Habari za Punde

Rais ZFA awagawa wadau. Jamhuri yahofia mechi yake na St. George kuvurugika



Na Haji Nassor, Pemba
SIKU chache baada ya Amani Ibrahim Makungu kutangaza kujiuzulu nafasi ya urais wa Chama cha Soka Zanzibar (ZFA), uamuzi huo umeonekana kuwagawa wadau wa soka kisiwani Pemba, huku wengine wakiiomba kamati tendaji ya ZFA kutomkubalia.
Wakizungumza na gazeti hili kwa nyakati tafauti, baadhi ya wadau hao wamesema Makungu ameshaonesha mwelekeo katika kuendeleza mpira wa miguu hapa Zanzibar, hivyo haitakuwa busara kumfungulia njia ya kuondoka madarakani.

Wamesema kiongozi huyo ndie pekee aliyeonesha nia ya kweli ya kukuza soka la visiwa hivi kutokana na mipango na mikakati yake ambayo muda mfupi tu baada ya kukaa madarakani imeanza kuonesha mwanga wa matumaini.

Meneja wa klabu ya Jamhuri Abdallah Abeid Mohammed ‘Elisha’, alisema hivi karibuni ZFA ilikuwa na mgogoro mkubwa ambao tayari umeshasuluhishwa kutokana na busara za Rais huyo, hivyo akasema si vyema kuendeleza mivutano isiyokuwa na tija kwa taifa.




Elisha amesema, hata kama Rais huyo alifuata taratibu za kuwasilisha barua ya kuomba kujiuzulu katika kamati tendaji, ni vyema kamati hiyo ilikatae ombi lake hilo, ili kumpa nafasi zaidi ya kutekeleza mipango yake ya kuendeleza soka hapa nchini.

Kwa upande mwengine, Meneja huyo alionesha wasiwasi juu ya kufeli kwa mpango wa timu yake kuwaleta washindani wenzao katika ligi ya mabingwa barani Afrika timu ya St. George ya Ethiopia, iwApo Makungu ataachiwe akiachIe kitI cha urais wa ZFA.

“Kutokana na hali ngumu ya kifedha inayotukabili, Makungu ametuhakikishia kutusaidia kwa asilimia kubwa, sasa sijui itakuwaje kama akiondoa mkono wake ndani ya ZFA. Mimi nasema kama kuna mgogoro viongozi wawekwe kitako ili waumalize’’, alifafanua Elisha.


Kwa upande wake, Msemaji wa timu ya Super Falcon Harith Bakari, alisema haoni sababu kwa Makungu kuachia ngazi, kwa kile alichodai kwamba viongozi wa ZFA Pemba wako makini katika kazi zao na haamini kuachia kwake ngazi kumetokana na kunyimwa ushirikiano.

Juzi, Amani Ibrahim Makungu aliandika barua kwa kamati tendaji ya ZFA kuomba kujiuzulu urais kwa madai ya kugomewa na wasaidizi wake wakuu kisiwani Pemba ambao haukuungana na ujumbe wa ZFA kutoka Unguja uliokwenda huko kuangalia maendeleo ya soka.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.