Habari za Punde

Vilio, simanzi maziko ya Padri Mushi. Dk. Shein asema wahusika lazima wakamatwe



Mwantanga Ame na Gilbert Massawe
 
 RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, ameungana pamoja na waumini wa dini ya kikristo na wananchi wa Zanzibar katika mazishi ya Padri Evaristus Gabriel Mushi, yaliyofanyika Kitope mkoa wa Kaskazini Unguja.
Awali Dk. Shein, alishiriki katika ibada ya misa ya kumuombea Padri huyo na baada alipata nafasi ya kutoa heshima zake za mwisho.
Misa hiyo ilifanyika katika kanisa la Minara miwili mjini Unguja, ambapo Kadinali Policarp Pengo aliongoza misa ya kumuombea Padri huyo.
Maziko hayo yalihudhuriwa na umati mkubwa wa waumini wa kikiristu na wananchi wa Zanzibar ambao waliguswa kwa karibu na kifo cha Padri huyo.

Vilio, simanzi na huzuni vilitawala katika mazishi hayo huku kukiwa na  misururu mikubwa ya magari na ulinzi ukiimarishwa kila kona.

Akitoa salamu zake kwa wananchi, viongozi wa dini wa kikristo na aaumini wa makanisa, Dk. Shein alisema serikali imepokea kwa mshtuko mkubwa kifo cha Pardi Mushi na itahakikisha wahusika wanakamatwa popote walipo.
Katika salamu zake  zilitolewa kwa niaba yake na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohammed Aboud Mohammed, Dk. Shein alisema kifo hicho hakijaacha pengo kwa familia yake bali kimeigusa sehemu kubwa ya jamii ya Watanzania na haiwezkani serikali kukaa kimnya kunyamazia uovu huo.
Alisema tayari serikali imeanza kufanya uchunguzi wa matukio yaliojitokeza na itahakikisha inakomesha matukio ya aina hiyo.

Alisema Padri Mushi alipenda kuhubiri mambo mema yenye kusimamia haki na kulinda heshima katika jamii na kuondoka kwake kumeiumiza jamii.

Alisema kitu kikubwa ni kuona wananchi wanaendelea kuishi kwa amani na upendo ili kuifanya Zanzibar kubaki salama.

Dk. Shein, alishiriki mazishi hayo akiwa pamoja na viongozi mbali mbali wa serikali akiwemo Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharif Hamad, Waziri wa Mambo ya Ndani, Dk. Emmanuel Nchimbi, Katibu Mkuu wa Chama cha CHADEMA, Wilbroad Slaa na  Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, James Mbatia.

Nae Rais wa Jamhuri ya Muungano, Jakaya Mrisho Kikwete, akitoa salamu zake ambazo ziliwakilishwa na mmoja wa watendaji wa kanisa hilo, alisema serikali imepokea kwa masikitiko makubwa kifo hicho na imewataka waumini wote wa dini ya kikristo kuendelea kuishi kwa amani na upendo.

Alisema serikali itahakikisha kuwa hatua stahiki zinachukuliwa kwa wahusika kwani itafanya upelelezi wa hali ya juu ili kuukata mzizi wa fitina wa matukio hayo.

Mmoja wanafamilia akitoa salamu kwa niaba ya familia, alisema msiba huo umeiumiza kwa kiasi kikubwa familia yao kwa vile Pardi Mushi hakufa kwa kuugua bali amedhulimiwa kwa kukatishwa maisha yake.

Alisema familia inaushukuru uongozi wa kanisa, serikali na daktari aliyemfanyia uchunguzi mwili wake na kusema wana matumaini makubwa kuweza kupata majibu mazuri ya uchunguzi unaofanywa.

Akitoa hotuba maalum katika misa ya sala ya kumuombea marehem, Rais wa Baraza la Maskofu Makanisa Katoliki Tanzania, Askofu, Tarikisius Ngalalekumtwa, alisema thamani ya maisha ya binadamu ni kuishi kwa upendo na haki.

Alisema kifo cha Padri Mushi, kisichukuliwe kama ni maadhimisho ya kifo ila watambue namna ya kujenga uhai kwa kuacha maovu kwa kutambua duniani ni mapito tu ya watu.

Kwa upande wake Dk. Slaa na Mwenyekiti wa NCCR Mageuzi, Jeams Mbatia walisema ipo haja kwa serikali kuyachukulia matukio hayo kwa uzito kwani kinachoonekana ni upepo mpya wa kuhujumu dhidi ya viongozi wa dini.

