Na Abdi Suleiman, Pemba
LICHA ya viongozi wa klabu mbalimbali kisiwani Pemba na
wengine wa Chama cha Soka Zanzibar
wilaya tafauti kushikilia msimamo wa kumtaka Amani Ibrahim Makungu asiachie
ngazi, Rais huyo wa ZFA amesema wakati umefika aondoke kuliko kuendeleza
malumbano na viongozi wanaojali maslahi binafsi.
Akizungumza na viongozi wa klabu za madaraja mbalimbali
na viongozi wa ZFA Wilaya ya Mkoani wakati akihitimisha ziara yake kisiwani
Pemba, Makungu alisema tangu aingie madarakani kukiongoza chama hicho takriban
miezi saba sasa, malumbano kutoka kwa baadhi ya viongozi wanaojali matumbo yao yameendelea kukitafuna
chama hicho.
“Sasa naona bora nishughulikie biashara zangu kuliko kuendeleza malumbano na watu wasiokuwa
na imani na chama. Natamka wazi kuwa nimefikia kikomo kukiongoza chama”,
alisema kwa masikitiko.
Akifafanua namna alivyokosa ushirikiano kutoka kwa
viongozi wa ngazi za juu wa chama hicho, Makungu alisema baadhi ya wajumbe
walifikia kumwambia kuwa uongozi wake mwisho Nungwi, hali aliyodai kuikubali
kufuatia wasaidizi wake muhimu kutokujumuika pamoja naye kwenye ziara yake
aliyoifanya Pemba hivi karibuni.
“Nashangaa sana,
baadhi ya watendaji wakuu wa chama kuniambia kuwa mabadiliko ninayoyataka
nitayasikia tu, na pia kusema wazi kwamba mwisho wangu Nungwi. Sasa nimekubali
kauli hizo na wakati umefika kuwaachia chama chao”, alieleza Makungu.
Hata hivyo, alisema anaona fahari kukiacha chama hicho
akiwa amejenga msingi mzuri wa kukiletea mabadiliko ambapo kwa miezi saba
aliyokalia kiti cha urais, angalau dalili za maendeleo zimeanza kuonekana
kutokana na juhudi zake binafsi.
Hata hivyo, pamoja na kunuia kung’atuka, Rais huyo
aliwataka viongozi wa ZFA wilaya zote, kuendeleza soka hasa la vijana, huku
akiahidi kuzitekeleza ahadi alizowapa ikiwemo kutoa zawadi za fedha kwa
washindi wa ligi za daraya la pili
wilaya, la tatu, central na ligi ya watoto (juvenile).
Aidha alisema kuna haja kubwa ya kuifanyia mabadiliko
katiba ya chama hicho, ingawa alisema
wapo baadhi ya viongozi wanaokwamisha dhamira hiyo kwa kulinda maslahi binafsi.
Viongozi wa klabu mbalimbali waliohudhuria mkutano huo,
walishauri kuifanyia marekebisho katiba, ili kuondosha matatizo na mivutano
isiyokuwa ya lazima inayodumaza soka la Zanzibar.
Mwenyekiti wa ZFA Wilaya ya Mkoani Seif Mohammed Seif,
na Katibu wa Central Nassor Hakim, wamesema ujio huo wa Rais wa ZFA umewapa
faraja kwani ni muda mrefu hakuna hata kiongozi mmoja wa juu aliyepata
kuwatembelea na kuzungumza nao.
“Ziara hii
imetufariji na kutujengea imani kwa
uongozi wa sasa wa ZFA, kwani ni jambo ambalo halijawahi kutokea kabla.
Ipo haja kwa viongozi wote kukaa pamoja na kumaliza tafauti zao kwa maslahi ya
timu zetu na taifa kwa jumla ”, alisema Hakim.
Pamoja na kusisitiza azma yake ya kujiuzulu, Makungu
alihitimisha mkutano na ziara hiyo kwa kuchangia shilingi milioni moja kwa
ajili ya kutafuta ofisi ya kudumu kwa ZFA wilaya hiyo.
No comments:
Post a Comment