Habari za Punde

Taasisi za umma zadaiwa kufanya uharibifu Mji Mkongwe

Mwanrafia Kombo,MCC  na Zuleikha Abdalla
MAMLAKA ya Uhifadhi na Uendelezaji Mji Mkongwe wa Zanzibar, imesikitishwa na hujuma zinazofanywa na baadhi ya taasisi na watu binafsi ndani ya mji huo.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kufanya ziara ya ghafla katika maeneo katika maeneo yaliyohujumiwa,Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka hiyo, Issa Sariboko Makarani, alisema mamlaka yake imesikitishwa na hujuma hizo zilizofanywa na taasisi binafsi kwa kushirikiana na taasisi za serikali.

Alisema katika kipindi hiki cha karibuni kumekua na matukio ya uharibifu wa viguzo vilivyowekwa maalum kwa ajili ya kuzuia gari zisifike maeneo ya ndani kwa lengo la kuzuia uharibifu wa nyumba katika eneo la mji huo.

“Tumekua tukiona uharibifu ukifanywa katika maeneo mbali mbali ya mji wetu ambapo sehemu nyengine hufanywa na watu binafsi na nyengine hufanywa na taasisi za serikali ambazo hufanya hivyo kwa lengo la kupata pesa bila ya kujali kuwa wanaweza kuhatarisha mji wetu kutolewa katika urithi wa kimataifa,” alisema.


Alisema uharibifu huo ni pamoja na ukataji wa miti ndani ya mji huo,kuharibu taa na viguzo vya vizuizi ambao umefanyika katika eneo la Shangani mbele ya hoteli ya Africa House, uharibifu wa taa katika eneo la Forodhani na ukataji wa miti uliofanywa eneo la Darajani.

Alisema walioharibu viguzo mbele ya hoteli ya Africa House ni dhahiri wameshirikiana na taasisi za serikali kwa vile walikwenda Mamlaka kutaka kibali cha kuviondoa na wakakataliwa.

Alisema baada ya mamlaka kukataa kutoa kibali ndipo wamiliki wa hoteli hiyo walipokwenda katika taasisi nyengine ya serikali kuchukua kibali vya kuviondoa viguzo hivyo, na bila kujali taasisi hiyo ilikubali kwa sababu tu itapata mapato.


Alishauri wafanyabiashara kuweka utaratibu wa kutumia maeneo mengine yalio nje ya mji huo kwa lengo la kuhakikisha msongamano unapungua.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.