Habari za Punde

Taarifa ya Serekali Kuhusi Ajali ya Boti ya Kilimanjaro 2

TAARIFAA YA SERIKALI KUHUSU TUKIO LA AJALI YA KUDONDOKA ABIRIA WALIOKUA WAKISAFIRI KUTOKA PEMBA KUJA UNGUJA LEO TAREHE   05-01-2014 KWA BOTI YA KILIMANJARO II

Ndugu Wanahabari

Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, tumewaita muda huu kuwaeleza kwa majonzi makubwa kuhusu tokeo la ajali ya kudondoka kwa baadhi ya abiria waliokua wakisafiri kutoka Pemba kuja Unguja, kwa boti ya MV.  Kilimanjaro II.


Ndugu Wanahabari

Kunako majira ya saa 3:00 za asubuhi wakati boti hiyo ikiwa safarini kutoka Pemba kuja Unguja ilipofika katika   maeneo ya bahari ya Nungwi ilikumbwa na mawimbi makali, mawimbi ambayo yalisababisha baadhi ya abiria waliokuwa wamekaa nje sehemu ya mbele kusombwa na mawimbi na kudondoka baharini.


Ndugu Wanahabari

Baada ya kutokea tukio hilo, vyombo vya Serikali vikisaidiwa na wananchi wa Nungwi na wa maeneo ya jirani walifika katika eneo la tukio kwa ajili ya kufanya uokozi. Katika zoezi hilo, vyombo hivyo vimefanikiwa kuokoa watu watatu (3) wote wanaume watu wazima wakiwa wako hai na hali zao zinaendelea vizuri katika hospitali ya Mnazi Mmoja. Aidha, jumla ya maiti watano (5) wamepatikana. Kati ya hao, wanaume watatu (mmoja mtu wazima na wawili watoto) na wanawake wawili (mmoja mtu mzima na mmoja mtoto).

Maiti tatu tayari zimeshatambuliwa na kukabidhiwa jamaa zao (wanaume wawili na mwanamke mmoja). Maiti wawili waliokuwa bado hawajatambuliwa wapo katika chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali kuu ya Mnazi Mmoja. Tunawaomba wananchi waende kuwatambua ndugu na jamaa zao na kukabidhiwa kwa ajili ya hatua za mazishi.


Ndugu Wanahabari

Vyombo vyetu bado vinaendelea na kazi za utafutaji wa abiria wengine na taarifa zaidi zitaendelea kutolewa kwa kadri hali itakavyoendelea.

Ndugu Wanahabari

Kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar natoa mkono wa pole kwa ndugu na jamaa wa waliopoteza maisha yao na tunamuomba Mwenyezi Mungu awalaze Marehemu mahala pema peponi AMIN.  Vilevile tunawaomba Mwenyezi Mungu awajaalie afya njema majeruhi wote.

Nachukua fursa hii kuwaomba wananchi wenzangu ambao hawajawaona ndugu na jamaa zao waliosafiri na chombo hicho wapeleke taarifa hizo kwa Masheha wa Shehia zao, Wakuu wa Wilaya, Vituo vya Polisi, Mamlaka ya Usafiri Baharini au Idaya ya Kukabiliana na Maafa Unguja na Pemba.

Ndugu Wanahabari

Naomba nichukue nafasi hii kwa mara nyengine tena, kuwaomba wananchi wote tuwe na subra wakati huu wa msiba na kwa wale tunaotumia bahari kwa usafiri na shughuli nyengine tuendelee kuchukua hadhari wakati huu wa upepo mkali na tufuatilie taarifa za Mamlaka ya Hali ya Hewa ili kuepukana na madhara ambayo yanaweza kupatikana.

Ahsanteni sana


Dkt. Khalid S. Mohamed
KATIBU MKUU
OFISI YA MAKAMU WA PILI RAIS

ZANZIBAR

1 comment:

  1. Katibu mkuu unasema watu wachukue tahadhari. Hivi kwani Serikali nzima hiyo haiwezi kuvizuia vyombo hivi visifanye safari pale ambapo hali ya hewa inaonekana mbaya kiasi hicho. Hasa ukizingatia kwamba Zanzibar hatuna vyombo na utaratibu wa uokozi kwa maafa haya.

    Teknolojia zilizojaa munashindwa na hata utaratibu wa kufuatilia mwenendo wa vyombo vya bahari na hali ya hewa.

    Baada ya kepteni wa meli hii kuona hali kua mbaya kwanini kusiwe na utaratibu wa kuwazuia watu wote wasikae nje ya boti hilo.

    Tutauana kizembe hadi lini.

    ReplyDelete

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.