Habari za Punde

Hotuba ya Waziri wa Afya Baraza la Wawakilishi


 
 
HOTUBA YA WAZIRI WA AFYA MHESHIMIWA JUMA DUNI HAJI KUHUSU MAKADIRIO NA MATUMIZI YA WIZARA YA AFYA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/15 KATIKA BARAZA LA WAWAKILISHI, ZANZIBAR
 
 


1.0 UTANGULIZI


1.0.1  Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja kwamba sasa Baraza lako tukufu likae katika kamati ya matumizi ili isikilize maelezo ya makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Afya kwa kazi za kawaida na kazi za maendeleo kwa mwaka wa fedha 2014/2015.

 

1.0.2  Mheshimiwa Spika, kabla ya yote, sina budi kuanza kumshukuru Mola wetu mtukufu kwa kutuwezesha kuwa na afya njema, usalama wa nchi uliotuwezesha kukutana hapa na kuniwezesha kutoa hotuba ya wizara yangu mbele ya wajumbe wa Baraza hili tukufu.  Pongezi maalum ziende kwa Mhe. Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Makamo wa Kwanza wa Rais na Makamo wa Pili wa Rais kwa busara na hekima za utawala katika kuiongoza nchi hii.

 

1.0.3  Mheshmiwa Spika, nichukuwe nafasi hii pia kuwashukuru wajumbe wa Baraza lako, viongozi wa mikoa, wilaya na kwenye jamii, pamoja na wananchi wenyewe.  Natambua michango yao ya hali na mali waliyoitoa, imeshajiisha kwa kiasi kikubwa kujenga dhamira, ari na imani kubwa kwa wafanyakazi wa sekta ya afya kutoa huduma zilizobora. Aidha naomba nichukue fursa hii kumpongeza Naibu Waziri wa Afya, Katibu Mkuu, Wakurugenzi, Watendaji na Wataalamu wote wa wizara yangu kwa juhudi na mashirikiano waliyonipa na utendaji wao wa kuwahudumia wananchi kwa uadilifu uliopelekea kufanikisha kazi zilizopangwa. Vile vile napenda kuchuchua fursa hii kuliomba Baraza lako tukufu kupitia Waheshimiwa wajumbe kuzidi kumuombea dua Mkurugenzi Mkuu wa Wizara ya Afya Dk. Malick Abdalla Juma baada ya kupata ajali ya kuvamiwa na majambazi alipokuwa Nairobi siku ya tarehe 23 Novemba 2013. 

 

1.0.4  Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa pongezi zangu hizo, naomba uniruhusu nitoe maelezo ya mapato na matumizi, utekelezaji wa majukumu na malengo makuu pamoja na changamoto zilizojitokeza kwa mwaka wa fedha 2013/2014. Hatimae nitoe malengo na makadirio ya mapato na matumizi kwa mwaka 2014/2015.

2.0     MAPATO NA MATUMIZI KWA MWAKA WA FEDHA 2013/2014


2.1     Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa rasilimali fedha una mchango mkubwa katika kutekeleza malengo ya wizara, kama msemo wa kiswahili unavyosema gogo haliendi ila kwa nyenzo. Kwa mwaka wa fedha 2013/2014 Wizara ya Afya ilipangiwa kuchangia jumla ya Tsh. 924,000,000 kwenye mfuko mkuu wa serikali kupitia vyanzo mbali mbali vya mapato.  Aidha, wizara iliidhinishiwa  kutumia Tsh 21,318,000,000, kati ya hizo Tsh 5,764,000,000 kwa kazi za kawaida, Tsh 1,536,585,000 ikiwa ni ruzuku na Tsh 14, 017,415,000 kwa mishahara na maposho. Kwa upande wa kazi za maendeleo jumla ya Tsh 6,333,000,000 ziliidhinishwa kutoka SMZ na Tsh 42,335,617,000 kutoka kwa wahisani wa maendeleo.

2.2     Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi wa Machi, 2014 wizara iliweza kuchangia Tsh 443,829,558 (48%) katika Mfuko Mkuu wa Serikali. Vile vile katika kipindi hicho wizara imeingiziwa jumla ya Tsh 1,502,189,520 (26%) kwa kazi za kawaida, Tsh 13,520,636,477 (96.4%) kwa mishahara na posho, Tsh 614,292,912(45%) ikiwa ni ruzuku. Kwa kazi za maendeleo wizara ilikwisha ingiziwa Tsh 1,767,181,149 (28%) kutoka SMZ na Tsh 13,042,037,000 (31%) kutoka kwa washirika wa maendeleo.

2.3     Mheshimiwa Spika, baada ya kueleza kwa muhtasari mapato na matumizi kwa mwaka wa fedha 2013/2014 sasa nieleze utekelezaji wa malengo makuu ya wizara na kazi za kila siku kupitia idara na taasisi ziliomo ndani ya wizara hii.

3.0     MAFANIKIO KWA MWAKA 2013/14


3.1   Mheshimiwa Spika, wizara imepata mafanikio mazuri katika utekelezaji wa majukumu yake ikiwa ni pamoja na utekelezaji wa malengo yake makuu ya mwaka 2013/2014. Mafanikio hayo yanatokana na kuwepo na usalama wa nchi kwa kipindi chote,  busara na hekima za utawala na uendeshaji wa nchi kutoka kwa viongozi wetu wa kitaifa.  Miongoni mwa mafanikio hayo ni pamoja na:-

1.    Kuongezeka kwa upatikanaji wa fedha za kununulia dawa na vifaa tiba kutoka Tsh 3,028,372,981 kwa mwaka 2012/2013 hadi kufikia Tsh 5,718,583,149 mwaka 2013/2014. Asilimia 25 ya fedha hizi zilitoka Serikalini na asilimia 75 kutoka kwa washirika wa maendeleo. Kufanikiwa huku kumepunguza manung’uniko makubwa ya ukosefu wa dawa katika hospitali na vituo vya afya.

2.    Kuwapatia wafanyakazi wa hospitali na vituo vya afya posho maalumu la mazingira hatarishi (Risk Allowance).

3.    Wizara imefanikiwa kusomesha wafanyakazi wake ambapo kwa mwaka 2013/2014 jumla ya wafanyakazi 142 wamepelekwa masomoni  kati yao wamo madaktari saba wanaosomea fani mbali mbali za udaktari bingwa.

4.      Kukamilika kwa jengo la ofisi ya Mradi Shirikishi wa Afya ya Uzazi na Mtoto (IRCH) liliopo Kidongo Chekundu.

5.    Kuongezeka kwa kinamama wanaojifungua katika vituo vya afya na hospitali kutoka asilimia 49.4 mwaka 2012 hadi asilimia 56.6 mwaka 2013.

6.    Kuongezeka kwa asilimia ya watoto chini ya mwaka mmoja waliopata chanjo (Penta 3) kutoka asilimia 81 mwaka 2012 hadi kufikia asilimia 84.4 mwaka 2013.

7.    Kupungua kwa ugonjwa wa Malaria katika jamii kutoka asilimia 0.06 mwaka 2010 hadi kufikia asilimia 0.03 mwaka 2013

8.    Kujengwa kwa jengo jipya kwa ajili ya kutolea huduma za upasuaji wa ubongo na uti wa mgongo (Neurosurgical Services) katika hospitali ya Mnazi Mmoja.

9.    Kukamilika ujenzi na kulipatia vifaa na samani jengo la wodi ya wagonjwa wa akili katika hospitali ya Wete Pemba.

10. Ujenzi wa vituo vya afya na nyumba za wafanyakazi Mzambarauni Pemba na Mwera  Unguja

11. Ujenzi wa  jengo la huduma za akinamama na huduma za uzazi ambalo limejumuisha wodi za wajawazito, magonjwa ya akinamama, chumba cha upasuaji, maabara, sehemu ya kufulia na kliniki  katika hospitali ya Wete

12.  Kufunga mtambo wa kuchomea taka katika hospitali ya Mnazi Mmoja

13. Ujenzi wa chumba cha maiti katika hospitali ya Wete pamoja na ukarabati mkubwa wa Wodi ya Mapinduzi Kongwe

14. Kuajiriwa  kwa wafanyakazi wapya 840 wa kada mbali mbali kama vile madaktari, wauguzi, wasaidizi wafamasia,madaktari wasaidizi, madaktari wasaidizi wa meno, mafundi sanifu wa maabara, maafisa afya ya mazingira,wapishi,walinzi,  maodali, makarani, madereva na kadhalika.

3.2   Mheshimiwa Spika, baada ya kueleza kwa muhutasari mafanikio yaliyopatikana kwa mwaka wa fedha 2013/2014, sasa naomba uniruhusu nieleze utekelezaji wa kazi kwa kila Idara na taasisi ziliomo ndani ya wizara hii.

4.0     IDARA YA KINGA NA ELIMU YA AFYA


4.0.1  Mheshimiwa Spika, Idara ya Kinga na Elimu ya Afya ina jukumu la kutoa huduma bora za kinga pamoja na elimu ya afya kwa wananchi ili kujikinga na maradhi ya kuambukiza na yasiyo ambukiza. Utekelezwaji wa kazi za Idara hii kwa mwaka 2013/2014 unaelezwa kupitia vitengo mbali mbali kama ifuatavyo:

4.1     Kitengo cha Kupambana na Magonjwa Yasiyoambukiza

4.1.1  Mheshimiwa Spika, kumekuwa na juhudi mbali mbali zinazofanywa ili kukuza uwelewa wa jamii juu maradhi yasiyoambukiza, mojawapo ni filamu maalum iliyoandaliwa yenye kueleza mambo hatarishi yanayochangia katika kupata maradhi haya. Filamu hii imetayarishwa kwa kushirikiana na Idara ya Habari maelezo na kuionesha katika vijiji mbali mbali vya Unguja. Pia vipindi mbali mbali vya televisheni na redio kuhusiana na lengo hilo vimerushwa hewani.

4.1.2  Mheshimiwa Spika, muongozo wa matibabu ya maradhi yasiyoambukiza umeandaliwa na wataalamu wetu pamoja na madaktari bingwa na tayari sasa unatumika. Muongozo huu umezingatia matibabu ya maradhi haya kwa upana wake. Aidha, kwa kushirikiana na Jumuiya ya Watu Wanaoishi na Kisukari, kumeanzishwa vikundi vya mazoezi katika Wilaya zote za Unguja na Pemba kwa nia ya kujikinga na maradhi haya. Vikundi hivi vimekuwa vikipitiwa mara kwa mara kwa kupewa maelekezo na pia kualikwa katika tamasha tofauti yanayohusiana na ufanyaji wa mazoezi.

4.1.3  Mheshimiwa Spika, utafiti unaongalia mtizamo, na uelewa juu ya maradhi yasioambukiza umefanyika katika Wilaya za Mjini, Magharibi, Kaskazini A, Chake Chake na Micheweni. Hatua inayoendelea kwa sasa ni uchambuzi wa taarifa zilizokusanywa. Matokeo ya utafiti huu yatasaidia katika kuweka mikakati itakayosaidia katika kupambana na maradhi haya thakili kwa afya na maisha ya wanadamu. 

4.1.4  Mheshimiwa Spika, katika kuadhimisha kutimia miaka 50 ya Mapinduzi kitengo kilitoa huduma ya upimaji wa hiari wa maradhi ya kisukari na shindikizo la damu. Jumla ya watu 574 walichunguzwa kati yao 85 walikuwa na dalili za shindikizo la damu na watu 10 walikuwa na  dalili za kisukari na kushauriwa kurudia uchunguzi katika vituo vya afya vilivyo karibu nao.

4.1.5 Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Daktari bingwa wa maradhi ya moyo kutoka hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar, huduma ya siku tano kwa wagonjwa wenye matatizo ya moyo na shindikizo la damu katika hospitali tatu za wilaya za Chake Chake, Wete na Abdalla Mzee zilitolewa. Jumla ya watu 92 walichunguzwa (wanawake 64; wanaume 28), kati yao watu 11 waligundulika kuwa na matatizo ya moyo wakiwemo watoto wawili ambao walipewa rufaa kwenda katika hospitali ya Mnazi Mmoja kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

 

4.1.6 Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Jumuiya ya Wanafunzi wa Udaktari - Tanzania Medical Students’ Association (TAMSA), kitengo kimefanya uchunguzi wa Kisukari na Presha katika Wilaya za Mjini, Magharibi, Kati, Kusini, Kaskazini A na Kaskazini B.  Jumla ya watu 1,800 walifanyiwa uchunguzi na matibabu yalitolewa kwa waliogunduliwa na matatizo.

4.1.7  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 kitengo kimepanga kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuanzisha kamati ya kitaalamu itakayojumuisha wajumbe kutoka sekta mbali mbali ambayo itakuwa na jukumu la kushauri, kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa mikakati mbali mbali ya kupambana na magonjwa yasiyoambukiza.

2.    Kuanzisha daftari la usajili wa magonjwa yasiyoambukiza

3.    Kuwasilisha matokeo ya utafiti uliolenga kupima uelewa na mitazamo ya jamii juu ya magonjwa yasiyoambukiza katika ngazi tofauti na kuyafanyia kazi.

4.2    Kitengo Cha Kufuatilia Mwenendo wa Maradhi


4.2.1  Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2013/2014 jumla ya watu 80 walitafunwa na mbwa (wanaume 57 na wanawake 23) kutoka katika wilaya tofauti za Zanzibar na kusababisha watu wawili kutoka maeneo ya Kiwengwa na Ndijani Mseweni kufariki dunia kutokana na ugonjwa wa kichaa cha mbwa (Rabies).  Hivyo, kwa kushirikiana na Wizara ya Mifugo na Uvuvi mikakati maalum ya kuweza kukabiliana na tatizo hilo imetayarishwa ikiwemo kuendesha zoezi la uchanjaji wa mbwa katika shehia za Unguja, kufuatilia taarifa za waliotafunwa na mbwa kwa kila siku, kutoa elimu kwa jamii na kusimamia upatikanaji wa chanjo kwa wale waliotafunwa.

 

4.2.2 Mheshimiwa Spika, jumla ya wafanyakazi wa afya 187 wanaoshughulika na utoaji wa taarifa za Wiki - Infectious Disease Weekly Ending (IDWE) wamepatiwa mafunzo yanayohusiana na ugonjwa wa mafua ya ndege (bird flu), ugonjwa wa bonde la ufa (Rift valley fever) na ugonjwa wa kichaa cha mbwa (Rabies). Mafunzo haya yalifanywa kwa ushirikiano na kitengo cha Epidemiolojia na Idara ya Mifugo.

4.2.3  Mheshimiwa Spika, sampuli za maji zilichukuliwa kutoka maeneo tofauti baada ya kubainika kuwepo kwa maradhi ya kuharisha katika maeneo hayo. Matokeo yalionesha maji kutoka visima vya Fuoni Kibondeni na Chunga yana vimelea vya maradhi ya kuharisha. Hatua za kutia dawa ya kuua vidudu kwenye maji hayo zimechukulia kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji.

