Na Mwandishi wetu
Kuna tishio kubwa dhidi ya Muungano
wetu. Tishio hilo liko zaidi kwenye
dhana kuliko udhaifu wa dhamira ya Muungano wenyewe. Tishio hilo limedhihirika
katika kipindi hiki cha Mchakato wa Kuandaa Katiba Mpya ya nchi yetu.
1)
Tatizo ni Muundo na Suluhisho ni Serikali
Tatu
2)
Zanzibar inanyonywa, Tanganyika inafaidi
kuliko Zanzibar (na kinyume chake)
Ipo dhana nyingine kuwa Zanzibar
inanyonywa ndani ya Muungano na Tanganyika inafaidi ndani ya Muungano.
Kinachostaajabisha, pia wapo wanaosema Tanganyika inanyonywa na Zanzibar
inafaidi. Zote hizi ni hoja ambazo msingi wake ni husuda, na husuda haiondolewi
na idadi ya Serikali. Watu wenye husuda wataendelea kuwa na husuda hiyo ndani
ya Serikali moja au tatu.
3)
Nje ya Muungano Zanzibar itanufaika zaidi
na Tanganyika itatua mzigo
Ipo dhana kuwa nje ya Muungano, Zanzibar
itanufaika zaidi na Tanganyika itatua mzigo. Wenye kujenga dhana hii, hujenga
hoja kuwa Zanzibar itaweza kujenga mashirikiano yake yenyewe na dunia na nchi
za kiarabu na kiislamu zenye uchumi imara. Wengine huzungumzia Zanzibar kuja
kuwa bandari huru kama ilivyo Singapore. Tanganyika au Muungano huonekana kuwa
ni kikwazo kwa Zanzibar kujiunga na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu (OIC). Tunazidi
kuaminishwa kuwa kwa kujiunga OIC, Zanzibar itajikwamua na umasikini.
Waumini wa Tanganyika wanatuaminisha
kwamba nje ya Muungano, Tanganyika itakuwa imetua mzigo. Hawa wanataka tuamini
kuwa Zanzibar inaielemea Tanganyika na kwamba gharama za kuendesha muungano
zingeliweza kutumika kwenye miradi ya maendeleo. Wanatuaminisha kuwa Tanganyika
imekuwa ikibeba gharama hizi peke yake na kwamba Tanganyika itaendelea kwa kasi
sana baada ya kuachana na Zanzibar.
Dhana hii kuwa Zanzibar itanufaika nje ya
Muungano ni dhana muflisi na potofu. Hoja ya kuwa kwa kujiunga na OIC Zanzibar
itaneemeka ni ya kusadikika. Visiwa vya Comoro vina ukubwa wa kilometa za mraba
2170, vina idadi ya watu wapatao 984,500 na ni mwanachama wa OIC na Jumuiya ya
Kiarabu (Arab League). Visiwa vya Comoro
vingali masikini kuliko Zanzibar na ukuaji wake wa uchumi kwa mwaka 2012
ulikuwa ni asilimia 2.7. Tunachokipata hapa ni kuwa sio OIC wala Arab League
yenyewe inayoweza kubadili uchumi na maisha ya mzanzibari.
Uchumi wa Zanzibar kama ilivyo Comoro kwa
muda mrefu umefifishwa na migogoro ya kisiasa. Zanzibar ina tabaka kubwa la
wanasiasa na utawala kuliko uwezo wa uchumi kuhimili, hivyo migogoro ya kisiasa
haiepukiki. Nje ya Muungano, wanasiasa wengi wa Zanzibar watakosa ajira, hawa
watajiunga na siasa za ndani za Zanzibar, hapatatosha. Migogoro ya kisiasa
baina ya visiwa huko Comoro ina athari kubwa kiuchumi kuliko migogoro ya
kisiasa baina ya Unguja na Pemba kutokana na siasa hizo kumezwa na siasa za
Muungano.
Isitoshe, nje ya Muungano, Tanganyika na
Zanzibar zote kwa pamoja zitalazimika kubeba mzigo wa kugharamia ulinzi na
usalama pamoja na uendeshaji wa Ofisi za Balozi nje ya nchi. Gharama hizi
zikigawanywa kwa kila nchi kuendesha mambo haya yenyewe ni kubwa kwa kila nchi.
Pengine tunapofushwa na gharama za kifedha pekee na kuacha kuangalia gharama za
kiusalama. Usalama wa Zanzibar na Tanganyika unategemeana sana na Muungano ni
chombo muhimu cha kuhakikisha usalama wa pande zote mbili. Tanganyika
itagharimika sana kiusalama nje ya Muungano kuliko tunavyofikiria, hususan
katika kipindi ambacho Tanganyika inatarajia kuvuna gesi katika pwani ya bahari
ya Hindi. Mahasimu wa Tanganyika watakuwa wamepata upenyo mzuri wa kutimiza
azma yao ya kuidhuru Tanganyika, au mahasimu wa Zanzibar kuidhuru Zanzibar.
Hivyo, ustawi wa Zanzibar na Tanganyika unategemeana, wala sio kweli kuwa yuko
mmoja anayembeba mwenzake au atakayekuwa salama zaidi nje ya Muungano.
4)
Wananchi wengi wa Zanzibar hawataki
Muungano na Wananchi wengi wa Tanganyika hawataki Muungano
Wanasiasa wetu wa pande mbili wasioupenda
Muungano kwa sababu wanazozijua wao, wanatuaminisha kwamba Muungano umechokwa
na Watanzania wa pande zote mbili.