Dk. Slaa, alisema serikali haipaswi kuendelea kuiamini matukio hayo yanakuja kwa nguvu za Mungu pekee bali ni mambo ambayo yanahitaji kufanyiwa uchunguzi wa kina kwani haiwezekani kukawa na muendelezo wa hujuma kwa viongozi wa dini.

Hata hivyo,aliwataka waumini wa dini ya kikrosto na wananchi wa Zanzibar , kuendeleza kuishi kwa amani ili kuifanya Tanzania kubaki kuwa yenye amani.

Mbatia kwa upande wake alisema matukio ya kuhujumiwa viongozi wa dini ni mambo ambayo serikali inapaswa kuyaangalia upya kama inafanya uzuri katika kuimarisha utawala bora na kulilaumu jeshi la polisi kutoweka ulinzi wa haraka nyumba za ibada.

Alisema inasikitisha kuona bado serikali haiajatambua chanzo cha matatizo yanayotokea na badala yake imekuwa ikiendelea kutegemea mataifa ya nje zaidi kwa ajili ya kuwabaini wanaofanya hujuma hizo.

Alisema katika kulishughulikia suala hilo tayari hivi sasa vyama vya siasa kupitia Baraza linaloshugulikia vyama vya upinzani katika kusimamia amani nchini vinakusudia kukaa pamoja na wadau mbali mbali ili kutafuta njia ya amani kuinusuru Tanzania kuingia katika mizozo isiyokuwa na maana.

Maziko hayo pia yalihudhuriwa na Mabalozi mbali mbali waanaoziwakilisha nchi zao Tanzania, akiwemo Balozi wa Ubelgiji, Balozi Mdogo wa Norway mwenye makaazi yake Zanzibar na Maaskofu kutoka mikoa mbali mbali ya Tanzania ukiwemo wa Kigoma, Tanga, Dodoama, Geita na Askofu Mkuu wa Jimbo la Dar es Salaam.

Mapema akisoma wasifu wa marehemu Mushi, Askofu Cosmas Shao, alisema  Padri Mushi alizaliwa Juni 15, 1957, kijiji cha Uru Kimanganuni, Mkoani Kilimanjaro ambapo baba yake ni Gabriel Wariro Andrea na mama yake ni Febronia Selemani Joseph.

Baada ya kuhitimu masomo ya elimu ya juu ya sekondari mwaka 1976, alijiunga na seminari kuu Kibosho alikopata elimu ya falsafa, 1978 na 1979 na mwaka 1980 alingia seminari kuu ya Mtakatifu Paulo, Kipalapala – Tabora, alikopata elimu ya tauhidi hadi mwaka 1982.

Baadae alirudi jimboni kwake Zanzibar 1983,  na mwaka uliofuata 1984 aliendelea na masomo yake huko Kipalapala na  mnamo Julai  15, 1984 alipata daraja la Ushemasi katika Parokia ya Bikira Maria wa Rosari, Kitope na Disemba 2,1984 akapewa daraja la Upadre na Mhashamu Baba Askofu Bernard Martin Ngaviliau, katika kanisa kuu la Mt. Yosefu Minara Miwili Zanzibar.

Aidha, alisema maisha yake akiwa Padre Mei 01, 1985 aliteuliwa kuwa Paroko wa Parokia ya Bikira Maria wa Rosari, Kitope, 1988 – Paroko, Parokia ya Moyo Safi wa Maria Wete Pemba, 1991 – Paroko, Parokia ya Mt. Antoni wa Padua Machui, 1995 – alipelekwa AMECEA PASTORAL INSTITUTE GABA, Eldoret Kenya, kwa masomo ya Kichungaji.

Mwaka 1997 – 2003 alipelekwa masomoni Marekani na kutunukiwa shahada ya uzamili, 2004 alipelekwa Gombera kituo cha Hekima  Cheju, 2006 – Paroko, parokia ya Bikira Maria wa Rosari Kitope. Machi  01, 2008 – Paroko Kanisa Kuu la Mt. Yosefu, Minara miwili.

Disemba 02, 2009 aliadhimisha Yubilei ya Fedha, miaka 25 ya upadre, na vile alifanya kazi nyingine akiwa ni Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo jimbo, mlezi wa magereza na jeshi la wananchi,  Mratibu wa Huduma za sfya Jimbo.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.