Na Shehe Semtawa
MWENYEKITI wa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM), Khamis Sadifa
Juma, amesema kuwa hajawahi kuugua ugonjwa wa akili (kichaa) kama anavyozushiwa
na wapinzani wake.
Alisema kuna watu wameandaliwa na mafisadi ili wamchafue, ikiwezekana aachie
ngazi kama ilivyokuwa kwa mtangulizi wake, Yusuf Hamad Masauni.
Akizungumza na Tanzania Daima kwa simu mwishoni mwa wiki, Sadifa alisema wapo
baadhi ya watu wamekuwa wakifanya vurugu hizo kwa ajili ya kutaka kujipatia
umaarufu kupitia mgogoro huo na kuwafurahisha wale wanaowafadhili kifedha.
Alisema miongoni mwa uchafu aliowahi kutupiwa na watu hao ni kuwa alighushi
umri ili aweze kugombea nafasi hiyo.
“Najua nimewekwa kwenye kundi la Edward Lowassa na huyo wamemtaja tangu
nagombea, ndiyo maana wananipiga vita kutoka mwanzo.
“Wamegonga ukuta, hao wanatapatapa tu ndugu yangu, hao si wanasiasa ni wana
si hasa, watatulia wenyewe, mimi sina muda wa kujibizana na mtu magazetini,”
alisema.
Akizungumzia tuhuma hizo, Sadifa, alisema kuwa yeye alizaliwa mwaka 1982 na
hivi karibuni ametimiza miaka 31, kwamba ambaye haamini anaweza kujiridhisha kwa
kuingia kweye mtandao ataziona taarifa zake zote.
Kuhusu ugonjwa wa kichaa, alisema hizo ni taarifa za kitabibu, hivyo ni vema
kwa wale wote wanaodai hivyo kuonesha ushahidi wa vyeti vya madaktari ambavyo
vinathibitisha madai yao.
“Mimi ni mbunge sasa kama kuna mtu ananituhumu hivyo basi waende mahakamani
kama alivyofanya Raila Odinga kwenda kupinga ushindi wa Uhuru na hatimaye haki
ikapatikana,” alisema.
Naye mmoja wa vijana wanaotuhumiwa kutaka kumwondoa madarakani mwenyekiti
huyo alisema: “Wakati umefika Sadifa ni lazima aondoke.”
Alisema ataondoka si kwa kuwa wana timu au mkakati uliosukwa wa kumwondoa
bali suala la msingi hapo ni kanuni.
“Mimi ni mjumbe wa UVCCM najua kanuni zetu. Sadifa ataondoka si kwa kuwa
hatumtaki, hatuutaki uwezo wake mdogo na kanuni alizovunja,” alisema.
Alisema kuwa Sadifa ni mbunge tangu 2010 lakini akahoji ni wapi aliwahi
kusikika akizungumzia hoja ya vijana kama vile ajira hata baada ya kuchaguliwa
UVCCM?
“Wapi Sadifa amefanya mkutano na kuvutia vijana wajiunge na CCM? Huwezi
kumlinganisha hata na John Heche, Mwenyekiti wa BAVICHA wa CHADEMA. Unategemea
atasaidia chama, huyu ana uwezo mdogo,” alisema kijana huyo.
Chanzo - Tanzania Daima
No comments:
Post a Comment