada ya marekebisho ya Sheria ya usajili Namba 7/2005 kupitishwa na Baraza la Wawakilishi.
e)       Kuendelea kutoa elimu kwa jamii juu ya matumizi bora na sahihi ya vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi kama ambavyo sera inavyoelekeza.
f)        Kuendelea kuwajengea uwezo kielimu wafanyakazi wa Ofisi.
g)       Kuendelea kununua malighafi za utengenezaji wa vitambulisho sambamba na kubadilisha mitambo iliyochakaa na kwisha muda wake zikiwemo seti za kupigia picha (Kits).
h)       Kuongeza ufanisi kazini ikiwemo kuwapatia wafanyakazi stahili zao

64.         Mheshimiwa Spika, ili Ofisi ya Usajili na Kadi za Utambulisho iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi, kwa mwaka wa fedha 2012/2013, naliomba Baraza lako Tukufu liidhinishe TZS 1,593 milioni kwa matumizi ya kazi za kawaida.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.