Wanasiasa hawa hawa walifanikiwa kutushawishi kuwa Watanzania wengi
wanataka Katiba mpya. Takwimu ya waliojitokeza mbele ya Tume kutoa maoni juu ya
Katiba mpya ni za kushtua. Katika nchi ya wapiga kura wanaokadiriwa kufikia
milioni 20 kwa mujibu wa Tume ya Uchaguzi, waliojitokeza kutoa maoni yao hawakufika
laki tano. Aidha, mwamko mdogo ulioonyeshwa katika ushiriki wa mabaraza ya
Katiba unaacha maswali mengi.
Wanasiasa na wanaharakati hutumia
shinikizo kama mojawapo ya nyenzo kufikia malengo yao. Mojawapo ya nyenzo
wanayoipenda sana ni kutumia umma kuhalalisha matakwa yao. Kwa sababu hiyo
haishangazi kwa wanasiasa kupenda kutumia njia ya maandamano na lugha ya
‘wingi’ katika kujenga hoja zao. Kwa mbinu hii, lugha ya ‘wingi’ imetumika
kutuaminisha kwamba wazanzibari wengi hawautaki muungano, hali kadhalika,
watanganyika wengi hawautaki muungano.
Lugha ya jumla imetumika pia kujenga dhana
kuwa wanachama wa CUF wote hawaupendi muungano, wapemba wote ni CUF na waunguja
wote ni CCM na wanaupenda Muungano tena wa Serikali mbili. Hali kadhalika,
tunaaminishwa kuwa wanachama wa CHADEMA wote wanapenda Serikali tatu na wana
CCM wanapenda Serikali mbili. Katika kunogesha dhana yenyewe, inajengwa hoja
kwamba, iwapo kura ya maoni ya kutaka au kutotaka muungano itapigwa, basi
haitapatikana theluthi mbili Zanzibar, kwa kuwa katika matokeo ya uchaguzi
uliopita, hakuna chama kilichopata theluthi mbili ya kura.
Wanaoshabikia dhana hii wanawachukulia
wananchi kama misukule. Wanaamini wananchi watapiga kura kwa mlinganyo ule ule
hata kama jambo ambalo wanalolipigia kura limebadilika. Kwa kutumia dhana hii,
tunakatishwa tamaa ya kuutafuta ukweli kwa kuwapa fursa wananchi ya kuchagua
iwapo wanautaka muungano au hawautaki, wanataka Serikali mbili au tatu. Hata
Tume ya Katiba imetuingiza katika mkenge huu kwa kutuambia kuwa ‘wengi’
waliohojiwa wametaka Serikali tatu. Hatujaambiwa waliotaka serikali mbili
wangapi na waliotaka moja wangapi. Tunatakiwa tukubaliane tu kuwa wengi
hawautaki muungano pande zote mbili.
Dhana hii haiakisi hali halisi.
Wazanzibari na Watanganyika wameoleana, kuzaliana na wengine wanaendesha
biashara kwa ubia. Ukisikiliza Sauti ya Radio Zanzibar katika taarifa za vifo
utastaajabu kuwa karibu kila msiba una ndugu na jamaa bara tena sio Dar es
Salaam pekee. Ukikaa katika bandari ya Dar es Salaam au Zanzibar utashangazwa
na idadi ya wasafiri kutoka pande zote mbili za mbili za Muungano. Wananchi wa
kawaida wa pande zote mbili hawana tatizo na muungano maana hauathiri maisha
yao ya kila siku zaidi ya kuyarahisisha. Hawa, haswa wafanyabiashara, wanazo
kero zinazohusiana na mifumo ya kodi zaidi kuliko muundo wa muungano, au
muungano wenyewe. Hapana shaka, watakapoulizwa juu ya uwepo au kutokuwepo kwa
muungano, maamuzi yao yatakuwa tofauti, kwa kuwa hatma ya muungano ina athari
kubwa sana kwao. Ni vyema tukaruhusu kura ya maoni juu ya uwepo au kutokuwepo
kwa muungano. Kura hii ya maoni, itatukwamua kutoka kwenye tope la wanasiasa,
ambao ndio kero kuu ya muungano.
5)
Muungano umepitwa na wakati
Waswahili husema, ukitaka kumuua mbwa mpe
jina baya. Ukimuita Mbwa Koko au Kichaa unapata uhalali wa kumuua. Ukimpa jina
zuri unamuhamishia sebuleni. Katika kutimiza azma yao, wale wasioupenda
Muungano hutoa dhana ya Muungano kupitwa na wakati. Kwao suala la Muungano
huchukuliwa kama tukio la kupita na sio suala la kudumu. Hivyo, tunatakiwa
tuamini kuwa muungano wetu umepitwa na wakati, na ulikuwa na mantiki tu wakati
ule wa vita baridi na umajumui wa Afrika (Pan-Africanism). Zama hizo zimepita
na hivyo Muungano nao umepitwa na wakati.
Hoja hii nayo inajibika. Muungano wowote
unaingiwa kwa lengo la kuwa Muungano wa kudumu. Chini ya Sheria za Kimataifa,
uko msingi kuwa nchi huingia Mkataba kwa dhamira njema ya kuutekeleza. Hivyo, Muungano wetu kama ilivyo miungano
mingine ikiwemo ule wa Marekani na Ujerumani, inadhamiriwa kuwa ya kudumu.
Tukirudi kwenye hoja yenyewe, Muungano
wetu haujapitwa na wakati, labda baadhi ya viongozi wetu wamepitwa na wakati.