4.2.4  Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumeshuhudia kuwepo kwa ugonjwa wa homa ya “dengue” hapa nchini unoambukizwa na virusi vinavyoenezwa na mbu aina ya “Aedeis”.  Hadi sasa Hospitali ya Mnazi Mmoja imepokea wagonjwa wanane  kutoka maeneo ya Mwera (3), Kwamtipura (1), Darajabovu (1), Kama (1) Fuoni (1) na Dar es Salaam (1) waliodhaniwa kuwa na ugonjwa huu kutokana na dalili walizokuwa nazo. Kati ya wagonjwa hao mgonjwa mmoja tu aliyetoka Darajabovu ndie aliyethibitishwa kuwa na ugonjwa huo ameshatibiwa na kupewa ruhusa.

4.2.6  Mheshimiwa Spika, Wizara imechukuwa hatua mbali mbali katika kukabiliana na maradhi haya zikiwemo kufanya mkutano na waandishi wa habari, kuelimisha jamii kupitia vyombo vya habari (redio na televisheni), kutafuta vifaa vya kufanyia uchunguzi na kuandaa mpango maalum wa kuwakumbusha wafanyakazi wa afya wa ngazi mbali mbali.  Nachukua fursa hii kuwaomba wananchi kufuata maelekezo yanayotolewa na wataalamu ili kuweka tahadhari ya kujikinga na maradhi haya.

4.2.7  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015, kitengo kimepanga kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kutoa mafunzo ya afya  maskulini juu ya maradhi ya miripuko kwa yale maradhi yanayoibuka na yanayo rejea (Emerging and Re-emmernging Infectious Diseases)

2.    Kuendelea kufuatilia mienendo ya maradhi mbali mbali  yanayo jitokeza katika jamii.

4.3    Kitengo cha Huduma za Matibabu ya Macho


4.3.1  Mheshimiwa Spika, kwa mashirikiano na uongozi wa Shirika la Alnour Charitable Agency liliopo hapa Zanzibar, kambi kubwa ya uchunguzi na matibabu ya macho ilifanyika kwa muda wa wiki mbili huko Pemba. Jumla ya watu 2,235 walipatiwa huduma, kati ya hao waliofanyiwa upasuaji wa mtoto wa jicho ni 152. Vile vile watu 750 walipatiwa miwani (wanaume 400 na wanawake 350).  Aidha, huduma za macho pia zilitolewa huko Pemba kwa ushirikiano na Shirika la Bilal Muslim Agency kutoka Arusha Tanzania Bara, jumla ya watu 250 walichunguzwa na wagonjwa 68 walifanyiwa upasuaji wa mtoto wa macho.

 

4.3.2  Mheshimiwa Spika, kwa upande wa watoto, huduma za upasuaji macho zimefanyika kwa kushirikiana na daktari bingwa wa macho wa watoto kutoka Tanzania Bara. Kwa mwaka 2013/2014 ni watoto wanane waliopelekwa  Tanzania Bara  kati ya watoto zaidi ya 30 waliokuwa wakihitaji huduma hiyo, hii ni kwa sababu madaktari hawa wanatoa huduma kwa Tanzania nzima hivyo huwepo nje ya Mkoa wa  Dar er Salaam  kwa kipindi kirefu. Aidha, ufuatiliaji wa watoto wanaofanyiwa upasuaji umefanyika kwa kuwatembelea watoto 69 (wanaume 29 na wanawake 40) kati yao watoto 34 walionekana wanaendelea vizuri.

 

4.3.3  Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na Kitengo cha Elimu mjumuisho na Stadi za Maisha cha Wizara ya Elimu kumeanzishwa mpango maalum wa kuwafundisha walimu jinsi ya kuwapima wanafunzi wao uwezo wa macho kuona (Vision Assessment). Hali hii inawezesha wanafunzi wengi kupimwa uwezo wa macho kuona na kugundua matatizo yao ya macho na kurahisisha kazi ya uchunguzi wa kitaalam kwa madaktari.  Jumla ya walimu 348 wa Unguja na Pemba wa skuli tofauti walipata mafunzo hayo na wao waliwagundua   wanafunzi 1,125 wana matatizo ya uoni.

 

4.3.4  Mheshimiwa Spika, vifaa kadhaa vya kufanyia kazi katika hospitali na huduma za vijijini vimepatikana ikiwemo gari moja kwa huduma za Macho Pemba,  pikipiki mbili,  vifaa vinne vya kupimia miwani “Trial case” (vitatu kwa Pemba na kifaa kimoja Unguja), mashine ya kupimia presha ya macho ya kisasa  imewekwa  Hospitali ya Wete. Aidha, kumenunuliwa mashine za kupimia macho (Slit lamps) na kupelekwa Pemba.

 

4.3.5  Mheshimiwa Spika, kwa mashirikiano na Maabara ya Afya ya Jamii (Public Health Laboratory) kumefanyika utafiti wa maradhi ya macho kwa watoto wachanga wenye umri wa siku 28 za kuzaliwa. Utafiti huu ulichukuwa takriban miezi 11 na kuhusisha watoto wote waliozaliwa kwa kipindi hicho na kuwachunguza  na kuwangalia  kama wana maambukizo ya macho tongo yanayosababishwa na vimelea (Clamidia na Gonococus). Jumla ya watoto 8,385 walizaliwa na kuingizwa katika utafiti huo, kati yao watoto 511 walibainika kuwa na matatizo ya macho hivyo walipatiwa huduma stahiki.

 

4.3.6  Mheshimiwa Spika, huduma za uchunguzi na matibabu ya macho zimeendelea kutolewa kupitia vituo vya Afya na mikusanyiko ya jamii katika siku za afya za  vijiji  zinazosimamiwa na Timu  za  Afya  za  Wilaya.  Jumla   ya  vijiji  na  vituo vya Afya 22 vilitembelewa  na kupatiwa huduma za macho ambapo wananchi 32,269 walifanyiwa uchunguzi, kwa wale waliobainika na matatizo walitibiwa na pia ushauri uliotolewa kulingana na matatizo yaliyobanika.

4.3.7  Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 kitengo kimepanga kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendeleza kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya macho kwa wananchi kwa mashirikiano ya Timu za Afya za Wilaya (DHMTs)

2.    Kutoa huduma za matibabu ya macho kwa watoto hususan za upasuaji kwa msaada mkubwa wa madaktari bingwa wa watoto kutoka Muhimbili chini ya mradi maalum wa Muhimbili Childhood Initiative (MCBI).

3.    Kuendelea kutoa mafunzo ya msingi ya muda mfupi ya uchunguzi na utibabu wa macho kwa wafanyakazi wa vituo vya Afya.

4.4     Kitengo cha Kupambana na Maradhi Yasiyopewa  Kipaumbele


 

4.4.1  Mheshimiwa Spika, wizara imo katika kutekeleza mpango nzima wa kuondoa kabisa maradhi ya kichocho na matende hapa visiwani.  Kwa kipindi cha mwaka 2013 jumla ya wananchi 1,902 wamekaguliwa Kichocho kati yao watu 1,249 walibainika na maradhi hayo sawa na  65.7%. Kwa upande wa matende wananchi 121 walikaguliwa na hakuna mtu hata mmoja aliyebainika na vimelea vya Matende.

 

4.4.2  Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kuondoa maradhi ya kichocho, wizara imetiliana saini na Serikali ya Watu wa China chini ya ushirikiano na usimamizi wa WHO kufanya utafiti wa kuondoa kabisa maradhi ya kichocho nchini.  Mpango huu ni wa miaka mitano na utashughulikia ufuatiliaji wa makonokono katika mito na mabwawa, mabadiliko ya tabia kwa wananchi dhidi ya maradhi ya kichocho na ulishaji wa dawa za kichocho.

 

4.4.3  Mheshimiwa Spika, ukaguzi katika baadhi ya mito na mabwawa 40 umefanyika kwa lengo la kuangalia makonokono wenye uwezo wa kusambaza maradhi ya kichocho. Ukaguzi huu ulifanyika katika sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba ambapo makonokono yanayosababisha ugonjwa wa kichocho  yaligunduliwa katika shehia 15. 

 

4.4.4  Mheshimiwa Spika, ulishaji wa dawa za kichocho, minyoo na matende unaendelea kwa lengo la kutibu na kupunguza maambukizo mapya ya maradhi hayo. Dawa hizi zinatolewa kwa wale wote wanaostahiki.  Kwa Unguja jumla ya  watu 744,434 walistahiki kula dawa, kati yao  watu 625,092 (84%) walikula dawa. Kwa upande wa Pemba waliostahiki kula dawa ni 348,570, kati yao watu 290,862 (83%) walikula dawa.

 

4.4.5  Mheshimiwa Spika, ili kukuza uelewa juu ya kujikinga na maradhi ya kichocho, wizara imetoa mafunzo katika shehia 15 na skuli zilizomo katika shehia ya Mwera, Dole na  Mwanakwerekwe. Aidha, wanafunzi 6,017 kati ya wanafunzi 7,317 wa skuli 15 zinazofanyiwa majaribio (82.2%) wamehamasishwa kujikinga na kichocho kwa njia za michezo salama ya kurekebisha tabia. Pia wanajamii 600 kutoka shehia 15 wameelimishwa kuhusu kinga dhidi ya maradhi ya kichocho. 

 

4.4.6  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 kitengo kimejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendeleza kazi za utafiti kwa ajili ya mapambano dhidi ya maradhi ya Kichocho, Minyoo, Matende  pamoja na maradhi  mengineyo yasiyopewa kipaumbele.

2.    Kitengo kitaendelea na kudumisha utafiti wa makonokono ambao ni walezi wa viini vya maradhi ya kichocho katika mito na maziwa.

 

4.5    Kitengo cha Lishe


4.5.1  Mheshimiwa Spika, ulishaji wa matone ya vitamini “A” na dawa za minyoo kwa watoto chini ya miaka mitano ulifanyika kwa awamu mbili. Taarifa zinaonesha kuongezeka kwa kiwango cha ulishaji wa matone ya vitamini A na dawa za minyoo kutoka 61.5% ya mwaka 2012 hadi kufikia 77.5% mwaka 2013. Matone ya Vitamin A yanasaidia kuwakinga watoto dhidi ya magonjwa mbali mbali yakiwemo ya uoni mdogo na maradhi ya ngozi.

4.5.2  Mheshimiwa Spika, ili kuongeza kiwango cha matumizi ya chumvi iliyowekewa madini joto katika jamii yetu, wizara imefanya mafunzo kwa wauzaji wa chumvi wa rejareja na jumla juu ya umuhimu wa ununuzi na usambazaji wa chumvi yenye madini hayo. Jumla ya wauzaji chumvi 35 kwa Unguja na 30 kwa Pemba pamoja na wazalishaji wa chumvi walishiriki mafunzo hayo.

4.5.3  Mheshimiwa Spika, ufuatiliaji shirikishi wa huduma za matibabu ya utapiamlo mkali kwa hospitali nane na vituo vyote vya afya, umefanyika. Mapungufu yaliyobainika ni pamoja na uwekaji wa taarifa za utapiamlo mkali kutoridhisha, jambo linalopelekea kukosa taarifa sahihi juu ya hali ya utapiamlo mkali. Suala la utapiamlo limehimizwa sana katika mkutano wa WHO Geneva na katika mikutano ya mawaziri wa afya waliokutana Luanda nchini Angola mwezi Aprili, 2014.

4.5.4  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 kitengo kimepanga kutekeleza kazi kuu zifuatazo;-

1.    Kuongeza kiwango cha utoaji wa matone ya Vitamin A kwa watoto chini ya umri wa miaka mitano kutoka asilimia 77.5 mwaka 2013 hadi asilimia 90 kwa mwaka 2014.

2.    Kutengeneza na kuchapisha miongozo mbali mbali juu ya unyonyeshaji na ulishaji wa watoto wadogo.

4.6    Kitengo cha Afya ya Wafanyakazi


4.6.1  Mheshimiwa Spika, uchunguzi wa wafanyakazi umefanyika kwa wafanyakazi 8,108, kati yao 106 walibainika kuwa na matatizo ya kiafya ikiwemo ugonjwa wa ini, homa ya tumbo, UKIMWI, shindikizo la damu na uoni mdogo. Wafanyakazi hawa wametokea sehemu tofauti ikiwemo maduka, mashirika ya uma, masoko, wafanyakazi wa viwanda. Kwa wale wote waliobainika na maradhi, walishauriwa kwenda hospitali na kupata matibabu. Taarifa hizi zinaongeza uelewa wa kuhitajika wafanyakazi tukiwemo sisi wawakilishi, kupima afya zetu mapema kabla hatujaugua.

4.6.2  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 kitengo kitaendelea na kazi za ukaguzi sehemu za kazi pamoja na kufanya uchunguzi wa afya za wafanyakazi.

4.7    Kitengo cha Afya ya Mazingira


4.7.1  Mheshimiwa Spika, katika hatua za utekelezaji wa sheria ya afya ya jamii na mazingira namba 11 ya mwaka 2012, kitengo kimeweza kutengeneza muongozo wa utekelezaji wa sheria kwa mujibu wa viwango vilivyowekwa. Kazi hii imefanywa kwa kushirikiana na wadau mbali mbali wakiwemo Chuo cha Afya Mbweni, Idara ya Mazingira, “Zanzibar Chamber of Commerce”, Umoja wa Walemavu Zanzibar, Mamlaka ya Maji, Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko, “Zanzibar Investment Promotion Authority”, na Baraza la Manispaa. 

 

4.7.2  Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 23/10/2013, wizara yetu iliadhimisha siku ya kunawa mikono duniani katika shehia ya Mangapwani wilaya ya Kaskazini B. Maadhimisho hayo yalitanguliwa na utoaji wa elimu katika skuli 12 za msingi juu ya unawaji sahihi wa mikono. Jumla ya wanafunzi 2,000 wanakisiwa kufaidika na elimu hii. Zoezi hili liliambatana na shindano la kujibu maswali mafupi ambapo washindi watatu kutoka skuli ya Nyerere, Kiongwe na Muungoni walipewa zawadi ya vifaa vya kunawia mikono mashuleni. Aidha, maadhimisho hayo yalijumuisha kurushwa kwa ujumbe mfupi kwenye Redio na Televisheni. Pia Vipeperushi 500 na fulana 250 zinazobeba ujumbe wa kuhamasisha juu ya umuhimu wa kunawa mikono zilichapishwa na kusambazwa kwa jamii.

