Habari za Punde

Mikutano, maandamano ya CCM, CHADEMA yasimamishwa


Na Rose Chapewa, MOROGORO
KAMANDA wa polisi mkoani hapa Faustine Shirogile amepiga marufuku maandamao  na  mikutano iliyokuwa imepangwa kufanywa na  vyama  vya  siasa vya Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) na chama cha  Mapinduzi (CCM).

Shirogile alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa kufutia maombi ya vyama hivyo kuomba mikutano hiyo kwa muda na tarehe zinazofanana.

Alisema jeshi hilo limeamua kupiga marufuku maandamano na mikutano kutokana na sherehe za Nanenane na mgomo wa walimu hadi hapo jeshi hilo litakapotoa taarifa nyengine.

Alisema kuwa CCM waliomba kufanya mkutano wa hadhara kuanzia   Agosti 4 hadi  Agosti 8 mwaka huu katika maeneo ya Manispaa ya Morogoro  katika  uwanja wa skuli ya Kiwanja cha Ndege huku CHADEMA nao wakiwa wameomba kwa tarehe hizo hizo na maeneo sawa.


Kamanda huyo alisema kuwa kutokana na kuwepo na shughuli hizo za kitaifa  waliona  jeshi hilo litazidiwa na hivyo kuamua kuzuia mikutano na maandamao hayo ili kutoa fursa kwa polisi kufanya shughuli zao kwa ufanisi.

“Askari tulionao ni wachache hatuwezi kuwagawanya katika shughuli zote hizo kwa wakati mmoja, maandamao na mikutano lazima yalindwe, na polisi kwa sasa wako mitaani kuangalia suala la walimu sambamba na shughuli za kitaifa za Nane nane hivyo mikutano hiyo tunasitisha hadi hapo tutakapoona shughuli hizo zimekwisha’’, alisema.

Hata hivyo aliwatahadharisha wananchi mkoani hapa kutojihusisha na mikutano na maandamano na kwamba atakayejihusisha atachukuliwa hatua za kisheria.

“Wananchi wasijihusishe na suala la mikusanyiko yeyote tumepiga marufuku, waendelee na shughuli zao kinyume na hapo hatua za kisheria zitachukuliwa kwa yeyote atakayejihusisha na mikusanyiko”, alisema Kamanda huyo.

Kwa upande wao CCM wamekiri kupokea barua ya katazo hilo na kudai kuwa wamesitisha mikutano yao kufutia amri hiyo ya polisi na hadi hapo watakapotaarifiwa kufanya hivyo.

Katibu wa CCM wilaya ya Morogoro mjini Ali Issa alisema kuwa walipanga kufanya mikutano hiyo na kwamba baada ya katazo hilo wamesitisha  kutokana na majukumu hayo ya kitaifa.

Naye Mwenyekiti wa CHADEMA mkoa wa Morogoro ambaye ndiye anaratibu shughuli hizo Suzan Kiwanga, alisema kuwa wao kama CHADEMA hawako tayari kutii agizo hilo na kwamba maandamano yako pale pale.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.