Taifa letu linapita katika dunia ya utandawazi. Katika dunia ya utandawazi,
nchi zinachukuliwa kuwa ni masoko. Muelekeo wa dunia ni kuunganisha nchi
kuelekea kwenye utaifa mkubwa zaidi na na sio kinyuke chake. Nchi ndogo zina
nafasi finyu katika dunia ya utandawazi hususan pale nchi zenyewe ndogo
zinapokuwa masikini. Nchi za Ulaya zinafanyia kazi wazo la kuungana kuwa nchi
moja chini ya Umoja wa Ulaya. Nchi ya Ubeligiji yenye pato kubwa la uchumi
kuliko jumla ya nchi zote kusini mwa jangwa la Sahara inajiunga na nchi
nyingine za Ulaya kujenga utaifa mkubwa kukabiliana na utandawazi. Aidha,
tunaona jinsi ambavyo nchi zenye watu wengi kama India, China na Brazil
zinavyotikisa katika utandawazi kutokana na kuwa na idadi kubwa ya watu. Ni
kichekesho kuwa sisi nchi masikini tunafanya kinyume chake. Tunadanganyana kuwa
tunayo fursa ya kuneemeka zaidi katika utandawazi tunapokuwa nje ya Muungano.
Ukweli ni kuwa hatujiimarishi kwa kuwa nje ya Muungano bali tunajidhoofisha.
Muungano unahitajika zaidi katika dunia ya utandawazi kuliko tunavyojifariji.
6)
“Sisi” ni Muhimu Kuliko “Wao”
Tunalo tatizo la kimtazamo miongoni mwa
watanganyika na wazanzibari ambalo kwa maoni yangu msingi wake ni ubaguzi. Iko
dhana ya ‘sisi’ na ‘wao’. Wananchi wa kila upande wamepandikizwa mitazamo dhidi
ya wenzao wa upande mwingine. Baadhi ya Wabara huwaona wazanzibari kama watu
goigoi na huwaita ‘yakhe’ au ‘mdebwedo’. Hali kadhalika baadhi ya wazanzibari
huwaona wabara kama watu wa shamba na wasio staarabika, huwaita ‘machogo’.
Mitazamo hii imeathiri kwa kiasi kikubwa mahusiano baina ya wananchi wetu,
lakini baya zaidi, imetulewesha kwa kutupa majivuno kuwa ‘sisi’ ni bora kuliko
‘wao’.
Athari kubwa itokanayo ni mitazamo hiyo ni
kujenga kutokuaminiana. Wabara wanadhani wazanzibari wote ni wazembe, hawana
uwezo wa kiakili. Wazanzibari hali kadhalika wanawaona wabara kama watu
wasiostaarabika, wenye majivuno na kupenda kuburuza. Matokeo yake, mitazamo hii
huambukiza vizazi na vizazi.
Wananchi wa Zanzibari na Tanganyika
waliopata bahati ya ama kuishi au kusoma na wenzao wa upande wa pili,
watakubaliana nami kuwa mitazamo hii ni potofu. Binafsi, nimesoma na
wazanzibari na kufanya kazi na wazanzibari wenye uwezo mkubwa sana kushinda
wabara. Kama ilivyo kwa wabara, tunao wazanzibari wengi nje ya nchi kwenye
mashirika ya kimataifa wanaotujengea heshima kubwa.
Changamoto ya kimfumo iliyopo ni kwamba,
kutokana na wingi wa wabara, wengi wao hujikuta hawajawahi kufika wala kuishi
Zanzibar, Isitoshe, hawajawahi kusoma ama kuishi na wazanzibari. Hivyo,
wanasiasa hutumia mwanya huo kupandikiza mitazamo ya ‘sisi’ na ‘wao’ katika
kutafuta kujijenga kisiasa. Maoni yangu ni kuwa, ‘sisi’ sio bora kuliko ‘wao’,
wala ‘wao’ sio bora kushinda ‘sisi’. Wazanzibari, kama walivyo watanganyika
wamelifia taifa letu la Tanzania katika kulinda na kutetea heshima na uhuru
wake. Watanganyika na Wazanzibar wamekufa katika vita vya Uganda wakipigania
taifa letu. Majuzi, watanganyika na mzanzibari wamekufa huko Darfur wakiwa
katika shughuli za kulinda amani. Maadui waliowaua wanajeshi wetu kule Darfur
hawakutofautisha mzanzibari wala mbara, waliua wanajeshi wa Tanzania katika
jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa. Haya yanayotuunganisha, ni muhimu
zaidi, kuliko yale yanayotugawa.
7)
Kero za Muungano lazima Zipate Majawabu ya
Kudumu na Ziondoke, Manung’uniko ni kufeli kwa Muungano
Muungano wetu wa miaka 49 unazo changamoto
zake. Changamoto hizi zimebatizwa jina la ‘kero’. Sidhani kama ‘kero’ ni neno
sahihi, na nachelea kama neno ‘kero’ lilizuka tu pasipo kuwa na lengo nyuma
yake. Kwa vyovyote vile, aliyezibatiza changamoto za muungano jina la ‘kero’
amefanikiwa sana. Sisi wengine huamini ‘maneno huumba’. Jina hili
limeshakubalika na sasa changamoto zinaitwa ‘kero’, yaani mambo yanayokera.
Dhana tunayoipata hapa ni kuwa utatuzi wa
‘kero’ ni tofauti na utatuzi wa changamoto. Tofauti yenyewe ni ya kimtazamo.
Changamoto ni vikwazo vya kutatulika, wakati kero ni vikwazo vilivyoshindikana.
Kero zinapaswa kuondoshwa zote, na kama haziondoshwi, basi huwa ni sugu, na
dawa yake ni kuvunja muungano wenyewe. Tunaaminishwa kuwa sio sahihi kuishi na
kero kama hazitatuliki, na kuwa, muungano uliojaa kero ni muungano mfu. Kero
hizi hudaiwa kwamba zinatokana na muundo wa muungano wenyewe. Suluhisho
linalotolewa ni aidha kuwa na serikali tatu ili ‘kuunusuru’ muungano, kinyume
na hivyo, ni muungano kuvunjika.
