Habari za Punde

Homa ya mapafu yaua mamia ya mbuzi



Na Hafsa Golo
MARADHI ya homa ya mapafu yanaendelea kuathiri katika kijiji cha Matemwe na kusababisha zaidi ya mbuzi 150 kufariki.

Wananchi wamepata hofu kuwa maradhi hayo huenda yakasambaa kwa binadamu kwa kuwa wamekuwa wakila nyama za mbuzi waliokufa kutokana na ugonjwa huo.

Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Daktari wa Mifugo Matemwe, Silima Mtwana Khamis maradhi hayo yamekuwa tishio kubwa kwa mbuzi, ambapo kati ya mbuzi 10 hadi  20 hufa kwa siku.

Alisema maradhi hayo yameingia katika kijiji hicho yakitokea Mkoani Tanga kutokana na ukiukwaji wa taratibu za kusafirisha wanyama.

"Wafugaji wana tabia ya kuingiza wanyama kwa njia za panya na kuacha kufuata taratibu hivyo wanyama huingia bila ya kuangaliwa na wahusika wa afya na maradhi haya yametokea Tanga,” alisema.


Aliiomba serikali kupeleka huduma za afya kwa wanyama ili kuepusha tatizo hilo kusambaa kwa mifugo mingine ikiwemo ng’ombe.

Aidha aliwataka wananchi kuwa na tahadhari wanapokula nyama ya mbuzi aliyefariki kutokana na ugonjwa huo.

Mfugaji wa mbuzi Mawazo Silima Mawazo, mkaazi wa Mbupurini Matemwe aliiomba serikali kuwapatia madaktari wa mifugo ili kuwapatia chanjo wanyama wao pamoja na  kuwaelimisha wafugaji  njia sahihi za kujikinga na ugonjwa huo.

Naye Mohamed Hamrani Khamis, mkaazi wa Tundanga alisema maradhi hayo yamekuwa yakienea kwa kasi katika vitongoji mbali mbali vya Matemwe, ambapo kwa siku zaidi ya mbuzi 50 hufa au kuchinjwa baada ya kuonekana kuwa na dalili za ugonjwa huo.

Tayari mbuzi 345 wameshapatiwa matibabu tokea ugonjwa huo uibuke.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.