Habari za Punde

Vyombo vya Dola viwajibike katika kusimamia haki

Na Khamis Amani
 
VYOMBO vya dola nchini, vimetakiwa kutekeleza ipasavyo wajibu na  majukumu yao kwa kusimamia haki kwa mujibu wa sheria.

Vyombo hivyo vimefahamishwa kuwa, kila mtu ana wajibu wa kupata haki zake za msingi anazostahiki kwa mujibu wa sheria, bila ya ubaguzi wala upendeleo wa aina yoyote.

Agizo hilo limetolewa na hakimu Ame Msaraka Pinja wa mahakama ya wilaya Mwanakwerekwe, kufuatia malalamiko yaliyowasilishwa na washitakiwa saba wa kesi ya uchochezi na kufanya fujo na vitendo vya ukiukwaji wa sheria wanavyofanyiwa wakiwa kizuizini mahabusu ya Chuo cha Mafunzo Kilimani mjini Unguja.


Kauli hiyo ya hakimu Pinja, ni msisitizo wa agizo lake alilolitoa mahakamani hapo katika kikao kilichopita cha Novemba 7 mwaka huu, la kutaka washitakiwa hao kutendewa haki kisheria kama wanavyotendewa mahabusu wengine.
 Katika kikao hicho, hakimu Pinja alisema kuwa vyombo vya dola vinavyohusika na usimamizi wa washitakiwa hao, vinapaswa kuwatendea haki kama raia wengine na kusimamia na kutekeleza wajibu wao bila ya ubaguzi.
 Washitakiwa walilalamika mbele ya hakimu kwamba hawatendewi vyema wakiwa rumande ikiwa ni pamoja na kunyimwa fursa ya kukutana na jamaa zao, kutopelekewa chakula kutoka kwa jamaa zao na kunyimwa fursa ya kuchanganyika na mahabusu wengine.
 
Mambo mengine wanayodaiwa kufanyiwa ni kuwekwa kila mshitakiwa ndani ya chumba chake bila ya kutoka nje isipokua nyakati za asubuhi kwenda haja na mchana wakati wa kula, pamoja na kutopewa haki ya kuabudu kwa kuchanganyika kusali sala ya jamaa na Ijumaa pamoja na mahabusu wengine.
 
Madai ya washitakiwa hao wakiwemo viongozi wakuu watatu wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiisilamu (JUMIKI) pamoja na wafuasi wao wanne,yaliwasilishwa mahakamani Na Mawakili Salum Taufik na Abdallah Juma.
 
Katika kikao cha jana, Wakili Abdallah Juma aliiomba mahakama Isisitize agizo lake la  wiki iliyopita kuhusu ukiukwaji wa sheria.
 
 "Mheshiwa kwanza nawapongeza maafisa wa Vyuo vya Mafunzo kwa kutekeleza agizo lako kwa baadhi ya mambo kama kubadilisha nguo, na kunyolewa ndevu, kwa masuala hayo hivi sasa wateja wetu hawafanyiwi kama unavyoona, wamebadilisha nguo na hawakunyolewa tena ndevu", alisedai Wakili huyo wa utetezi.
 
 
Sambamba na hoja hizo, Wakili huyo wa utetezi aliiomba mahakama hiyo kuwapunguzia masharti ya dhamana wateja wao hao, kwani masharti yaliopo hivi sasa ni mazito na hayawezi kutekelezeka.
 
Alidai kuwa, suala la kumpata mfanyakazi wa serikali kwa wateja wao ni ngumu kutokana na mazingira ya kesi hiyo, na suala la fedha taslimu shilingi 1,000,000 ni kikwazo kutokana na wengi wa Wazanzibari wanaishi katika kiwango cha umasikini halikadhalika na wateja wao.
 
 Ukijibu hoja hizo upande wa mashitaka ulioongozwa na Mwanasheria wa serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) Ramadhan Abdallah, pamoja na kudai kutoamini kwake kama washitakiwa hao wamekosa wadhamini wenye sifa kwa mujibu wa kauli ya Wakili wao, lakini kwa upande wake hakukuwa na hoja juu ya ya suala hilo.
 