Tunadanganywa kuwa tunachojaribu kunusuru
ni 'muungano'. Tunachotakiwa kunusuru ni 'utaifa' sio 'muungano', muungano ndio
wenye kunusuru utaifa wetu, sio kinyume chake. Muungano wetu ni muungano
unaoishi. Muungano unaoishi hupita katika nyakati na mazingira tofauti ya kisiasa,
kiuchumi na kijamii katika maisha yake. Watu hubadilika, matarajio hubadilika
na hali kadhalika mitazamo hubadilika. Changamoto za muungano ni kielelezo cha
uhai wa muungano wenyewe na sio vinginevyo. Wala hakuna muungano duniani usio
kuwa na changamoto, wenye kufurahisha watu wote, wakati wote. Changamoto za
muungano ni fursa ya kuuimarisha muungano na sio kuuvunja. Huko tuendako
tutarajie kujitokeza kwa changamoto nyingine hata tutakapofanikiwa kuzikabili
zilizopo leo. Hivyo, dhana ya kuona changamoto za muungano ni kero na maana
yake ni kufeli kwa muungano ni dhana potofu.
Changamoto za muungano ni kipimo cha
uongozi. Changamoto hujitokeza ili zitatuliwe. Zisipotatuliwa ni udhaifu wa
kiuongozi. Sina budi hapa kuwapongeza viongozi waliotangulia kwa kukabiliana na
Changamoto hizi kila zilipoibuka. Uhodari wao ndio unaoufanya muungano wetu leo
utimize miaka 49 na kuwa muungano pekee ulioweza kudumu katika Afrika. Kwa
uongozi wao tumevuka jaribio la kuvunja muungano mwaka 1984, ambapo Mhe. Seif
Sharrif Hamad, wakati ule alionyesha uzalendo wa kutukuka kulinda muungano wetu
wa Serikali mbili (leo kageuka). Aidha tumevuka jaribio la kuvunjika kwa
Muungano mwaka 1992-93 kufuatia Zanzibar kujiunga na OIC na Wabunge 55 wa
Tanzania (G55) kudai Serikali ya Tanganyika. Tukavuka pia majaribio kadhaa kama
hayo ndani ya mfumo wa vyama vingi hadi sasa.
Katika kitabu cha Uongozi Wetu na Hatma ya
Tanzania, Mwalimu Nyerere alisema, “Maadamu matatizo halisi ya muungano
hayazungumzwi wala hayashughulikiwi, watu wenye nia mbaya, wa bara na visiwani,
wanaopenda kutumia hali hiyo kuivunja nchi yetu wanaendelea kufanya hivyo. Na
wale wa huku na huku, wanachocheana kama mifukuto ya shetani. Na hiyo
inawafanya hata watu wasio na nia mbaya, ila kwa ujinga tu, waamini kuwa inafaa
wote tushiriki na tujiandae kuivunja Tanzania tusije tukashtukia kuwa Tanzania
imevunjika na tumeachwa kwenye mataa! Anayedhani viongozi wetu ni wajinga yafaa
achunguze akili zake! Wanajua wafanyalo”
Changamoto nyingi za Muungano zinaweza
kutatuliwa chini ya muundo wa Serikali mbili kama ambavyo tumefanikiwa siku
zote. Pengine, kilichotakiwa ni ubunifu tu wa mfumo mpya ya kutatua kero hizo
kutokana na mifumo ya zamani kupitwa na wakati. Katika hili, ninayo kila sababu
ya kumpongeza Mheshimiwa Rais Jakaya Mrisho Kikwete na Rais wa Zanzibar
Mheshimiwa Mohamed Ally Shein kwa ubunifu wao. Nahodha mzuri hupimwa kwa uwezo
wake wa kuhihimili chombo wakati wa dhoruba sio kukiendesha chombo wakati wa
utulivu wa bahari. Chini ya uongozi wao, umeanzishwa
mfumo rasmi wa kukutanisha Serikali ya Muungano na Serikali ya Zanzibar chini
ya uenyekiti wa Makamu wa Rais kushughulikia changamoto hizo. Tangu kuanza kwa
mfumo huo, changamoto 13 zimeshajadiliwa, changamoto 6 zimeshapatiwa ufumbuzi,
hoja tatu ziko katika hatua za mwisho za kutatuliwa na hoja nne zinaendeea
kushughulikiwa. Tokea mwaka 2011 hadi Aprili 2013, vikao 9 baina ya Serikali
mbili vimekaa katika ngazi ya makatibu wakuu na mawaziri.
Kilicho dhahiri ni kuwa, changamoto nyingi
zilitokana na viongozi wa pande mbili kutokutana rasmi. Kutokana na kuzoeana,
mambo mengi yalikuwa yakimalizwa kwa mazungumzo baina ya viongozi wa ngazi za
juu. Tatizo la utaratibu huo wa kindugu, ni kushindwa kupima ufanisi na
kukosekana kwa mrejesho katika ngazi za chini ukiacha viongozi. Aidha, wakati
mwingine kwa sababu za kisiasa, viongozi walipenda kuhodhi mchakato huu na
taarifa zake. Pamoja na kwamba mfumo huo umetuvusha huko nyuma, kilicho wazi ni
kuwa sio mfumo endelevu. Yawezekana ulifanya kazi vizuri chini ya mfumo wa
Chama kimoja, lakini mazingira ya vyama vingi yanahitaji kurasimisha mfumo huu
ili kuwezesha wadau wote wa muungano ndani na nje ya Serikali kupata mrejesho,
na ikiwezekana kushirikishwa. Kinachostaajabisha, hili halizungumzwi,
kinachozungumzwa ni muundo tu. Baadhi ya wanasiasa wamechagua kutoyazungumzia
haya hadharani kwa kuwa yanakinzana na lengo lao la kuvunja muungano. Busara na
umakini unatutaka kusikiliza tu sio kile tunachoambiwa, bali pia na kile
tusichoambiwa na huyo anayetuambia
8)
Muungano wetu ni Batili na hauna Uhalali,
ni wa Ajabu
Wanasheria nao hawako nyuma katika mjadala
wa muungano na hatma yake. Baadhi ya Wanasheria wamehoji juu ya uhalali wa
muungano kisheria. Wamekwepa siku zote kujadili uhalali wa muungano kisiasa kwa
kujificha katika kile kinachoitwa uweledi. Mtazamo wa baadhi ya wanasheria
umejikita katika kuangalia mchakato uliozaa hati ya muungano na matokeo ya
mkataba huo. Mtazamo huo unachagiza dhana kuwa muungano wetu ni batili. Ubatili
huo unatokana na kukosekana unyoofu katika mtiririko wa matukio katika kuelekea
kufikiwa kwa Mkataba wa Muungano. Aidha, muungano wetu kutokufanana na miungano
iliyoko kwenye vitabu vya kisheria kunawakwaza wanasheria. Maana, miungano
iliyoko vitabuni ni mfumo wa muungano wa Serikali moja au mfumo wa majimbo wenye serikali kadhaa za
majimbo na moja ya muungano.