 

4.7.3  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 kazi kuu zifuatazo zitatekelezwa:-

1. Kufanya uhamasishaji wa sheria ya afya ya jamii na          mazingira ili kuweza kueleweka.

2. Kutengeneza mwongozo wa maradhi ya kipindupindu.

4.8    Kitengo cha Afya Bandarini


4.8.1  Mheshimiwa Spika, kitengo hiki kinajumuisha huduma za afya za bandarini, Uwanja wa ndege na chanjo kwa wasafiri wa kimataifa. Kitengo kimepewa dhamana ya kuzuia uingizwaji na usafirishwaji wa maradhi pamoja na wadudu wasababishao maradhi toka nje ya Zanzibar pamoja na kukabiliana na majanga ya kiafya.

4.8.2  Mheshimiwa Spika, kiasi cha wasafiri 1,125 walitarajiwa kuchanjwa, kati ya hao waliochanjwa ni wasafiri 814 (72.3%). Mbali na uchanjaji huo, ukaguzi wa vyombo vya usafiri wa baharini na mizigo pia umefanyika, vyombo vilivyotarajiwa kuingia kukaguliwa vilikuwa 1,557 ingawa vyombo vilivyoingia na kukaguliwa vilikuwa zaidi ya matarajo na kuifikia 1,996 sawa na asilimia 128.1. Matokeo ya ukaguzi yamebainisha kuwepo kwa vyombo 45 vilivyopatikana na wadudu, vyombo 31 kati ya hivyo vimefanyiwa ufukizwaji (fumigation) na Vyombo 14 vimefanyiwa hatua za usafi (upuliziaji/mitego). Aidha, mabaharia 98 wamekaguliwa, kati yao 46 walibainika kuwa hawajapima afya zao hivyo kupatiwa chanjo zilizostahiki.

4.8.3  Mheshimiwa Spika, kontena 270 za mitumba na vifaa vilivyotumika zimekaguliwa zikiwemo tani za nguo 88, tani za viatu 16, mikoba na friji tani 123. Jumla ya tani 15 za nguo na tani 1.7 za viatu zimeangamizwa baada kuonekana hazifai kwa matumizi ya binadamu. Pia kontena zote zilizoingia zimefanyiwa ufukizaji.

4.8.4  Mheshimiwa Spika, ukaguzi wa maiti 93 na wagonjwa 172 waliopitishwa bandarini na uwanja wa ndege ulifanyika na hakukuwa na mgonjwa wala maiti aliyeonesha dalili za maradhi ya kuambukiza.  Aidha, wageni 62,736 walifayiwa ukaguzi kati yao 13,805 walibainika hawana kadi za chanjo, 13,328 walitoka katika maeneo yasio hatarishi, wenye sababu za kiafya walikuwa 453 na 24 walichanjwa wakati wa kuwasili.

4.8.5  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 kitengo kinatarajia kufanya kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendelea kutoa chanjo kwa wasafiri wa kimataifa.

2.    Kuendelea na ukaguzi wa mazingira ya bandari na utoaji wa elimu ya afya kwa mabaharia.

5.0    IDARA YA TIBA


5.1.1  Mheshimiwa Spika, Idara ya Tiba ina jukumu la kutoa huduma za tiba kupitia hospitali za Chake Chake, Abdalla Mzee, Wete, Kivunge, Makunduchi, Micheweni na Vitongoji. Pamoja na utoaji wa huduma za tiba, Idara hii pia inasimamia uendeshaji wa Mpango wa Damu Salama, Mradi wa Chuo cha Madaktari Zanzibar na usafirishaji wa wagonjwa nje ya nchi.

5.1.2  Mheshimiwa Spika, Hospitali hizi zimeendelea kutoa huduma za matibabu kwa wagonjwa wa ndani na wa nje pamoja na kutoa huduma za uchunguzi wa maradhi mbali mbali. Hadi kufikia Machi, 2014 jumla ya wagonjwa wa nje 227,251 walipokelewa na kupatiwa huduma za matibabu ya nje (101,708 wanaume na 125,543 wanawake). Wagonjwa waliolazwa walikuwa ni 25,465 (6,272 wanaume, 19,193 wanawake), kati yao 389 (2%) walifariki dunia ukilinganisha na 1.02% mwaka 2013/14. Ufafanuzi unaonekana kwenye kiambatisho namba1.

5.1.3  Mheshimiwa Spika, wastani wa idadi ya siku za wagonjwa ambazo hulazwa katika hospitali zetu ni siku mbili, hali hii iko chini ya kiwango kilichopendekezwa na Shirika la Afya Ulimwenguni (WHO) ya kuwa kila mgonjwa anapaswa kulazwa hospitali kati ya siku tatu hadi saba. Mambo ambayo yanafikiriwa kuchangia ni pamoja kukosekana vyumba vya kupumzikia wagonjwa (retention room) mara baada ya kupewa matibabu na kuwa chini ya uangalizi wa daktari na changamoto za uwekaji wa kumbukumbu za wagonjwa. Hata hivyo, matumizi ya vitanda yanaonekana kuwa yapo chini ya kiwango kinacho stahili kulingana na viwango vya matibabu vilivyowekwa ambacho ni (60%), hospitali za Makunduchi (69%) na Micheweni (63%) pekee ndizo zilizofikia kiwango kinachostahili.

5.1.4  Mheshimiwa Spika, huduma za mama wajawazito kujifungua katika hospitali zimeendelea kutolewa katika hospitali zote zilizo chini ya Idara ya Tiba. Jumla ya kina mama wajawazito 10,913 walilazwa, kati yao wajawazito 8,189 walijifungua kwa njia ya kawaida, na wajawazito 651 walijifungua kwa njia ya upasuaji. Aidha, akina mama 21 walifariki dunia kwa sababu mbali mbali za kiafya zikiwemo kutoka damu kwa wingi kabla au baada ya kujifungua, kifafa cha mimba na shindikizo la damu. Ufafanuzi zaidi unaonekana katika kiambatisho namba 2.

5.1.5  Mheshimiwa  Spika, hospitali hizi pia zinahusika na utoaji wa huduma za kliniki  maalum  zikiwemo huduma za maradhi ya kisukari, shindikizo la damu, macho, pua, masikio, koo, kifua kikuu pamoja na magonjwa ya wanawake.  Kwa kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, jumla ya wagonjwa 66,856 walipatiwa huduma katika kliniki hizo ukilinganisha na wagonjwa 83,557 mwaka 2012/13. Ufafanuzi zaidi unaonekana katika kiambatisho namba 3.

5.1.6  Mheshimiwa Spika, vifaa vilipokelewa kutoka kwa wafadhili wa ndani na nje ya nchi kwa hospitali ya Kivunge, vikijumuisha vifaa kwa ajili ya chumba cha upasuaji pamoja na vitanda sita kwa ajili ya wodi ya kina mama wajawazito   na vitanda 20 kwa ajili ya wodi ya watoto, mashine 20 za kupimia presha, “Stethoscope” 20, “vacum exrtractors na Doppler. Aidha,nguo za kuvaa katika chumba cha upasuaji (Theatre) zilipokelewa katika hospitali ya Abdalla Mzee.

5.2    Matibabu Nje ya Zanzibar


5.2.1  Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 jumla ya wagonjwa 234 walifanyiwa tathmini. Kati ya hao wagonjwa 120 walihitaji kupatiwa matibabu nje ya Zanzibar. Wagonjwa 110 (92%) walipelekwa nje ya nchi na wagonjwa 28 (21%), walipelekwa Tanzania Bara. Jumla ya Tshs 2,564,627,947 zilitumika kwa matibabu nje ya nchi ya Tanzania na Tsh 32,487,750 zilitumika kutibia wagonjwa nje ya Zanzibar. Idadi hii ya fedha zilizotumika ni kubwa ukilinganisha na fedha zilizopangwa ambazo zilikuwaTsh 500,000,000.

5.3    Mpango wa Damu Salama

5.3.1  Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka 2013/2014 Mpango wa Damu Salama ulipanga kukusanya “unit” 8,200 za damu kwa mwaka kutoka kwa wachangiaji wa hiari, hadi kufikia Machi 2014 jumla ya ‘units’ za damu 6,671 (81.3%) zilikwisha kusanywa. Damu hiyo ilifanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya “HIV”, “Syphilis”, “Hepatitis B” na “Hepatitis C” kabla ya kusambazwa katika hospitali mbali mbali Unguja na Pemba. Damu iliyokusanywa iligawiwa katika hospitali zote 14 zinazotoa huduma ya damu.

5.3.2  Mheshimiwa Spika, elimu ya afya juu ya uchangiaji wa damu kwa hiari imeendelea kutolewa katika skuli, vyuo, mikusanyiko ya kidini, vilabu vya mipira na sanaa, vikosi vya ulinzi, vilabu vya damu na vikundi vya mazoezi.  Jambo hili linasaidia kupata damu nyingi na kuwa na wachangiaji wa kudumu.

5.3.3  Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/2015 Idara ya Tiba imejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.           Kufufua kitengo  cha kuratibu shughuli za  uchunguzi (Diagnostic Unit)

2.           Kuimarisha upatikanaji wa chakula kwa wagonjwa wote wanaolazwa katika hospitali.

3.           Kukusanya damu units 10,000.

4.           Kusambaza damu kwa asilimia 100 kwa hospitali zote zinazotoa tiba ya damu.

 

6.0    IDARA YA HOSPITALI YA MNAZI MMOJA


 

6.0.1  Mheshimiwa Spika, Idara ya Hospitali ya Mnazi Mmoja ina jukumu la kutoa huduma za rufaa za matibabu na uchunguzi wa maradhi mbali mbali. Idara hii inajumuisha hospitali za Mnazi Mmoja, Mwembeladu na Kidongo Chekundu.

 

6.0.2  Mheshimiwa Spika, nimeshawahi kueleza mbele ya Baraza hili azma ya Wizara kuifanya idara hii kuwa ni taasisi yenye kujitegemea kiuendeshaji, kwa nia ya kuimarisha utoaji wa huduma na kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa majukumu yake. Kwa nia ya kulifanikisha suala hili wizara imewasilisha waraka rasmi katika kamati ya Baraza la Mapinduzi na kueleza gharama za kuendesha hospitali hizo. Kimsingi kamati hiyo ya Baraza la Mapinduzi iliridhia mapendekezo hayo na kuagiza waraka huo uwasilishwe katika kikao cha Makatibu Wakuu.

 

6.0.3  Mheshimiwa Spika, kikao cha makatibu wakuu kiliagiza wizara kuipitia tena rasimu ya sheria hiyo ili kuiimarisha zaidi. Aidha, kikao kiliagiza kwa mwaka 2014/15 Idara ya Hospitali ya Mnazi Mmoja ipewe kasma (vote) yake badala ya kutegemea kasma ya Wizara. Nachukuwa fursa hii kuliarifu Baraza hili kwamba tayari kasma kwa ajili ya idara hii imeshaanzishwa na itaanza kutumika mwaka huu wa fedha.

 

6.0.4  Mheshimiwa Spika, upatikanaji wa wafanyakazi wenye ujuzi ni miongoni mwa mambo muhimu ya kufanikisha utoaji wa huduma bora. Kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2013/2014, Idara ilipokea na kuwapangia kazi wafanyakazi 115 wakiwemo madaktari wa kawaida (Medical Doctors) tisa, wauguzi watatu wenye shahada ya pili, wauguzi 11 wenye shahada ya kwanza, wauguzi wanane wenye stashahada, wahudumu wa Hospitali 80 na madereva wanne. Aidha, idara imepata daktari bingwa wa maradhi ya akinamama (Gynaecologist) kupitia ushirikiano na Chuo Kikuu cha Haukeland ambae atatoa huduma hospitalini hapo kwa muda wa miaka miwili.

6.1    Hospitali ya Mnazi Mmoja


 

6.1.1  Mheshimiwa Spika, huduma katika hospitali hii ziliendelea kutolewa kama kawaida. Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, jumla ya wagonjwa wa nje 44,545 (wanawake 22,942 na wanaume 21,603) walitibiwa. Wagonjwa waliolazwa kwa kipindi hicho ni 27,654 kati yao 822 walifariki dunia kwa maradhi tofauti. Angalia kiambatisho namba 4. Vile vile kiambatisho namba 5 kinaonesha wagonjwa waliotibiwa katika  kliniki maalum zikiwemo za meno, macho, masikio,koo na pua, maradhi ya mifupa,  maradhi ya kina mama, maradhi ya ngozi,maradhi ya kisukari na shindikizo la damu.

 

6.1.2  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/14 Wizara imeanzisha huduma ya uchunguzi wa saratani katika hospitali hii, ambapo hadi kufikia Machi 2014 jumla ya wagonjwa 50 wamechunguzwa (biopsy), kati yao 35 wamegundulika kuwa na saratani na asilimia 43 ya waliobainika walikuwa na saratani ya shingo ya kizazi. Idadi hii ni kubwa na ya kutisha sana katika maendeleo ya afya ya kizazi. Hali hii inatoa umuhimu wa kinamama kufanya uchunguzi wa afya zao mapema hususan katika suala la saratani ya kizazi.

 

6.1.3  Mheshimiwa Spika, hospitali imeanza kutoa huduma ya uchunguzi wa maradhi ya kifua kikuu kwa kutumia mashine mpya ya kisasa (Gene expert) yenye uwezo mkubwa wa kugundua vimelea vya maradhi hayo kwa haraka na kubainika hata kama vimelea vya maradhi ni kidogo.

 

6.1.4  Mheshimiwa Spika, mafanikio mengine yaliyopatikana kwa hospitali hii ni kuanzishwa kwa huduma za uchunguzi wa maradhi na tiba za mfumo wa chakula (Gastro-enterology Endoscopic services). Aidha, huduma hizi zimewezekana kutolewa baada ya kupata msaada wa vifaa na mtaalamu wa kutoa huduma hizo kutoka Jamhuri ya Watu wa China.  Hadi sasa ni wagonjwa 95 ambao wameweza kupatiwa huduma hizo.

 

6.1.5  Mheshimiwa Spika, katika hotuba yangu ya mwaka 2013/14 nilieleza kwamba wizara imeajiri kampuni binafsi kwa ajili ya kusimamia ulinzi katika hospitali hii, jambo ambalo limesaidia kupunguza msongamano wa jamaa wanaokwenda kuangalia wagonjwa wao. Sambamba na hili wizara inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa jengo la kusubiria jamaa wa wagonjwa waliolazwa. Kwa sasa hatua iliyofikiwa ni kupatiwa eneo na ruhusa ya ujenzi kutoka Wizara ya Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati pamoja na kutayarisha michoro. Hatua inayoendelea ni mazungumzo kati ya Wizara ya Afya na Mamlaka ya Mji Mkongwe ili kuweza kujuwa ni jengo la aina gani lijengwe bila ya kuathiri uhifadhi wa Mji Mkongwe.

 

6.1.6  Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma na kuipunguzia gharama serikali za kupeleka wagonjwa nje ya nchi, hospitali imeendeleza kuhudumia kambi za madakatari bingwa kutoka Spain, Uholanzi na Ujerumani. Hadi kufikia Machi 2014 jumla ya wagonjwa 114 walichunguzwa na madaktari wa Uholanzi, kati yao wagonjwa 77 walifanyiwa upasuaji ikiwemo matatizo ya njia ya mkojo na matatizo ya maradhi ya uti wa mgongo.

