Na Mwashamba Juma
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameeleza umhimu wa
Tanzania
kuwa na vitambulisho vya Taifa kwa kufafanua mambo kadhaa muhimu yatayopatikana
kutokana na vitambulisho hivyo.
Alisema
vitambulisho vya taifa vitaisaidia serikali katika utendaji wake ikiwemo
kufanikisha juhudi zake za kudhibiti wafanyakazi hewa.
Aidha alisema
vitasaidia kuimarisha usalama pamoja na kurahisisha kupeleka huduma za
kijamii kwa wananchi ikiwemo miundombinu.
Dk. Shein
aliyasema hayo jana viwanja vya Baraza la Wawakilishi Chukwani katika sherehe
za utoaji wa vitambulisho vya taifa awamu ya kwanza kwa Zanzibar.
Alisema
vitambulisho vya taifa pia vitawarahisishia wananchi kupata huduma muhimu
zikiwemo mikopo kutoka taasisi za kifedha, wanafunzi kupata mikopo kwa ajili ya
masomo, sambamba na kuzirahisishia
taasisi hizo kupata wepesi wa kurejeshewa fedha zao kutoka kwa wakopaji.
Aliwataka wananchi
kuitumia fursa hiyo kwa kuandaa nyaraka zao muhimu zitakazotoa taarifa sahihi
na kuachana na kasumba za wasioipendelea mema nchi kwa kulichukulia suala la
vitambulisho kuwa ni la kisiasa.
Aidha amewataka
wafanyakazi wa NIDA kuweka mbele maslahi ya nchi wakati wa utoaji wa
vitambulisho hivyo kwa kuhakikisha mtu asiestahiki hapatiwi kitambulisho hicho.
Akizungumzia suala
la vitambulisho vya Mzanzibari mkaazi, Dk. Shein alisema vitaendelea kutumika
kama kawaida kwa mahitaji yote kama
ilivyopangwa.
Hata hivyo, alizitaka
mamlaka husika kuwa na ushirikiano wa hali ya juu ili kukamilisha zoezi la
utoaji wa vitambulisho vya taifa kama
ilivyokusudiwa.
Naibu Waziri wa
Mambo ya Ndani ya Nchi, Pereira Ame Silima alisema mfumo wa ugawaji
vitambulisho vya taifa utaisaidia serikali kuwa taarifa sahihi za wananchi
wake, wageni ,wakimbizi mahalali wanamoishi na kazi wanazofanya.
Kwa upande wake
Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambusho vya Taifa, Dickson Maimu alisema lengo
la kuanzishwa vitambulisho ni kutambua raia halali wa Tanzania pamoja na wageni wanaoishi
nchini.
Mkurugenzi huyo
alisema licha ya mradi kukabiliwa na changamoto mbalimbali zikiwemo fedha kwa
ajili ya uendeshaji lakini walifanikiwa kutoa vitambulisho hivyo kwa awamu ya
kwanza Februari 7 mwaka huu katika ukumbi wa Karimjee jijini Dar es Salaam ambapo Rais Jakaya Kikwete alikuwa Mtanzania wa kwanza
kupatiwa kitambulisho hicho.
Aliongeza kuwa
changamoto nyengine ni wananchi kutokuwa na baadhi ya taarifa sahihi ikiwemo
kukosa viambatanisho muhimu vitakavyoweza kumtambulisha kwa urahisi.
Hata hivyo,
Mkurugenzi huyo alizitaka kamati za ulinzi na usalama ngazi ya shehia na mitaa,
Idara ya Uhamiaji,jeshi la polisi na usalama wa taifa kuwa na mashirikiano ya
karibu kuhakikisha waombaji wasiokuwa raia Watanzania wanaenguliwa.
Katika hafla hiyo, Dk. Shein alikabidhiwa
kitambulisho chake na Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani.
Baadae Dk. Shein
alikabidhi vitambulisho hivyo kwa viongozi mbali mbali akiwemo Spika wa Baraza
la Wawakilishi, Pandu Ameir Kificho, Jaji Mkuu wa Zanzibar, Omar Othman Makungu,
Mwanasheria Mkuu, Othman Masoud, wakuu wa vikosi vya ulinzi na usalama
Zanzibar, pamoja na Mkuu wa majeshi ya ulinzi, Davis Mwamunyange.
Wengine ni Makamu
wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi, Mawaziri wa serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi, Makatibu wakuu na watendaji wengine
wa serikali, pamoja na wawakilishi wa vyama vya siasa na wananchi wa Pemba na Unguja.
No comments:
Post a Comment