Wanasheria wengi wana matatizo makubwa ya
aina mbili; kwanza wanajiamini kuwa wanajua (wanajiita kimombo ‘learnerd’);
pili, jamii nayo imetokea kuamini kuwa
wanasheria wanajua. Wanasheria hawa hupenda kuwa na kauli ya mwisho kwenye kila
jambo, na hawapendi kukosolewa na mtu asiye mwanasheria. Kinyume na mtazamo huo
wa wanasheria, Muungano ni suala la dhamira kwanza, sheria baadae. Muungano
hauanzi na sheria bali huhitimishwa na sheria, wala sheria pekee haibatilishi
dhamira ya watu kuungana. Sheria yaweza kufa dhamira ikabaki. Watu ama nchi
haziungani kwa lengo la kutekeleza sheria, bali wanaungana kwa malengo ya kupanua maslahi ya kiuchumi au ya kiusalama
au ya ustawi. Sheria na Katiba zinatumika kulinda dhamira hiyo sio kuiumba.
Hivyo, Hati ya Muungano sio lengo, Hati ya Muungano ni matokeo. Hivyo, muungano
wetu, na muundo wake wa Serikali mbili haulazimiki kukidhi au kufanana na
miungano mingine kwenye vitabu, maana kila muungano huibuka katika nyakati,
mazingira na malengo tofuti.
Ufafanuzi mzuri juu ya dhana ya uhalali wa
Muungano imezungumziwa na Mwalimu Nyerere katika kitabu chake cha Uongozi wetu
na Hatma ya Tanzania. Bahati, mbaya Hayati Abeid Karume, hakuishi muda mrefu
kuweza kuacha maandiko, hivyo rejea kuhusu chimbuko la muungano zimetawaliwa na
kauli za Mwalimu Nyerere. Katika kitabu hicho, Mwalimu Nyerere alisema, “Tanzania
ni lulu ya pekee kabisa katika historia ya Afrika huru. Nchi nyingine zote ni za
kurithi kutoka kwa wakoloni. Wako watanzania wa ajabu kabisa wanaosema kuwa
uamuzi huo, au vyombo vilivyotumiwa au njia iliyotumiwa, au vyote, havikuwa
halali. Hao hawana shaka na uhalali wa Tanganyika, ambayo iliunganishwa na
Wajerumani, na ikamegwa megwa na Waingereza na wenzao. Kwa hao, kama Rwanda na
Burundi na Tanganyika zisingetengwa na mabeberu, tukazirithi kama zilivyokuwa
chini ya Wajerumani, wasingeushuku uhalali wa nchi moja hiyo. Lakini kama baada
ya uhuru, Rwanda na Burundi na Tanganyika zingeamua kuungana ziwe nchi moja,
kwa utaratibu wowote ambao zingekubaliana, ‘wazalendo’ hawa wangesema muungano
huo sio halali.”
Katika aya inayofuatia, Mwalimu Nyerere
akaendelea kujenga hoja juu ya mtiririko wa matukio uliopelekea kufikiwa kwa
makubaliano ya nchi zetu kuungana. Alisema, “Hatukutafuta maoni ya watu kwa
njia ya demokrasia wanayoijua wao. Wajerumani na Waingereza walitafuta maoni ya
wazee wetu kwa mtutu wa bunduki! Hiyo ilikuwa halali. Nchi walizounda kwa njia
hizo zilikuwa halali. Tunatakiwa tujivunie utanganyika na uzanzibari uliopatikana
kwa njia hizo, lakini tuuonee haya Utanzania, tunda la uhuru wetu wenyewe.
Sikuamini kama wakoloni walifaulu kiasi hiki katika kuzinywesha kasumba na
kuzitawala akili za baadhi yetu!”
9)
Muungano na haswa Muundo wa Serikali Mbili
ni Sera ya CCM
Suala la Muundo wa Serikali mbili limekuwa
likihusishwa na CCM. Bahati mbaya, wana CCM nao wametokea kuamini kuwa suala
hili ni Sera yao. Kuunasibisha muundo wa Serikali mbili na CCM kunafanya wale
wengine wasiokubaliana na CCM kutokukubaliana pia kwenye suala la muundo wa
Serikali mbili. Matokeo yake, suala la muundo wa Serikali mbili linapoteza sura
ya utaifa, hivyo wanaopinga mfumo huo, wanaukataa wakati mwingine bila hata ya
kuuelewa na kuuchambua. Ukiondoa CCM hakuna Chama chochote kingine cha siasa Tanzania
kinachosimamia muundo wa Serikali mbili.