 

6.1.7  Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na jumuiya isiyokuwa ya kiserikali Zanzibar Out Reach Programme (ZOP), idara imeendelea kuendesha kambi za matibabu 48 zikiwemo za upasuaji katika maeneo tofauti ya visiwa vyetu.  Idadi ya wagonjwa walioonwa ni 6,961 na waliofanyiwa upasuaji ni 433, pia jumla ya watu 643 walipatiwa miwani. Naomba nichukue fursa hii kuipongeza jumuiya hii kwa jitihada zao za kusaidiana na Serikali katika kuhakikisha upatikanaji wa huduma za afya kwa wananchi.

 

6.1.8  Mheshimiwa Spika, huduma za kujifungua ni moja ya huduma inayopewa kipaumbele katika hospitali hii, ambapo kufikia Machi 2014, jumla ya wajawazito 8,420 walilazwa, kati yao 6,553 walijifungua kwa njia ya kawaida (normal delivery) na wajawazito 1,557 walijifungua kwa njia ya upasuaji.  Pia   wajawazito 21 walifariki dunia kutokana na sababu mbali mbali ikilinganishwa na wajawazito 24 waliofariki mwaka jana. Kiambatisho namba 6 kinaeleza zaidi.

 

6.2    Hospitali ya Wazazi Mwembeladu


 

6.2.1  Mheshimiwa Spika, hospitali hii ni maalum kwa ajili ya huduma za kujifungua ambapo hadi kufikia Machi 2014 jumla ya kinamama 5,230 walipokelewa na kinamama 4,873 walijifungua kwa njia ya kawaida  na 14 walijifungua kwa njia ya upasuaji na kwa bahati nzuri hakukutokea kifo cha uzazi.

 

6.2.2  Mheshimiwa Spika, napenda kuwaarifu wananchi kuwa baada ya kupata madaktari wazelendo pamoja na wataalamu wa kutoa dawa za usingizi kuanzia mwezi wa Februari mwaka huu huduma za kujifungua kwa njia ya upasuaji zinaendelea vizuri katika hospitali hii.

 

6.3    Hospitali ya Kidongo Chekundu


 

6.3.1  Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Kidongo Chekundu ni hospitali pekee ya rufaa kwa wagonjwa wa akili. Kwa kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014, jumla ya wagonjwa waliolazwa ni 995 (651 wanaume na 344 wanawake), hili ni ongezeko la wagojwa 479 ukilinganisha na mwaka uliopita. Aidha, hospitali hii hutoa huduma za msingi ambapo jumla ya wagonjwa wa nje 10,831 walipatiwa matibabu (5,240 wanaume na 5,591 wanawake). Mgonjwa mmoja wa kike alifariki dunia.

 

6.3.2  Mheshimiwa Spika, kupitia mpango wa ubadilishanaji wafanyakazi kati ya Idara ya Hospitali ya Mnazi Mmoja na Hospitali ya Chuo Kikuu cha Haukeland, wafanyakazi wawili wa Hospitali ya Kidongo Chekundu wamepelekwa Norway kupata uzoefu wa namna ya utoaji wa huduma hizo na muuguzi mmoja kutoka Norway yupo Hospitali ya Kidongo Chekundu. Muuguzi huyo anatoa mafunzo kwa wafanyakazi wa hospitali hii na vijana walioamua kuacha dawa za kulevya waliokuwemo katika nyumba zinazotoa huduma za matibabu hayo (Sober House).

 

6.3.3  Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya wizara ya mwaka 2013/14 nilieleza kuwa wizara iliazimia kuimarisha huduma za mikoba kwa wagonjwa wa akili. Napenda kuliarifu Baraza hili kuwa madakatari kutoka hospitali hii hufanya matibabu ya huduma za mikoba katika hospitali za Wete Pemba mara moja kwa mwezi na hospitali ya Makunduchi mara moja kwa kila wiki. Utaratibu huu umesaidia kwa kiasi kikubwa kuweza kuwafikia na kuwapatia huduma mapema watu wenye matatizo ya akili.

 

6.3.4  Mheshimiwa Spika, Wizara imeshatengeneza ramani ya jengo la kutolea huduma za matibabu kwa vijana walioathirika na madawa ya kulevya (Detoxification centre). Kwa sasa hatua inayofuata ni kuitisha zabuni ya ujenzi wa jengo hilo litakalogharamiwa na Hospitali ya Chuo Kikuu cha Huakeland.

 

6.3.5  Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/15, Idara inategemea kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendelea kufanya marekebisho ya rasimu ya sheria ya kuifanya Hospitali ya Mnazi Mmoja kuwa ni taasisi yenye kujitegemea.

2.    Kujenga jengo la kutolea huduma kwa waathirika wa madawa ya kulevya (detoxification centre) katika hospitali ya Kidongo Chekundu.

3.    Kufanya ukarabati wa wodi ya wanawake na wanaume.

4.    Kujenga jengo la wagonjwa mahututi (ICU).

 

7.0    OFISI YA MFAMASIA MKUU WA SERIKALI


7.1     Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Mfamasia Mkuu wa Serikali ina jukumu la kusimamia utekelezaji wa Sera ya Dawa (National Medicine Policy), ikiwa ni pamoja na kuhakikisha upatikanaji na utumiaji sahihi wa dawa (Rational Use of Medicine).

7.2     Mheshimiwa Spika, kuwepo kwa dawa muhimu na vifaa tiba ni moja kati ya nyenzo muhimu katika kuimarisha afya ya mwananchi. Kwa mwaka wa fedha 2013/14 wizara iliendelea kununua dawa na vifaa tiba kwa kutumia fedha kutoka serikalini na washirika wa maendeleo. Kwa upande wa Serikali kati ya Tsh. 2,166,801,000 zilizotengwa kwa mwaka 2013/14 Tsh. 1,443,804,904 (67%) zimepatikana. Pia Wizara imepokea dawa na vifaa tiba vyenye thamani ya Tsh. 4,274,778,245 kutoka kwa Washirika wa Maendeleo na misaada ya aina hiyo kutoka kwenye Taasisi mbali mbali. Kiambatisho namba 7 kinatoa ufafanuzi.

7.3     Mheshimiwa Spika, wizara inaendelea na juhudi za kuanzisha mfuko maalumu wa dawa (Essential Medicine Account) ambapo serikali na washirika wa maendeleo wataingiza fedha katika mfuko huo. Hatua za kufungua akaunti pamoja na kusaini hati ya makubaliano (Memorandum of understanding) ya mfuko huu zimeshakamilika. Aidha, hatua za ununuzi wa dawa kupitia mfuko huu zimeshaanza, ni matarajio yetu kwamba mfuko huu utasaidia kudumisha upatikanaji wa dawa muhimu na vifaa tiba kwa wananchi.

7.4     Mheshimiwa Spika, ofisi pia imeweza kukamilisha Mpango Mkakati (Strategic Plan) wa Miaka Mitano kwa kazi za uimarishaji wa huduma za dawa hapa Zanzibar. Wizara imeshaanza kuutangaza mpango huo kwa Washirika wa Maendeleo kwenye mkutano wa Washirika wa Maendeleo uliofanyika Dar-es-salaam tarehe 21/02/2014. Mashirika ya USAID, CDC, DANIDA, UNFPA, JSI na GF yameonesha nia ya kusaidia utekelezaji wa mpango huo. 

7.5     Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015 Ofisi ya Mfamasia Mkuu imejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:- 

1.    Kuendelea kununua dawa na vifaa tiba kwa kutumia mfumo wa ‘Framework Contract’

2.    Kuendelea kusimamia utumiaji sahihi wa dawa na vifaa tiba (Rational use of Medicine).

8.0    IDARA YA BOHARI KUU YA DAWA


8.1     Mheshimiwa Spika, Idara ya Bohari kuu ya Dawa ina jukumu la kupokea, kutunza, kusambaza na kufanya ukaguzi wa dawa katika hospitali na vituo vyote vya afya vinavyo milikiwa na serikali Unguja na Pemba.

8.2     Mheshimiwa Spika, katika kuimarisha huduma za usambazaji wa dawa na vifaa tiba, idara inaendelea kuuimarisha mfumo wa usambazaji kwa kulingana na mahitaji (Pull system). Aidha, Mfumo huu umeonesha mafanikio makubwa na ya kuridhisha ambapo idara imefanikiwa kuingiza vituo vyote 144 katika mfumo wa “Pull System” Unguja na Pemba kuanzia Disemba 2013, ambapo mahitaji halisi ya dawa na vifaa tiba hubainishwa na kituo cha afya kupitia timu ya afya ya wilaya husika, wakati huo huo mafunzo juu mfumo wa utunzaji na uwekaji mzuri wa dawa (mSupply), yalitolewa kwa wafanyakazi wa Bohari Kuu ya Dawa.

8.3     Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2014/2015 Idara imejipangia kutekelaza kazi zifuatazo:-

1.    Kuandaa rasimu ya sheria ya Bohari kuu ya Dawa.

2.    Kuendelea kuimarisha mifumo ya uendeshaji kwa kazi za Bohari.  Mfumo wa usambazaji wa mSupply katika kuhifadhi, kutoa na kusambaza dawa.

3.    Kuendelea kuwajengea uwezo watendaji wa Bohari kwa kuwapatia mafunzo mbalimbali ili waweze kuitumia mifumo iliyopo kwa umakini na ufanisi.

9.0    MAABARA YA MKEMIA MKUU WA SERIKALI


9.1     Mheshimiwa Spika, Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ina jukumu la kutoa huduma za kitaalamu  na za kisayansi kwa kuangalia ubora na usalama wa vyakula, madawa, udhibiti wa kemikali na kufanya uchunguzi wa vielelezo vinavyowasilishwa kutoka taasisi tofauti vikiwemo vile vinavyohusiana na makosa ya jinai.

9.2     Mheshimiwa Spika, maabara imeendelea na kazi zake za kufanya uchunguzi ambapo jumla ya vielelezo 489 vilichunguzwa kati ya Julai 2013 hadi Machi 2014. Vielelezo hivi vinatoka Jeshi la Polisi, Vikosi vya SMZ na watu binafsi kama inavyoonekana katika kiambatisho namba 8.

9.3     Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha uliopita maabara imetayarisha sheria ya kemikali na hivi sasa rasimu (draft) ya kwanza ya sheria hii imepelekwa kwa Mkurugenzi wa Mashtaka kwa ushauri zaidi wa kitaalamu wa kisheria.

9.4     Mheshimiwa Spika, shughuli nyengine zilizofanyika katika kipindi kilichopita ni pamoja na kufanya ziara ya kimasomo huko Tanzania Bara katika Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali ili kuweza kujifunza kwa vitendo shughuli zinavyofanyika katika maabara hiyo.  Aidha, Mpango Mkakati wa miaka mitano (2013 – 2018) umetayarishwa na hivi sasa upo katika hatua za mwisho kukamilika.

9.5     Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/15 maabara imejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.     Kuendelea kufanya uchunguzi wa sampuli mbali mbali zitakazowasilishwa katika maabara

2.    Kukamilisha rasimu ya sheria ya kemikali pamoja na kanuni zake.

3.    Kuendelea na ukarabati wa jengo la Mkemia Mkuu wa Serikali.

10.0  IDARA YA SERA, MIPANGO NA UTAFITI


10.1   Mheshimiwa Spika, Idara hii ina jukumu la kutayarisha sera, miongozo, na mipango mikuu ya wizara pamoja na kusimamia utekelezaji wake.  Aidha, Idara inaratibu tafiti zote za afya na kusimamamia ukusanyaji, uchambuzi na usambazaji wa taarifa za afya.

10.2   Mheshimiwa Spika, Idara inaendelea kuufanyia gharama Mpango Mkakati wa Tatu wa Sekta ya Afya (2013/14 – 2018/19), kazi hii inafanyika kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) kwa kutumia programu maalum ya Computer (One Health Costing Tool). Program hii itasaidia kujua gharama halisi za utekelezaji wa mpango huu kwa kipindi cha miaka mitano ijayo na kutoa matokeo ya muda mrefu hadi mpango huu utakapomaliza kipindi cha utekelezaji wake. Kazi inayoendelea hivi sasa ni ukusanyaji wa taarifa na kuziingiza katika program hiyo.

10.3   Mheshimiwa Spika, kwa mara ya kwanza wizara imefanya utafiti wa kujua matumizi ya huduma za afya (National Health Accounts) kutoka serikalini, washirika wa maendeleo, jumuia zisizo za serikali, waajiri na watu binafsi kwa mwaka 2011/12 na mwaka 2012/13. Matokeo ya utafiti huo yameonesha kwamba bado matumizi ya fedha kwa ajili ya huduma za afya kwa mtu mmoja ni kidogo ($27 per capita) ukilinganisha na kiwango kilichowekwa na Shirika la Afya Ulimwenguni ($60).

10.4   Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho asilimia 32 ya fedha za uendeshaji wa huduma za afya zimetoka kwa washirika wa maendeleo, asillimia 37.9 zilitoka serikalini na asilimia 25.8 zilitoka kwa wananchi. Matokeo mengine ya utafiti huu yanaonesha kuwa kwa kulinganisha matumizi yote ya serikali, sekta ya afya imepata asilimia 6.9 tu, kima ambacho ni kidogo ukilinganisha na Azimio la Abuja la kuwa sekta ya afya ipatiwe asilimia 15 ya matumizi yote ya serikali. Hali hii inadhihirisha kuwa kuna haja ya kutafuta njia mbadala za kugharamia huduma za afya ikiwemo serikali kuongeza mgao wake kwa sekta ya afya.

10.5   Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, moja ya lengo kubwa kati ya malengo ya makuu ya wizara ni suala zima la kuangalia njia mbadala za kugharamia huduma za afya. Lengo hili limekuwa likitekelezwa na kusimamiwa na Idara ya Sera, Mipango na Utafiti.  Hatua zilizofikwa hadi sasa ni kuanza kuzifanyia kazi njia kuu mbili endelevu za upatikanaji wa fedha ambazo ni bima ya afya na kuazisha kodi maalum kwa wasafiri wa kimataifa kupitia tiketi za ndege (International Arrivals Levy) kwa ajili ya huduma za malaria na afya ya uzazi.

 

10.6  Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa bima afya ripoti ya awali ya mapendekezo (Zero Draft) imewaslishwa kwa kamati ya wataalamu na kujadiliwa. Mapendekezo hayo yatapimwa kwa kutumia takwimu za idadi ya watu na za kiuchumi (Acturial study) ili kuangaliwa uwezo wa wananchi kuchangia mfuko wa bima pamoja na uendeshaji wake. Aidha mapendekezo ya kodi kwenye tiketi za ndege kwa ajili ya kugharamia huduma za kumaliza malaria nchini pamoja na huduma za afya ya uzazi yamewasilishwa kwa Makatibu wa wakuu kwa njia ya semina na wametoa maoni yao ikiwemo kuangalia zaidi vyanzo vya fedha vya ndani. 

