Na
Said Ameir
RAIS
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein,
amesema Zanzibar na Israeli zina kila sababu za kuimarisha ushirikiano wao
ambao wakati wote umeonesha mafanikio kwa kila upande.
Akizungumza
na Balozi wa Israeli nchini Tanzania anayemaliza muda wake,Gill Haskel, Dk.
Shein alisema ushirikiano kati ya Zanzibar na Israeli umeshuhudia matokeo
mazuri hususan katika sekta za afya na kilimo.
Alisema
chini ya ushirikiano huo Israeli imekuwa ikisaidia matibabu kwa watoto wenye
matatizo ya afya kupitia Mpango wa Huduma ya Afya kwa Watoto ambapo hadi sasa
watoto zaidi 200 hasa wenye matatizo ya moyo wamefaidika na mpango huo.
Alisema
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
ingependa kuona ushiriki zaidi wa Israeli katika kuunga mkono mpango wa serikali
kuimarisha kilimo hasa katika kuwajengea uwezo watafiti wa Zanzibar na kuleta
mabadiliko katika sekta ya kilimo.
Alisema
chini ya mpango huo wa serikali, moja ya lengo ni kujitosheleza kwa chakula kwa
kuongeza uzalishaji kupitia uimarishaji wa kilimo cha umwagiliaji na matumizi
ya mbinu za kisasa za kilimo.
Aliongeza
tangu kuanza kwa mpango huo uzalishaji katika kilimo cha mpunga umeongezeka
mara tano hivyo lengo la kufikia angalau asilimia 50 ya mahitaji ya chakula
ifikapo mwaka 2015/2016 linaelekea kufikiwa.
Sambamba
na kilimo cha mpunga alisema fursa pia
zimeelekezwa katika kuwasiaidia wakulima katika mazao mengine ikiwemo kilimo
cha mbogamboga zikiwemo tungule asili ambazo zinalimwa maeneo kame.
Alitumia
fursa hiyo pia kuiomba serikali ya Israel kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar katika kukabiliana na maafa yakiwemo katika usafiri wa majini.
Alibanisha
kuwa Zanzibar inahitaji kuwa na vifaa na utalaamu kujiandaa na kukabiliana na
maafa ili kupunguza vifo na upotevu wa mali maafa yanapotokea.
Kwa
upande mwingine Dk. Shein alimueleza Balozi huyo fursa zilizopo katika sekta ya
utalii na kueleza matumaini yake kuwaBalozi huyo atatumia fursa ya kuwepo wake
Tanzania kuzitangaza fursa hizo kwa wananchi wa Israeli kuwekeza na kuja
Zanzibar wakiwa watalii.
Alisema
serikali inafanya jitihada kuitangaza Zanzibar katika masoko ya utalii ya China
na Bara Asia ambapo kwa sasa ni watalii wachache kutoka sehemu hizo za dunia
hufika Zanzibar.
Alimueleza
Balozi huyo kuwa mbali ya vivutio vilivyoko,sifa nyingine kubwa ya Zanzibar ni ukarimu wa watu wake na wakati
wote ni salama na tulivu.
Kwa
upande wake, Balozi Gill Haskel ambaye alikuwa amefuatana na mkewe,
alimhakikishia Dk. Shein juu ya azma ya serikali ya nchi yake ya
kuendeleza ushirikiano na misaada yake kwa Zanzibar.
Alisema
anaondoka huku akiwa anaamini kuwa katika kipindi chote alipokuwa akiitumikia
nchi yake ameweza kuimarisha uhusiano kati ya Israel na Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Aliongeza
kuwa anahakika kuwa Balozi ajaye sio tu ataendeleza na kuimarisha ushirikiano
katika maeneo ya ushirikiano yaliyopo sasa bali pia ataangalia uwezekano wa
kupanua maeneo mapya.
No comments:
Post a Comment