Muundo wa Serikali mbili kama
zitakavyokuwa Serikali tatu au moja sio mwarobaini wa Muungano. Muundo wa
Serikali mbili ulichaguliwa baada ya waasisi kujiridhisha kuwa katika mazingira
ya tofauti za kimaumbile za Tanganyika na Zanzibar, ni muundo wa Serikali mbili
tu ndio ungeweza kukidhi hitaji la unafuu wa gharama za uendeshaji na kinga
dhidi ya hatari ya utaifa wa mzanzibari kutoweka. Si muundo wa Serikali mbili
wala tatu ambao ulionyesha kuleta msawazo katika mahitaji hayo mawili wakati
huo na hata sasa. Hoja ya kuwa muundo huu ni wa CCM kwa kuwa ulifikiwa chini ya
vyama vya TANU na ASP ambavyo viliungana na kuzaa CCM ni hoja muflisi. TANU na
ASP ndio vyama vilivyokuwa madarakani wakati huo, na mrithi wao CCM kiko
madarakani hadi sasa. Ukweli huu haufanyi muundo huu kuwa wa CCM. Suala la
Muundo lafaa kuwa suala la Kikatiba ili vyama vyote viuheshimu.
Muundo wa Serikali mbili unalo chimbuko
lake. Haukutokana na nasibu bali tathmini na maamuzi yenye upeo wa hali ya juu.
Mfumo wa Serikali mbili waweza usiwe mfumo bora kushinda mingine duniani,
lakini ni bora kushinda mfumo wa Serikali tatu na moja katika mazingira ya
Tanzania. Hili pia limezungumziwa na Mwalimu Nyerere kwenye kitabu chake cha
Uongozi wetu na Hatma ya Tanganyika, alisema:
“Tanganyika na Zanzibar
zilipoamua kuungana na kuwa nchi moja, tungeweza kufuata mojawapo ya mifumo ya
kawaida. Lakini tulishindwa kufanya hivyo kwa sababu ya udogo wa Zanzibar na
ukubwa wa Tanganyika. Zanzibar ilikuwa na watu laki tatu (300,000) na
Tanganyika watu milioni kumi na mbili (12,000,000). Muungano wa Serikali moja
ungefanya ionekane kama Tanganyika imeimeza Zanzibar. Tulikuwa tunapigania
uhuru na Umoja wa Afrika, hatukutaka tudhaniwe hata kwa makosa kwamba tunaanzisha
ubeberu. Kwa hiyo mimi nilipinga mfumo wa Serikali moja. Shirikisho la Serikali
Tatu lingekuwa ni gharama kubwa mno kwa Tanganyika. Zanzibar ingeendesha
Serikali yake na kuchangia gharama za kuendesha Serikali ya Shirikisho; na
Tanganyika ingefanya hivyo hivyo. Lakini ni dhahiri kwamba mchango wa
Tanganyika ndio hasa ungeendesha Serikali ya shirikisho. Kwa hiyo, Tanganyika
ingeendesha Serikali ya watu milioni 12 na pia ingetoa sehemu kubwa ya
kuendesha Serikali ya Shirikisho la watu milioni 12,300,000. Ni watu
wanaofikiri kwa ndimi zao wanaodhani kuwa gharama ya Serikali yoyote kati ya
hizi ingekuwa ndogo. Gharama ya Serikali ya Tanganyika isingekuwa ndogo, hata
bila ya gharama za mambo yasiyo ya Shirikisho. Na gharama zote hizo kwa kweli
zingebebwa na Tanganyika. Kwa hiyo ilitupasa tujiulize kwa nini tunataka
kuibebesha Tanganyika gharama zote hizo; na hasa kwa nini tunataka Serikali ya
Tanganyika? Hivi tuna hofu ya kwamba Tanganyika, bila kuwa na Serikali yake,
itaonekana imemezwa na Zanzibar? Hofu yetu ni kwamba tukiwa na Serikali moja
Tanganyika itaonekana kuwa imeimeza Zanzibar. Basi na tutafute mfumo ambao
utaiondolea Zanzibar hofu hii ya kumezwa bila kuibebesha Tanganyika mzigo
wa kuendesha Serikali mbili zenye uzito unaolingana. Hivyo ndivyo tulivyofanya,
na hiyo ndio asili ya muundo wa Muungano wa serikali mbili. Badala ya kutungua
mfumo uliopo kama wapumbavu, tulitazamia hali halisi yetu ilivyokuwa, na
tukabuni mfumo uliotufaa zaidi".
Tukienda na maelezo hapo juu, lililo
dhahiri ni kuwa, zipo sababu kwa nini muundo wa Serikali mbili ulibuniwa.
Aidha, katika maelezo hayo, kilicho wazi ni kuwa sababu zilizozaa Serikali
mbili hazikuwa sababu za kichama bali kitaifa. Hivyo, dhana kuwa muundo wa
Serikali mbili ni suala la CCM ni dhana potofu. Hali kadhalika, muundo huu sio
msahafu na unaweza kubadilika. Wala hakuna sababu ya kuendekeza muundo ambao
hautakiwi. Muhimu ni kujadili kwa uwazi iwapo mazingira yaliyozaa Serikali
mbili yamebadilika, na kama kwa kubadilika huko, sasa mbadala wake ni Serikali
moja, tatu au kuvunja muungano.
10)
Kuvunja Muungano ni sawa na kuvua koti
Baadhi ya wanasiasa wanazungumzia suala la
kuvunja muungano kwa wepesi sana. Suala la kuvunja muungano linachukuliwa kama
jambo la usiku mmoja. Dhana hii inajengwa kwa makusudi ya kuwatoa hofu wananchi
kwamba hakutakuwa na athari ikiwa tutafanya hivyo. Wanapozungumzia suala la
kuvunjika kwa muungano, hutanguliza picha ya ‘pepo nzuri’ itakayokuja punde
baada ya kuuvunja. Katika kurahisisha hoja yenyewe, inasemwa kuwa ‘muungano ni
kama koti, ukilichoka unalivua’.