10.7   Mheshimiwa Spika, katika kuinua viwango vya huduma za afya zinazotolewa, wizara imeanza kutekeleza rasmi mfumo wa kuwazawadia wafanyakazi ‘Performance Based Financing’ kwa vituo vya afya, kwa kuanzia na wilaya ya Mkoani kwa Pemba na Magharibi kwa Unguja kwa majaribio. Mfumo huu pia una shabaha ya kuwafanya wafanyakazi wavutiwe na kazi wanayoifanya na waweze kubakia kazini badala ya kutafuta kazi nje ya wizara hii. Hivyo viashiria maalumu huangaliwa kabla ya kuwazawadia wafanyakazi.

10.8   Mheshimiwa Spika, matokeo ya awali kwa kipindi cha miezi sita (Julai 2013 – Disemba 2013), yameonesha kuongezeka kwa utumiaji sahihi wa miongozo ya matibabu, kuongezeka kwa wateja wa huduma za uzazi wa mpango, kuongezeka ufuatiliaji wa watoto waliokosa chanjo mbali mbali majumbani, huduma baada ya kujifungua na huduma nyengine za mama na mtoto, kuwepo kwa mazingira salama (IPC) na pia kuengezeka kwa kiwango cha idadi ya watoto wa kike kupatiwa chanjo ili kujikinga dhidi ya pepopunda. 

10.9   Mheshimiwa Spika, katika kuendelea na ukusanyaji, uchambuzi na uwasilishaji wa taarifa za afya, Idara ilifanya ukaguzi elekezi wa usahihi wa taarifa za afya (DQA). Aidha, katika kupunguza vifo vya kinamama na watoto ili kufikia malengo ya MKUZA, wizara imeanzisha programu maalum ya kompyuta ili kuwezesha kufuatilia kwa urahisi taarifa za afya za mama kuanzia anapobeba ujauzito hadi kujifungua kwake na mtoto kuanzia anapozaliwa hadi kufikia umri wa miaka miwili. Kwa kuanzia programu hii iinatekelezwa kwa majaribio katika hospitali ya Chake Chake.

10.10 Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha kwamba maradhi yaliyoongoza katika hospitali na vituo vya afya kwa mwaka 2013 ni maradhi ya njia ya hewa (18.5%) maradhi mengineyo ya ngozi (4.7%),  maradhi mengine ya kuharisha yasiyokuwa kuharisha damu na kipindupindu (4.4%) masikio pua na koo (4.08%) maradhi ya nimonia (3.2%), maradhi ya maambukizo ya njia ya mkojo (2.3%), majeraha (2.2%), minyoo (1.7%), maradhi ya macho (1.5%), maradhi ya kinywa (1.5%) na magonjwa yote yaliyobaki (55.4%).

10.11 Mheshimiwa Spika, shughuli za tafiti zinazohusu afya  zimeendelea kuratibiwa katika wizara kwa kufanya  tafiti mbali mbali ukiwemo utafiti wa mahitaji na matumizi ya damu  ambao umehusisha Hospital za Unguja na Pemba ili kujua usahihi wa mahitaji ya damu katika hospital zetu, Aidha jumla ya tafiti tisa zimepokelewa na kupitiwa ambazo kati ya hizo tafiti sita zimeruhusiwa kuendelea na tafiti tatu zinaendelea kupata maelekezo zaidi  ili ziendane na maadili ya tafiti za afya.

10.12 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015, Idara ya Sera, Mipango na Utafiti imejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendelea kutafuta njia mbadala za kugharamia huduma za afya;

2.    Kutayarisha Mfumo wa Ufuatiliaji na Tathmini wa Wizara;

3.    Kuendelea na ukusanyaji, uchambuzi na uwasilishaji wa taarifa za afya;

4.    Kushajiisha ufanyaji wa tafiti mbali mbali za kiafya (Clinical Research) ili kuibua mambo zaidi ya kitaaluma yanayohusiana na magonjwa

5.    Kufanya tathmini ya utekelezaji wa mfumo wa kuzawadia wafanyakazi kwa wilaya mbili za majaribio ( Mkoani na Magharibi)

6.    Kutayarisha  na kupitia miongozo mbali mbali kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za afya;

11.0  IDARA YA UENDESHAJI NA UTUMISHI


11.0.1 Mheshimiwa Spika, Idara ya Uendeshaji na Utumishi ina majukumu ya kusimamia uwajibijikaji kazini, maslahi, haki, nidhamu na stahiki na kujenga uwezo wa nguvu kazi ya afya.  Aidha, idara hii husimamia masuala ya usafiri utunzaji wa kumbukumbu pamoja na miundombinu yote iliyomo ndani ya wizara.

11.1  Nguvukazi ya Sekta ya Afya


11.1.1 Mheshimiwa Spika, katika hotuba ya wizara ya mwaka 2013/2014 wizara iliahidi kuwaombea wafanyakazi kulipwa posho la kufanyakazi katika mazingira hatarishi (Risk allowance). Napenda kulijulisha baraza lako kuwa baada ya makubaliano na sekta husika posho hilo limeshaanza kulipwa kwa wafanyakazi wa hospitali na Vituo vya Afya.    

11.1.2 Mheshimiwa Spika, katika mwaka 2013/2014 jumla ya wafanyakazi 142 wa kada mbali mbali wamepelekwa masomoni ndani na nje ya nchi. Hivyo kufanya idadi ya wafanyakazi wote wanaoendelea na masomo kufikia 246 (wanaume 110 na wanawake 136.  Aidha, jumla ya wafanyakazi 44 wamerudi masomoni na kupangiwa kazi kwa mujibu wa taaluma zao. Kiambatisho namba 9 kinatoa ufafanuzi. Sambamba na hilo Wizara imeajiri wafanyakazi 840 wa kada tofauti, jumla ya  wafanyakazi 83 (Unguja 57 na Pemba 26) wamestaafishwa kwa mujibu wa sheria na wafanyakazi tisa (5 Unguja na 4 Pemba) wamefariki dunia.

11.2  Utawala na Uendeshaji


11.2.1 Mheshimiwa Spika,katika kuimarisha miundombinu ya wizara vituo vya afya 20 vinaendelea na matengenezo chini ya ufadhili wa Shirika la Danida.  Vituo hivyo ni pamoja na kituo cha Afya Mtangani ambacho kinajengwa upya, kituo hiki kimefikia katika hatua ya kuezekwa. Vituo vyengine vinafanyiwa upanuzi kwa kujengwa chumba cha kuzalia “matenity ward” vituo hivyo ni Selem,Chumbuni, Fundo, Sebleni na Muyuni.  Ujenzi katika vituo hivyo upo katika hatua tofauti.

11.2.2 Mheshimiwa Spika, matengenezo mengine yaliyofanyika ni katika  kituo cha Wesha, Ukutini, Makangale na Kombeni. Pia Kituo cha Nungwi, Kiombamvua, Bumbwini Misufini na Chwaka tayari vimeshamalizika.  Vituo vya Afya viwili vinavyofadhiliwa na ufadhili wa ADB ambavyo ni Mzambarauni kwa upande wa Pemba na Mwera kwa upande wa Unguja  vipo katika hatua ya mwisho za kumalizika.  Vile vile vituo vya  Afya 21 vinatarajiwa kutengenezwa na Mradi wa Orio ingawa bado ujenzi haujaanza lakini wakandarasi wameshaanza hatua za kupima.

11.2.3 Mheshimiwa Spika, wizara imefanikiwa kuanzisha mfumo wa ufuatiliaji          wa miundo mbinu ya wizara ikiwemo majengo, usafiri pamoja na vifaa. Katika kulisimamia hili mfumo maalum wa uwekaji kumbu kumbu wa vyombo vyote vya moto umetayarishwa. Mfumo huu una lengo la kuweza kufuatilia kazi zote ambazo zitatumia vyombo vya usafiri ili kuweza kujua gari hizo zimepangiwa kazi gani. Zoezi hili tayari limeshaanza ambapo jumla ya gari 80 kati ya 134 zimeshaingizwa kwenye mfumo huo.

11.2.4 Mheshimiwa Spika, Idara imeweza kupitisha zabuni mbali mbali za ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya, nyumba za wafanyakazi, pamoja na ununuzi wa vifaa mbalimbali vya hospitali kama vile “Mobile X-Ray” na Mashine ya kuchomea taka “Incenerator” kwa ajili ya hospitali ya  Mnazi Mmoja pamoja na kusimamia zabuni ya ununuzi wa gari tatu, gari mbili kwa ajili ya  kitengo shirikishi cha Ukimwi, Kifua Kikuu na Ukoma, na gari moja ya  Ofisi ya Mfamasia Mkuu. Zabuni nyengine zilizopitishwa ni pamoja na  zabuni ya upanuzi wa wodi ya wanawake na wanaume Micheweni Pemba na zabuni ya ujenzi wa jengo la upasuaji wa uti wa mgongo (Neurosurgery) ya hospitali ya Mnazi Mmoja.

11.2.5 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Idara imejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kukamilisha mpango utakaosaidia kuwahamasisha wafanyakazi kubaki kazini (Retension Strategy)

2.    Kuendeleza kuwapa mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi wafanyakazi wa afya

3.    Kutayarisha sera ya usafiri ya wizara.

 

12.0  TAASISI MAALUM


12.1  Chuo cha Taaluma za Sayansi za Afya - Zanzibar


12.1.1 Mheshimiwa Spika, Chuo kinaendelea kutoa taaluma za afya kwa kiwango cha stashahada katika fani mbali mbali. Kwa sasa chuo kina jumla ya wanafunzi 821 wakiwemo wauguzi (204), wasaidizi madaktari (198), Maafisa afya ya mazingira (136), Ufundi sanifu wa maabara (122), Wasaidizi madaktari wa afya ya kinywa na meno (21), Wafamasia (127), na Ufundi sanifu wa vifaa tiba “Biomedical Engineers” (13). Ili kuweka mazingira mazuri kiutendaji na hatimae kuongezeka kwa motisha kwa wafanyakazi wa Chuo, Muundo wa Utumishi kwa wafanyakazi wa Chuo umetayarishwa na tayari umeshawasilishwa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Kazi na Utumishi wa Umma kwa utekelezaji.

12.1.2 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014 chuo kinatarajia kutoa wahitimu 281 wakiwemo; wauguzi 67, Maafisa tabibu 51, Maafisa Afya Mazingira 49, Mafundi dawa 48, Madaktari wasaidizi wa afya ya kinywa na meno 13, mafundi sanifu wa maabara 40 na mafundi sanifu wa vifaa tiba 13. Wahitimu hawa pindipo wakiajiriwa watasaidia sana katika kutatua tatizo la uhaba wa nguvu kazi ya afya katika maeneo tofauti visiwani.

12.1.3 Mheshimiwa Spika, chuo kimeanzisha masomo ya kujiendeleza kwa wafanyakazi wenye cheti kwa muda mrefu na hawakupata bahati ya kujiendeleza kielimu katika fani zao. Hivyo kwa mwaka wa masomo 2013/14, jumla ya wanafunzi 183 wanaendelea na mafunzo chuoni hapo na pia wanafunzi 11 wanaendelea na mafunzo ya elimu masafa kupitia AMREF.

12.1.4 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Chuo kimejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendelea kutoa mafunzo ya sayansi za afya na utabibu ambayo inakidhi mahitaji na viwango vya kitaaluma  kitaifa  na kimataifa.

2.    Kuanzisha Stashahada ya Physiotherapy na Shahada ya Uuguzi kwa mwaka wa masomo 2014/2015

3.    Kuandaa Mpango  wa Chuo wa kujiendesha (Bussiness Plan)

 

12.2  Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi


12.2.1 Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2013/2014, Bodi ilisajili jumla ya maduka 284 ya Chakula ya jumla na rejareja, Ghala 25 za Chakula, Bekari 18, Hoteli 64, Mikahawa 45, viwanda vya chakula tisa,supermarket” tisa, maduka ya kuuzia nyama 81, vyumba vya baridi tisa, bidhaa za vyakula 10, maduka ya dawa 106, maduka ya vipodozi 31, duka moja la vifaa tiba, ghala mbili za dawa, dawa 12 na virutubisho saba.

12.2.2 Mheshimiwa Spika, Bodi ilikagua maduka 537 kutoka maduka 637 ya chakula ya jumla na rejareja ambayo yalikaguliwa mwaka uliopita, ghala 18 za chakula, hoteli 56, mikahawa 39, viwanda vya chakula tisa,supermarket” tisa, maduka ya kuuzia nyama 100, vyumba vya baridi tisa, machinjio tisa, tani 247.72 za chumvi yenye madini joto, lita 1,488,073 za maziwa, tani 33.64 za bidhaa na mazao ya baharini, maduka ya dawa 132, ghala mbili za dawa, maduka ya vipodozi 35 na duka moja la vifaa tiba.

 

12.2.3 Mheshimiwa Spika, maabara ya bodi hii ilipokea na kuchunguza sampuli 824 za chakula, sampuli 812 zilikua salama na sampuli 12 hazikufaa kwa matumizi ya binadamu. Aidha, sampuli 15 za dawa zilichunguzwa na zote ziligundulika kuwa zinafaa kwa matumizi. Sampuli 16 za vipodozi zilichunguzwa na hazikuonekana kuwa na madhara yoyote. Pia sampuli 10 za dawa za mitishamba zilichunguzwa ambazo zote zilionekana zinafaa kwa matumizi ya binadamu.

 

12.2.4 Mheshimiwa Spika, jumla ya tani 40 za bidhaa za chakula na tani mbili za bidhaa za dawa na vipodozi zisizofaa kwa matumizi ya binaadamu ambazo zilikamatwa kwenye maduka na bandari ndogo ndogo ziliteketezwa. Aidha, jumla ya tani 573.8 za bidhaa za chakula zisizofaa kwa matumizi ya binaadamu zilirejeshwa zilikotoka. 

12.2.5Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 bodi imejipangia kazi kuu zifuatazo:-

1.     Kusimamia marekebisho ya sheria ili kuifanya Bodi kuwa na Mamlaka kamili.

2.     Kumalizia ujenzi wa ofisi mpya za Bodi katika eneo la Mombasa, Zanzibar.

12.3  Bodi ya Ushauri wa Hospitali Binafsi


12.3.1 Mheshimiwa Spika, Bodi ya Hospitali Binafsi ina jukumu la kusimamia mwenendo wa hospitali binafsi kwa mujibu wa sheria za kuendesha hospitali hizo (Private Hospital Regulation) Act No. 04 of 1994, Kazi kubwa ya bodi hii ni kusajili, kutoa leseni kwa hospitali zinazokidhi viwango, kukagua, kusimamia uanzishaji na uendeshaji wa hospitali na vituo binafsi vya afya pamoja na kuzifungia zisizofikia viwango.