Kuhusu kutotendewa haki kwa washitakiwa hao, pande huo wa mashitaka ulidai kuwa suala hilo lipo juu ya mahakama kwani tayari imeshatoa maelekezo kwa mamlaka zinazohusika zitekeleze matakwa yao kwa mujibu wa sheria.
 
Hivyo alishauri kama wanaona matakwa hayo hayatekelezwi, wanapaswa watumie uzoefu na usomi wao kwa kufuata taratibu nyengine za kisheria kwa kwenda Mahakama Kuu kwa lengo la kutafuta haki za wateja wao.
 
Akitetea hoja hizo, Wakili Abdallah Juma alisema kuwa, sehemu pekee ya kutoa malalamiko hayo ni mahakamani, kwani mahakama inapaswa itambue kuwa wateja wao wamepelekwa rumande kwa amri yake, na mahakama haikusema wafanyiwe vitendo hivyo vya ukiukwaji wa sheria wanavyofanyiwa.
 
"Mheshimiwa suala la chakula na matibabu ni haki yao ya msingi, hivi leo wakiumwa kama hawapatiwi matibabu tupeleke malalamiko Mahakama Kuu", alihoji Wakili huyo wa utetezi.
 
Baada ya hoja hizo na kuzitolea maamuzi hayo, hakimu Pinja pia aliridhika na hoja za pande mbili hizo juu ya suala la dhamana kwa washitakiwa hao, na kuwataka kuwasilisha fedha taslimu shilingi 500,000 kila mshitakiwa badala ya 1,000,000 za awali, pamoja na kiwango kama hicho cha fedha taslimu kwa wadhamini wawili badala ya wote watatu.
 
Sambamba na sharti hilo, wadhamini wawili wawe ni wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), badala ya watatu waliowekwa awali na masharti mengine yataakia kama yalivyo.
 
Washitakiwa katika kesi hiyo ni Mselem Ali Mselem (52) mkaazi wa Kwamtipura, Farid Had Ahmed (41) wa Mbuyuni ambaye ni msemaji mkuu wa Jumuiya hiyo, pamoja na Azan Khalid Hamdani (43) anayeishi Mfenesini.
 
Wengine ni Mussa Juma Issa (37) mkaazi wa Makadara, Suleiman Juma Suleiman wa Makadara, Khamis Ali Suleiman (59) anayeishi Mwanakwerekwe na Hassan Bakari Suleiman (39) mkaazi wa Tomondo.
 
Wote hao wanakabiliwa na mashitaka ya uchochezi wa kufanya fujo, tukio ambalo lilidaiwa kutokea saa 11:00 za jioni ya Agosti 17 mwaka huu.
 
Kinyume na kifungu cha 45 (1) (a) (b) cha kanuni ya adhabu sheria namba 6/2004 sheria za Zanzibar, walidaiwa kutoa matamko ya uchochezi yanayoashiria uvunjifu wa amani na kusababisha fujo, maafa mbali mbali na mtafaruku kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
 
Tukio hilo lilidaiwa kutokea maeneo ya Magogoni Msumbiji wilaya ya Magharibi Unguja, wakati washitakiwa hao wakiwa ni wahadhiri toka Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiisilamu.
 
Upelelezi wa kesi hiyo ya jinai namba 380/2012 bado haujakamilika, na imeahirishwa hadi Disemba 4 mwaka huu kwa kujwa na washitakiwa wote hao wamerejeshwa rumande wakiwa chini ya ulinzi mkali wa askari Polisi wa Kikosi maalumu cha kutuliza ghasia (FFU).
 
Hali ya amani ilitawala kwa muda wote wakati washitakiwa hao wakiwa mahakamani hapo, kutokana na eneo zima linalolizunguka mahakama hiyo kudhibitiwa na askari Polisi wenye silaha mikononi wakisaidiwa na askari wa Vikosi.
 
 Waandishi wa habari wa vyombo mbali mbali hasa wapiga picha, jana walijikuta katika wakati mgumu katika utendaji wa kazi zao baada ya kutakiwa kukaa mbali na eneo la mahakama kufanya shughuli zao.
 
Ndugu na jamaa wa washitakiwa hao, nao pia kwa upande wao walitakiwa kukaa mbali na mahakama hiyo wakiwa wamezuiwa barabara kuu itokayo Amani kuelekea Kiembesamaki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.