Funzo tunalolipata katika maisha ya
kawaida na uzoefu kutoka nchi zilizopita njia tunayoshawishiana kupita,
zinatufunza vinginevyo. Kuvunjika kwa ndoa tu huambatana na changamoto nyingi
na wakati mwingine kusambaratika kwa familia na mali. Uzoefu wa kusambaratika
kwa dola ya kisovieti ya Urusi na dola ya Yugoslavia kuliambatana na machafuko.
Aidha, kuvunjika kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki mwaka 1977, pamoja na kuwa
ulikuwa ni ushirikiano wa kikanda tu, uliambatana na ukakasi mkubwa. Hivyo,
hatuna sababu yoyote ya kuamini kuwa kuvunjika kwa muungano wa Tanganyika na
Zanzibar uliodumu kwa miaka 49 litakuwa ni jambo jepesi na rahisi.
Msingi wa kuvunja muungano ni dhamira
zinazosukumwa na kutoaminiana na chuki miongoni mwa wanasiasa na baadhi ya
wananchi. Hatuwezi kutarajia matokeo ya kuvunjika kwa muungano huo yazae upendo
na mashirikiano. Upo uwezekano mkubwa wa wazanzibari walioko Tanganyika na
watanganyika walioko Zanzibar kupita katika msukosuko mkubwa. Msukosuko huu
waweza kuhatarisha usalama wa maisha na mali zao. Tayari vipo viashiria vya
biashara za wabara kuchomwa moto na watu wasiojulikana Zanzibar. Njia hii,
haitaweza kuzaa mazingira ya mashirikiano nje ya muungano. Hili likitokea,
ustawi wa nchi mbili hizi utakuwa mashakani ikizingatiwa kuwa usalama wa nchi
hizi mbili unategemeana.
Jambo la kuhofia zaidi iwapo muungano
utavunjika ni kuendelea kuwepo kwa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya
Zanzibar. Sina mashaka kuwa, hoja zilezile zilizofanikisha kuvunja muungano
ndizo zitakazovunja jamhuri hizi mbili. Ni vigumu kuweka ukomo wa kutumika kwa
hoja za mgawanyiko, ilihali watu watakuwa wamedhihirisha kuwa zinafanya kazi
vizuri. Sioni ni kwa sababu gani maeneo mengine yasitake kujitenga kwa
kujificha katika Sera ya Majimbo hususan kule zinakotoka rasilimali kama
Mtwara, kanda ya Ziwa na Kanda ya Kaskazini. Nao watahoji uhalali wa Tanganyika
na watasema ‘utaifa ni kama koti, likikubana unalivua’.
Ni hofu yangu kuwa Zanzibar nayo haitabaki
moja. Mgawanyiko wa kisiasa kati ya kisiwa cha Unguja na Pemba, na waunguja na
wapemba ni dhahiri. Chaguzi za Zanzibar kabla ya mapinduzi na baada ya
mapinduzi zimeambatana na mgawanyiko mkubwa. Katika chaguzi mbili za mwaka 2000
na 2010, Chama cha Mapinduzi kinachoaminika kuungwa mkono na waunguja wengi
hakikupata kiti hata kimoja cha Ubunge na Uwakilishi kisiwani Pemba. Ni vyema
kukumbuka kuwa, uwepo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar hakujamaliza
tofauti za wapemba na waunguja. Kikundi cha Wazee wa Pemba kilichoandika barua
Umoja wa Mataifa kikitaka Pemba kujitenga hakijafa. Uamsho nao ni kikundi cha
kukiangalia kwa makini sana. Mgawanyiko huu katika jamii ya wazanzibari
ulijionyesha pia katika utoaji wa maoni ya Katiba mpya.
Tukiangalia kijiografia na kiutawala,
umbali kati ya Tanganyika na Unguja na Tanganyika na Pemba ni mdogo sana
ukilinganisha na umbali kati ya Pemba na Unguja. Mazingira haya ya kijiografia,
na fukuto la mgawanyiko ndani ya Zanzibar, yataipa changamoto kubwa sana
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kujitawala nje ya muungano. Mazingira haya
yanatoa fursa nzuri sana kwa wasioitakia mema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kukamilisha azma yao ya kujitenga kwa Pemba. Gharama ya hili kwa wazanzibari na
ustawi wao itakuwa kubwa sana. Mazingira haya, hayatavutia huo uwekezaji unaotumainiwa
kutoka OIC wala uarabuni. Maana, ustawi hautokani na kuwa na rasilimali pekee,
bali kuwepo kwa amani na utulivu. Hali kadhalika iwapo Zanzibar itaingia kwenye
machafuko na kusambaratika, Tanganyika haitakuwa salama pia maana usalama wetu
unategemeana.
Hitimisho
Hakuna siasa rahisi kama siasa ya kugawa
watu na siasa ya kubomoa. Kuutetea muungano na haswa muundo wa Serikali mbili
kunahitaji ujasiri na uongozi. Ujasiri na uongozi hukaa vifuani mwa viongozi
makini. Wanasiasa makini huunganisha watu na ni jukumu gumu. Ndio maana
haishangazi kuwa tuna wanasiasa wengi wanaohubiri mgawanyiko kuliko wanaohubiri
umoja.
Ukweli unabaki, kutokuendelea kwa
Tanganyika au Zanzibar hakutokani na Muungano bali Muungano ni 'bangusilo' tu.