12.3.2 Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2013/2014, bodi ilifanya ukaguzi wa hospitali nne na vituo vya afya 67, katika ukaguzi huo vituo 10 vilisimamishwa kutoa huduma na vituo vitano kupewa onyo kali kutokana na kwenda kinyume na sheria na miongozo ya uendeshaji wa hospitali binafsi. Aidha, jumla ya vituo vipya viwili vimesajiliwa navyo ni Lancent Laboratory na F&M Rehabilitation Clinic, hadi sasa kuna jumla ya vituo vya afya binafsi 71 (60 Unguja na 11 Pemba).

12.3.3 Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2014/2015 bodi imejipangia  kufanya kazi zifuatazo:-

1.    Kupitia sheria ya kuendesha Hospitali binafsi.

2.    Kufanya ukaguzi wa pamoja na wakaguzi kutoka Kamisheni ya utalii kwa Hospitali zilizomo ndani ya Mahoteli ya Kitalii.

        

12.4  Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala


12.4.1 Mheshimiwa Spika, Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala (Traditional and Alternative Medicine Council) ni baraza liliopo chini ya sheria No.8 ya mwaka 2008, baraza hili  linafanyakazi  zake kisheria katika kusimamia shughuli zote za tiba asili, kutoa usajili, kudhibiti, kutangaza, kuelimisha jamii na kusaidia katika maendeleao ya shughuli za tiba asili na tiba mbadala, pamoja na kuelimisha jamii kwa kutumia vyombo vya habari kama TV, redio, mikutano ya waganga kupitia kwa masheha na madiwani au wakuu wa wilaya na pia kutumia vipeperushi.

12.4.2 Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha 2013/2014 baraza la tiba asili liliweza kuongeza idadi ya waganga waliosajiliwa na kufikia 193 Unguja na Pemba kwa kuweza kutimiza masharti ikiwa ni pamoja na kuwa na sehemu maalum ya kutoa huduma kwa wagonjwa. Aidha, jumla ya maduka ya dawa za asili 31 yalisajiliwa kwa kutimiza masharti ya sheria za baraza, Kliniki za tiba asili na tiba mbadala ni 11, (Unguja 9 na Pemba 2), wasaidizi waganga 58, na vilinge 112, na sampuli za dawa asili zilizochunguzwa na Maabara ya Bodi ya Chakula, Dawa na Vipodozi ni 23 na zote zilionekana zinafaa kwa matumizi ya binaadamu.

12.4.3 Mheshimiwa Spika, Baraza limefanya utafiti mdogo juu ya tiba asili na tiba mbadala ambapo imegunduwa kwamba mahusiano ni madogo yaliyopo baina ya waganga wa asili na waganga wa kisasa. Katika utafiti huo imeonekana kutokuweko kwa mashirikiano baina yao katika kutoa huduma za matibabu, kitu ambacho kinapelekea hata mgonjwa anapoanza kufuata matibabu kwa mganga wa asili inakuwa ngumu kumpa rufaa kwenda kwa mganga wa kitaalam. 

12.4.4 Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2014/15 Baraza la Tiba Asili limedhamiria kufanya kazi kuu zifuatazo:

1.    Kuendelea kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa tiba asili na utumiaji mzuri na unaofaa wa dawa za miti shamba kwa kutumia vyombo vya habari kama TV, Redio na pia kutumia vipeperushi.

2.    Kuhamasisha usajili na kushajihisha hasa kwa waganga.

3.    Kuendelea na ukaguzi wa mara kwa mara katika sehemu wanazofanyia kazi  waganga(vilinge) na wanazouza dawa hasa misikitini na barabarani,na  kufanya ukaguzi wa kliniki za tiba mbadala na maduka ya dawa asili .

12.5 Baraza la Wauguzi na Wakunga


12.5.1 Mheshimiwa Spika, Baraza la wauguzi na wakunga limefanya ukaguzi katika vyuo binafsi na vya Serikali vinavyotoa mafunzo ya uuguzi ili kuhakikisha kiwango kinachotolewa kama kinakidhi mahitaji ya taaluma na kutoa ushauri. Ukaguzi huo uliangalia mitaala ya kufundishia kama inafuatwa ipasavyo, kuangalia utaratibu wa kujiunga na chuo kama unafuatwa kwa mujibu wa miongozo, uendeshaji na usimamizi wa mitihani ya mwisho ya kila daraja. Vyuo vilivyokaguliwa ni pamoja na Chuo Kikuu cha Zanzibar (Zanzibar University) na Zanzibar School of Health. Mambo yaliyobainika katika ukaguzi huo yalionekana mapungufu mbali mbali yakiwemo ya kimitaala na ukosefu wa walimu wa kudumu.

12.5.2 Mheshimiwa Spika, Baraza limeweza kuandaa mkutano wa pamoja wa kutayarisha “Scope of Midwifery Practice” kwa kushirikiana na shirika la UNFPA na Jhipiego. Lengo la kikao hicho ni kuwa na muongozo wa wauguzi ambaoutapelekea kutambua mipaka na majukumu katika utoaji wa huduma za uuguzi. Aidha, Baraza limeweza kukisimamia kwa kutoa maelekezo ya kitaalamu kwa Chuo cha Zanzibar School of Health katika kujiunga na mamlaka ya elimu ya juu Tanzania National Commission for Technical Education (NACTE). 

12.5.3 Mheshimiwa Spika, Baraza limeipitia upya sheria ya Uuguzi na kuifanyia marekebisho na hivi sasa inasubiri kupelekwa Baraza la Mapinduzi kwa mara ya pili. Aidha, Baraza limeendeleza ushirikiano na mabaraza ya Wauguzi ya Afrika Mashariki na Kati kwa kuhudhuria mikutano na kutekeleza maamuzi ya mikutano hiyo.

12.5.4 Mheshimiwa Spika, katika kuadhimisha siku ya wauguzi duniani Baraza lilifanya uchunguzi wa awali wa saratani ya shingo ya kizazi (Cervix Carcinoma) kwa kinamama, Jumla ya kinamama 350 wamefanyiwa uchunguzi kati yao 14 wamegundulika na matatizo hayo na kupewa huduma zinazostahiki.

12.5.5 Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2014/2015 Baraza limejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kukamilisha mapitio ya sheria ya Baraza la Wauguzi na Wakunga

2.    Kufanya ukaguzi katika hospitali Unguja na Pemba

3.    Kutayarisha “Nursing Procedure Manual”

4.    Kuendelea kusimamia maadili na haki za uuguzi.

12.6  Maabara ya Afya ya Jamii -Pemba


 

12.6.1Mheshimiwa Spika, Maabara ya Afya ya Jamii (PHL) imeanzishwa kwa lengo la kuiwezesha sekta ya afya kuwa na chombo cha kufanya tafiti za afya, kuangalia nyendo za maradhi mbali mbali na kutafuta mbinu za  kuyadhibiti.

12.6.2Mheshimiwa Spika, kwa mashirikiano na Chuo Kikuu cha John Hopkins maabara inaendelea kutekeleza mradi wa miaka mitatu wa “Chlorehexdine Study” kwa lengo la kupunguza vifo vya watoto wachanga walio katika umri wa siku 28 tokea kuzaliwa (reduction of neonatal deaths). Katika kutekeleza hili watoto wote wanaozaliwa katika kipindi hiki wanapatiwa huduma za vitovu (cord care). Katika kipindi cha Julai, 2013 hadi Machi 2014 jumla ya watoto 9,973 (wanaume 4,968; wanawake 5,005) wamepatiwa huduma hizo.

12.6.3Mheshimiwa Spika, katika kufanya uchunguzi wa kupandikiza makohozi kwa ajili ya kuona vimelea vya TB (sputum Culture), maabara imepandikiza sampuli 574 za  makohozi

kati ya hizo sampuli43  ziligundulika kuwa na vimelea vya TB na sampuli 531 zilionekana kuwa hazina vimelea vya TB.

12.6.4Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/15 maabara itaanza kutekeleza mradi wa kutokomeza Kichocho katika shehia za Mtangani, Wingwi na Kiuyu Minungwini.

 

13.0 MIRADI YA MAENDELEO


13.1  Mradi Shirikishi wa Ukimwi, Kifua Kikuu na Ukoma.


13.1.1Mheshimiwa Spika, mradi huu una lengo la kupambana na maradhi ya UKIMWI, Kifua Kikuu na Ukoma ili kuwakinga wananchi wote wa Zanzibar kutokana na maradhi haya. Mradi huu unahusisha utoaji wa huduma mbali mbali zikiwemo za ushauri nasaha na uchunguzi, huduma za tiba pamoja na huduma za wagojwa majumbani.

13.1.2Mheshimiwa Spika, jumla ya vituo 91 vinatoa huduma ya ushauri nasaha na upimaji wa VVU ukilinganisha na vituo 87 mwaka 2012 kati ya hivyo Unguja 58 na Pemba 33. Katika vituo hivyo jumla ya watu 61,921 walichunguzwa (wanawake 32,477 na wanaume 29,444).  Katika uchunguzi huo jumla ya watu 966 (1.56%) waligundulika kuwa wanaishi na Virusi vya Ukimwi (VVU); wanawake ni 520  (54%) na wanaume  446 (46%).

13.1.3 Mheshimiwa Spika, katika utoaji wa huduma za tiba, hadi kufikia mwishoni wa mwezi wa Machi 2014, jumla ya wagonjwa 6,982 walikuwa tayari wameshasajiliwa kwenye kliniki za tiba, miongoni mwao wagonjwa 4,494 (64% - lengo lilikuwa ni kufikia asilimia 65%) wanatumia dawa za ARVs, kati yao watoto ni 397 (9%) Hili ni ongezeko la asilimia sita ukilinganisha na mwaka 2012. Pia, kitengo kimeanzisha kliniki ya tiba kwa wanaoishi na VVU kwenye Taasisi isiyo ya Serikali (NGO) ya ZAYEDESA. Hii inafanya jumla ya kliniki hizo kufikia 11 (7 Unguja na 4 Pemba) ukilinganisha na mwaka 2012 ambapo kulikuwa na kliniki 10.

13.1.4Mheshimiwa Spika, katika mapambano dhidi ya maradhi ya Ukoma elimu ya afya ilitolewa kwa wananchi. Jumla ya vijiji 24 vya Unguja na Pemba vilifanyiwa mikutano na kupatiwa elimu ya Ukoma, jumla ya watu 1,280 (Unguja 805, Pemba 475 walihudhuria mikutano hiyo, kati yao watu 31 walishukiwa kuwa na dalili za Ukoma na watu saba waligundulika na Ukoma. Kupitia juhudi za waratibu wa Kifua Kikuu na Ukoma vituo vitatu vya kutoa huduma za kujitunza ili wasiweze kupata ulevamu zaidi vimeanzishwa. Madhumuni ni kuwafundisha wagonjwa namna ya kujitunza na kujilinda na ulemavu na baadae waweze kujihudumia katika vikundi vyao.

13.1.5Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/2015, mradi utatekeleza kazi kuu zifuatazo:-

  1. Kuongeza na kupanua huduma za ushauri nasaha na upimaji kutoka vituo 91 2013/14 hadi kufikia 100. 
  2. Kufanya tathmini ya VVU na maradhi mengine ya kujamiiana katika makundi mbali mbali yakiwemo kundi la mama wajawazito na  wavuvi ili kuweza kufuatilia mwenendo wa maradhi hayo.
  3. Kuanzisha huduma za ushauri nasaha na upimaji VVU majumbani (HBHTC) katika Wilaya ya Kati kwa kufikia nyumba 1,846 za Shehia saba zilizomo katika wilaya ya kati.

13.2  Mradi wa Kumaliza Malaria Zanzibar


13.2.1Mheshimiwa Spika, katika jitihada za kumaliza Malaria visiwani Zanzibar, mradi huu ulipanga kupiga dawa jumla ya nyumba 51,546 katika wilaya zote isipokua wilaya ya Mjini, Kati ya nyumba hizo nyumba 50,869 (98.6%) zimefanikiwa kupigwa dawa. Upigaji huu wa dawa ulihusisha maeneo maalumu yaliobainika kuwepo kwa wagonjwa wengi wa Malaria.

13.2.2Mheshimiwa Spika, unyunyizaji dawa kwenye madimbwi ya maji yenye viluilui vya mbu pia umefanyika. Kwa Unguja maeneo yaliyohusishwa ni Kaburi kikombe, Kwa Binti Amrani, Sebleni, Mnazi Mmoja, Karakana,  Kilimani, Mbuyuni, Kijitoupele, Kwa Mtumwajeni  na Chumbuni.  Kwa upande wa Pemba kazi hii imefanyika katika maeneo ya Chimba, Tumbe, Minungwini, Chwale, Uwandani na Gando.

13.2.3Mheshimiwa Spika, kwa vile  kila homa si malaria kuna umuhimu mkubwa wa kuchunguza damu kwanza ili kuhakikisha iwapo ina vimalea vya malaria au la kabla ya kuanza kutumia dawa.  Katika kipindi cha Julai 2013 hadi Machi 2014 jumla ya watu 346,626 walichunguzwa damu,  watoto chini ya  miaka mitano walikuwa 108,074. Kati ya waliochunguzwa, waliobainika kuwa na vimelea vya malaria ni 2,680 (0.8%), kati ya hao watoto chini ya umri wa miaka mitano walikuwa 406 (0.4%). Asilimia 33 ya kinamama wajawazito waliohudhuria kliniki (76,584), walichunguzwa damu. Kati yao akinamama 77 (0.1%) waligundulika kuwa na malaria na kupewa tiba sahihi juu ya kinga dhidi ya malaria.

13.2.4Mheshimiwa Spika, kazi ya kuwafuatilia wagonjwa majumbani na kuchunguza familia zao iliendelea kufanyika. Wagonjwa 771 (76%) pamoja na familia zao (3,053) waliweza kufuatiliwa hadi majumbani kwao. Kati ya 3,053, wanakaya 245 (8%) waligunduliwa kuwa na vimelea vya malaria bila ya kuwa na dalili wala ishara ya kuumwa.

13.2.5Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 mradi unalenga kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuupitia na kuufanyia marekebisho muongozo wa uchunguzi na tiba ya malaria hapa Zanzibar kuendana na hali halisi ya malaria hapa visiwani.

2.    Kutengeneza mwongozo wa Uchunguzi wa malaria  kwa kinamama wajawazito baada ya kusimamisha tiba ya tahadhari kwa wajawazito.

3.    Kuendelea kupiga dawa kwa maeneo yatakayobainika kuwa na wagonjwa wengi wa malaria.

4.    Kuendelea na kunyunyiza dawa kwenye madimbwi ya mazalio ya mbu.

5.    Kuendelea kugawa vyandarua kwa mama wajawazito, watoto walio chini ya umri wa miaka mitano na kwa familia ambazo vyandarua vyao vimeharibika.