Zanzibar imerudishwa nyuma na matatizo yanayotokana na historia yake kabla na
baada ya mapinduzi. Vivyo hivyo Tanganyika imerudishwa nyuma na matatizo ya
kiutawala ikiwemo ubadhirifu na ufisadi. Matatizo ya Tanzania bara na Zanzibar
hayatokani na muungano wala muundo wa
Serikali mbili. Kinyume chake Muungano umeijengea Tanganyika na Zanzibar umoja
na utaifa, umoja uliotuwezesha kukabili misukosuko ikiwemo vita dhidi ya
Uganda. Tusijifiche nyuma ya Muungano, tutafute suluhu ya matatizo yetu ya
ndani ya pande zote.
Suala la muungano na muundo wake lafaa
kufafanuliwa na kujadiliwa kwa kina na uwazi. Ikiwa tutajiridhisha kuwa
mazingira yetu yamebadilika kiasi cha kuhitaji muundo mwingine si vibaya
tukaubadili. Ni vizuri tu kuwaeleza wananchi kinagaubaga kuwa, kama ambavyo
muundo wa serikali mbili unawagharimu, mabadiliko kwenda katika mfumo wowote
tutakaokubaliana yatakuwa na gharama zake pia, tena zaweza kuwa kubwa kuliko
zilizopo. Ni vyema wananchi wakafahamishwa gharama hizo ili wawe tayari kufanya
maamuzi sahihi na kuzibeba.
Swali tunalopaswa kujiuliza kwa dhati
mioyoni mwetu ni kama tunataka muungano uendelee au la. Ikiwa tunautaka, Napata
shida kuamini kuwa tunaweza kuuendeleza nje ya muundo wa Serikali mbili. Maoni
yangu, upo uwezekano mkubwa kuwa nje ya muundo wa Serikali mbili, na ikiwa
muungano utaendelea kuwepo hatutakuwa na serikali mbili, bali muundo wa
serikali nne ambazo ni serikali za Tanganyika, Pemba, Unguja na Shirikisho.
Maana ni vigumu kupangua mbili ukasimamia kwenye tatu. Kupangua ni rahisi
kuliko kupanga, kubomoa ni rahisi kuliko kujenga.
Hatimaye, ustawi na hatma ya nchi yetu,
muungano wetu na vyote vile tunavyovithamini viko mikononi mwetu. Wakati
umefika, wanaoamini katika utaifa wa Tanzania wasimame na waseme sasa au wanyamaze na kuishi na majuto milele!
Mimi nimechagua kusema!
Ni mada nzuri na iliyokwenda shule lkn. ni kubwa mno na inachosha kusoma.
ReplyDeleteW'tza wengi hatuna utamaduni wa kusoma na mada ikiwa kubwa kama hii ndio kabisa!
Natamani mwandishi angeigawa vipande vipade na kuileta ktk siku tofaiti tofauti ingeleta maana zaidi.
Hata hivyo, nampongeza sana mleta mada kwa kutenga muda na kutumia elimu yake kusaida wengine....BIG UP!!
sasa kwa nini tusifikirie kuwauliza wananchi wa nchi mbili hizi ya kuwa wanautaka au hawautaki muungano na kwa upande wa zanzibar tukawaomba UN kama walivyofanya kule sudan wakasimamia
ReplyDeletena ikiwa hivyo kwanini basitusifikirie serekali 3 ambazo kila nchi muhusika itakuwa ni dola kamili
katika mambo saba yatumeya warioba yakapunguzwa mambo ya sarafu na benk,uhamiaji mambo ya yanje nauhusiano wakimataifa uasjili wavyama vya siasa haya yakasimamiwa na nchi wahusika
pia ni kwa nini tusifikirie kuungana kwa muungano wa kimkataba
vyvoyote vire ndugu yangu kwani lazima tuungane? wazanzibari hawataki , kwanini mnawangangania tu hii kitu muungano , hebu tuwaachie waripumuwe na sisi watuachie tuendereze tanganyika yetu, waone vipi tutaweza kupiga hatua na wao wakabaki nyuma na visiwa vyao
ReplyDeleteAgain Pumba, The only solution ni Wananchi wa Nchi hizi mbili kuulizwa kama wanautaka na ikiwa wanautaka ni muungano wa aina gani. Vyama, wanaharakati, masheikh, mapadri hawana mamlaka ya kuwalazimisha wananchi kuhusu mustakbali wa maisha yao.
ReplyDeleteNdugu zangu, suala la kusema kwamba W'bari hawataki muungano ni uongo na lisilo na ushahidi wowote!
ReplyDeleteUkweli ni kwamba wasiotaka muungano ni viongozi wa chama cha CUF, UWAMSHO na baadhi ya viongozi wachache wa CCM-Z'bar.
Sisi wananchi tulio wengi bado hatuna msimamo wa moja kwa moja juu ya jambo hili na badala yake tunawasikiliza viongozi wetu tu!
Leo hii, ukimuuliza mwanachama yeyote wa cuf, kwanini mnataka N'KATABA' atakwambia 'Maalim kashasema'
Kukubaliana na kutokubaliana na viongozi wetu itategemea namna watakavyo tuonesha namna Z'bar itakavyostawi nje ya muungano na sio tu "Mnautaka hamuutaki!
Kusemea watu wengi ni udikteta. Sio wazanzibari wote hawataki muungano.
ReplyDeleteTatizo hapa znz kuna watu wanao jiona wanakuraya turufu, huo nkataba anao taka mdau wananchi wingi hatuja uwelewa tulizani hihifursa tulio ipata tuta itumiavizuri kudai mustakbali wa visiwavyetu mnatokea wehu mnataka nkataba huku vitendo vya kikatili inafanyika bila hata ibu mnafikri nani atakuacheni mpumue, iwe znz, pepo ya magaidi tuchangini katiba tuache ujuha
ReplyDelete