3.3    Mradi wa Kustawisha Siha za Wazanzibari


13.3.1Mheshimiwa Spika, mradi huu una jukumu la kuhakikisha kwamba jamii ya wazanzibari inapata elimu ya kutosha jinsi ya kujikinga na maradhi mbali mbali yakiwemo ya kuambukiza na yale yasiyoambukiza.

13.3.2 Mheshimiwa Spika, elimu ya afya iliendelea kutolewa kwa wananchi kwa njia ya redio na televisheni ambapo jumla ya vipindi 80 vya aina mbali mbali vimerushwa hewani.  Miongoni mwa mada zilizozungumzwa ni pamoja na afya ya akili, maradhi ya minyoo, afya ya uzazi, maradhi ya kuharisha,  maradhi ya kichaa cha mbwa, madhara ya pombe na athari za unyanyapaa kwa wagonjwa wa UKIMWI, ugonjwa wa kisukari, shindikizo la damu na ugonjwa wa kupooza. Aidha, uoneshaji wa filamu inayohamasisha umuhimu wa kutumia choo inaendelea kuonyeshwa katika shehia 15 za wilaya sita za Unguja.

13.3.3 Mheshimiwa Spika, elimu ya afya pia iliendelea kutolewa maskulini ambapo jumla ya skuli 125 (80 kwa Unguja na 45 kwa Pemba) zilipatiwa mafunzo kuhusu kinga ya maradhi mbali mbali. Aidha, uchunguzi wa afya ya kinywa na meno kwa wanafunzi wa skuli za msingi Unguja na Pemba pia ulifanyika. Jumla ya wanafunzi 3,420 walikaguliwa kati yao 1,437 (42%) walionekana na matatizo mbali mbali ya meno hivyo kupatiwa matibabu pamoja na elimu ya afya.

13.3.4Mheshimiwa Spika, nilieleza katika hotuba zangu zilizopita kwamba Wizara ina nia ya kuanzisha redio maalumu kwa ajili ya kuelimisha jamii masuala yanayohusu afya (Afya FM Redio). Hatua iliyofikia sasa ni kupatiwa vyumba katika jengo jipya la Mradi wa Afya ya Uzazi na Mtoto lililopo Kidongo Chekundu vitakavyotumika kwa ajili ya kufanyia matangazo yake.

13.3.5Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Mkakati wa Afya ya Jamii (Community Health Strategy), mradi umetayarisha muongozo wa pamoja wa utekelezaji wa Mkakati huu na muongozo wa kufundishia kamati Kiongozi za Afya za Shehia. Kwa kuanzia Kamati Kiongozi za Afya za Shehia 30 zinatarajiwa kuundwa katika wilaya ya Mkoani na Magharibi, mkutano wa uhamasishaji wa viongozi wa wilaya umefanyika na hatua za uundaji wa kamati zinaendelea katika wilaya ya Magharibi.

13.3.5Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha  matatizo mbali mbali ya afya yaliyomo katika jamii yanaibuliwa mapema hasa katika maeneo ambayo yako mbali na vituo vya afya na ni vigumu kufikika kwa urahisi, mradi umefanya zoezi maalumu katika Shehia ya Kandwi Wilaya ya Kaskazini A. Zoezi hili limebainisha kwamba asilimia 31 ya wakuu wa kaya hawaelewi muda wa kuhudhuria kliniki kwa mama wajawazito, akina mama wengi bado wanajifungulia majumbani (76%), matumizi ya vyoo yako (51%) na matumizi ya chumvi yenye madini joto (9%) tu ya kaya zote.

13.3.6Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2014/15 mradi umejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuunda na kuzifundisha kamati kiongozi za Afya za shehia.

2.    Kuongeza kasi ya utoaji wa elimu ya afya katika jamii ili waweze kujiepusha na vihatarishi vinavyopelekea kupata magonjwa ya kuambukiza na yasiyoambukiza.

13.4  Mradi Shirikishi wa Afya ya Uzazi na Mtoto


13.4.1Mheshimiwa Spika, mradi huu una lengo la kuimarisha afya ya uzazi na mtoto pamoja na kupunguza vifo vitokanavyo na uzazi. Idadi ya vifo vya uzazi vilivyotokea katika hospitali zetu kwa mwaka 2013 ni 103 (Unguja 68, Pemba 35) ambavyo ni ongezeko la vifo 37 kwa mwaka 2012. Sababu kuu zilizochangia kutokea kwa vifo hivyo ni kutoka damu kwa wingi baada ya kujifungua (PPH), matatizo ya shindikizo la damu “hypertensive disorder”, kutoka damu kwa wingi kabla ya kujifungua, upungufu mkubwa wa damu na kupasuka kwa fuko la uzazi.

13.4.2Mheshimiwa Spika,taarifa zinaonesha kwamba, asilimia ya akina mama waliojifungulia katika vituo vya afya imeongezeka kwa asilimia 7.2 kutoka 49.4%  mwaka 2012 hadi kufikia 56.6 % ya mwaka 2013. Nachukua fursa hii kuwapongeza kinamama  na kina baba kwa kuwa na mwamko na kuuona umuhimu wa   kujifungua  katika hospitali na vituo vya afya, pia  nawaomba wazidi kuwa na moyo huu kwani inasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza vifo  vya mama na watoto kabla  na baada ya kujifungua.

13.4.3Mheshimiwa Spika, uzazi wa mpango ni moja ya mikakati inayotumika katika kuimarisha afya ya mama na mtoto, taarifa zinaonesha kwamba kina mama waliojiunga na uzazi wa mpango  kwa njia za kisasa (new family planning acceptance) kwa Unguja imepungua kutoka 6.6% (2012) hadi 5.5% (2013) na Pemba imeonekana kuengezeka kutoka 3.1%  (2012) hadi 6.9% (2013).  Kwa Zanzibar hali inaonesha kuongezeka kutoka 5.3% (2012) hadi 5.8% (2013). Naomba kuchukuwa fursa hii kuwaomba kinababa kutoa mashirikiano katika matumizi ya huduma hizi ili kuimarisha afya ya mama na mtoto.

13.4.4Mheshimiwa Spika, hatua ya akinamama wajawazito kufika kwa wakati katika kliniki ni moja ya njia inayosaidia kutambua mapema matatizo yanayowakabili hivyo kuweza kuchukua hatua za kufaa kwa muda unaotakiwa. Kwa upande wa Pemba akinamama waliopata huduma za ujauzito kabla ya wiki 16 (ANC visits before 16 weeks) imeongezeka kutoka 14.5% mwaka 2012 kufikia   23.4% mwaka 2013. Kwa upande wa Unguja imeongezeka kutoka 20.8% mwaka 2012  hadi  22.8% mwaka 2013. Kitaifa, hali pia imeonekana kuongezeka kutoka 19.5% (2012) hadi kufikia 21.3% (2013).  Ni vyema tukajenga tabia ya kuwahimiza kinamama kufika hospitali mara tu watakapojibaini kuwa ni wajawazito ili waweze kujua maendeleo ya afya zao na watoto walio tumboni.

13.4.5Mheshimiwa Spika, jumla ya wajawazito 47,978 waliweza kuchunguzwa VVU katika kliniki na wodi za wazazi.  Kati ya hao, kina mama wajawazito 171 waligundulika kuwa na VVU na jumla ya kina mama wajawazito 158 walipewa dawa za kupunguza makali ya VVU. Vile vile watoto 114 waliozaliwa na mama wenye VVU walipewa dawa za nevirapin (NVP). Aidha, wenza/kina baba 880 waliweza kupimwa na kati yao kina baba/wenza watano waligundulika kuwa na VVU.

13.4.6Mheshimiwa Spika, kitaifa kiwango cha uchanjaji watoto chini ya mwaka mmoja kimeongezeka kutoka 81% mwaka 2012 na kufikia 84.4% mwaka 2013. Wilaya zote zimeweza kufikia asilimia  zaidi ya 80 ya uchanjaji  isipokuwa wilaya ya Magharibi Unguja  ambayo imechanja 66.7% na wilaya ya Mkoani ambayo imechanja 56%. Kiambatisho namba 10 kinafafanua.

13.4.7Mheshimiwa Spika, jumla ya wagonjwa 664 wa surua wameweza kuripotiwa ambapo Wilaya za Mjini na Magharibi zimeoneesha kuongoza kuwa na wagonjwa wengi zaidi. Asilimia 53.2 ya wagonjwa wote wa surua ni watoto chini ya umri wa miaka mitano.  Hii inaashiria kuwa wapo watoto wengi ambao hawajachanjwa na wamo hatarini kuambukizwa. Wizara inaendelea kutekeleza mkakati maalumu wa kuwafikia watoto wote. (Reach Every Child).

13.4.8Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 mradi umejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kutoa mafunzo ya IMCI kwa njia ya masafa, mafunzo ya kuangalia maendeleo na makuaji ya mtoto na mafunzo ya huduma ya watoto wachanga.

2.    Kuinua kiwango cha chanjo zote kufikia zaidi ya asilimia 90 kwa wilaya zilizo chini ya lengo.

3.    Kuanzisha dozi ya pili ya chanjo ya surua (measles 2nd dose) na kufanya kampeni ya surua.

4.    Kuimarisha usimamizi, ufatiliaji na tathmini ya kazi za chanjo katika ngazi zote. 

5.    Kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji wa magonjwa yanayokingwa kwa chanjo (Surua, Pepopunda ya watoto wachanga na ulemavu wa ghafla) ili kufikia viwango na malengo yaliyowekwa kimataifa.

13.5  Mradi wa Uimarishaji wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali


13.5.1Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza Mradi wa Uimarishaji wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali - Pemba maabara iliweza kuchora ramani na kufanya makisio ya ujenzi.  Jumla ya Tsh 16,000, 000/- zinahitajika kwa ajili ya uchoraji wa ramani, Tsh. 22,535,000/- zinahitajika kwa ajili ya uchunguzi wa udongo, na Tsh. 11,465,000/- kwa ajili ya kuzungusha uzio. Kwa mwaka wa fedha 2014/2015 Maabara imeazimia kujenga jengo la maabara ya Mkemia huko Pemba.

13.6  Mradi wa Kupandisha Hadhi Hospitali za Wilaya na Vijiji


13.6.1 Mheshimiwa Spika, mradi huu umeanzishwa kwa lengo la kuzipandisha hadhi hospitali za vijiji kuwa za wilaya na hospitali mbili za wilaya kuwa za mkoa (Abdalla Mzee na Wete).

Hospitali za Wilaya

13.6.2Mheshimiwa Spika, kwa upande wa ujenzi wa hospitali ya Abdalla Mzee, wizara imeshalipa fidia kwa wamiliki wa nyumba, mashamba na majengo ya ibada kwa wahusika ambapo jumla ya Tsh 900,000,000 zimetumika.  Vile vile mkandarasi kwa ajili ya ujenzi huu ameshapatikana na ujenzi unatarajiwa kuanza hivi karibuni.

Hospitali za Vijiji

13.6.3Mheshimiwa Spika, ujenzi wa wodi ya wanawake na wanaume katika hospitali ya Micheweni unaendelea ambao utaenda sambamba na ujenzi wa chumba maalum cha upasuaji zimetumika. Aidha, matengenezo ya nyumba za wafanyakazi, chumba cha upasuaji na ukarabati wa wodi za watoto katika hospitali ya Kivunge yamefanyika.

13.6.4 Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/15 mradi umejipangia kutekeleza kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kuendelea na kazi ya ujenzi wa hospitali ya Abdalla Mzee.

2.    Kuzipatia hospitali vifaa na zana za tiba.

3.    Kumalizia ujenzi wa wodi ya wanawake na wanaume na chumba cha upasuaji katika hospitali ya Micheweni.

13.7  Mradi wa Kupandisha Hadhi Hospitali ya Mnazi Mmoja.


 

13.7.1Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014, wizara kupitia mradi huu imeanza ujenzi wa jengo litakalotumika kwa ajili ya huduma za  upasuaji wa maradhi ya mgongo na ubongo (neurosurgical services). Ujenzi  unatarajiwa kumalizika Oktoba mwaka 2014. Kumalizika kwa ujenzi wa jengo hilo litakalokuwa na chumba cha upasuaji, chumba cha ICU  na wodi za wagonjwa watakaofanyiwa upasuaji kutaimarisha  upatikanaji wa huduma hii na kuwapunguzia wananchi na serikali gharama za kupeleka wagonjwa  wa maradhi hayo nje ya nchi.  Kitengo hiki kitasaidia kuwapatia ujuzi madaktari wetu pindi wakiwa kazini.

 

13.7.2 Mheshimiwa Spika, moja kati ya changamoto niliyoieleza katika hotuba ya Wizara ya mwaka 2013/14 ni kukosekana kwa mtambo wa kuchomea takataka za hospitali (Incenerator), napenda kuwaarifu wajumbe wa Baraza lako kuwa, wizara imefanikiwa kununua kifaa hicho, tayari kimeshafungwa na kinaendelea kufanya kazi.

 

13.7.3Mheshimiwa Spika, mradi wa Orio unaoendeshwa kwa mashirikiano na Serikali ya Uholanzi  tayari umeanza utekelezaji wake kwa kutangaza zabuni za ujenzi. Wakandarasi watatu tayari wamepatikana  na wameshapewa nyaraka za zabuni ili ziweze kutathminiwa. Kazi hiyo itahusisha ujenzi wa kliniki za maradhi maalumu, wodi ya kina mama ya kujifungulia na baada ya kujifungua na chumba cha huduma za dharura (Emergency Units/casuality). Eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi huu ni katika majengo ya zamani ya kiwanda cha dawa kilichopo katika eneo la hospitali ya Mnazi Mmoja.

 

13.7.4Mheshimiwa Spika, ujenzi  mwengine unahusisha wodi mpya ya watoto itakayokuwa na sehemu ya  kutibu wagonjwa wenye maradhi ya figo (Dialysis). Ujenzi huu unatarajiwa kuanza mwezi wa Julai 2014, tayari ramani ya jengo imeshatengenezwa, zabuni imeshaitishwa na mkadandarasi ameshapatikana na kukabidhiwa kazi hiyo.

 

13.7.5Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/15, mradi unatarajia kutekeleza  kazi kuu zifuatazo:-

1.    Kukamilisha ujenzi wa jengo litakalotoa huduma za upasuaji wa maradhi ya uti wa mgongo na ubongo (neurosurgical services).

2.    Kuendelea na ujenzi wa  jengo la watoto lenye sehemu ya matibabu ya maradhi ya figo (Dialysis)

3.    Kuanza ujenzi wa jengo la kliniki za maradhi maalumu, wodi ya kina mama ya kujifungulia na baada ya kujifungua na chumba cha huduma za dharura (Emergency Units/casuality).

4.    Kulifanyia matengenezo jengo la kutolea huduma za matibabu ya macho.

13.8  Mradi wa Kusaidia Kupunguza Vifo Vitokanavyo na Uzazi


13.8.1Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusaidia Kupunguza Vifo Vitokanavyo na Uzazi umetekelezwa kupitia Mkopo kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika (ADB). Mradi huu umetelekezwa kwa awamu ya kwanza kwa kipindi cha miaka mitano (2007-2012). Awamu ya pili ilianza Januari 2013 - June 2014, kipindi ambacho mradi uliongezewa muda wa mwaka mmoja na nusu.

13.8.2Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha nyongeza mradi uliweza kufanikisha kazi za ujenzi wa kituo cha afya na nyumba ya wafanyakazi Mzambarauni Pemba. Kwa upande wa Unguja ujenzi wa kituo kipya cha afya Mwera, nyumba ya wafanyakazi pamoja na matengenezo makubwa ya kituo kikongwe ambacho kitatumika kwa ofisi za afya wilaya ya kati ulifanyika. Mradi pia uliweza kufanya utanuzi na matengenezo ya jengo la wodi ya wazazi na watoto katika hospitali ya Wete. Aidha, ununuzi wa vifaa kwa ajili ya wodi ya wagonjwa wa akili (Mental Wing) katika hospitali ya Wete umefanyika.

13.9  Mradi wa Chuo cha Madaktari Zanzibar (Zanzibar Medical School)


13.9.1Mheshimiwa Spika, Chuo cha Madaktari kinachoendeshwa kwa mashirikiano  na Chuo Kikuu cha Matansus  cha Cuba kimeendelea kutoa mafunzo ya udaktari kwa wanafunzi  (Unguja 38 na Pemba 12), mafunzo hayo yanatolewa kwa ushirikiano mkubwa na madaktari wazalendo wa hapa Zanzibar.

13.9.2Mheshimiwa Spika, chuo hiki kimepata mafanikio makubwa kwani tayari kinatambuliwa na Taasisi ya Umoja wa Vyuo Vikuu Tanzania (TCU). Mafanikio mengine yaliyopatikana ni pamoja na kuvifanyia matengenezo vifaa mbali mbali kama vile “photocopy mashine” na computer pamoja na kuboresha miundombinu ya mawasiliano ya “internet” katika eneo la chuo, ili kuleta mazingira mazuri ya kujifunza. Aidha, wanafunzi 38 kwa Unguja wanatarajia kumaliza masomo yao ifikapo Julai, 2014.

13.9.3Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 wizara itahakikisha kwamba wanafunzi 12 wa udaktari waliopo mwaka wa tano Pemba wanaendelea vizuri kimasomo kwa kuwapatia nyenzo zote zitakazohitajika katika masomo yao.

13.10 Mradi wa Kuimarisha Huduma za Afya Wilayani


 

13.10.1Mheshimiwa Spika, mradi huu unatekelezwa kupitia mfuko wa fedha wa pamoja ‘Basket Fund’ ambao hupata fedha zake kutoka Serikalini na washirika wa maendeleo. Katika utekezaji wake mradi umelenga kusaidia maendeleo ya afya wilayani ambapo kila wilaya hulazimika kuandaa mpango kazi kulingana na mahitaji na vipaumbele vya wilaya husika.

 

13.10.2Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2013/2014 kamati za afya za wilaya Unguja na Pemba zilipata mafanikio makubwa; mafanikio hayo ni pamoja na kuchimba visima kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kwamtipura na Chumbuni, kukipatia umeme kituo kipya cha Pwani Mchangani na vituo sita vya Wilaya Kaskazini “A” vilipatiwa matangi mapya ya maji. Wakati huo huo, matengenezo ya sakafu, madirisha, mapaa, milango na sehemu ya kuhifadhia dawa yalifanywa katika vituo vya Donge Mchangani, Mtende, Muyuni na Muungoni.

 

13.10.3Mheshimiwa Spika, matengenezo mengine yaliyofanywa ni kukamilisha ujenzi wa kituo cha Afya Bwagamoyo pamoja na kufanyiwa matengenezo madogo madogo kwa vituo vya Kiwani, Vumba, Junguni na Minungwini. Aidha, kituo cha afya cha Mgelema kimefanyiwa “fitting” ya umeme na kupatiwa maji, pia ujenzi wa mashimo maalum ya kutupia mazalio kwenye vituo vya Wingwi, Maziwa ng’ombe na Tundauwa ulifanyika.

 

13.10.4 Mheshimiwa Spika, kazi nyengine iliyofanywa na mradi huu ni kununua vifaa vya usafi na kuvisambaza katika vituo vyote vya afya. Kuwepo kwa vifaa hivi kumeongeza usafi katika vituo hivyo. Aidha, wilaya zimeweza kulipia bili za umeme na maji katika vituo vyote vya afya jambo ambalo limeleta faraja kwa uendeshaji wa vituo hivyo; hata hivyo wizara bado inakabiliwa na changamoto kubwa ya kulipishwa umeme na maji kama ni taasisi za kibiashara na hivyo kukwamisha hatua za kumaliza madeni ya umeme yanayotukabili.

 

13.10.5 Mheshimiwa Spika, kazi za utoaji wa huduma za mkoba za chanjo zimeendelea kutolewa katika maeneo ambayo ni tabu kufikika kirahisi. Huduma hizi zimechangia sana kuongeza kiwango cha chanjo na kufikia asilimia 84.4 kutoka asilimia 81 ya mwaka 2012. Halkadhalika, ushirikishwaji na uhamasishaji wa jamii juu ya utoaji wa huduma za afya za mama na mtoto kwa wasambazaji wa dawa za mpangilio majumbani, wakunga wa kienyeji, masheha pamoja na utoaji wa elimu ya afya mashuleni kuhusu afya ya  kinywa na meno umefanyika.

 

13.10.6Mheshimiwa Spika, moja ya mkakati unaotumiwa na wizara katika kufikisha huduma za afya kwa jamii ni kuendesha siku za afya vijijini. Katika siku hizi huduma mchanganyiko zilitolewa ikiwemo elimu ya afya, uchunguzi wa macho, afya ya kinywa na meno, masikio, koo na pua, Kifua Kikuu na Ukoma, upimaji wa hiari wa VVU (VCT), Shindikizo la damu, kutoa  matibabu na rufaa kwa wale ambao wana matatizo zaidi. Huduma hizi zimetolewa katika shehia tofauti katika wilaya zote kumi.

 

13.10.7 Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza hapo awali kuwa kila wilaya husika hupanga mpango kazi kulingana na mahitaji yake. Katika mwaka 2013/14 wilaya ya Micheweni, Chakechake na Wete zilipanga kuongeza idadi ya vyoo katika jamii. Kwa kufanikisha suala hilo wilaya hizo zilinunua vifaa na kuzipatia familia zote zilizoamua kuchimba vyoo. Jumla ya mashimo ya vyoo 150 yalichimbwa katika wilaya ya Micheweni, 130 Wete, na jumla ya vyoo 75 vilichimbwa kwa Wilaya ya Chake.

14.0  CHANGAMOTO


14.1   Mheshimiwa Spika, wizara katika utekelezaji wa majukumu na malengo yake imekuwa ikikabiliwa na changamoto za aina mbali mbali. Baadhi ya changamoto hizo zinahitaji mashirikiano yetu sote kuzipatia ufumbuzi.

14.2  Mheshimiwa Spika, moja ya changamoto inayoikabili sekta ni ongezeko la maradhi yasiyoambukiza yakiwemo maradhi ya kisukari, saratani, shindikizo la damu na athari zinazotokana na ajali za barabarani. Ukuaji wa maradhi haya yenye gharama kubwa ya matibabu umeathiri uwezo wa sekta kuwahudumia wanaopatwa na maradhi haya. Aidha, mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kuendelea kuonekana kama jukumu la sekta ya afya pekee na ugumu wa wananchi kutobadili mfumo wa maisha ikiwemo kuacha kufanya mazoezi, utumiaji wa vyakula visivyo mlo kamili (Balance Diet) na kutopima afya zetu mara kwa mara.

14.3   Mheshimiwa Spika, changamoto nyengine inayotukabili ni kuibuka kwa wauzaji wasio rasmi wa dawa za asili mitaani na katika sehemu za ibada jambo ambalo linaathiri juhudi za wizara katika kuimarisha na kustawisha huduma za tiba asili hapa nchini. Aidha, kuwepo kwa waganga wanaojitangaza katika vyombo vya habari kinyume na taratibu za afya kuwa wanatibu maradhi fulani kunakwamisha juhudi hizi. 

14.4   Mheshimiwa Spika, zipo changamoto ambazo hujitokeza kila mwaka kwa mfano, kukosekana au kuchelewa kupata fedha kumeendela kuathiri upatikanaji wa vitendea kazi kunakopelekea kuzorota au kukosekana kabisa baadhi ya huduma zetu kwa jamii.  Vitendea kazi hivyo ni pamoja na usafiri, mafuta, dawa, vifaa vya tiba na kinga.  Aidha, hali hii imeathiri matengenezo na upanuzi wa majengo hasa vituo vya afya, kutokana na kujengwa zamani na udogo wake kulingana na kutanuka kwa huduma zinazotolewa.

14.5   Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za serikali kuajiri na kupeleka masomoni wafanyakazi wake, wizara bado inakabiliwa na tatizo la uhaba wa wataalamu hali inayoathiri utoaji wa huduma kwenye hospitali na vituo vya afya.

14.6   Mheshimiwa Spika, hali ya lishe kwa wananchi wa Zanzibar bado si ya kuridhisha hususan kwa mama wajawazito na watoto. Hali hii inachangiwa na kuwepo kwa upungufu wa matumizi ya vyakula vyenye virutubishi wakati wa kipindi cha ujauzito, unyonyeshaji, ulishaji usio sahihi kwa watoto na matunzo hafifu ambayo hupelekea lishe duni.

15.0  MALENGO MAKUU YA WIZARA YA AFYA KWA MWAKA WA FEDHA 2014/2015


15.1   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2014/2015 kazi kuu zilizopangwa kutekelezwa na Wizara ya Afya ni pamoja na:-

1.    Kuendelea na mchakato wa kuanzisha vyanzo mbadala vya upatikanaji wa rasilimali fedha ikiwemo Bima ya Afya.

2.    Kuongeza upatikanaji wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi kwa hospitali na vituo vya afya vya Serikali.

3.    Kuimarisha mfumo wa ufuatiliaji na tathmini katika sekta ya afya.

4.    Kuimarisha miundombinu ya afya ikiwemo:-

a.          Ujenzi wa  jengo la watoto lenye sehemu ya matibabu ya maradhi ya figo (Dialysis), katika hospitali ya Mnazi Mmoja

b.          Kuanza ujenzi wa jengo la kliniki za maradhi maalumu, wodi ya kina mama ya kujifungulia na baada ya kujifungua na chumba cha huduma za dharura (Emergency Units/casuality) katika hospitali ya Mnazi Mmoja

c.          Kulifanyia matengenezo jengo la macho katika Hospitali ya Mnazi Mmoja

d.          Kujenga jengo la kutolea huduma kwa waathirika wa madawa ya kulevya (Detoxification Centre) katika hospitali ya Kidongo Chekundu.

e.          Kuendelea na ukarabati wa majengo na vituo vyote vya afya.

5.    Kuimarisha huduma za afya kwa jamii ili kupunguza maradhi ya kuambukiza na yasiyo ya kuambukiza.

6.    Kutayarisha na kupitia miongozo mbali mbali kwa ajili ya utekelezaji wa shughuli za afya.

7.    Kuanzisha mfumo wa kupima utendaji wa wafanyakazi (Performance Appraisal System).

16.0  HITIMISHO


16.1   Mheshmiwa Spika, mafanikio yaliyopatikana hayatokani na juhudi za wizara ya afya na sekta ya watu binafsi tu, bali pia kwa mashirikiano, ushauri na misaada ya hali na mali kutoka mashirika ya kitaifa na kimataifa pamoja na nchi marafiki, taasisi za serikali na siziso za serikali, wananchi wa ndani na nje ya nchi.  Wizara inawashukuru kwa dhati kubwa na inawaomba wasichoke kwani misaada yao ina thamani kubwa kwetu. Shukrani makhsusi ziende kwa Serikali ya Denmark, Cuba, Marekani, India, China, Korea, Hispania, Uingereza, Urusi, Omani, Israili, Uholanzi, Norway na Uturuki.

Aidha, shukurani zetu pia ziende kwa mashirika mbali mbali yakiwemo ADB, CDC, CLINTON FOUNDATION, DANIDA, WHO, PEPFAR, USAID,  GLOBAL FUND, ITALIAN COOPERATION, SAVE THE CHILDREN, IVODE CARENER FOUNDATION, JHIEPIGO, UNICEF, UNFPA, WDF, UNDP, SIGHT SAVERS, PATH FINDER, ICAP, SCORE/ZEST, HIPZ, PROJECT HOPE, KOICA na wale  wote ambao sikuweza kuwaorodhesha kwenye hotuba hii.

16.2   Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha wa 2014/2015 wizara imepangiwa kuchangia Tsh 124,000,000 na kwa Hospitali ya Mnazi Mmoja imepangiwa kuchangia Tsh 550,000,000 na kuingiza katika mfuko mkuu wa serikali. Kiambatisho namba 11 kinatoa ufafanuzi. Pia wizara kupitia SMZ imepangiwa kutumia Tsh 7,253,200,000 kwa kazi za kawaida, Tsh 1,219,200,000 ruzuku na Tsh 14,274,800,000 kwa mishahara na maposho. Kiambatisho namba 12 kinatoa ufafanuzi. Kwa upande wa kazi za maendeleo wizara imepangiwa kutumia Tsh 3,850,000,000 kutoka Serikalini na Tshs 24,356,897,000 ambazo ni misaada kutoka washirika wa maendeleo. Kiambatisho namba 13 kinatoa ufafanuzi.

16.3   Mheshimiwa Spika, naomba Baraza hili liipokee na wajumbe waijadili hotuba yangu, kutoa ushauri na hatimae kuipitisha ili wizara ipate uwezo wa kuwahudumia wananchi kupata huduma bora za afya kwa wepesi. Baada ya maelezo hayo naomba Baraza hili liidhinishe jumla ya Tsh 22,747,200,000 kwa kazi za kawaida, ruzuku, mishahara na maposho, pia naomba Baraza lako liidhinishe jumla ya Tsh 8,282,000,000 kwa ajili ya hospitali ya Mnazi Mmoja kwa matumizi ya kawaida mishahara na maposho. Kwa upande wa kazi za maendeleo baraza liidhinishe jumla ya Tsh 3,850,000,000 kutoka mfuko mkuu wa serikali na Tsh 24,356,897,000 kutoka kwa washirika wa maendeleo.

Kwa heshima kubwa na taadhima, kwa idhini yako NAOMBA KUTOA HOJA.

 

MHESHIMIWA JUMA DUNI HAJI

WAZIRI WA AFYA,

ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.